Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w14 15/10 uku. 7-12
  • Ukuwe na Imani Yenye Nguvu Katika Ufalme

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Ukuwe na Imani Yenye Nguvu Katika Ufalme
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • AHADI AMBAYO INAONYESHA NAMNA KUSUDI LA MUNGU LITATIMIA
  • AGANO AMBALO LINATAMBULISHA ULE UZAO
  • AGANO AMBALO LINAHAKIKISHA KWAMBA UFALME NI WA MILELE
  • AGANO LA KUWA KUHANI
  • MAAGANO NI MUSINGI WA KISHERIA KWA AJILI YA UFALME
  • Mutakuwa “Ufalme wa Makuhani”
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Agano Lenye Linakuhusu
    Buku ya Mukutano Utumishi na Maisha ya Mukristo—2020
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
w14 15/10 uku. 7-12
Ufalme wa Mungu unatawala duniani na wanadamu wanafurahia maisha katika paradiso

U kuwe na Imani Yenye Nguvu Katika Ufalme

“Imani ni tarajio lililohakikishwa la mambo yanayotumainiwa.” —EBR. 11:1.

UNAWEZA KUELEZA?

Kwa kutumia habari “Namna Mungu Atatimiza Kusudi Lake,” rudilia kwa kifupi . . .

  • ahadi ya Edeni.

  • agano na Abrahamu, agano na Daudi.

  • agano la kuwa kuhani kwa mufano wa Melkizedeki.

1, 2. Ni nini itatusaidia kuwa hakika kwamba Ufalme utatimiza kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu, na sababu gani? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

SISI Mashahidi wa Yehova, kila mara tunaambia watu kwamba Ufalme wa Mungu ndio utamaliza matatizo yetu yote, na tunawafundisha kwa bidii kweli hiyo ya Biblia ya maana sana. Sisi pia tunafarijiwa sana wakati tunafikiria yale Ufalme huo utatimiza. Je, tunasadiki kabisa kwamba Ufalme ni jambo la kweli kabisa na kwamba utatimiza kusudi la Mungu? Sababu gani tunapaswa kuwa na imani yenye nguvu katika Ufalme?—Ebr. 11:1.

2 Ufalme wa Masiya ni mupango ambao Mungu Mweza-Yote ameanzisha ili kutimiza kusudi lake kuhusu uumbaji wake. Ufalme huo unategemea musingi wenye nguvu; ni kusema, Yehova ndiye iko na haki kabisa ya kutawala. Mufalme wa Ufalme huo ni nani? Ni nani watatawala pamoja naye? Ni nani watatawaliwa na Ufalme huo? Mambo hayo yamehakikishwa kisheria kupitia maagano mbalimbali, ni kusema, maagano ao makubaliano ya kisheria ambayo yamefanywa na Mungu ao na Mwana wake, Yesu Kristo. Kuchunguza maagano hayo kutatusaidia tuelewe vizuri zaidi namna kusudi la Mungu litatimia na kutatusaidia kuona namna Ufalme ni jambo la kweli kabisa.—Soma Waefeso 2:12.

3. Tutazungumuzia nini katika habari hii na ile ambayo inafuata?

3 Biblia inazungumuzia maagano sita ya lazima sana ambayo yanahusiana na Ufalme wa Masiya ambao utatawaliwa na Kristo Yesu. Maagano hayo ni (1) agano na Abrahamu, (2) agano la Sheria, (3) agano na Daudi, (4) agano la kuwa kuhani kwa mufano wa Melkizedeki, (5) agano jipya, na (6) agano la Ufalme. Tuchunguze sasa namna kila agano linahusiana na Ufalme na namna linasaidia kutimiza kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia na kwa ajili ya wanadamu.—Ona habari yenye kichwa “Namna Mungu Atatimiza Kusudi Lake.”

AHADI AMBAYO INAONYESHA NAMNA KUSUDI LA MUNGU LITATIMIA

4. Kulingana na kitabu cha Mwanzo, Yehova aliamuru mambo gani?

4 Kisha kutayarisha bustani nzuri sana kwa ajili ya wanadamu, Yehova aliamuru mambo matatu kuhusiana na wanadamu: (1) mwanadamu angeumbwa kwa mufano wake, (2) wanadamu wangefanya dunia yote ikuwe paradiso na kuijaza na wazao wao wenye haki, na (3) wanadamu walikatazwa kula matunda ya muti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwa. 1:26, 28; 2:16, 17) Mungu hakukuwa na lazima ya kuamuru mambo mengine. Amri ya kwanza ilitimia kisha mwanadamu kuumbwa; lakini kulikuwa kunabakia amri zingine mbili. Kuishi kulingana na amri hizo mbili kungefanya kusudi la Mungu litimie. Kwa hiyo, sababu gani ilikuwa jambo la lazima kufanya maagano?

5, 6. (a) Namna gani Shetani alijaribu kuzuia kusudi la Mungu? (b) Yehova alifanya nini wakati uasi ulitokea katika Edeni?

5 Kwa sababu ya nia mbaya ya kutaka kuzuia kusudi la Mungu, Shetani Ibilisi alianzisha uasi. Alifanya hivyo kwa kuchagua amri ambayo angetumia kwa urahisi ili kushawishi wanadamu, ni kusema, ile ambayo ilimuomba mwanadamu kutii. Alimushawishi Eva, mwanamuke wa kwanza, akatae kutii amri ambayo iliwaomba wasikule matunda ya muti wa ujuzi wa mema na mabaya. (Mwa. 3:1-5; Ufu. 12:9) Kwa kufanya hivyo, Shetani alitilia shaka haki ya Mungu ya kutawala viumbe Vyake. Kisha, Shetani alishitaki watumishi waaminifu wa Mungu kwa kusema kwamba wanamutumikia Mungu kwa sababu ya faida zao wenyewe.—Ayu. 1:9-11; 2:4, 5.

6 Yehova angefanya nini ili kumaliza upinzani huo ambao ulitokea katika Edeni? Ikiwa angeharibu waasi hao, uasi wao ungemalizika. Lakini hilo lingefanya pia kusudi lake la kujaza dunia na watoto wa Adamu na Eva likose kutimia. Kwa hiyo, hakuwaharibu palepale. Kwa sababu yeye ni Muumbaji mwenye hekima alitoa unabii wa maana sana, ni kusema, ahadi ya Edeni. Alifanya hivyo ili kuhakikisha kwamba, hata mambo madogo-madogo kuhusu ahadi yake kwa ajili ya dunia na kwa ajili ya wanadamu yafikie kutimia.—Soma Mwanzo 3:15.

7. Ahadi ya Edeni inatupatia uhakika gani kuhusu nyoka na uzao wake?

7 Kupitia ahadi ya Edeni, Yehova alitoa hukumu juu ya nyoka na uzao wake, ni kusema, Shetani Ibilisi na wale wote ambao wangejiunga naye ili kupinga haki ya Mungu ya kutawala. Tena kupitia ahadi hiyo, Mungu alipatia uzao wa mwanamuke mamlaka ya kumuharibu Shetani. Kwa hiyo, ahadi ya Edeni inaonyesha kwamba yule mwenye alianzisha uasi katika Edeni ataharibiwa na kwamba matokeo yote ya uasi huo yataisha. Pia ahadi hiyo inaonyesha njia ambayo Mungu atatumia ili kutimiza mambo hayo.

8. Tunajifunza nini juu ya mwanamuke na uzao wake?

8 Uzao wa mwanamuke ni nani? Kwa sababu uzao huo unapaswa kuponda kichwa cha nyoka, ni kusema, ‘kuangamiza’ Shetani Ibilisi ambaye ni kiumbe wa kiroho, uzao huo pia ni wa kiroho. (Ebr. 2:14) Na mwanamuke anayetokeza uzao huo ni mwanamuke wa kiroho pia. Wakati uzao wa nyoka uliendelea kuongezeka, mwanamuke na uzao wake walibakia bila kujulikana kwa miaka karibu 4000 kuanzia wakati Yehova alitoa ahadi katika Edeni. Lakini katika kipindi hicho, Yehova alifanya mupango ili kukuwe maagano mbalimbali ambayo yangetambulisha uzao wa mwanamuke na ambayo yangewahakikishia watumishi wake kwamba atatumia uzao huo ili kumaliza magumu yote ambayo Shetani amewaletea wanadamu.

AGANO AMBALO LINATAMBULISHA ULE UZAO

9. Agano na Abrahamu ni nini, na lilianza kutumika wakati gani?

9 Miaka 2000 hivi kisha Shetani kuhukumiwa, Yehova alimuambia Abrahamu aache makao yake ambayo yalikuwa katika Uru ya Mesopotamia na aende katika inchi ya Kanaani. (Mdo. 7:2, 3) Yehova alimuambia hivi: ‘Enda zako kutoka katika inchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na kutoka kwa nyumba ya baba yako mupaka katika inchi ambayo nitakuonyesha. Nami nitafanya taifa kubwa kutokana na wewe, nitakubariki na kulifanya jina lako kuwa kubwa; na wewe utakuwa baraka. Nami nitawabariki wale wanaokubariki, na yule anayekulaani nitamulaani, na familia zote za inchi zitajibariki kupitia kwako.’ (Mwa. 12:1-3) Maneno hayo yanazungumuzia agano na Abrahamu, ni kusema, agano ambalo Yehova Mungu alifanya pamoja na Abrahamu. Hatujue kabisa ni wakati gani Yehova alifanya agano hilo. Lakini, agano hilo lilianza kutumika katika mwaka wa 1943 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, wakati Abrahamu mwenye miaka 75 alitoka Harani na kuvuka Muto Efrati.

10. (a) Namna gani Abrahamu alionyesha imani yenye nguvu katika ahadi za Mungu? (b) Kuhusu uzao wa mwanamuke, Yehova alitoa maelezo gani hatua kwa hatua?

10 Yehova alirudilia mara nyingi ahadi yake kwa Abrahamu, na kila wakati alikuwa anatoa maelezo zaidi. (Mwa. 13:15-17; 17:1-8, 16) Abrahamu hakusita kumutoa mutoto wake wa pekee kwa sababu alikuwa na imani yenye nguvu katika ahadi za Mungu. Kwa hiyo, Yehova alikazia agano lake kwa kumuhakikishia kwamba atatimiza ahadi yake. (Soma Mwanzo 22:15-18; Waebrania 11:17, 18.) Kisha agano na Abrahamu kuanza kufanya kazi, Yehova alitoa hatua kwa hatua maelezo ya maana kuhusu uzao wa mwanamuke. Uzao huo ungetokea katika kizazi cha Abrahamu, ungekuwa na watu wengi, ungekuwa na daraka la kifalme, ungeharibu maadui wote, na pia wanadamu wengi wangebarikiwa kupitia uzao huo.

Abrahamu anaenda kumutoa Isaka

Abrahamu alionyesha imani yenye nguvu katika ahadi za Mungu(Ona fungu la 10)

11, 12. Namna gani Biblia inaonyesha kwamba agano na Abrahamu litatimia pia kwa njia ya kiroho, na hilo litatuletea faida gani?

11 Agano na Abrahamu lilitimia kwa njia ya kimwili wakati wazao wa Abrahamu waliingia katika Inchi ya Ahadi. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba agano hilo lilipaswa pia kutimia kwa njia ya kiroho. (Gal. 4:22-25) Kuhusu utimizo huo wa pili, roho ya Mungu ilimuongoza mutume Paulo afasirie kwamba sehemu ya kwanza ya uzao wa Abrahamu ni Kristo na kwamba sehemu ya pili ni Wakristo watiwa-mafuta 144000. (Gal. 3:16, 29; Ufu. 5:9, 10; 14:1, 4) Mwanamuke ambaye anatokeza uzao huo ni ‘Yerusalemu wa juu,’ ni kusema, sehemu isiyoonekana ya tengenezo la Mungu ambayo inafanyizwa na viumbe waaminifu wa kiroho. (Gal. 4:26, 31) Kulingana na ahadi ambayo ilitolewa kupitia agano na Abrahamu, uzao wa mwanamuke utawaletea wanadamu baraka nyingi.

12 Agano na Abrahamu linafanya Ufalme wa mbinguni ukuwe na musingi wa kisheria; jambo hilo linafanya Mufalme wa Ufalme wa Mungu na wale watatawala pamoja naye wastahili kuriti Ufalme huo. (Ebr. 6:13-18) Agano hilo litaendelea kufanya kazi mupaka wakati gani? Andiko la Mwanzo 17:7 linasema kwamba agano hilo ni la ‘wakati usio na kipimo [ao milele].’ Litaendelea kufanya kazi mupaka wakati Ufalme wa Masiya utaharibu maadui wote wa Mungu, na mupaka wanadamu wote watakuwa wamebarikiwa. (1 Kor. 15:23-26) Kwa hiyo, wale wote ambao wataishi katika dunia watafaidika milele na baraka za agano hilo. Agano ambalo Mungu alifanya pamoja na Abrahamu linaonyesha kabisa kwamba Yehova ameazimia kutimiza kusudi lake la ‘kujaza dunia’ na wanadamu wenye haki.—Mwa. 1:28.

AGANO AMBALO LINAHAKIKISHA KWAMBA UFALME NI WA MILELE

13, 14. Agano na Daudi linatuhakikishia nini kuhusu utawala wa Masiya?

13 Kupitia ahadi ya Edeni na agano na Abrahamu tunajifunza jambo la maana sana: utawala mukubwa wa Yehova ambao unaonyeshwa kupitia Ufalme wa Masiya unategemea kanuni za Mungu za haki. (Zab. 89:14) Kuna siku serikali hiyo ya Masiya itashindwa kufanya kazi na kwa hiyo kuondolewa? Agano lingine la kisheria ambalo Mungu alifanya linatuhakikishia kwamba jambo hilo halitatokea hata siku moja.

14 Tuchunguze sasa ahadi ya Yehova kwa Mufalme Daudi ambayo ilitolewa kupitia agano na Daudi. (Soma 2 Samweli 7:12, 16.) Wakati Daudi alikuwa mufalme wa Yerusalemu, Yehova alifanya naye agano hilo kwa kumuahidi kwamba Masiya atatokea katika kizazi chake. (Lu. 1:30-33) Kwa hiyo, kisha kipindi fulani Yehova alitoa mafasirio zaidi kuhusu kizazi ambamo uzao ungetokea na akaonyesha kwamba muriti wa Daudi atakuwa na “haki ya kisheria” ya kukaa kwenye kiti cha Ufalme wa Masiya. (Eze. 21:25-27) Kupitia Yesu, ufalme wa Daudi ‘utafanywa imara mupaka wakati usio na kipimo [ao milele].’ Bila shaka, uzao wa Daudi ‘utakuwa mupaka wakati usio na kipimo; na kiti chake cha ufalme kama vile jua.’ (Zab. 89:34-37) Utawala wa Masiya hautaharibiwa hata kidogo, na baraka za utawala huo ni za milele.

AGANO LA KUWA KUHANI

15-17. Kulingana na agano la kuwa kuhani kwa mufano wa Melkizedeki, uzao wa mwanamuke utakuwa na daraka gani lingine, na sababu gani?

15 Kupitia agano ambalo Mungu alifanya na Abrahamu na lile ambalo alifanya na Daudi, tuko hakika kwamba uzao wa mwanamuke utakuwa na daraka la kifalme. Lakini, inaomba jambo lingine la maana sana. Kwa sababu, ili wanadamu wa mataifa yote wabarikiwe kabisa, ni lazima wakombolewe kutoka katika utumwa wa zambi na kuingizwa katika familia ya Yehova ya ulimwenguni pote. Ili kutimiza jambo hilo, inaomba uzao ukuwe pia na daraka la kuhani. Muumbaji mwenye hekima amefanya mupango mwengine wa kisheria ili jambo hilo liwezekane. Mupango huo ni agano la kuwa kuhani kwa mufano wa Melkizedeki.

16 Yehova alionyesha kupitia Mufalme Daudi kwamba atafanya agano la pekee pamoja na Yesu. Agano hilo lina kusudi mbili: Kumufanya Yesu ‘aikale kwenye mukono wa kuume [wa Mungu]’ mupaka atiishe maadui wake, na kumufanya akuwe ‘kuhani mupaka wakati usio na kipimo kwa mufano wa Melkizedeki.’ (Soma Zaburi 110:1, 2, 4.) Sababu gani anapaswa kuwa kuhani ‘kwa mufano wa Melkizedeki’? Kwa sababu mbele watoto wa Abrahamu waingie katika Inchi ya Ahadi, Melkizedeki, mufalme wa Salemu, alikuwa “kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi.” (Ebr. 7:1-3) Ni Yehova mwenyewe ndiye alimufanya kuwa kuhani. Maandiko ya Kiebrania yanaonyesha kwamba ni yeye tu ndiye mwanadamu ambaye alikuwa mufalme na kuhani kwa wakati mumoja. Tena, kwa sababu hakuna mwanadamu aliyetimiza daraka hizo mbele yake na kisha yeye, anastahili kuitwa “kuhani daima” ao kuhani wa milele.

17 Kupitia agano hilo, Yehova mwenyewe amemufanya Yesu kuwa kuhani. Kwa hiyo, Yesu atakuwa ‘kuhani milele kwa mufano wa Melkizedeki.’ (Ebr. 5:4-6) Agano hilo linaonyesha wazi kwamba Yehova ameapa mwenyewe kisheria kwamba atatumia Ufalme wa Masiya ili kutimiza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu na kwa ajili ya dunia.

MAAGANO NI MUSINGI WA KISHERIA KWA AJILI YA UFALME

18, 19. (a) Kila agano ambalo tumezungumuzia linaonyesha nini kuhusu Ufalme? (b) Tutazungumuzia jambo gani katika habari ambayo inafuata?

18 Wakati tunafikiria maagano ambayo tumechunguza, tunaelewa namna kila agano linahusiana na Ufalme wa Masiya na tunaelewa namna kila agano ni musingi wa kisheria kwa ajili ya Ufalme. Ahadi ya Edeni inatuhakikishia kabisa kwamba Mungu atatimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia na kwa ajili ya wanadamu kupitia uzao wa mwanamuke. Agano ambalo Yehova alifanya na Abrahamu linafasiria uzao wa mwanamuke ni nani na utakuwa na daraka gani.

19 Agano ambalo Yehova alifanya na Daudi linatoa mafasiriyo zaidi kuhusu kizazi ambamo sehemu ya kwanza ya uzao ingetokea, na linamupatia haki ya kutawala dunia ili kuwaletea wanadamu baraka za milele kupitia Ufalme wa Masiya. Agano la kuwa kuhani kwa mufano wa Melkizedeki linatuhakikishia kwamba uzao utakuwa na daraka la kuhani. Lakini, Yesu hatakuwa peke yake ili kufikisha wanadamu kwenye ukamilifu. Wanadamu fulani wametiwa mafuta ili wao pia wakuwe wafalme na makuhani. Wanadamu hao watatoka wapi? Habari ambayo inafuata itazungumuzia jambo hilo.

NAMNA MUNGU ATATIMIZA KUSUDI LAKE

Yesu anamurudishia Mungu Ufalme

Ahadi ya Edeni inaonyesha kwamba Mungu atatumia Ufalme ili kutimiza kusudi lake kwa ajili ya dunia na kwa ajili ya wanadamu. Hapa chini, kuna maagano sita ambayo yanasaidia kutimiza kusudi la Mungu:

AGANO NA ABRAHAMU

AGANO KATI YA: Yehova na Abrahamu

KUSUDI: Linaweka musingi wa kisheria ili kuwezesha “uzao” wa ‘mwanamuke,’ ambaye anatajwa katika Mwanzo 3:15, utawale katika Ufalme

AGANO LA SHERIA

AGANO KATI YA: Yehova na Israeli wa kimwili

KUSUDI: Linalinda “uzao” wa mwanamuke na linaongoza watu kwa Masiya

AGANO NA DAUDI

AGANO KATI YA: Yehova na mufalme Daudi

KUSUDI: Linaonyesha kwamba Masiya Mufalme atatokea katika kizazi cha Mufalme Daudi na kwamba baraka za Ufalme zitakuwa za milele

AGANO LA KUWA KUHANI KWA MUFANO WA MELKIZEDEKI

AGANO KATI YA: Yehova na Yesu

KUSUDI: Linatokeza mupango wa kisheria ili Yesu, ambaye ni sehemu ya kwanza ya “uzao” wa mwanamuke, akuwe mufalme na kuhani milele

AGANO JIPYA

AGANO KATI YA: Yehova na Israeli wa kiroho

KUSUDI: Linaweka musingi wa kisheria ili Wakristo 144000 wafanyize sehemu ya pili ya “uzao” wa mwanamuke, na wakubaliwe kuwa wana wa Mungu

AGANO LA UFALME

AGANO KATI YA: Yesu na Israeli wa kiroho

KUSUDI: Linawapatia Wakristo watiwa-mafuta nafasi ya kuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo mbinguni

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine