Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w15 1/3 uku. 13-15
  • Zawadi Zenye Zilistahili Mufalme

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Zawadi Zenye Zilistahili Mufalme
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • KUVUKA JANGWA LA ARABIA
  • “SIRI YA BIASHARA ILIYOCHUNGWA MUZURI SANA WAKATI WOTE”
  • Matumizi ya Vitu vya Kujipodoa Wakati wa Zamani
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
w15 1/3 uku. 13-15
Vikolezo mbalimbali vyenye harufu ya muzuri

Zawadi Zenye Zilistahili Mufalme

‘Wanajimu kutoka sehemu za mashariki . . . wakafungua hazina zao na kumutolea zawadi, zahabu na ubani na manemane.’— Mathayo 2:1, 11.

NI ZAWADI gani unaweza kuchagua kutolea mutu wa maana sana? Wakati wa zamani vikolezo fulani vilikuwa vya maana sana kama zahabu, vilikuwa vya bei sana na kwa hiyo vilifanyiza zawadi zenye zilistahili kupewa mufalme.a Ndiyo maana kati ya zawadi zenye wanajimu (watu wenye kutabiri matukio kwa kuangalia nyota) walipatia ‘mufalme wa Wayahudi,’ zawadi mbili zilikuwa vikolezo vyenye harufu ya muzuri.—Mathayo 2:1, 2, 11.

Mafuta ya Zeri

Mafuta ya Zeri

Biblia inasema tena kama wakati malkia wa Sheba alimutembelea Mufalme Sulemani, ‘alimupatia talanta 120 za zahabu, na mafuta ya zeri kwa wingi sana, na mawe ya samani; na kulikuwa hakujapata kuwa na mafuta ya zeri kama yale ambayo malkia wa Sheba alimupatia Mufalme Sulemani.’b (2 Mambo ya Nyakati 9:9) Wafalme pia walimutumia Sulemani mafuta ya zeri ili kumuonyesha nia yao ya muzuri.—2 Mambo ya Nyakati 9:23, 24.

Sababu gani vikolezo na vitu vingine vyenye vilitokana na vikolezo hivyo vilikuwa vya maana sana na vya bei wakati wa zamani? Kwa sababu vilikuwa na kazi nyingi za maana; kwa mufano vilitumiwa ili kupamba mwili, katika mambo ya dini, na katika mazishi. (Soma kisanduku “Namna Vikolezo Vyenye Harufu ya Muzuri Vilitumiwa Wakati wa Zamani.”) Vikolezo vilikuwa na bei sana kwa sababu watu wengi walivinunua na kwa sababu iliomba garama kubwa ili kuvisafirisha na kuviuzisha.

KUVUKA JANGWA LA ARABIA

Kida

Kida

Wakati wa zamani, mimea fulani ya vikolezo iliota katika Bonde la Yordani. Lakini, vikolezo vingine vilitoka katika inchi zingine. Biblia inataja aina mbalimbali za vikolezo. Kati ya vikolezo vilivyojulikana sana kuna zafarani, udi, zeri, mudalasini, ubani, na manemane. Zaidi ya hivyo, kulikuwa pia vikolezo vya chakula vilivyojulikana sana kama vile bizari, mnanaa, na dili.

Vikolezo hivyo vya kigeni vilitoka katika inchi gani? Udi, kida, na mudalasini vilipatikana katika inchi zenye kujulikana leo kuwa China, India, na Sri Lanka. Vikolezo kama vile manemane na ubani vilitoka katika miti na vichaka vyenye viliota katika maeneo ya jangwa yenye kuanzia kusini mwa Arabia mupaka Somalia katika Afrika. Na nardo ni kikolezo chenye kilitoka tu India katika milima ya Himalaya.

Zafarani

Zafarani

Ili kufika Israeli, vikolezo vingi vilipaswa kusafirishwa kupitia Arabia. Kulingana na kitabu kimoja, hilo lilikuwa kati ya sababu zenye zilifanya Arabia ikuwe “inchi pekee iliyosafirisha biashara kati ya eneo la Mashariki na eneo la Mangaribi” katika kipindi cha miaka 2000 mbele tu ya kuzaliwa kwa Yesu. (The Book of Spices) Katika eneo la Negebu kusini mwa Israeli kulipatikana miji ya zamani, ngome, na nafasi magari ya kukokotwa yalisimama; hivyo vyote vinaonyesha kuwa wafanyabiashara wa vikolezo walikuwa wanapita hapo. Ripoti moja ya shirika la UNESCO inasema kama nafasi hizo “zinaonyesha biashara yenye faida sana . . . kutoka Arabia ya kusini mupaka Mediterania.”

“Vikolezo havikukuwa vikubwa-vikubwa, vilikuwa vya bei kali, na watu walivitafuta sana. Ilikuwa biashara yenye kupendwa sana.”—The Book of Spices

Magari ya kukokotwa yenye kubeba vikolezo hivyo vyenye harufu ya muzuri yalisafiri kwa kawaida kilometre 1800 kupitia Arabia. (Ayubu 6:19) Biblia inazungumuzia wasafiri Waishmaeli waliobeba vikolezo kama vile “ubani mweusi na zeri na gome lenye utomvu” kutoka Gileadi kuenda Misri. (Mwanzo 37:25) Watoto wa Yakobo waliuzisha Yosefu, ndugu yao, kuwa mutumwa kwa wafanyabiashara hao.

“SIRI YA BIASHARA ILIYOCHUNGWA MUZURI SANA WAKATI WOTE”

Dili

Dili

Wafanyabiashara wa Arabia waliongoza karibu biashara yote ya vikolezo kwa miaka mingi. Ni wao tu ndio walikuwa wanaleta vikolezo vya kutoka Asia, kama vile kida na mudalasini. Ili kuzuia watu wa maeneo ya Mediterania wasiende wao wenyewe kununua vikolezo katika maeneo ya Mashariki ambako kulikuwa vikolezo, wafanyabiashara wa Arabia walieneza habari za kutunga juu ya hatari za kupata vikolezo. Kulingana na kitabu kimoja, nafasi kwenye vikolezo vilitoka “labda ndiyo siri ya biashara iliyochungwa muzuri sana wakati wote.” (The Book of Spices)

Bizari

Bizari

Wafanyabiashara wa Arabia walieneza habari gani? Herodote, mwanahistoria Mugiriki aliyeishi kati ya mwaka wa 401 na 500 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, alieleza juu ya ndege wa kuogopesha waliojenga nyumba zao kwa kutumia ngozi za mumea wa mudalasini katika miteremuko isiyoweza kufikiwa. Aliandika kama, ili kupata kikolezo hicho cha bei, watu walitia nyama nyingi kwenye mwanzo wa muteremuko. Ndege walibeba nyama nyingi sana katika nyumba zao na hilo lilifanya nyumba hizo ziangukie chini na kupasuka. Hivyo, watu wangeweza kukamata ngozi hizo za mudalasini na kuziuzishia wafanyabiashara. Habari kama hizo zilienea sana. Kitabu kimoja kinasema kama “[mudalasini] uliuzishwa kwa bei kali sana kwa sababu ya hatari za kuwazia za kuupata.” (The Book of Spices)

Mnanaa

Mnanaa

Mwishowe, siri ya wafanyabiashara wa Arabia ilivumbuliwa na watu wengine wakaanza kuuzisha vikolezo. Katika miaka 100 ya kwanza mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, muji wa Alexandria, katika Misri, ulifikia kuwa bandari (port) na nafasi kubwa ya biashara ya vikolezo. Wakati wanamaji walijifunza namna ya kusafiri kwa kufuata mwendo wa pepo za Bahari ya India za wakati wa mvua kali, mashua za Waroma zilisafiri kutoka bandari za Misri mupaka India. Kwa hiyo, vikolezo hivyo vya bei kali vikakuwa vingi na bei yavyo ikashuka.

Leo, hatuwezi kulinganisha bei ya vikolezo na bei ya zahabu. Na hatuwezi kuona vikolezo kuwa zawadi zenye kustahili mufalme. Lakini, watu wengi sana katika dunia wanaendelea kutumia vikolezo katika marashi (parfum) na katika madawa, na pia ili kufanya chakula chao kuwa kitamu. Kwa kweli, harufu ya muzuri ya vikolezo inafanya watu wengi wavipende sana leo, kama vile ilikuwa maelfu ya miaka iliyopita.

fungu la ngozi za mudalasini

Mudalasini

a Katika Biblia, maneno ya luga ya kwanza yaliyotafsiriwa “kikolezo” ao “vikolezo” yanahusu zaidi sana vitu vyenye kutokana na mimea yenye harufu ya muzuri lakini haiko vikolezo vya chakula.

b “Mafuta ya zeri” ni mafuta yenye harufu ya muzuri ao umajimaji wenye kunata uliotoka katika miti na vichaka.

Namna Vikolezo Vyenye Harufu ya Muzuri Vilitumiwa Wakati wa Zamani

Mafuta yaliyotumiwa kutia mafuta na uvumba mutakatifu. Yehova alimuambia Musa namna ya kutengeneza mafuta yaliyotumiwa kutia mafuta, ao marhamu, na uvumba mutakatifu. Vyote viwili vilikuwa na vikolezo ine tofauti. (Kutoka 30:22-25, 34-38) Makuhani fulani walikuwa wanajua muzuri kufanya mafuta matakatifu na walisimamia kazi ya kutoa vitu hivyo.—Hesabu 4:16; 1 Mambo ya Nyakati 9:30.

Marashi na mafuta ya marhamu. Watu wenye walikuwa na uwezo walitumia unga-unga (poudre) wenye harufu ya muzuri ili kuweka harufu ya muzuri katika nyumba, kwenye mavazi, vitanda, na mwili wao. (Esta 2:12; Methali 7:17; Wimbo wa Sulemani 3:6, 7; 4:13, 14) Maria, dada ya Lazaro alimwanga “mafuta yenye marashi, nardo halisi” ya bei kali juu ya nywele na miguu ya Yesu. Bei ya chupa hiyo ndogo ya “nardo halisi” ilikuwa mushahara wa mwaka moja.—Marko 14:3-5; Yohana 12:3-5.

Kutayarisha miili kwa ajili ya mazishi. Nikodemu alitoa ‘musokoto [muchanganyiko] wa manemane na udi’ ili kutayarisha mwili wa Yesu kwa ajili ya mazishi. (Yohana 19:39, 40) Na wanafunzi fulani wa Yesu walitayarisha “manukato na mafuta yaliyotiwa marashi” na kuyapeleka kwenye kaburi lake.—Luka 23:56–24:1.

Kukoleza chakula. Inawezekana Waisraeli walitumia pia vikolezo ao viungo ili kufanya samaki ao nyama ikuwe tamu. Vikolezo vingine vilitumiwa ili kufanya divai ikuwe kali.—Wimbo wa Sulemani 8:2.

Maelezo Juu ya Vikolezo Viwili Vyenye Yesu Alipewa

Ubani na manemane vilitokana na umajimaji wenye kunata uliopatikana kwa kukata ngozi ya miti midogo-midogo ao vichaka vyenye miiba.

Miti ya ubani iliota Arabia katika maeneo ya kusini yaliyo pembeni ya bahari, na miti ya manemane iliota sana katika inchi zilizo kama jangwa zenye kuitwa leo Somalia na Yemeni. Vikolezo hivyo viwili vilionwa kuwa vya maana sana kwa sababu vilikuwa na harufu ya muzuri. Yehova mwenyewe alichagua vikolezo hivyo vitumiwe katika ibada yake: manemane ilikuwa kati ya vitu vyenye vilitumiwa kutengeneza mafuta matakatifu yaliyotumiwa kutia mafuta, na ubani ulikuwa kati ya vitu vyenye vilitumiwa kutengeneza uvumba mutakatifu. (Kutoka 30:23-25, 34-37) Lakini vikolezo hivyo vilitumiwa kwa njia tofauti.

Ubani, wenye ulitumiwa sana kama uvumba, ulipaswa kuchomwa ili kutoa harufu yake ya muzuri. Lakini umajimaji wenye kunata uliotoka katika muti wa manemane, ulitumiwa moja kwa moja. Manemane inatajwa mara tatu katika habari zenye kuhusu Yesu: alipewa zawadi ya manemane wakati alikuwa mutoto (Mathayo 2:11), alipewa manemane yenye kuchangwa na divai ili kupunguza maumivu wakati alikuwa kwenye muti wa mateso (Marko 15:23), na ilikuwa kati ya vikolezo vyenye vilitumiwa ili kutayarisha mwili wake kwa ajili ya mazishi (Yohana 19:39).

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine