Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w19 Mwezi wa 2 uku. 26-30
  • Uriti Muzuri wa Kikristo Ulinisaidia Niendelee Muzuri

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Uriti Muzuri wa Kikristo Ulinisaidia Niendelee Muzuri
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2019
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • WAZAZI WETU WALITUPENDA
  • KAZI ZA MWANZO-MWANZO
  • UTUMISHI WENYE KUFURAHISHA KATIKA INCHI YA NIGERIA
  • MIGAO YA MUPYA
  • Kumutumainia Yehova Kuliniletea Usalama wa Kweli
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2023
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2019
w19 Mwezi wa 2 uku. 26-30
Woodworth Mills

HABARI JUU YA MAISHA YA WATU

Uriti Muzuri wa Kikristo Ulinisaidia Niendelee Muzuri

Woodworth Mills Anaeleza Maisha Yake

KATIKATI ya usiku, muto mukubwa sana wenye kuitwa Niger wenye upana wa kilometre 1.6, ulikuwa mbele yetu, ulikuwa unateremuka haraka. Vita ya watu wenyewe kwa wenyewe mu inchi ya Nigeria ilikuwa inapamba moto, kwa hiyo, kuvuka Muto Niger kungeleta hatari ya kifo. Lakini tulipaswa kutia uzima wetu katika hatari, zaidi ya mara moja. Namna gani nilijikuta mu hali hiyo? Acha kwanza nieleze mambo fulani yenye ilitokea mbele nizaliwe.

Mu mwaka wa 1913, baba yangu, John Mills, alibatizwa katika Muji wa New York wakati alikuwa na miaka 25. Ndugu Russell njo mwenye alitoaka hotuba ya ubatizo. Wakati mufupi kisha pale, Baba alihamia kwenye kisiwa cha Trinité na kule alimuoa Constance Farmer, Mwanafunzi wa Biblia mwenye bidii. Baba alikuwa anasaidia rafiki yake William Brown kuonyesha watu “Foto-Drama ya Uumbaji.” Waliendelea kufanya vile mupaka wakati Brown na bibi yake walitumwa kutumikia katika Afrika ya Mangaribi mu mwaka wa 1923. Baba yangu na mama yangu, wenye walikuwa na tumaini la kuenda mbinguni, waliendelea kutumikia katika kisiwa cha Trinité.

WAZAZI WETU WALITUPENDA

Wazazi wangu walikuwa na watoto kenda, walipatia mutoto wao wa kwanza jina la Rutherford, jina la ndugu mwenye wakati huo alikuwa musimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society. Wakati nilizaliwa tarehe 30 Mwezi wa 12, 1922, wazazi wangu waliniita Woodwoth, jina la ndugu mwenye wakati huo alikuwa musimamizi wa uandikaji wa L’Âge d’Or (leo ni Amuka!). Wazazi wetu walitusomesha sisi wote ili tupate elimu ya musingi, lakini walikazia sana miradi ya kiroho. Mama alikuwa na uwezo wa ajabu wa kufikiri juu ya Maandiko ili kusadikisha mutu. Baba alifurahia kutuelezea habari za Biblia kwa kutumia mwili wake wote ili kufanya ishara za mwili juu ya kutusaidia tuone picha ya mambo katika akili.

Bidii yao ilileta matokeo ya muzuri. Kati yetu sisi watoto tano wanaume, tatu walisoma Masomo ya Gileadi. Kati ya dada zetu, tatu walifanya kazi ya upainia kwa miaka mingi katika visiwa vya Trinité na Tobago. Kupitia mafundisho na mufano muzuri wa wazazi wetu, walitupanda sisi watoto “katika nyumba ya Yehova.” Walikuwa wanatutia moyo na hilo lilitusaidia tubakie mu nyumba hiyo na kuendelea muzuri “katika viwanja vya Mungu wetu.”​—Zb. 92:13.

Mipango ya mahubiri ilikuwa inafanywa mu nyumba yetu. Mapainia walikuwa wanakutana mule na mara mingi walikuwa wanazungumuza juu ya Ndugu George Young, misionere kutoka mu inchi ya Kanada mwenye alikuwa ametembelea kisiwa cha Trinité. Wazazi wangu walikuwa wanazungumuza kwa furaha juu ya wale wenye walikuwa wanahubiri nao zamani, ni kusema, Brown na bibi yake, wenye walikuwa wanatumikia mu Afrika ya Mangaribi wakati huo. Ile mambo yote ilinichochea nianze kuhubiri wakati nilikuwa na miaka kumi.

KAZI ZA MWANZO-MWANZO

Magazeti yetu ilikuwa moto-moto wakati huo, ilifunua waziwazi dini ya uongo, wafanya-biashara wenye pupa, na wakubwa wa politike wenye udanganyifu. Kwa hiyo, mu mwaka wa 1936, viongozi wa dini walichochea gavana wa kisiwa cha Trinité akataze vichapo vyote vya Watch Tower. Tulificha vichapo, lakini tuliendelea kuvitumia mupaka wakati vyote viliisha. Tulikuwa tunafanya maandamano ya kutangaza habari na ya kutembeza kinga, wakati wa ile maandamano tulikuwa tunagawia watu mialiko na tulikuwa tunavaa pankarte. Tulihubiri hata mu maeneo ya mbali sana ya kisiwa cha Trinité pamoja na kikundi chenye kilitoka mu muji wa Tunapuna, chenye kilikuwa na motokari yenye ilikuwa na chombo cha kuongeza sauti. Hilo lilifurahisha sana! Ile matukio yenye kufurahisha ilinichochea nibatizwe wakati nilikuwa na miaka 16.

Kikundi cha Tunapuna chenye kuhubiri na motokari yenye kuwa na chombo cha kuongeza sauti

Kikundi cha Tunapuna chenye kuhubiri na motokari yenye kuwa na chombo cha kuongeza sauti

Uriti wenye tulipata mu familia yetu na ile mambo yenye nilifanya wakati nilikuwa ningali mutoto, ilinichochea nikuwe na tamaa ya kuwa misionere. Nilikuwa ningali na tamaa hiyo wakati nilienda kwenye kisiwa cha Aruba mu mwaka 1944 na kujiunga na Ndugu Edmund Cummings. Tulifurahia kukusanyika pamoja na watu kumi ku Ukumbusho wa mwaka wa 1945. Mwaka wenye alifuata, kutaniko la kwanza lilianzishwa katika kisiwa hicho.

Oris na Woodworth Mills katika miaka yao ya ujana

Pamoja na Oris, nilifurahia tena maisha kwa njia ingine

Wakati kidogo kisha pale, nilimuhubiria ku kazi Oris Williams, mufanyakazi mwenzangu. Oris alijikaza sana ili kutetea mafundisho yenye alikuwa amefundishwa. Hata hivyo, kujifunza Biblia kulimusaidia ajue mambo yenye Neno la Mungu linafundisha kabisa na akabatizwa tarehe 5 Mwezi wa 1, 1947. Kisha wakati fulani, tulipendana na tukaoana. Alianza kufanya kazi ya upainia mu Mwezi wa 11, 1950. Pamoja na Oris, nilifurahia tena maisha kwa njia ingine.

UTUMISHI WENYE KUFURAHISHA KATIKA INCHI YA NIGERIA

Mu mwaka wa 1955, tulialikwa kusoma Masomo ya Gileadi. Ili kujitayarisha kwa ajili ya masomo hayo, mimi na Oris tuliacha kazi zetu za kimwili, tuliuzisha nyumba yetu na vitu vyetu vingine, na tukatoka Aruba. Tarehe 29 Mwezi wa 7, 1956, tulimaliza kusoma darasa la 27 la Masomo ya Gileadi, na tulitumwa kutumikia mu inchi ya Nigeria.

Woodworth Mills na Oris pamoja na familia ya Beteli katika Lagos, Nigeria, mu mwaka wa 1957

Tuko pamoja na familia ya Beteli katika Lagos, Nigeria, mu mwaka wa 1957

Wakati alikumbuka maisha yetu, Oris alisema hivi: “Roho ya Yehova inaweza kusaidia mutu ajipatanishe na magumu ya kazi ya umisionere. Tofauti na bwana yangu, sikukuwa ninapenda hata kidogo kuwa misionere. Nilipenda kuwa na nyumba yangu na kuzaa watoto. Nilibadilisha mawazo wangu wakati nilielewa kama kazi ya kuhubiri habari njema inapaswa kufanywa haraka sana. Wakati tulimaliza masomo ya Gileadi, niliazimia kabisa kufanya kazi ya kueneza injili nikiwa misionere. Wakati tuliingia mu mashua yenye iliitwa Queen Mary, Ndugu Worth Thornton, mwenye alikuwa anatumikia mu biro ya Ndugu Knorr, alituaga kwa kusema hivi: ‘Muende muzuri! Alituambia kama tutatumikia ku Beteli. Nilivuta pumuzi na kusema hivi: ‘Ee, hapana!’ Lakini bila kukawia, nilibadilisha mawazo yangu na nilifikia kupenda sana Beteli, kwenye nilitumikia migao mbalimbali. Mugao wenye nilifurahia zaidi ni kutumika mahali pa kukaribisha wageni. Ninapendaka watu, na mugao huo ulinipatia nafasi ya kuonana moja kwa moja na ndugu wa Nigeria. Wengi walikuwa wanafika na wamejaa vumbi, wenye kuchoka, wenye kiu, na njaa. Nilifurahia kuwatimizia mahitaji yao kwa kuwapatia kitu fulani cha kuwatuliza na kuwafariji. Ile yote ilikuwa utumishi mutakatifu kwa Yehova, na ile njo ilikuwa inaniletea furaha na kutosheka.” Kwa kweli, kila mugao ulitusaidia tuendelee muzuri.

Mu mwaka wa 1961, wakati tulikutana pamoja katika familia kwenye kisiwa cha Trinité, Ndugu Brown alituelezea mambo fulani yenye kufurahisha yenye alijionea katika Afrika. Kisha nikawaelezea ongezeko lenye tulikuwa nalo katika Nigeria. Kwa upendo, Ndugu Brown alinizungusha mikono yake na kumuambia baba yangu hivi: “Johnny, haujaweza kufika katika Afrika, lakini Woodworth ameweza!” Baba yangu alijibu hivi: “Uendelee, Worth! Uendelee!” Watumishi hao wenye bidii wenye walitumikia Yehova kwa miaka mingi walinitia moyo sana. Na hilo lilinifanya nikuwe na tamaa zaidi ya kutimiza muzuri sana utumishi wangu.

Woodworth Mills, Antonia Brown, William “Bible” Brown, na Oris Mills

William “Bible” Brown na bibi yake, Antonia, walitutia moyo sana

Mu mwaka wa 1962, nilipata pendeleo la kupewa mazoezi zaidi kwa miezi kumi katika darasa la 37 la Masomo ya Gileadi. Ndugu Wilfred Gooch, mwenye alikuwa mwangalizi wa tawi katika Nigeria wakati huo, alisoma darasa la 38 la Masomo ya Gileadi na alitumwa kutumikia katika Uingereza. Wakati huo nilipewa daraka la kuwa mwangalizi wa tawi ya Nigeria. Kwa kufuata mufano wa Ndugu Brown, nilikuwa ninasafiri sana, na nilifikia kujua na kupenda ndugu na dada wapendwa wa Nigeria. Hata kama hawakukuwa na vitu mingi vya kimwili, vyenye watu wengi wenye kuishi mu inchi zenye kuendelea sana wako navyo, walikuwa na furaha na wenye kutosheka. Hilo lilionyesha wazi kama haiombe kuwa na feza ao vitu mingi vya kimwili ili mutu akuwe na maisha yenye maana. Hata kama walikuwa na hali ngumu, ilifurahisha sana kuwaona ku mikutano wako safi, wenye kujitengeneza muzuri, na wenye kuvaa kwa njia ya heshima. Wakati walikuwa wanakuja ku mikusanyiko, wengi wao walikuwa wanakuja katika motokari kubwa-kubwa na katika bolekajasa (bisi zenye kuwa wazi zenye zilitengenezwa mu inchi hiyo). Mara mingi, ku bisi hizo kulikuwa kunaandikwa maandishi yenye kuvutia. Maandishi moja ilisema hivi: “Matone kidogo-kidogo njo inafanyaka bahari kubwa.”

Ile maandishi ni ya kweli kabisa! Bidii ya kidogo yenye kila mutu anafanya ni ya maana; na sisi tulitoa muchango wetu. Kufikia mwaka wa 1974, kutosha inchi ya Amerika, Nigeria ikakuwa inchi ya kwanza yenye ilifikia hesabu ya wahubiri 100 000. Kulikuwa ongezeko kabisa!

Wakati huo wa ongezeko, kulikuwa vita kali ya watu wenyewe kwa wenyewe mu inchi ya Nigeria kuanzia mwaka wa 1967 mupaka 1970. Kwa miezi fulani, ndugu na dada zetu wenye walikuwa katika Biafra, upande mwingine wa Muto Niger, hawakuweza kuwasiliana na biro ya tawi. Tulikuwa na daraka la kuwapelekea chakula cha kiroho. Kama vile nilionyesha ku mwanzo wa habari hii, kusali na kumutegemea Yehova kulitusaidia kuvuka muto huo mara mingi.

Ninaendelea kukumbuka safari hizo za kuvuka Muto Niger, zilitutia mu hatari ya kifo kwa sababu ya maaskari wenye walifurahia kupiga masasi bila sababu, magonjwa, na hatari zingine. Ilikuwa hatari kupita upande wa maaskari wa serikali, lakini ilikuwa hatari zaidi kupita upande wa waasi ngambo ingine ya muto. Siku moja usiku, kwa kutumia mutumbwi wenye kubeba watu, nilivuka Muto Niger kutoka Asaba mupaka Onitsha na nilienda kutia moyo wazee katika Enugu. Mu safari ingine, nilitia moyo wazee mu muji wa Aba katika wakati wa giza kwa sababu watu hawakuruhusiwa kuwa na mwangaza wa umeme. Mu muji wa Port Harcourt, mukutano wetu uliisha mbiombio kwa sala wakati maaskari wa serikali walishambulia maaskari waasi katika eneo la Biafra, karibu na muji huo.

Mikutano hiyo ilikuwa ya maana ili kuwahakikishia ndugu zetu wapendwa kama Yehova anawahangaikia kwa upendo, na ili kuwatolea mashauri yenye walikuwa nayo lazima kabisa juu ya kuepuka kuunga mukono upande wowote, na juu ya kuendelea kuwa na umoja. Ndugu na dada wa Nigeria waliweza kabisa kuvumilia muvurugo huo mubaya sana. Upendo wao ulikuwa wenye nguvu sana kupita chuki ya ukabila, na waliendelea kuonyesha umoja wa Kikristo. Nilifurahi sana kuwa pamoja nao wakati huo wa magumu!

Mu mwaka wa 1969, Ndugu Milton Henschel alikuwa musimamizi wa Mukusanyiko wa Kimataifa “Amani Duniani” wenye ulifanyika katika Uwanja wa Michezo wa Yankee, New York. Kwa sababu nilikuwa musaidizi wake, nilijifunza mambo mingi. Nilijifunza ile mambo kwa wakati wenye kufaa kwa sababu mu mwaka wa 1970, tulifanya Mukusanyiko wa Kimataifa “Watu wa Nia Njema” mu muji wa Lagos katika Nigeria. Tulifanya mukusanyiko huo kisha tu vita ya watu wenyewe kwa wenyewe, kwa hiyo ulipita muzuri kwa sababu tu ya baraka ya Yehova. Mukusanyiko huo ulikuwa tukio kubwa sana. Ulifanywa mu luga 17, na watu 121 128 walihuzuria. Ndugu Knorr na Henschel na wageni wenye walifanya safari za ndege za kukodiwa kutoka Amerika na Uingereza waliona moja kati ya ubatizo mukubwa zaidi wa Kikristo tangu ule wenye ulifanywa ku Pentekoste; kwenye mukusanyiko huo watu 3 775 walibatizwa! Kusaidia kutayarisha tukio hilo pengine njo wakati wenye nimekuwa na kazi mingi sana za kufanya mu maisha yangu. Ongezeko hilo la wahubiri lilikuwa ongezeko la ajabu sana!

Mukusanyiko wa Kimataifa “Watu wa Nia Njema” katika Lagos, Nigeria, mu mwaka wa 1970

Watu 121 128 wenye kuzungumuza luga 17, kutia ndani luga ya Ibo, walihuzuria Mukusanyiko wa Kimataifa “Watu wa Nia Njema”

Kwa miaka zaidi ya 30 yenye nilitumikia katika Nigeria, wakati fulani nilifanya kazi ya mwangalizi mwenye kusafiri na ya mwangalizi wa eneo katika Afrika ya Mangaribi. Wamisionere walikuwa wanafurahi sana kuona kama wanahangaikiwa kipekee na kutiwa moyo! Nilifurahi sana kuwahakikishia kama hawakukuwa wamesahauliwa! Kazi hiyo ilinifundisha kama kupendezwa na kila mutu kipekee njo siri ya kusaidia watu waendelee muzuri na waendelee kuwa na nguvu na umoja mu tengenezo la Yehova.

Ni kwa musaada tu wa Yehova njo tuliweza kupambana na magumu yenye ilitokezwa na vita ya watu wenyewe kwa wenyewe na magonjwa. Sikuzote, tuliona kabisa baraka za Yehova. Oris alisema hivi:

“Sisi wote wawili tuligonjwa malaria mara mingi. Wakati fulani, Worth alizimia na kupelekwa mu hospitali katika muji wa Lagos. Niliambiwa kama pengine hatapona, lakini, jambo la kufurahisha ni kwamba alipona! Wakati alirudiliwa na ufahamu, alizungumuza juu ya Ufalme wa Mungu na munganga mwenye alikuwa anamuchunga. Kisha wakati fulani, nilienda na Worth ili kutembelea munganga huyo, Bwana Nwambiwe, ili kumusaidia aendelee kupendezwa na ujumbe wa Biblia. Alikubali kweli na alifikia kuwa muzee wa kutaniko katika Aba. Na mimi niliweza kusaidia watu wengi wakuwe watumishi wa Yehova wenye bidii, hata Waislamu wenye walikuwa wanashikilia sana dini. Tulifurahi sana wakati tulifikia kujua na kupenda watu wa Nigeria, desturi yao, namna yao ya kuishi, na luga yao.”

Jambo lingine lenye tulijifunza ni hili: Ili tuendelee muzuri katika mugao wetu mu inchi ya kigeni, tulipaswa kupenda ndugu na dada zetu hata kama desturi zao hazikufanana na zetu.

MIGAO YA MUPYA

Kisha kutumikia ku Beteli ya Nigeria, mu mwaka wa 1987, tulipewa mugao mupya wa kuwa wamisionere wenye kutumikia katika shamba. Tulitumwa kwenye kisiwa cha muzuri sana cha Sainte Lucie katika Karibea. Mugao huo ulikuwa wenye kupendeza sana, lakini ulikuwa na magumu yake. Tofauti na Afrika, kwenye mwanaume alikuwa anaoa wanamuke mingi, hapa katika kisiwa cha Sainte Lucie, shida ilikuwa kwamba bibi na bwana walikuwa wanaishi pamoja bila kuoana kulingana na sheria. Neno la Mungu lenye nguvu lilisaidia wengi kati ya wanafunzi wetu wa Biblia kufanya mabadiliko yenye ilihitajiwa.

Woodworth Mills na Oris katika miaka yao uzee

Nilimupenda Oris sana kwa miaka yote 68 yenye tulifanya naye mu ndoa

Wakati nguvu zetu ziliendelea kupunguka kwa sababu ya uzee, Baraza Lenye Kuongoza lilitutendea kwa upendo kwa kutuhamishia ku makao makubwa katika Brooklyn, New York, Amerika, mu mwaka wa 2005. Ninamushukuru Yehova kila siku kwa sababu alinipatia Oris, mwanamuke muzuri sana. Adui yetu, ni kusema, kifo alimushinda mu mwaka wa 2015, na ninaendelea kusikia huzuni sana ya kumupoteza. Alikuwa rafiki muzuri na bibi mwenye upendo, mwenye sifa za mingi za muzuri. Nilimupenda sana kwa miaka yote 68 yenye tuliishi pamoja. Tulielewa kama siri ya kuwa na furaha, mu ndoa na mu kutaniko, ni kuheshimia ukichwa, kusameheana kwa kupenda, kuendelea kuwa wanyenyekevu, na kuonyesha sifa za tunda la roho.

Wakati tulivunjika moyo, tulimutegemea Yehova ili atusaidie tuendelee kumutumikia. Wakati tuliendelea kujipatanisha na hali, tuliona kama mambo iliendelea kuwa muzuri kila wakati, na mambo ya muzuri zaidi ingali mbele yetu!​—Isa. 60:17; 2 Ko. 13:11.

Kwenye visiwa vya Trinité na Tobago, Yehova alibariki kazi ya wazazi wangu na ya wengine. Kulingana na ripoti ya hivi majuzi, watu 9 892 wamejiunga na ibada safi. Kwenye kisiwa cha Aruba, wengi walitumika ili kutia nguvu kutaniko la kwanza lenye nilikuwaka ndani. Leo, kuko makutaniko 14 yenye kuendelea muzuri kwenye kisiwa hicho. Kuhusu Nigeria, hesabu ya wahubiri imeongezeka sana kufikia wahubiri 381 398. Na kwenye kisiwa cha Sainte Lucie, wahubiri 783 wanaendelea kutegemeza Ufalme wa Yehova.

Sasa niko na miaka zaidi ya 90. Zaburi 92:14 inasema hivi juu ya wale wenye wamepandwa katika nyumba ya Yehova: “Hata wakati wa uzee wataendelea kusitawi [ao, kuendelea muzuri]; wataendelea kuwa na nguvu na kuwa wabichi.” Niko mwenye shukrani sana juu ya maisha yenye nimeishi katika utumishi wa Yehova. Uriti muzuri wa Kikristo wenye nilipata umenichochea nimutumikie Yehova kwa ukamili. Juu ya upendo wake mushikamanifu, Yehova ameniruhusu ‘nisitawi katika viwanja vya Mungu [wangu].’​—Zb. 92:13.

a Ona Amuka! ya tarehe 8 Mwezi wa 7, 1972, uku. 24-26 (katika kifaransa).

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine