Je! Unao “Mwiba Katika Mwili”?
1 Tunatamani kwa hamu kutimiza utume wetu wa kuhubiri habari njema kwa uwezo wetu wote. Hata hivyo, wengi wa ndugu na dada zetu wapendwa wanaona vigumu kushiriki kikamili kwa sababu magonjwa makali ya kimwili au ulemavu hujitokeza, vikifanya iwe vigumu kufanya kwa kadiri ambavyo wangetaka. Kwao, linaweza kuwa jambo gumu kushindana na hisia za kuvunjika moyo, zaidi wanapoona wengine kuwazunguka wakiwa wenye kutenda sana katika huduma.—1 Kor. 9:16.
2 Kielelezo cha Kuiga: Mtume Paulo alilazimika kupigana na “mwiba katika mwili.” Mara tatu alimsihi Yehova amwondolee kizuizi hicho chenye kulemea, alichoeleza kuwa “malaika wa Shetani” aliyefuliza kumpiga kofi. Walakini, ingawa hilo, Paulo alivumilia na kuendelea mbele katika huduma yake. Hakusikitikia hali yake au kuwa mlalamikaji asiyekoma. Yeye alijitoa kikamili. Siri ya fanikio lake katika pigano ilikuwa uhakikisho kutoka kwa Mungu: “Fadhili yangu isiyostahiliwa yakutosha wewe; kwa maana nguvu yangu inafanywa kamilifu katika udhaifu.” Udhaifu wa Paulo uligeuka kuwa nguvu wakati alipojifunza kukubali hali yake na kumtegemea Yehova na roho takatifu ili kuvumilia.—2 Kor. 12:7-10.
3 Namna Unavyoweza Kuvumilia: Je! udhaifu wa kibinadamu unatia mipaka juu ya utumishi wako kwa Mungu? Ikiwa ni hivyo, iga mtazamo wa Paulo. Hata ikiwa ugonjwa wako au ulemavu wako hauna dawa ya kuukomesha katika mfumo huu wa mambo, unaweza kutia tumaini lako kamili katika Yehova, ambaye anaelewa mahitaji yako na ambaye ataandaa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida.” (2 Kor. 4:7) Faidika na msaada unaopatikana kwako katika kutaniko, bila kuwa mwenye kujitenga. (Mez. 18:1) Ikiwa unaona kuwa vigumu kushiriki katika kazi ya nyumba kwa nyumba, tafuta njia zenye kutenda za kufanya mahubiri ya vivi hivi au ushahidi kwa njia ya simu.
4 Ingawa mwiba katika mwili unaweza kupunguza kile uwezacho kufanya katika huduma, hauhitaji kuhisi kana kwamba haushiriki katika huduma. Kama vile Paulo, wewe pia waweza “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili isiyostahiliwa ya Mungu,” ukifanya kile ambacho nguvu na hali yako vinakuruhusu kufanya. (Mdo. 20:24) Kadiri unavyofanya jitihada ya kutimiza huduma yako, jua kwamba Yehova anafurahi sana.—Ebr. 6:10.