Yehova hutoa nguvu
1 Wewe unamwonaje mtume Paulo? Kadiri tunavyosoma kitabu cha Matendo, tunatambua jinsi alivyokuwa mwenye bidii katika utumishi wa Yehova. Paulo alitimizaje yale yote aliyofanya? Alisema: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.” (Flp. 4:13) Sisi pia tunaweza kufaidika na nguvu ambayo Yehova hutoa. Namna gani? Kwa kufaidika na maandalizi sita ambayo anafanya ili kututia nguvu kiroho.
2 Neno la Mungu: Kama vile tu tunavyopaswa kula chakula ili kudumisha nguvu yetu ya kimwili, tunapaswa kujilisha Neno la Mungu ili tubaki hai kiroho. (Mt. 4:4) Biblia inatoa nguvu kwa ajili ya kututegemeza. Ili kudumisha bidii na shauku yetu kwa ajili ya kweli, tunahitaji kujitoa katika funzo la kibinafsi na kutafakari kwenye maana, kila siku ikiwezekana.—Zab. 1:2, 3.
3 Sala: Ni jambo la maana kumkaribia Yehova, zaidi sana wakati tunapokuwa na mahitaji ya pekee. Kupitia roho yake, yeye hutoa nguvu kwa wale wanaomwomba hiyo katika sala. (Luka 11:13; Efe. 3:16) Maandiko yanatutia moyo ‘tudumu katika sala.’ (Rom. 12:12) Je, unafanya hivyo?
4 Kutaniko: Tunapata pia nguvu na kitia-moyo kutokana na mikutano ya kutaniko na kutokana na ushirika wenye shauku tunaofurahia huko pamoja na ndugu na dada zetu. (Ebr. 10:24, 25) Wakati tunapovurugika akili, wanatutia moyo na kutusaidia kwa upendo.—Mez. 17:17; Mhu. 4:10.
5 Huduma ya shambani: Kushiriki kikawaida katika huduma kunatusaidia tuendelee kukaza fikira juu ya Ufalme na baraka zake. Roho zetu zinainuliwa wakati tunaposaidia wengine wajifunze kuhusu Yehova. (Mdo. 20:35) Sisi sote hatuwezi kuhama ili kutumikia mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi au kushiriki katika utumishi wa wakati wote, lakini tunaweza katika njia nyinginezo kushiriki vya kutosha katika huduma.—Ebr. 6:10-12.
6 Waangalizi Wakristo: Tunafaidika kutokana na kitia-moyo na msaada ambao wazee hutoa. Yehova amewapa mgawo wa kulichunga kundi la Mungu wanalolitunza. (1 Pet. 5:2) Waangalizi wasafiri hujenga makutaniko wanayohudumia, kama vile tu Paulo alivyofanya katika siku yake.—Rom. 1:11, 12.
7 Mifano ya watu waaminifu: Ni jambo lenye kutia nguvu kufikiria mifano yenye kutia moyo ya wafanyakazi waaminifu wenzetu, wa kale na wa kisasa. (Ebr. 12:1) Wakati unapohitaji kutiwa nguvu, kwa nini usisome moja ya masimulizi ya maisha yenye kutia moyo katika magazeti yetu, ripoti yenye kujenga katika Kitabu-Mwaka, au mengine kati ya masimulizi yenye kusisimua kuhusu historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova katika kitabu Wapiga-Mbiu?
8 Ndugu mmoja, ambaye sasa yuko kati-kati ya miaka yake ya 90, alikubali kweli akiwa kijana mchanga. Wakati alipokuwa bado mchanga, imani yake ilijaribiwa. Kwanza kabisa, wengine ambao walikuwa wakitenda kwa kushirikiana na kutaniko waliacha tengenezo la Yehova. Kisha kulikuwa kazi ya nyumba kwa nyumba, ambayo aliona kuwa ngumu. Hata hivyo, alitegemea Yehova sikuzote. Bila kukawia, akawa mwenye kufurahia huduma. Na leo? Ingawa afya yenye kudhoofika, yeye bado ni mshiriki wa familia ya Betheli ya Brooklyn, akitumikia katika Baraza Linaloongoza. Hajuti kuona ameshikamana na tengenezo la Yehova.
9 Dada mmoja ambaye ni mshiriki wa familia ya Betheli ya Uingereza alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 13. Akaanza kupainia pamoja na ndugu yake mwaka uliofuata, na mwaka mwingine uliofuata, baba yake akafungwa gerezani kwa sababu ya kutounga kwake mkono upande wowote wakati wa Vita ya Ulimwengu II. Aliendelea kumtegemea Yehova ili kupata nguvu, naye aliendelea kumtumikia Mungu wa kweli. Baada ya wakati fulani, akaolewa na ndugu mwaminifu, nao wakaendelea pamoja kufanya mapenzi ya Yehova. Baada ya miaka 35 ya ndoa, mume wake akafa kwa ghafula. Dada huyo alipata tena nguvu kutoka kwa Yehova, naye ameendelea kumtumikia Yehova mpaka leo, akitazamia kutumikia milele akiwa mshiriki wa familia ya kidunia ya Yehova.
10 Yehova husaidia na kutia nguvu watumishi wake waaminifu. “Anawapa nguvu wenye kuzima roho, naye anamwongezea uwezo yeye asiye na nguvu.” Tunaweza kupata chanzo hicho cha nguvu kisicho na mipaka kwa kufaidika na maandalizi yote sita yaliyotajwa hapo juu. Kumbuka: “Wao wanaongojea BWANA watapata nguvu mpya; . . . watapiga mbio na hawatachoka; watatembea, wala hawatazimia roho.” (Isa. 40:29-31) Paulo alimtegemea sana Yehova ili kupata nguvu, nasi tunapaswa kufanya hivyo.