Je, Inakuzuia Usihubiri?
1 Watu wengi wana maisha yenye shughuli sana. Mashahidi wa Yehova wako kati ya watu wenye shughuli zaidi—wakijifunza Neno la Mungu, wakihudhuria mikutano ya kutaniko, na kushiriki katika utumishi wa shambani. Zaidi ya hayo, sisi tuna shughuli ya kufanya kazi ya kimwili, kazi ya nyumbani au ya shuleni, na madaraka mengine mengi, ambayo yote huchukua wakati. Hilo ni jambo gumu hasa kwa vichwa vya familia.
2 Kwa sababu ya hali mbaya za kiuchumi mahali pengi, huenda vichwa vya familia wakalazimika kutumika saa nyingi na kufanya jitihada kubwa ili kupata riziki. Wakati kazi za kimwili zenye kuomba wakati mwingi na jitihada nyingi zinapochukua sehemu kubwa ya wakati wao na nguvu yao, wao hubaki na wakati mdogo na nguvu ndogo kwa ajili ya mahubiri. Kwa kuwa wanalazimika kutoa vitu vya kimwili kwa familia zao, huenda wengine wakafikiri kwamba wanaweza kushiriki katika huduma kwa kiasi kidogo tu. (1 Tim. 5:8) Ni kweli kwamba leo kuna mikazo mingi yenye kuhusiana na kupata mambo ya lazima maishani. Lakini kazi ya kimwili ya mtu haipaswi kumzuia asihubiri habari njema. (Mk. 13:10) Kwa sababu hiyo, ni vizuri tuchunguze hali yetu halisi.
3 Kwa kuwa hali ya ulimwengu ni yenye kubadilika sikuzote, huenda kichwa cha familia akaelekea kutumia wakati wenye kupita kiasi kazini ili kuongeza akiba zake za kifedha kwa ajili ya hali mbaya zinazoweza kutokea bila kutazamiwa. (1 Kor. 7:31) Ingawa huenda kazi ya kimwili yenye kuongezeka ikaonekana kuwa yenye kutoa vitu vya kimwili vya zaidi au nafasi zaidi za kujiburudisha, je, kazi hiyo itafanya familia iwe yenye furaha na yenye kutosheka zaidi ikiwa inachukua wakati unaotumiwa katika mambo ya kiroho na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida? Bila shaka, tunataka kuepuka jambo lolote ambalo linaweza kuhatarisha hali yetu ya kiroho. Kufuata shauri la Yesu la ‘kujiwekea akiba ya hazina mbinguni’ na kuwa “tajiri kuelekea Mungu” ndio mwendo wa hekima.—Mt. 6:19-21; Luka 12:15-21.
4 Tafuta Faida za Ufalme Kwanza: Yesu alifundisha wafuasi wake waweke mambo ya kiroho mbele ya kitu kingine chochote. Aliwahimiza: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tule nini?’ au, ‘Tunywe nini?’ au, ‘Tuvae nini?’ ” Kwa nini alisema hivyo? Alieleza: “Kwa maana Baba yenu wa kimbingu ajua mwahitaji vitu hivi vyote.” Ikiwa tunasadiki jambo hilo kwelikweli, hakutakuwa kitu kitakachotuzuia tusifanye yale ambayo Yesu alisema baadaye: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu . . . vyote hivi [vya kimwili vya lazima] mtaongezewa.” Mungu atashughulikia mambo hayo ya lazima! (Mt. 6:31-33) Kwa kweli, huu sio wakati wa kuvutwa na mahangaiko yasiyofaa kuhusu kupata riziki, au kuvutwa na tamaa ya kuwa na hali ya raha katika mfumo huu wa mambo ambao karibuni utapitilia mbali.—1 Pet. 5:7; 1 Yn. 2:15-17.
5 Kusudi la msingi la kazi ya kimwili ni kutolea mtu vitu vya kimwili vinavyohitajiwa. Lakini ni kiasi gani tunachohitaji? Mtume Paulo aliandika: “Tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.” Je, tunajaribu kupata zaidi ya vitu hivyo? Ikiwa ndiyo, huenda tukawa wenye kuvuna matokeo ambayo kuhusu hayo Paulo alionya: “Wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo.” (1 Tim. 6:8, 9; Mt. 6:24; Luka 14:33) Tunawezaje kutambua ikiwa sisi ni wenye kuzuiwa na tamaa zenye kupita kiasi?
6 Ikiwa mambo ya kimwili tunayofuatia yanatufanya tushiriki kwa kiasi kidogo tu katika utumishi wa shambani au kushindwa kuona uhitaji wa kujinyima vitu kwa ajili ya habari njema, hapo kuna uhitaji wa kurekebisha mambo tunayotanguliza. (Ebr. 13:15, 16) Maisha yenye kiasi zaidi yatasaidia sana ili kuondoa kizuizi hicho kinachotufanya tusihubiri. Faida za Ufalme zinapaswa sikuzote kuja pa nafasi ya kwanza kuhusiana na matumizi ya wakati wetu na nguvu yetu.
7 Kazi Isiyo ya Bure: Maneno ya Paulo yanatutia moyo tuwe sikuzote na ‘mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana, tukijua kwamba kazi yetu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.’ (1 Kor. 15:58) “Kazi ya Bwana” iliyo ya kwanza kabisa ni ile ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Ili kushiriki zaidi iwezekanavyo, tunapaswa kupanga wakati kwa ajili ya utumishi wa shambani kila juma na kujitahidi tusitumie wakati huo katika jambo jingine lolote. (Efe. 5:15-17) Tunapofanya hivyo, kazi ya kimwili wala jambo jingine lolote halitazuia huduma yetu.
8 Wakati tunapojitoa ili kushiriki kweli za Biblia pamoja na wengine, tunapata ile furaha ya juu zaidi inayotokana na kutoa. (Mdo. 20:35) Kwa kufuatia kazi ya kuhubiri Ufalme, tunaweza kungojea wakati ujao tukiwa na uhakika, ‘kwa maana Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yetu na upendo tulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’—Ebr. 6:10.