Onyesheni Hangaiko Lenye Upendo Kwa ‘Wavulana Wasio na Baba’
1 Yehova ni “baba ya yatima.” (Zab. 68:5) Hangaiko lake kuhusu hali yao njema linaoneshwa katika amri hii aliyotolea taifa la Israeli la kale: “Musitese mujane au yatima. Kama ukiwatesa katika njia yo yote, na wanalia kwangu, hakika nitasikia kilio chao.” (Kut. 22:22, 23) Sheria ya Mungu ilitia ndani pia maandalizi ili kutosheleza mahitaji ya kimwili ya watu hao. (Kumb. 24:19-21) Chini ya mpango wa Kikristo, waabudu wa kweli wanaonywa “kutazama mayatima na wajane katika dhiki yao.” (Yak. 1:27) Jinsi gani tunaweza kuiga hangaiko hilo lenye upendo la Yehova kwa wale wanaokomaa katika familia za mzazi mwenye kulea pekee watoto au zinazogawanyika kidini?
2 Mazoezi ya Kiroho: Ikiwa wewe ni mzazi mwenye kulea watoto pekee yako au ikiwa una mwenzi asiyeamini, huenda kuongoza funzo la Biblia pamoja na watoto wako liwe jambo gumu. Lakini funzo la Biblia lenye ukawaida na lenye maana ni la lazima ili wawe watu wenye kukomaa na wenye kusawazika. (Mez. 22:6) Kuwa na mazungumzo kuhusu mambo ya kiroho kila siku pamoja nao ni jambo la maana pia. (Kumb. 6:6-9) Mara kwa mara, huenda ujisikie kuwa mwenye kuvunjika moyo, lakini usikate tamaa. Umgeukie Yehova ili kupata nguvu na mwongozo ‘unapoendelea kuwalea [watoto wako] katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’—Efe. 6:4.
3 Ikiwa unahitaji msaada fulani katika kuchukua madaraka yako ya Kimaandiko, julisha wazee mahitaji yako. Wanaweza kukutolea mapendekezo yenye kutumika au kukusaidia katika kuweka mpango mzuri wa kawaida wa kiroho kwa ajili ya nyumba yako.
4 Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia: Katika karne ya kwanza, Timotheo alifikia kuwa mtumishi wa Yehova mwenye bidii ingawa alikomaa katika nyumba iliyogawanyika kidini. Bila shaka, jitihada zenye bidii za mama yake na nyanya yake za kumfundisha katika maandiko matakatifu katika ujana wake zilitimiza fungu la maana. (Mdo. 16:1, 2; 2 Tim. 1:5; 3:15) Hata hivyo, yeye alifaidika pia kutokana na ushirika pamoja na Wakristo wengine, kutia ndani mtume Paulo, aliyemtaja Timotheo kuwa ‘mtoto wake mpendwa na mwaminifu katika Bwana.’—1 Kor. 4:17.
5 Hivyohivyo leo, ni jambo lenye faida kama nini wakati ndugu na dada waliokomaa kiroho wanapokuwa na hangaiko lenye upendo kuelekea wavulana na wasichana wasio na baba katika kutaniko! Je, unamjua kila mmoja kwa jina? Je, unaongea nao kwenye mikutano ya Kikristo na kwenye pindi nyingine? Waalike waungane nawe katika huduma ya shambani. Labda mara kwa mara unaweza kufanya mzazi anayelea pekee watoto wake au mzazi aliye pekee mwenye kuamini awe pamoja na watoto wake, katika funzo la familia yako au katika mipango kwa ajili ya tafrija inayofaa. Vijana hawa wanapokuona kama rafiki wao, inaelekea waige mfano wako na kukubali kitia-moyo chako.—Flp. 2:4.
6 Yehova anahangaikia sana wavulana na wasichana wasio na baba, na ana thawabisha jitihada zetu zenye upendo za kuwasaidia waifanye kweli kuwa mali yao wenyewe. Wengi waliokua katika familia yenye mzazi mwenye kulea watoto pekee yake au katika nyumba yenye kugawanyika walipata kitia-moyo kama hicho na sasa wanatumika kwa uaminifu wakiwa mapainia, watumishi wa huduma, wazee, waangalizi wasafiri, wamishonari, au washiriki wa familia ya Betheli. Na sisi wote tutafute njia za ‘kupanuka’ katika upendo wetu kwa wale wasio na baba katika kumwiga Baba wetu wa kimbingu.—2 Kor. 6:11-13.