Kisanduku Cha Maulizo
◼ Tunapaswa kuwa waangalifu juu ya mambo gani tunapotolea wafungwa ushahidi?
Ulimwenguni pote kuna wafungwa karibu milioni nane, ambao wengi kati yao huonyesha kwamba wanapendezwa na habari njema. (1 Tim. 2:4) Ofisi moja ya tawi inapokea barua 1,400 hivi kila mwezi kutoka kwa wafungwa na washiriki wa familia zao wakiomba vichapo au ziara ya kibinafsi. Ingawa wafungwa wengi wanaonyesha kupendezwa kwa unyofu, mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba wengine wanafanya kana kwamba wanapendezwa, wakitafuta faida za kichoyo kutoka kwa watu wa Mungu. Kwa sababu hiyo, sote tunapaswa kuwa waangalifu juu ya mambo yafuatayo kuhusiana na kutolea wafungwa ushahidi.
Katika visa vingi wafungwa hutolewa ushahidi kwa njia ya barua. Inapendekezwa kwa mkazo kwamba dada wasiwaandikie wafungwa wa kiume, hata ikiwa ni kwa kusudi la kutoa msaada wa kiroho. Daraka hilo linapaswa kushughulikiwa tu na ndugu wenye kustahili. Dada wenye kustahili wanaweza kutolewa mgawo wa kuandikia wafungwa wa kike ambao kwa unyofu wanaonyesha kwamba wanapendezwa na Biblia. Fedha au zawadi za kibinafsi hazipaswi kutumwa kwa wafungwa, ijapokuwa jambo hilo linaweza kuombwa.
Mfungwa anapoonyesha kupendezwa, jina lake na anwani yake vinapaswa kutolewa kwa kutaniko linalopatikana katika eneo la gereza. Kwa kawaida ndugu wenye kustahili katika kutaniko hilo wanajua jinsi ya kushughulikia hali mbalimbali zinazoweza kutokea. Ikiwa kutaniko halijulikani, habari hizo zinapaswa kutumwa kwenye ofisi ya tawi.
Si vibaya kwa ndugu waliochaguliwa kufanya mikutano na wafungwa ili wengi waweze kujifunza wakati mmoja. Hata hivyo, matukio ya pekee ambayo katika hayo wahubiri wanachangamana na wafungwa bila kujizuiza hayapaswi kufanyika katika magereza. Zaidi ya hiyo, si jambo la hekima kwa wahubiri kutembelea gereza na kushirikiana kwa ukaribu na wafungwa ikiwa mambo hayo hayakupangwa kimbele.
Acheni tuwe “wenye hadhari kama nyoka na bado kuwa wasio na hatia kama njiwa” tunaposhiriki habari njema na wafungwa.—Mt. 10:16.