Kazi Inayotegemezwa na Mungu
1 Kati ya watumishi wa Mungu leo, wachache ndio wenye kuwa na elimu sana, mali, au umashuhuri katika mfumo wa mambo wa sasa. Kwa sababu hiyo, watu fulani wanakataa huduma yetu wakiiona kuwa isiyo ya maana. (Isa. 53:3) Lakini, kazi tunayofanya ya kufundisha Biblia imeletea mamilioni ya watu faraja na tumaini ulimwenguni pote. Watu wa kawaida wamepataje matokeo hayo yenye kutokeza? Ni kupitia tu tegemezo la Mungu. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 1:8) Mtume Paulo alieleza: “Mungu alivichagua vitu dhaifu vya ulimwengu, ili aviaibishe vitu vyenye nguvu.”—1 Kor. 1:26-29.
2 Mitume na Wakristo wengine wa karne ya kwanza walikuwa kwa kiasi kikubwa “wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Mdo. 4:13) Lakini, walifuatia kwa ujasiri utume wao wa kuhubiri habari njema, na Yehova alibariki jitihada zao. Ijapokuwa vizuizi na upinzani, ‘neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi katika njia yenye nguvu.’ Kwa kuwa kazi ilitegemezwa na Mungu, hakuna jambo ambalo lingeweza kuisimamisha. (Mdo. 5:38, 39; 19:20) Hali imekuwa hivyohivyo katika nyakati za kisasa. Hata upinzani mkali kutoka kwa watawala wenye nguvu haujaweza kuzuia habari njema kusitawi na kukua.—Isa. 54:17.
3 Sifa Yote Imwendee Mungu: Je, hali yetu yenye upendeleo kama wahudumu wa Mungu, inatutolea sababu ya kujisifu? Hata kidogo. Akirejezea kwenye huduma ya Kikristo, Paulo aliandika: “Sisi tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili nguvu zinazopita zile za kawaida ziwe za Mungu na si zile za kutoka ndani yetu wenyewe.” (2 Kor. 4:7) Paulo alitambua kwamba aliweza kutimiza huduma yake kwa sababu tu alikuwa na nguvu ambazo Mungu alimpa.—Efe. 6:19, 20; Flp. 4:13.
4 Sisi pia tunatambua kwamba kazi ya kuhubiri ni yenye kutimizwa kwa sababu tu ‘tumepata msaada kutoka kwa Mungu.’ (Mdo. 26:22) Kupitia tangazo la ulimwenguni pote kama hilo, Yehova ni mwenye kututumia katika njia ya ajabu ili kusababisha mtikiso katika mataifa—alama ya hukumu yenye kuharibu itakayokuja hivi karibuni. (Hag. 2:7) Sisi ni wenye pendeleo kama nini kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” katika mavuno makubwa ya kiroho!—1 Kor. 3:6-9.