“Panukeni”
1 Katika undugu wa Kikristo, kila mmoja wetu analo daraka la kufanya kutaniko liwe lenye uchangamfu. (1 Pet. 1:22; 2:17) Uchangamfu huo unakuzwa wakati ‘tunapopanuka’ katika upendo mwororo mmoja na mwenzake. (2 Kor. 6:12, 13) Kwa nini ni jambo la lazima kupata kujua ndugu na dada zetu vizuri?
2 Urafiki Wenye Nguvu: Kadiri tunavyofahamiana vizuri sana na waamini wenzetu, tunafikia kuthamini kabisa imani yao, uvumilivu wao, na sifa zao nyingine. Makosa yao yanaonekana kuwa na umaana mdogo kwetu, na vifungo vya urakifi vinakuwa vyenye nguvu. Kwa kujuana vizuri, tunakuwa katika hali nzuri inayotuwezesha kujengana na kufarijiana. (1 Thes. 5:11) Tunaweza kuwa ‘msaada wenye kutia moyo’ kwa mmoja na mwenzake ili kupinga uvutano wa ulimwengu wa Shetani unaodhuru kiadili. (Kol. 4:11) Kwa kuwa kuna mikazo hii ya siku za mwisho, sisi ni wenye shukrani kama nini kwa kuwa na marafiki wema kati ya watu wa Yehova!—Met. 18:24.
3 Marafiki wa karibu sana wanaweza kuwa chanzo cha pekee cha nguvu na faraja tunapopambana na majaribu makali. (Met. 17:17) Mkristo mmoja aliyepiganisha hisia za kujiona kwamba hafai kitu anakumbuka hivi: “Walikuwa marafiki ambao walisema nami kuhusu mambo yenye kutia moyo ili kunisaidia kushinda tatizo la mawazo yasiyofaa niliyokuwa nayo.” Marafiki kama hao ni zawadi kutoka kwa Yehova—Met. 27:9.
4 Onyesha Kupendezwa na Wengine: Tunawezaje kupanuka katika upendo wetu mwororo kwa waamini wenzetu? Zaidi ya kusalimia wengine kwenye mikutano ya Kikristo, fanya jitihada ya kushiriki nao katika mazungumzo yenye maana. Bila kuingilia mambo yao ya kibinafsi, onyesha kuwa unapendezwa nao kibinafsi. (Flp. 2:4; 1 Pet. 4:15) Njia nyingine ya kuonyesha kupendezwa na wengine ni kwa kuwaalika kwenye mlo. (Luka 14:12-14) Au unaweza kupanga kutumika pamoja nao katika huduma ya shambani. (Luka 10:1) Tunapochukua hatua ya kwanza ili kujua ndugu zetu vizuri, tunasitawisha umoja katika kutaniko.—Kol. 3:14.
5 Je, tunaelekea kuchagua marafiki zetu wa karibu kati ya wale tu wa umri wetu au wale wanaopendezwa na mambo tunayopendezwa nayo? Hatupaswi kuacha mambo kama hayo kuwa kizuizi cha urafiki tunaokuza katika kutaniko. Daudi na Yonathani vilevile Ruthu na Naomi walisitawisha urafiki wa nguvu ingawa tofauti zao za miaka na malezi. (Rut. 4:15; 1 Sam. 18:1) Je, unaweza kupanua urafiki wako? Kufanya hivyo kunaweza kukuletea baraka zisizotazamiwa.
6 Kwa kupanuka katika upendo wetu mwororo kwa wengine, tunatiana nguvu na kuendeleza amani katika kutaniko. Zaidi ya hiyo, Yehova anatubariki kwa sababu ya upendo tunaoonyesha ndugu zetu. (Zab. 41:1, 2; Ebr. 6:10) Kwa nini usijiwekee mradi wa kupata kufahamiana vizuri na ndugu wengi iwezekanavyo?
[Maulizo ya Funzo]
1. Kila mmoja wetu analo daraka gani?
2. Kwa nini ni jambo la lazima kukuza urafiki na waamini wenzetu?
3. Tunawezaje kuwa msaada wenye kutia moyo kwa wengine?
4. Tunawezaje kujua wengine vizuri katika kutaniko?
5. Taja njia moja ya kupanua urafiki wetu?
6. Kupanuka katika upendo wetu mwororo kwa ndugu zetu kunaleta faida gani?