Onyesha Roho ya Upainia
1 Wahubiri wote wa Ufalme, iwe wanaweza kupainia sasa au hapana, wanaweza kuonyesha roho ya upainia. Wote wanahangaikia kweli amri ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 18:5) Wanashughulikia watu na wanajinyima ili kutimiza huduma yao. (Mt. 9:36; Mdo. 20:24) Watumishi wa Yehova wako tayari kufanya yote inayohitajiwa ili kusaidia wengine wajifunze kweli. (1 Kor. 9:19-23) Acheni tuchunguze mfano wa yule aliyeonyesha roho hiyo, mweneza-evanjeli Filipo.
2 Kuhubiri na Kufundisha: Filipo alikuwa na madaraka mazito katika kutaniko la karne ya kwanza. (Mdo. 6:1-6) Hata hivyo, yeye alikuwa kwanza mhubiri mwenye bidii wa habari njema. (Mdo. 8:40) Leo pia, wanaposhughulikia migawo waliyopewa, wazee na watumishi wa huduma wanaweza kuonyesha roho ya upainia kwa kutoa mwongozo wenye shauku katika huduma ya shambani. Hilo linachochea sana roho ya upainia katika kutaniko.—Rom. 12:11.
3 Baada ya kifo cha Stefano, wimbi la upinzani lilitokeza misukosuko sana katika maisha za wanafunzi. Hata hivyo, Filipo aliendelea kuhubiri, na alitimiza sehemu ya maana katika kuanzisha kazi kati ya Wasamaria. (Mdo. 8:1, 4-6, 12, 14-17) Tunaweza kuiga mfano wake kwa kuendelea kujulisha habari njema tunapokuwa chini ya majaribu na kwa kuhubiri bila ubaguzi wale wote tunaokutana nao.—Yoh. 4:9.
4 Ufundi wa Filipo akiwa mwalimu wa Neno la Mungu unaweza kuonekana katika simulizi kuhusu kugeuka kwa towashi Mwethiopia. (Mdo. 8:26-38) Kusitawisha uwezo wa kutumia Biblia na ‘kujadiliana kwa kutumia Maandiko’ ni njia nyingine pia ambayo katika hiyo tunaonyesha roho ya upainia. (Mdo. 17:2, 3) Kama Filipo, tunajaribu kuhubiri habari njema mahali pote watu wanapoweza kupatikana na kutumia kila nafasi inayojitokeza.
5 Familia na Kutaniko: Bila shaka mtazamo wa akili na mfano wa Filipo vilikuwa na uvutano mzuri kwa binti zake. (Mdo. 21:9) Pia, wazazi Wakristo wanaofanya maisha yao yategemee faida za Ufalme wanatia watoto wao moyo kufanya hivyohivyo. Ijapokuwa anaweza kuwa mwenye kuchoka mwishoni mwa juma, kwa sababu ya shughuli nyingi, mzazi anayehubiria wengine kwa shauku anaweza kuacha maoni yenye kudumu katika moyo wa mtoto.—Met. 22:6.
6 Filipo aliwakaribisha Paulo na Luka, Wakristo wenye bidii waliokuwa wakitumika kwa nguvu katika utumishi wa Yehova. (Mdo. 21:8, 10) Tunawezaje kuonyesha shukrani yetu na kutegemeza wale walio na bidii leo? Labda tunaweza kuwaomba mapainia tutumike pamoja nao asubuhi au kisha mchana-kati fulani siku ambayo watu wachache wanashiriki katika huduma ya shambani. (Flp. 2:4) Tunaweza pia kuwaalika nyumbani kwetu kwa ajili ya ushirika wenye kujenga. Ijapokuwa hali zetu ziwe namna gani, sisi sote na tujitahidi kuonyesha roho ya upainia.
[Maulizo ya Funzo]
1. Roho ya upainia ni nini?
2. Wazee na watumishi wa huduma wanawezaje kuiga bidii ya Filipo kuhusu huduma ya shambani?
3. Tunawezaje kuonyesha roho ya upainia tunapopambana na majaribu?
4. Ni mfano gani ambao Filipo alituachia akiwa mwalimu?
5. Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazazi Wakristo waingize roho ya upainia katika mioyo ya watoto wao?
6. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini mapainia katika kutaniko letu?