Saidia Mwanafunzi Wako wa Biblia Apendezwe na Sifa za Yehova za Pekee
1 Katika kazi yetu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, tunafanya mengi zaidi ya kufundisha tu wengine kweli za Biblia za msingi. Tunasaidia watu wajue kwamba Yehova ni mtu na wapendezwe na sifa zake za pekee. Watu wenye moyo mnyoofu wanapojifunza kweli kumhusu Mungu, kweli hiyo inawagusa sana, na inawachochea wafanye mabadiliko katika maisha zao ‘ili watembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili.”—Kol. 1:9, 10; 3:9, 10.
2 Kitabu Chetu Kipya cha Funzo: Kitabu Biblia Inafundisha kinazungumzia sifa za Yehova kuanzia mwanzo. Sura ya kwanza inajibu maulizo yafuatayo: Je, kweli Mungu anakujali?, Mungu ana utu wa aina gani?, na Je, tunaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu? Sura hiyo pia inazungumzia utakatifu wa Yehova (fu. 10), haki na huruma yake (fu. 11), upendo wake (fu. 13), uwezo wake (fu. 16), rehema, neema, tayari kusamehe, uvumilivu, na ushikamanifu (fu. 19). Fungu la 20 linatoa wazo lifuatalo: “Unapozidi kujifunza kumhusu Yehova, atakuwa halisi zaidi kwako nawe utampenda na kumkaribia zaidi.”
3 Tunawezaje kutumia kitabu Biblia Inafundisha ili kusaidia wanafunzi wa Biblia wamkaribie Yehova? Kisha kuchunguza fungu fulani linalokazia sifa moja ya Yehova, tunaweza kuuliza mwanafunzi hivi: “Habari hii inakufundisha kwamba Yehova ni mtu wa namna gani?” au “Namna gani jambo hili linaonyesha kwamba Mungu anapendezwa nawe kipekee?” Kwa kutumia mara kwa mara maulizo kama hayo wakati wa funzo, tunafundisha wanafunzi wetu kufikiri sana juu ya mambo wanayojifunza na kuwasaidia waendelee kupendezwa na sifa za Yehova za pekee.
4 Tumia Kisanduku cha Kujikumbusha: Kwenye mwisho wa kila sura, omba mwanafunzi atoe maelezo kwa maneno yake mwenyewe juu ya kila jambo linalopatikana katika kisanduku “Mambo Ambayo Biblia Inafundisha.” Msaidie afikirie maandiko yanayotajwa. Ili kumtia mwanafunzi moyo aseme mambo yaliyo katika moyo wake, unaweza kumwuliza hivi nyakati nyingine: “Unaonaje yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu jambo hili?” Kwa kufanya hivyo, utakazia mambo makuu ya sura na kutambua waziwazi yale ambayo mwanafunzi anaamini kabisa. Hilo litasaidia mwanafunzi aanze kukomaza urafiki wa karibu na Yehova.