“Mfuateni Kristo!”—Mkusanyiko wa Wilaya wa Mashahidi wa Yehova wa 2007
1 Musa aliamuru Waisraeli wote na wakaaji wageni wakusanyike pamoja kila miaka 7 ili wasomewe Sheria. Kwa kusudi gani? “Ili wasikilize na ili wajifunze.” (Kum. 31:10-12) Yehova aliona kwamba ni lazima kukusanya watu wake katika vikundi vikubwa. Karibuni Mashahidi wa Yehova watakusanyika tena kwa ajili ya Mikusanyiko ya Wilaya ya siku tatu yenye kichwa “Mfuateni Kristo!”
2 Je, umeanza kujitayarisha? Je, una lazima ya kuomba bwana wako wa kazi mapumziko? Je, unaweza kusaidia wanafunzi wako wa Biblia au washiriki wa familia wasioamini ili wahuzurie mkusanyiko pamoja nawe? Je, kuna wengine katika kutaniko ambao wanahitaji msaada ili kuhuzuria? Je, unafanya mipango ili kuhuzuria mkusanyiko mahali pengine? Je, utahitaji kupangishwa? Habari zenye kufuata zitakusaidia ili kujitayarisha.
3 Huzuria Siku Zote Tatu: Yehova anatolea watu wake chakula kingi cha kiroho. (Isa. 25:6) Hilo linahusu pia karamu ya kiroho inayotolewa kwenye mikusanyiko yetu ya kila mwaka. Imeonekana kwamba watu wanaohuzuria mkusanyiko Siku ya Tano ni wachache sana kwa kulinganisha na wale wanaohuzuria siku zingine. Jiwekee mradi wa kuhuzuria siku zote tatu za mkusanyiko wenye kutia nguvu ambao tengenezo la Yehova limetayarisha kwa ajili yetu! Ikiwa una lazima ya kuomba bwana wako wa kazi mapumziko, sali kuhusu jambo hilo. Kisha hapo ‘jipe ujasiri’ wa kuongea na bwana wako wa kazi wakati tarehe ya mkusanyiko wenu inapotangazwa. (1 The. 2:2; Neh. 2:4, 5) Inaweza kuwa vizuri kumfasiria kwamba mkusanyiko huo unaofanyika kila mwaka ni sehemu ya ibada yako. Kufanya hivyo mbele ya wakati kutafanya iwe rahisi kwa bwana wako wa kazi kufanya marekebisho kwenye kazi kupatana na ombi lako.
4 Kutayarisha Wanafunzi Wako wa Biblia na Washiriki wa Jamaa: Ni jambo lenye kufurahisha sana kuhuzuria mkusanyiko pamoja na wanafunzi wako wa Biblia, wakijionea wenyewe uchangamfu wa undugu wetu wa Kikristo katika “kutaniko kubwa”! (Zab. 22:25) Uwajulishe vizuri mbele ya wakati ili waweze kupangia wakati wa kuhuzuria. Uwaelezee sababu zinazokufanya wewe mwenyewe ufurahie kuhuzuria mikusanyiko. Unaweza kutayarisha wanafunzi kuhusu mambo watakayoona kwa kuwaonyesha video zetu zilizo na habari na picha za mikusanyiko ya miaka iliyopita, hasa zaidi video Unis grâce à l’enseignement divin. Julisha pia washiriki wa jamaa wasioamini mipango yako. Labda wanaweza kufanya mipango ili waje kuona drama au kuhuzuria mkusanyiko pamoja nawe hata siku moja.
5 Kusaidia Ndugu na Dada Zako: Mtume Paulo alishauria Wakristo ambao walikuwa na mali “wafanye mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki.” (1 Tim. 6:17, 18) Tunaweza kuonyesha roho ya ukarimu (utoaji) ambayo Paulo alikuwa nayo ikiwa tunafikiria hali ya wazee na walemavu, wale walio katika utumishi wa wakati wote, familia zenye mzazi mmoja na labda wengine katika kutaniko ambao wanaweza kuhitaji msaada ili kuhuzuria mkusanyiko. Kutimiza mahitaji ya watu kama hao ni daraka la ndugu katika imani, lakini wazee na wengine wanaweza kuonyesha utambuzi na kutoa msaada wenye upendo inapohitajiwa.—Gal. 6:10; 1 Tim. 5:4.
6 Kuhuzuria Mkusanyiko Mahali Pengine: Ili kuhakikisha kwamba kuna viti, vitabu, vyumba vya kupanga vya kutosha na mambo mengine, unatiwa moyo kuhuzuria mkusanyiko wa mahali ambapo kutaniko lenu limealikwa. Hata hivyo, ikiwa hali zako hazikuruhusu kuhuzuria mkusanyiko wa mahali ambapo kutaniko lenu limealikwa, basi, uko huru kuhuzuria mkusanyiko wa mahali pengine.
7 Upangishaji: Upangishaji katika mji wa mkusanyiko unafanywa kwa kawaida katika nyumba za ndugu, katika Majumba ya Ufalme au katika nyumba za washiriki wa jamaa. Karatasi yenye kuonyesha mahali pote ambapo mkusanyiko utafanywa, itawekwa kwenye ubao wa matangazo wa kutaniko kisha kuchunguza nyongeza hii kwenye Mkutano wa Utumishi. Inapendekezwa kwamba wote wafikirie katika sala mahali ambapo watahuzuria mkusanyiko katika mwaka wa 2007.
8 Ikiwa ungependa kupangishwa katika nyumba ya ndugu au katika Jumba la Ufalme, tunapendekeza kwamba mwandishi aandike mbele ya wakati majina ya wahubiri wote wanaotaka kupangishwa na kuituma kwenye Idara ya Upangishaji ya mkusanyiko. Kwenye karatasi hiyo, anapaswa kuandika jina, ikiwa mtu ni mwanamume au mwanamuke, umri na uhusiano wa kifamilia wa kila mhubiri. Hilo litasaidia ndugu wanaohusika na Idara ya Upangishaji wawe na wakati wa kutosha ili kupata mahali pa kupangisha wote. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inapaswa kuchunguza sifa za kila mhubiri mbele ya kutuma maombi hayo kwenye Idara ya Upangishaji. Tukiisha kupewa mahali pa kupanga, halitakuwa jambo lenye kufaa kufanya mipango yetu wenyewe baadaye ili kwenda kukaa pamoja na ndugu au rafiki mwingine. Jambo hilo linaweza kuvuruga kazi ya ndugu wanaoshugulika na Idara ya Upangishaji. Hata hivyo, ikiwa yeyote anakusudia kukaa pamoja na mshiriki wa jamaa asiye ndugu wa kiroho muda wa mkusanyiko, hapaswi kuomba mwandishi atie jina lake kwenye karatasi ya wenye kuomba kupangishwa.
9 Tunawatolea maagizo fulani hapa kuhusu namna ya kushugulikia upangishaji katika Jumba la Ufalme. Halmashauri ya Mkusanyiko wa Wilaya itampatia mzee fulani mgawo ili asimamie mpango huo. Atakuwa na msaidizi, kwa kawaida mzee mwingine au mtumishi wa huduma mwenye kustahili, aliye na sifa za kiroho. Jumba linapaswa kugawanywa katika sehemu mbili: sehemu moja kwa ajili ya dada na watoto wao, na pia mabinti na sehemu nyingine kwa ajili ya ndugu na washiriki wengine wa kiume. Jumba la Ufalme litatumiwa kwa kulala tu. Wote wanapokuwa mahali pa mkusanyiko mchana, kazi ya ulinzi itapangwa kwa kugomboana ili kuzuia vitu vya ndugu visiibwe. Ndugu wenye kujiheshimu, wenye sifa za kiroho ndio wanaopaswa kutumiwa ili kufanya kazi ya ulinzi. Haitaruhusiwa kupikia chakula ndani ya Jumba la Ufalme. Kibanda cha muda kinaweza kujengwa katika uwanja, ili kitumiwe kuwa mahali pa kupikia muda wa mkusanyiko tu. Mwishoni mwa mkusanyiko, kibanda hicho kitabomolewa. Ni jambo la maana kwamba Jumba la Ufalme na vilevile uwanja, vilindwe katika hali ya usafi na utaratibu. Inafaa kuwa waangalifu ili kitu chochote kisiharibiwe. Wale wanaokaa katika Jumba la Ufalme watafanya yote wawezayo ili waonyeshe mwenendo unaostahili Wakristo wa kweli, kati yao wenyewe na vilevile kuelekea majirani.—1 Kor. 10:31.
10 Unga Mkono Mipango Inayochukuliwa: Tunapofika mahali pa mkusanyiko, ni wazi kwamba kazi nyingi imefanywa ili kutayarisha kuja kwetu. Ndugu wenye upendo wanaotumika kama wakaribishaji wanatusalimu, wanatutolea programu na kutusaidia kupata viti. Ndugu na dada wamesafisha mahali pa mkusanyiko na kutengeneza jukwaa nzuri. Kazi ya maana ambayo hatuoni namna imefanywa, imetimizwa pia ili kutayarisha sehemu mbalimbali za programu, upangishaji na mambo mengi madogo madogo.
11 Watu wengi wamekuwa wakitumika kwa miezi mingi kwa ajili ya kila mkusanyiko ili kufanya mipango inayoombwa, na washiriki wa familia zao wemechangia pia katika kazi hizo kwa kukubali kwamba wakati wao ambao washiriki hao wa familia wangepitisha pamoja nao utolewe kwa mambo hayo ya maana. Je, hatusamini kazi hizo za kujinyima ambazo zimefanywa kwa faida yetu? Tunaweza kuonyesha shukrani kwa kutii maagizo yaliyo katika habari hii na mwongozo mwingine wowote ambao tunaweza kutolewa mbele ya mkusanyiko wetu. (Ebr. 13:17) Nia ya kila mtu ya kutumika kwa kuungana mkono inawezesha mambo yote “yatendeke kwa adabu na kwa mpango.”—1 Kor. 14:40.
12 Mikusanyiko ya watu wa Mungu ndilo jambo la maana zaidi kwa kadiri ‘tunavyoona siku ile kuwa inakaribia.’ (Ebr. 10:25) Kwenye mikusanyiko yetu ya Kikristo, jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara inatutolea habari za kutusaidia “kuwa waangalifu kuyatimiza maneno yote” ambayo Yehova anataka tufuate. (Kum. 31:12) Anza kufanya mipango sasa ili kuhuzuria siku zote tatu za Mkusanyiko wa Wilaya wenye kichwa “Mfuateni Kristo!” na hivyo ufaidike kutokana na mafundisho ya kiroho na ushirika wenye kufurahisha!
[Maulizo ya Funzo]
1, 2. (a) Namna gani Musa alitia moyo Waisraeli wafaidike kutokana na kukusanyika pamoja? (b) Ni matayarisho gani ambayo tunaombwa kufanya tangu sasa?
3. (a) Namna gani andiko la Isaya 25:6 linatimizwa leo? (b) Ni jambo gani ambalo limeonwa kuhusu huzurio la mkusanyiko la Siku ya Tano, na kila mmoja wetu anapaswa kufanya nini?
4. Namna gani tunaweza kutayarisha wanafunzi wetu wa Biblia na washiriki wa jamaa wasioamini kwa ajili ya mkusanyiko?
5. Namna gani tunaweza kuonyesha roho ya ukarimu (utoaji) inayozungumziwa kwenye 1 Timotheo 6:18?
6. Kwa nini tunapaswa kuhuzuria mkusanyiko wa mahali ambapo kutaniko letu limealikwa?
7-9. (a) Ni mambo gani ya maana tunayopaswa kuchunga akilini tunapohitaji kupangishwa, na kwa nini? (b) Ni mipango ya aina gani inayopaswa kuchukuliwa ikiwa ndugu na dada wanapangishwa katika Jumba la Ufalme? (c) Ni mambo gani fulani unayopaswa kufikiria unapopanga kuhuzuria mkusanyiko wa wilaya? (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 4.)
10, 11. (a) Ni matayarisho gani ambayo yamefanywa kwa ajili yetu mbele ya sisi kufika kwenye mahali pa mkusanyiko? (b) Namna gani tunaweza kuonyesha usamini na shukrani kwa ajili ya kazi yote iliyofanywa kwa ajili yetu? (Soma Waebrania 13:17.)
12. (a) Kwa nini mikusanyiko ya watu wa Yehova ni jambo la maana sana katika wakati wetu? (b) Kila mmoja wetu anaweza kufanya nini sasa?
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Saa za Programu
――
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Siku ya Tano na Siku ya Posho
3:20 asubuhi - 11:05 kisha mchana-kati
Siku ya Yenga
3:20 asubuhi - 10:10 kisha mchana-kati
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 4]
Mambo Fulani ya Kufikiria Unapotazamia Kuhuzuria Mkusanyiko wa Wilaya
1. Ikiwa unaombwa kufanya safari ndefu ili kuhuzuria mkusanyiko, hivyo basi anza kuchunga feza mapema zaidi iwezekanavyo ili uhakikishe kwamba utapata feza za kutosha za usafirishaji na chakula kwa ajili yako mwenyewe na familia yako.
2. Fikiria pia kutegemeza mipango ya mkusanyiko kupitia zawadi zako za kujipendea. ‘Mtu yeyote asionekane mbele za Yehova mikono mitupu,’ lakini ‘Mheshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye samani’—Kum. 16:16; Met. 3:9.
3. Wakati wa mkusanyiko, tunatukuza jina la Yehova kupitia mwenendo wetu mzuri, na mavazi yetu safi na yenye heshima.—1 Kor. 10:31.
4. Kusudia kuunga mkono ndugu wanaokaribisha watu na ndugu wengine wenye kuwa na daraka la kulinda utaratibu. Usichungie watu viti, isipokuwa washiriki wa karibu wa familia yako na wale wanaosafiri pamoja nawe.
5. Ili ufaidike kabisa na kipindi cha kisha mchana-kati, tumia tu chakula chepesi mwishoni mwa kipindi cha asubuhi. Chakula kizito kinaweza kuleta usingizi.—Luka 8:18.
6. Usafi unamletea Yehova heshima. Mwishoni mwa kila kipindi, kila mmoja wetu anaweza kutimiza daraka lake ili kuacha mahali pa mkusanyiko pakiwa safi kwa kuokota vikaratasi na takataka nyingine na kuzitupa katika mapipa ya kutupia takataka yaliyotayarishwa kwa kusudi hilo.—1 Pet. 1:15, 16.