Kuhubiria Watu kwa Njia ya Telefone Kunaweza Kuwa na Matokeo Mazuri
1. Kwa nini kuhubiria watu kwa njia ya telefone kunapaswa kuonwa kuwa sehemu ya maana ya kazi yetu ya kuhubiri?
1 Kwa nini tufikirie kuhubiria watu kwa njia ya telefone? Kwa kuwa hiyo ni njia nyingine ya kusaidia watu wapate ujuzi sahihi ili waokolewe. (2 Pet. 3:9) Hata ikiwa kuhubiri nyumba kwa nyumba ndio njia ya kwanza tunayotumia ili kutangazia watu habari njema ya Ufalme wa Mungu, tuko tayari kutumia njia zingine ili kuwahubiria wale ambao ni vigumu kuwakuta nyumbani.—Mt. 24:14; Luka 10:1-7; Ufu. 14:6.
2. Mahubiri kwa njia ya telefone yanapangwa jinsi gani?
2 Jinsi Mahubiri kwa Njia ya Telefone Yanavyopangwa: Kama tunavyofanya tunapohubiri nyumba kwa nyumba, wahubiri wanapaswa pia kutolewa eneo ambamo watahubiria watu kwa njia ya telefone. Mahubiri hayo yanaweza kufanywa na mutu mmoja ao labda kikundi kidogo cha watu wawili ao watatu. Ni vizuri kuwa mahali penye ukimya ambapo hapana mambo ya kukengeusha. Wengi wanaona kwamba ni vizuri kukaa kwenye kiti na kuweka mezani vitabu ambavyo wanatumia wanapohubiri nyumba kwa nyumba.
3. Tunapaswa kukumbuka nini tunapohubiria watu kwa njia ya telefone?
3 Jinsi ya Kuhubiria Watu kwa Njia ya Telefone: Tunapohubiria watu kwa njia ya telefone, tunapaswa kuzungumza kwa njia ya maongezi. Wanapoanza kuhubiria watu kwa njia ya telefone, wahubiri fulani wanasomea wasikilizaji wao habari iliyo katika kitabu lakini wanafanya hivyo kwa njia ya maongezi. Maneno ya kuanzisha mazungumzo yanayopatikana katika kitabu Kutoa Sababu, Huduma Yetu ya Ufalme, na takti Je, Ungependa Kujua Kweli? yanaweza kusaidia. Unapotayarisha utoaji wako mwenyewe, fikiria habari ya kutolea msikilizaji wako, fikiria ulizo unaloweza kumwuliza kuhusu habari hiyo, na uwe tayari kumsomea maandiko machache yanayojibu ulizo hilo. Kwa kawaida ni vizuri kuzungumzia pia vitabu tunavyotolea watu katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba mwezi huo. Fikiria mambo yafuatayo: Uwe mwenye kutulia na usizungumze harakaharaka. Uwe mwenye adabu na mvumilivu, na uzungumze kwa njia ya urafiki, kwa kuwa msikilizaji wako anaweza kutambua sifa hizo kupitia telefone. Umsikilize msikilizaji wako anapotoa maoni yake, na kisha umshukuru kwa maelezo yake. Uwe mwangalifu ili usimwelezee kuhusu michango, kwa kuwa anaweza kufikiri kwamba hiyo ni namna ya kuombaomba feza kwa njia ya telefone.
4. Kuhubiria watu kwa njia ya telefone kunaweza kutuwezesha tufanye nini katika eneo tulilogawiwa?
4 Mutu tunayezungumza naye kwa njia ya telefone anaweza kuwa mgonjwa asiyeweza kutoka kitandani ao mutu ambaye programu yake ya kazi inafanya iwe vigumu kukutana naye tunapohubiri nyumba kwa nyumba. Kuna watu wengine wanaoishi katika majengo ao maeneo yenye kulindwa sana ambamo watu hawaingie bila ruhusa ya wakaaji. Kwa hiyo, tunapojikaza kutimiza kwa ukamili kazi yetu ya kuhubiri, tufikirie kuhubiria watu kwa njia ya telefone kwa kuwa njia hiyo ina matokeo mazuri.