Tutoe “Nafsi Zetu” kwa Ajili ya Wanafunzi Wetu
1. Ni nini kinachohitajiwa ili kumsaida mwanafunzi wa Biblia?
1 Ili kumsaidia mwanafunzi wa Biblia afikie kujiweka wakfu, mambo mengi yanahitajiwa zaidi ya kujifunza tu naye Biblia kwa ukawaida. Mtume Paulo alionyesha kwamba uhusiano aliokuwa nao pamoja na wale aliofundisha unalingana na ule wa mama mwenye kunyonyesha anayewatunza kwa upendo watoto wake. Sisi pia tunapendezwa kutoa “nafsi zetu wenyewe” ili kusaidia wanafunzi wetu wakomae kiroho.—1 The. 2:7-9.
2. Kwa nini tupendezwe na mwanafunzi wetu wa Biblia, na namna gani tunaweza kufanya hivyo?
2 Tupendezwe Nao: Mwanafunzi wa Biblia anapotumia mambo anayojifunza, zamiri yake itamchochea aache kufanya urafiki wa karibu na wale wasiotii kanuni za Biblia. (1 Pet. 4:4) Watu wa familia yake wanaweza kumkataa. (Mt. 10:34-36) Tunapopendezwa naye, tunaweza kumsaidia ajisikie kwamba kuna watu wanaompenda. Ndugu mmoja mishonari mwenye kuzoea kazi ya kuhubiri anapendekeza hivi: “Usiondoke haraka baada ya kujifunza na mutu. Ikiwa inafaa, ubaki na uzungumze na mwanafunzi kwa muda kidogo.” Uwe tayari kumtolea mwanafunzi msaada anaohitaji. Kwa mfano, unaweza kuzungumza naye kwa njia ya telefone ao kumtembelea ikiwa anagonjwa. Unaweza kukaa karibu naye kwenye mikutano na kumsaidia kuchunga watoto, ikiwa inafaa.
3. Namna gani tunaweza kumsaidia mwanafunzi wetu apate kutiwa moyo na ndugu na dada wa kutaniko?
3 Msaada wa Kutaniko: Ikiwa tunahubiri karibu na makao ya mwanafunzi wetu wa Biblia, kwa nini tusipite kwake na kumjulisha kwa wahubiri wenzetu? Inapofaa, omba wahubiri wengine, kutia ndani wazee, wakusindikize mara kwa mara unapoenda kuongoza funzo. Pia, baada tu ya kuanzisha funzo, umtie moyo mwanafunzi wako wa Biblia ahuzurie mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Hilo litamtolea nafasi ya kuwa na uhusiano wenye kujenga pamoja na ndugu na dada wa kutaniko, ambao wanaweza kuwa familia yake ya kiroho.—Marko 10:29, 30; Ebr. 10:24, 25.
4. Bidii yetu inaweza kuwa na matokeo gani?
4 Mzazi anayesaidia watoto wake kiroho bila kuchoka anapata furaha nyingi wanapoamua kumtumikia Yehova na kutembea katika kweli. (3 Yoh. 4) Tunaweza kupata furaha ya namna hiyo tunapotoa nafsi zetu ili kusaidia wanafunzi wa Biblia.