Tuige Mufano wa Manabii—Yona
1. Yona alionyesha sifa gani nzuri?
1 Unapofikiria nabii Yona, unawaza alikuwa mutu wa namna gani? Watu fulani wanaweza kuwaza alikuwa mwoga ao mwenye moyo mugumu. Hata hivyo, ni wazi kwamba alionyesha unyenyekevu, ujasiri, na roho ya kujitoa. Namna gani tunaweza kuiga sifa zake nzuri?—Yak. 5:10.
2. Namna gani tunaweza kuiga unyenyekevu wa Yona?
2 Unyenyekevu: Mwanzoni, Yona alikimbia mugawo wake na akaenda mahali pengine. Hilo halishangaze kwa sababu watu wa Ashuru walikuwa wenye jeuri sana, na Ninawi lilifikia kuitwa ‘jiji la umwangaji wa damu.’ (Nah. 3:1-3) Yehova alimurekebisha, na kwa unyenyekevu Yona alikubali kuenda katika mugawo wake. (Met. 24:32; Yona 3:1-3) Ijapokuwa alikimbia mugawo wake, mwishowe alifanya mapenzi ya Yehova. (Mt. 21:28-31) Je, sisi pia tunaazimia kuhubiri habari njema, hata ikiwa tunarekebishwa ao tuna eneo ngumu?
3. Sababu gani tunahitaji ujasiri na roho ya kujitoa katika mahubiri?
3 Ujasiri na Roho ya Kujitoa: Yona alipotambua kwamba uamuzi wake mubaya unahatarisha uzima wa wale aliosafiri nao katika mashua, alikuwa tayari kutoa uzima wake. (Yona 1:3, 4, 12) Baadaye, alipokuwa akitimiza mugawo wake huko Ninawi, aliingia ndani zaidi ya jiji hilo, labda akitafuta mahali panapofaa ili kutangaza hukumu ya Yehova. Matendo hayo hayakuwa ya mwoga, lakini ya nabii wa Mungu mwenye ujasiri! (Yona 3:3, 4) Namna gani sisi leo? Tunahitaji ujasiri unaotoka kwa Mungu ili kuhubiri kwa bidii ijapokuwa upinzani. (Mdo 4:29, 31) Ni lazima tuwe na roho ya kujitoa ili kutumia wakati na mali yetu katika mahubiri.—Mdo 20:24.
4. Sababu gani tunapaswa kuchukua wakati ili kufikiri juu ya mufano ambao manabii wa Yehova walituachia?
4 Kila mara unaposoma habari kuhusu nabii wa Yehova, utafaidika ikiwa unajitia pa nafasi yake. Ujiulize: ‘Ingekuwa mimi ningefanya nini? Namna gani ninaweza kuiga sifa zake nzuri katika maisha yangu?’ (Ebr. 6:11, 12) Wakati unaokuja, Huduma Yetu ya Ufalme itakuwa na habari zitakazozungumuzia mambo yenye kufaa tunayoweza kujifunza kutokana na manabii wengine waaminifu wa Yehova.