HABARI YA KUJIFUNZA YA 27
Juu ya Nini Tunapaswa Kumuogopa Yehova?
“Urafiki wa karibu pamoja na Yehova ni wa wale wenye kumuogopa.”—ZB. 25:14.
WIMBO 8 Yehova Ni Kimbilio Yangu
KIFUPI YA HABARIa
1-2. Kulingana Zaburi 25:14, tunapaswa kufanya nini kama tunapenda kuwa na urafiki wa karibu pamoya na Yehova?
UNAWAZA ni sifa gani zenye zinaweza kukusaidia kama unapenda kuendelea kuwa na urafiki wa karibu pamoya na mutu fulani? Pengine utajibia kama marafiki wa karibu wanapaswa kupendana na kutegemezana. Pengine unaweza kuwaza kama woga haiko sifa ya maana yenye inaweza kufanya watu wakuwe na urafiki wa karibu. Lakini, sawa vile andiko ya musingi ya hii habari inasema, wale wenye wanapenda kuwa na urafiki wa karibu pamoya na Yehova wanapaswa “kumuogopa.”—Soma Zaburi 25:14.
2 Hata kama tulishamutumikia Yehova kwa miaka ngapi, siye wote tunapaswa kuendelea kumuogopa mu njia yenye kufaa. Lakini, kumuogopa Yehova kunamaanisha nini? Namna gani tunaweza kujifunza kumuogopa Yehova? Mufano wa musimamizi-nyumba Obadia, Kuhani Mukubwa Yehoyada, na Mufalme Yehoashi, unaweza kutufundisha nini kuhusu kumuogopa Mungu?
KUMUOGOPA YEHOVA KUNAMAANISHA NINI?
3. Fasiria namna woga unaweza kutulinda.
3 Tunaweza kuwa na woga kama tunajua kuwa jambo fulani inaweza kutuumiza. Woga wa vile ni wenye kufaa juu unaweza kutusaidia tukamate maamuzi ya muzuri. Kuogopa kuanguka kutatuzuia tusitembee karibu sana na mwisho wa muteremuko wa maji. Kuogopa kujiumiza kunaweza kufanya tuepuke kujiingiza mu hali zenye kuwa hatari. Kuogopa kuharibisha urafiki wetu pamoya na mutu mwenye tunapenda kutatufanya tuepuke kusema ao kufanya jambo fulani ya mubaya kumuhusu.
4. Shetani anapenda tumuogope Yehova mu njia gani?
4 Shetani anapenda tumuogope Yehova mu njia yenye haifae. Anapenda tukuwe na mawazo sawa ya Elifazi, ni kusema, anapenda tuamini kama Yehova ni Mungu mwenye kulipiza kisasi, mwenye anakuwaka na hasira, na kama haiwezekani mutu amufurahishe. (Yob. 4:18, 19) Shetani anapenda tumuogope Yehova mu njia yenye haifae juu tuache kumutumikia. Ili tuepuke ule mutego, tunapaswa kumuogopa Yehova mu njia yenye kufaa.
5. Kumuogopa Mungu kunamaanisha nini?
5 Mutu mwenye anamuogopa Mungu mu njia yenye kufaa anamupendaka na hafanyake jambo yoyote yenye inaweza kuharibisha urafiki wake pamoya naye. Yesu “alimuogopa Mungu” mu ile njia. (Ebr. 5:7) Hakumuogopa mu njia yenye haifae. (Isa. 11: 2, 3) Lakini, alimupenda sana na alipenda kumutii. (Yoh. 14:21, 31) Sawa vile Yesu, tunamuheshimiaka sana Yehova ao kumutii juu iko na upendo, hekima, haki, na nguvu. Tunajua pia kama Yehova anatupendaka sana na kama anahangaikiaka namna tunatenda wakati anatupatia muongozo. Tunaweza kuhuzunisha ao kufurahisha moyo wake.—Zb. 78:41; Mez. 27:11.
TUJIFUNZE KUMUOGOPA MUNGU
6. Ni njia gani moya yenye inaweza kutusaidia kujifunza kumuogopa Mungu? (Zaburi 34:11)
6 Mutu hazaliwake na tayari iko namuogopa Yehova. Inaomba ajifunze. (Soma Zaburi 34:11.) Njia moya yenye inaweza kutusaidia kufanya vile ni kuchunguza uumbaji. Wakati tunaona namna “vitu vyenye vilifanywa” vinaonyesha vile Yehova iko na hekima, nguvu, na namna anatupenda sana, ile itafanya tumuheshimie na kumupenda zaidi. (Ro. 1:20) Dada Adrienne anasema hivi: “Wakati naangaliaka kila kitu yenye Yehova aliumba na kuona namna iko na hekima, inanishangazaka sana na inanisaidiaka kuona kama anajua mambo yenye kuwa ya muzuri sana kwangu.” Juu kila mara alifikiri sana juu ya ile, anasema hivi: “Sipendake kufanya jambo yoyote yenye inaweza kuharibisha urafiki wangu pamoya na Yehova mwenye alinipatia uzima.” Unawaza nini kama hii juma unapitisha wakati fulani ili kufikiri sana juu ya kitu fulani yenye Yehova aliumba? Kama unafanya vile, utamuheshimia na kumupenda sana.—Zb. 111: 2, 3.
7. Namna gani sala inaweza kutusaidia tumuogope Yehova mu njia yenye kufaa?
7 Njia ingine yenye inaweza kutusaidia kumuogopa Mungu ni kusali kila mara. Kila mara wakati tunasali kwa Yehova, tunafikia kumujua muzuri zaidi. Na kila mara wakati tunamuomba atupatie nguvu ya kuvumilia jaribu fulani, tunakumbuka kama iko na nguvu sana. Wakati tunamushukuru juu alitutolea Mwana wake, tunakumbuka kama anatupendaka sana. Na wakati tunamuomba atusaidie saa yenye tuko na magumu fulani, tunakumbuka kama iko na hekima sana. Sala za vile, zinafanyaka tumuheshimie sana; na zinafanyaka tuazimie kabisa kuepuka kufanya jambo yoyote yenye inaweza kuharibisha urafiki wetu pamoya naye.
8. Tunapaswa kufanya nini juu tuendelee kumuogopa Mungu?
8 Juu tuendelee kumuogopa Mungu, tunapaswa kujifunza mambo fulani kupitia mifano ya muzuri na ya mubaya ya watu wenye kuzungumuziwa mu Biblia. Tuzungumuzie mifano mbili ya watumishi waaminifu wa Yehova. Obadia, mwenye alikuwa musimamizi-nyumba wa Mufalme Ahabu na Kuhani Mukubwa Yehoyada. Kisha, tutaona mambo yenye tunaweza kujifunza kupitia Mufalme Yehoashi wa Yuda, mwenye ku mwanzo alianza muzuri, lakini kisha aliacha kumutumikia Yehova.
UKUWE HODARI SAWA VILE OBADIA
9. Namna gani kumuogopa Yehova kulimusaidia Obadia? (1 Wafalme 18:3, 12)
9 Mara ya kwanza yenye Biblia inataya Obadiab inasema hivi: “Obadia alimuogopa sana Yehova.” (Soma 1 Wafalme 18:3, 12.) Namna gani ile ilimusaidia Obadia? Kwanza, ilifanya akuwe munyoofu na mwenye kutumainika. Njo maana, mufalme alimuweka ili asimamie nyumba ya kifalme. (Linganisha na Nehemia 7:2.) Pili, juu alimuogopa Yehova, ile ilifanya akuwe na uhodari sana, sifa yenye alikuwa kabisa nayo lazima. Aliishi wakati mufalme muovu Ahabu alikuwa natawala. Ule mufalme “alikuwa muovu mbele ya macho ya Yehova kuliko wale [wafalme] wote wenye walimutangulia.” (1 Fa. 16:30). Tena bibi ya Ahabu, Yezebeli mwenye aliabudu Baali, alimuchukia sana Yehova na hakupenda mutu yeyote mu makabila 10 ya ufalme wa Israeli aendelee kumuabudu Yehova. Aliua hata manabii wengi wa Mungu. (1 Fa. 18:4) Kusema kweli, Obadia alimuabudu Yehova wakati wa nguvu sana.
10. Namna gani Obadia alionyesha kama alikuwa na uhodari sana?
10 Namna gani Obadia alionyesha kama alikuwa na uhodari sana? Wakati Yezebeli alianza kutafuta manabii wa Mungu ili kuwaua, Obadia alikamata manabii 100 kati yao na kuwaficha “katika vikundi vya watu 50 katika pango moja na kuendelea kuwapatia mukate na maji.” (1 Fa. 18:13, 14) Kama Yezebeli angejua mambo yenye Obadia mwenye kuwa na uhodari alifanya, angemuua. Pengine, Obadia aliogopa na hakupenda kukufa. Lakini, alimupenda Yehova zaidi na wale wenye kumutumikia kuliko uzima wake.
Hata kama kazi yetu imekatazwa, kwa uhodari, ndugu moya iko napatia Mashahidi wenzake chakula ya kiroho (Ona fungu ya 11)d
11. Namna gani watumishi wa Yehova leo wako sawa vile Obadia? (Ona pia picha.)
11 Leo, watumishi wengi wa Yehova wako wanaishi mu mainchi kwenye kazi yetu inakatazwa. Sawa vile Obadia, wanaendelea kuheshimia wenye mamlaka, hata vile hawaache kumutumikia Yehova! (Mt. 22:21) Wanaonyesha kama wanamuogopa Mungu kwa kumutii kuliko kutii wanadamu. (Mdo. 5:29) Wanafanya vile kwa kuendelea kutangaza habari njema na kukusanyika kwa siri. (Mt. 10:16, 28) Wanahangaikia ndugu na dada zao kwa kuwapatia chakula ya kiroho. Fikiria mufano wa Henri, mwenye anaishi mu inchi moya ya Afrika kwenye kazi yetu ilikatazwa kwa wakati fulani. Mu ile wakati, Henri alijitolea ili kupelekea Mashahidi wenzake chakula ya kiroho. Anasema hivi: “Nakuwaka mutu wa haya. Niko hakika kama kumuheshimia sana Yehova njo kulifanya nikuwe na uhodari wenye nilikuwa nao lazima.” Unawaza kama unaweza kuwa na uhodari sawa wa Henri? Ndiyo, kama unamuogopa Mungu mu njia yenye kufaa.
UKUWE MUSHIKAMANIFU SAWA VILE KUHANI MUKUBWA YEHOYADA
12. Kuhani Mukubwa Yehoyada na bibi yake walifanya nini ili kuonyesha kama walikuwa washikamanifu sana kwa Yehova?
12 Kuhani Mukubwa Yehoyada alimuogopa Yehova, na ile ilimusaidia akuwe mushikamanifu na aendeleze ibada ya kweli. Alifanya vile wakati Atalia, mutoto wa Yezebeli, alianza kutawala kwa nguvu mu Yuda. Watu hawakumuogopa bure Atalia. Alikuwa mubaya sana na alipenda sana kutawala, kwa hiyo, alianza kuua hata ukoo wote wa kifalme, ni kusema, wajukuu wake! (2 Ny. 22:10, 11) Yehoashi alikuwa mumoja wa wale watoto, lakini yeye hakukufa juu Yehoshabeati, bibi ya Yehoyada, alimuokoa. Yeye na bwana yake walimuficha Yehoashi na walimuhangaikia. Juu walifanya vile, walilinda ukoo wa kifalme wa Daudi. Yehoyada alikuwa mushikamanifu kwa Yehova na hakutetemeka mbele ya Atalia.—Mez. 29:25.
13. Wakati Yehoashi alikuwa na miaka saba, Yehoyada alifanya nini ingine ili kuonyesha kama alikuwa mushikamanifu kwa Yehova?
13 Wakati Yehoashi alikuwa na miaka saba, Yehoyada alifanya jambo ingine yenye kuonyesha kama alikuwa mushikamanifu kwa Yehova. Alifanya mupango fulani. Kama ule mupango ungewezekana, Yehoashi angekuwa mufalme, muriti wa Daudi, mwenye kuwa na haki ya kutawala. Lakini kama ule mupango ungeshindikana, bila shaka Yehoyada angeuawa. Jambo ya kufurahisha, Yehova alibariki juu ule mupango uliwezekana. Wakubwa na Walawi walimutegemeza Yehoyada na walimufanya Yehoashi kuwa mufalme. Kisha Atalia aliuawa. (2 Ny. 23:1-5, 11, 12, 15; 24:1) Ku mwisho, Yehoyada “akafanya agano kati ya Yehova na mufalme na watu, kwamba wataendelea kuwa watu wa Yehova.” (2 Fa. 11:17) “Aliweka pia walinzi wa milango mikubwa karibu na milango mikubwa ya nyumba ya Yehova, ili mutu yeyote mwenye haiko safi kwa njia yoyote asiingie.”—2 Ny. 23:19.
14. Namna gani Yehoyada aliheshimiwa juu alimuheshimia Yehova?
14 Yehova alikuwa alishasema hivi: “Wale wenye kuniheshimia nitawaheshimia.” Bila shaka, alimubariki Yehoyada. (1 Sa. 2:30) Kwa mufano, aliweka habari ya Yehoyada mu Biblia ili tujifunze mambo fulani. (Ro. 15:4) Na wakati Yehoyada alikufa, alipewa heshima kwa kuzikwa “katika Muji wa Daudi pamoja na wafalme, kwa sababu alikuwa ametenda mema katika Israeli kuhusiana na Mungu wa kweli na nyumba yake.”—2 Ny. 24:15, 16.
Sawa vile Kuhani Mukubwa Yehoyada, kumuogopa Mungu kunapaswa kutuchochea kusaidia ndugu zetu kwa ushikamanifu (Ona fungu ya 15)e
15. Habari ya Yehoyada inaweza kutufundisha nini? (Ona pia picha.)
15 Habari ya Yehoyada inaweza kutusaidia siye wote kujifunza kumuogopa Mungu. Waangalizi Wakristo wanaweza kumuiga Yehoyada kwa kuendelea kuwa macho na kwa kulinda kundi ya Mungu kwa ushikamanifu. (Mdo. 20:28) Mufano wa Yehoyada unaweza kufundisha wale wenye kuzeeka kama ikiwa wanamuogopa Yehova na wanaendelea kuwa washikamanifu kwake, anaweza kuwatumia ili kutimiza kusudi yake. Hawaachake hata kidogo. Vijana wanaweza kumuiga Yehova mu namna alitendea Yehoyada kwa kuheshimia ndugu na dada wenye kuzeeka, zaidi sana wale wenye walishamutumikia Yehova kwa miaka mingi. (Mez. 16:31) Mufano wa wakubwa na Walawi wenye walimutegemeza Yehoyada unaweza pia kutufundisha siye wote mambo fulani. Tutegemeze basi kwa ushikamanifu “wale wenye wanaongoza” kwa kuwatii.—Ebr. 13:17.
USIKUWE SAWA VILE MUFALME YEHOASHI
16. Nini njo inaonyesha kama Mufalme Yehoashi hakuendelea kuwa mushikamanifu?
16 Yehoyada alimusaidia Mufalme Yehoashi kuwa mutu muzuri. (2 Fa. 12:2) Ile ilifanya kijana Yehoashi apende kumufurahisha Yehova. Lakini kisha kifo ya Yehoyada, Yehoashi alianza kusikiliza wakubwa wenye walikuwa waasi-imani. Ile ilimufikisha wapi? Yeye na wale wakubwa “wakaanza kutumikia miti mitakatifu na sanamu.” (2 Ny. 24: 4, 17, 18) Hata kama Yehova alikasirika sana juu ya ile, “aliendelea kutuma manabii kati yao ili kuwarudisha . . . , lakini walikataa kusikiliza.” Hawakumusikiliza hata Zekariac, mutoto wa Yehoyada, mwenye alikuwa nabii wa Yehova na kuhani, lakini pia binamu (cousin) wa Yehoashi. Jambo ya kuhuzunisha, Mufalme Yehoashi alimuua Zekaria hata kama familia ya Zekaria njo ilimuokoaka.—2 Ny. 22:11; 24:19-22.
17. Namna gani mambo ilimuendea Yehoashi?
17 Yehoashi hakuendelea kumuogopa Yehova mu njia yenye kufaa, na mambo ilimuendea mubaya. Yehova alisemaka hivi: “Wale wenye kunizarau watazarauliwa.” (1 Sa. 2:30) Kisha, jeshi kidogo ya Siria ilishambulia “jeshi kubwa sana” ya Yehoashi na ‘kumuumiza sana.’ Kisha Waasiria kutoka, watumishi wa Yehoashi walimuua juu naye aliuaka Zekaria. Ule mufalme muovu hakustahili hata kuzikwa “katika makaburi ya wafalme.”—2 Ny. 24:23-25.
18. Kulingana na Yeremia 17:7, 8, tunaweza kufanya nini juu tusikuwe sawa vile Yehoashi?
18 Mufano wa Yehoashi unaweza kutufundisha nini? Alikuwa sawa vile muti wenye ulitegemezwa na muti ingine juu mizizi yake haikukuwa nakamata muzuri mu udongo. Wakati Yehoyada, ni kusema, muti wenye ulimutegemeza alikufa, Yehoashi alianza kusikiliza waasi-imani na hakuendelea kuwa muaminifu kwa Yehova. Ile mufano inaonyesha kama hatupaswe kumutii Mungu juu tu watu wa familia yetu na wengine mu kutaniko wanatuwekea mufano muzuri wa kufuata. Juu tuendelee kuwa nguvu kiroho, tunapaswa kujikaza kumupenda na kumuheshimia Yehova kwa kujifunza kwa ukawaida, kufikiri sana, na kusali.—Soma Yeremia 17:7, 8; Kol. 2:6, 7.
19. Yehova anatuomba tufanye nini?
19 Yehova hatuombe mambo mingi kupita uwezo wetu. Andiko ya Muhubiri 12:13 inaonyesha kwa kifupi mambo yenye anatuomba, inasema hivi: “Ogopa Mungu wa kweli na ushike amri zake, kwa maana hilo ndilo jambo lote lenye mwanadamu anapaswa kufanya.” Sawa vile Obadia na Yehoyada, ikiwa tunamuogopa Mungu, tutaendelea kuwa washikamanifu kwake. Hata kutokee nini, hakuna jambo yoyote yenye inaweza kuharibisha urafiki wetu pamoya naye.
WIMBO 3 Nguvu Yangu, Tumaini Yangu, Ninakutegemea
a Wakati Maandiko inatumia neno “woga,” inaitumiaka mu maana yenye kupanuka. Kulingana na hali, ile neno inaweza kumaanisha hofu ao heshima kubwa. Hii habari itatusaidia tukuwe na woga wenye kufaa wenye utatufanya tukuwe na uhodari na washikamanifu wakati tuko namutumikia Baba yetu wa mbinguni.
b Hapa hatuzungumuzie Obadia mwenye alikuwa nabii, mwenye aliishi karne mingi kisha na mwenye aliandikaka kitabu ya Biblia yenye kuwa na jina yake.
c Matayo 23:35 inasema kama Zekaria alikuwa mutoto wa Barakia. Inasemekana kama pengine Yehoyada alikuwa na majina mbili, sawa vile watu wengine wenye kutajwa mu Biblia (linganisha Matayo 9:9 na Marko 2:14), ao kama Barakia alikuwa tate ao babu ya Zekaria.
d MAFASIRIO YA PICHA: Mu hii picha, ndugu fulani iko napatia ndugu moya chakula ya kiroho wakati kazi yetu imekatazwa.
e MAFASIRIO YA PICHA: Dada moya mwenye kuzeeka iko nafundisha dada moya kijana namna ya kuhubiri kupitia telefone; ndugu moya mwenye kuzeeka anaonyesha uhodari kwa kuhubiri fasi ya watu wengi; ndugu fulani mwenye uzoefu anazoeza wengine kuhusu namna ya kutunza Jumba ya Ufalme.