Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • Mutu Anaweza Kufanya Matendo ya Muzuri Siku ya Sabato?
    Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
    • Yesu anazungumuza na mwanaume mugonjwa pembeni ya kiziwa cha maji cha Betzata

      SURA YA 29

      Mutu Anaweza Kufanya Matendo Ya Muzuri Siku Ya Sabato?

      YOHANA 5:1-16

      • YESU ANAHUBIRI KATIKA YUDEA

      • ANAPONYESHA MWANUME MWENYE KUGONJWA KWENYE KIZIWA CHA MAJI

      Yesu amefanya mambo mengi wakati wa utumishi wake katika Galilaya. Lakini, wakati anasema, “Ni lazima pia nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu katika miji mingine,” Yesu anafikiria maeneo mengine zaidi ya Galilaya. Kwa hiyo, anaenda “kuhubiri katika masinagogi ya Yudea.” (Luka 4:43, 44) Hilo linafaa kwa sababu sasa ni kipindi cha kuchipuka kwa majani na siku ya sherehe katika Yerusalemu inakaribia.

      Wakati tunalinganisha mambo yenye tulisoma juu ya utumishi wa Yesu katika Galilaya na yale anafanya katika Yudea, tunaona kuwa Injili zinatoa habari kidogo juu ya kazi ya Yesu katika Yudea. Hata kama watu wengi katika Yuda hawapendezwe, hilo halimuzuie Yesu kuhubiri kwa bidii na kufanya matendo ya muzuri kila mahali kwenye anapatikana.

      Sasa Yesu anaenda katika Yerusalemu, muji mukubwa wa Yudea, kwa ajili ya Pasaka ya mwaka wa 31 wakati wetu. Katika nafasi kwenye watu wengi wanapatikana karibu na Mulango wa Kondoo, kuko kiziwa kikubwa cha maji chenye kuzungukwa na nguzo chenye kuitwa Betzata. Wagonjwa wengi, vipofu, na vilema wanakuja kwenye kiziwa hicho. Sababu gani? Kwa sababu watu wanazoea kuamini kuwa mutu anaweza kuponyeshwa ikiwa anaingia katika kiziwa wakati maji yanavurugwa.

      Sasa ni siku ya Sabato, na Yesu anaona mwanaume fulani kwenye kiziwa hicho mwenye amekuwa mugonjwa kwa miaka 38. Yesu anamuuliza hivi: “Je, unataka kupona?” Mwanaume huyo anajibu hivi: “Bwana, sina mutu wa kuniweka ndani ya kiziwa cha maji wakati maji yanavurugwa, lakini wakati ninakuja, mutu mwingine anaingia mbele yangu.”—Yohana 5:6, 7.

      Yesu anasema jambo fulani lenye linapaswa kushangaza mwanaume huyo na mutu yeyote mwenye angelisikia: “Simama! Kamata kitanda chako na utembee.” (Yohana 5:8) Na mwanaume huyo anafanya kabisa hivyo. Kisha tu kuponyeshwa, mwanaume huyo anakamata kitanda chake na anaanza kutembea!

      Wayahudi wanazungumuza na mwanaume mwenye Yesu aliponyesha

      Kuliko kufurahi juu ya jambo la muzuri sana lenye limefanyika, Wayahudi wanaona mwanaume huyo na kumuhukumu kwa kusema: “Ni Sabato, na hauruhusiwe kubeba kitanda.” Mwanaume huyo anawajibu hivi: “Ule mwenye aliniponyesha aliniambia, ‘Kamata kitanda chako na utembee.’” (Yohana 5:10, 11) Wayahudi hao wanaona kuwa haifae kuponyesha watu siku ya Sabato.

      Wanapenda kujua; kwa hiyo wanamuuliza hivi: “Ni nani ule mwenye alikuambia, ‘Ukikamate na utembee’?” Sababu gani wanauliza mwanaume huyo ulizo hilo? Kwa sababu Yesu “alikuwa amepotea katikati ya watu wengi,” na mwanaume mwenye ameponyeshwa hajue jina la Yesu. (Yohana 5:12, 13) Lakini mwanaume huyo atakutana tena na Yesu. Kisha, katika hekalu, mwanaume huyo anakutana na Yesu na anapata nafasi ya kujua mutu mwenye alimuponyesha kwenye kiziwa cha maji.

      Mwanaume mwenye aliponyeshwa anakutana na Wayahudi wenye walimuuliza ni nani mwenye alimuponyesha. Anawaambia kama ni Yesu. Wakati wanajua jambo hilo, Wayahudi wanaenda kumuona Yesu. Je, wanaenda ili kujua ni kupitia njia gani Yesu iko na uwezo wa kufanya mambo hayo ya ajabu? Hapana. Lakini, wanaenda ili kumuonyesha Yesu kama amefanya kosa kwa kufanya mambo ya muzuri siku ya Sabato. Na wanaanza hata kumutesa!

      • Sababu gani Yesu anaenda katika Yudea, na ni mambo gani anaendelea kufanya?

      • Sababu gani watu wengi wanaenda kwenye kiziwa cha maji chenye kuitwa Betzata?

      • Yesu anafanya muujiza gani kwenye kiziwa cha maji, na Wayahudi fulani wanatenda namna gani?

  • Uhusiano wa Yesu Pamoja na Baba Yake
    Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
    • Wayahudi wanamushitaki Yesu kuwa anavunja Sabato

      SURA YA 30

      Uhusiano wa Yesu Pamoja na Baba Yake

      YOHANA 5:17-47

      • MUNGU NI BABA YA YESU

      • AHADI YA UFUFUO

      Wakati Wayahudi fulani wanamushitaki Yesu kuwa anavunja Sabato kwa kumuponyesha mwanaume fulani, Yesu anajibu hivi: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mupaka sasa, na mimi ninaendelea kufanya kazi.”—Yohana 5:17.

      Lakini, mambo yenye Yesu anafanya hayakatazwe na sheria ya Mungu juu ya Sabato. Anaiga matendo ya muzuri ya Baba yake kwa kuhubiri na kuponyesha watu. Kwa hiyo, Yesu anaendelea kufanya matendo ya muzuri kila siku. Lakini jibu lenye anapatia wale wenye kumushitaki linawafanya wakasirike hata zaidi, na wanatafuta kumuua Yesu. Sababu gani wanakasirika?

      Zaidi ya kuwa na mawazo yenye makosa kama Yesu iko anavunja Sabato kwa kuponyesha watu, wanaona kuwa Yesu amefanya kosa kubwa kwa kusema kama yeye ni Mwana wa Mungu. Wanaona kama anatukana kwa kumuona Mungu kuwa Baba yake; wanaona kuwa wakati Yesu anasema kama Yehova ni Baba yake anajifanya sawasawa na Mungu. Lakini, Yesu haogope na anajibu kwa kuwafasiria zaidi juu ya uhusiano wake wa pekee pamoja na Mungu. Anasema hivi: “Baba anapenda Mwana na anamuonyesha mambo yote yenye yeye mwenyewe anafanya.”—Yohana 5:20.

      Baba ndiye Mupaji-Uzima, na zamani alionyesha hilo kwa kupatia wanaume fulani uwezo wa kufufua watu. Yesu anaongeza hivi: “Kama vile Baba anafufua wafu na kuwafanya kuwa wazima, ni vile Mwana pia anafanya kuwa wazima wale wenye anataka.” (Yohana 5:21) Maneno hayo ni yenye maana sana na yanatoa tumaini kwa ajili ya wakati wenye kuja. Hata leo, Mwana iko anafufua watu kiroho. Ndiyo sababu Yesu anasema hivi: “Kila mutu mwenye anasikia neno langu na kumuamini Ule mwenye alinituma iko na uzima wa milele, na haingie katika hukumu lakini amevuka kutoka katika kifo na kuingia katika uzima.”—Yohana 5:24.

      Hakuna maandishi yenye kuonyesha kuwa Yesu amekwisha kabisa kufufua mutu mwenye alikuwa amekufa kimwili, lakini anaambia wale wenye kumushitaki kuwa ufufuo kama huo utafanyika. Anasema hivi: “Saa inakuja yenye wale wote wenye kuwa katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

      Hata kama Yesu iko na daraka kubwa zaidi, anaonyesha waziwazi kuwa Mungu ni mukubwa kuliko yeye, kwa kusema hivi: “Siwezi kufanya jambo lolote kwa uamuzi wangu mwenyewe. . . . Sitafute mapenzi yangu mwenyewe, lakini mapenzi ya ule mwenye alinituma.” (Yohana 5:30) Hata hivyo, Yesu anazungumuzia daraka lake la maana katika kusudi la Mungu, jambo lenye alikuwa hajafanya mupaka sasa mbele ya watu wengi. Lakini zaidi ya ushuhuda wa Yesu mwenyewe, wale wenye kumushitaki wanajua mengi zaidi juu ya mambo hayo. Yesu anawakumbusha hivi: “Mumetuma watu kwa Yohana [Mubatizaji], na ametoa ushahidi juu ya kweli.”—Yohana 5:33.

      Inawezekana wale wenye kumushitaki Yesu walikuwa wamesikia jambo hilo kumepita karibu miaka mbili; Yohana aliambia viongozi wa dini ya Kiyahudi juu ya Ule mwenye kuja nyuma yake, mwenye aliitwa “Nabii” na “Kristo.” (Yohana 1:20-25) Yesu anawakumbusha namna walimuheshimu Yohana mwenye sasa ni mufungwa. Anasema hivi: “Kwa wakati mufupi mulikuwa tayari kufurahi katika mwangaza wake.” (Yohana 5:35) Hata hivyo, Yesu anatoa ushahidi mukubwa zaidi kuliko Yohana Mubatizaji.

      “Kazi hizi zenye ninafanya [kutia ndani muujiza wa kuponyesha wenye ametoka tu kufanya] zinatoa ushahidi kwamba Baba alinituma.” Zaidi ya hilo, Yesu anaongeza hivi: “Baba mwenye alinituma ametoa ushahidi yeye mwenyewe juu yangu.” (Yohana 5:36, 37) Kwa mufano, Mungu alitoa ushahidi juu ya Yesu wakati alibatizwa.—Matayo 3:17.

      Kwa kweli, wale wenye kumushitaki Yesu hawana sababu yoyote ya kukosa kumuamini. Maandiko yenye wanasema kuwa wanachunguza yanatoa ushahidi juu yake. Yesu anamalizia hivi: “Kama mungemuamini Musa, mungeniamini mimi pia, kwa maana aliandika juu yangu. Lakini kama hamuamini mambo yenye aliandika, namna gani mutaamini mambo yenye ninasema?”—Yohana 5:46, 47.

      • Sababu gani kufanya matendo ya muzuri siku ya Sabato haiko kuvunja Sabato?

      • Yesu anasema nini juu ya daraka lake la maana katika kusudi la Mungu?

      • Ni ushuhuda gani mbalimbali unaonyesha kama Yesu ni Mwana wa Mungu?

  • Wanakata Masuke ya Nafaka Siku ya Sabato
    Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
    • Wanafunzi wa Yesu wanakata masuke ya nafaka na kula mbegu siku ya Sabato

      SURA YA 31

      Wanakata Masuke Ya Nafaka Siku Ya Sabato

      MATAYO 12:1-8 MARKO 2:23-28 LUKA 6:1-5

      • WANAFUNZI WANAKATA MASUKE YA NAFAKA SIKU YA SABATO

      • YESU NI “BWANA WA SABATO”

      Sasa, Yesu na wanafunzi wake wanasafiri kuenda upande wa kaskazini, katika Galilaya. Ni kipindi cha kuchipuka kwa majani, na mbegu zimekwisha kukomaa. Kwa sababu ya njaa, wanafunzi wa Yesu wanakata masuke ya nafaka na kula. Lakini siku hiyo ni ya Sabato, na Wafarisayo wanaangalia kile wanafunzi wako wanafanya.

      Kumbuka kama hivi karibuni, Wayahudi katika Yerusalemu walipenda kumuua Yesu, kwa kumushitaki kuwa anavunja Sabato. Sasa Wafarisayo wanaleta shitaka lingine lenye kutegemea matendo ya wanafunzi. Wanamuambia Yesu hivi: “Angalia! Wanafunzi wako wanafanya jambo lenye hairuhusiwe kufanya siku ya Sabato.”—Matayo 12:2.

      Wafarisayo wanasema kuwa kukata masuke na kutosha maganda kwa mikono ili kula ni kazi ya kuvuna na kupiga-piga mbegu. (Kutoka 34:21) Mawazo yao yenye kuvuka mipaka kuhusu matendo yenye yanaweza kuonwa kuwa kazi, inafanya Sabato ikuwe muzigo. Lakini, kusudi la Sabato ilikuwa kufanya siku hiyo ikuwe yenye kuleta furaha na yenye kujenga kiroho. Yesu anapinga mawazo yao yenye makosa kwa kutumia mifano ili kuonyesha kuwa Yehova Mungu hakutaka hata kidogo sheria Yake juu ya Sabato itumiwe hivyo.

      Mufano moja wenye Yesu anatoa ni wa Daudi na watu wake. Wakati walisikia njaa, walienda kwenye tabenakulo na kula mikate ya toleo. Mikate hiyo, yenye ilikuwa tayari imeondolewa mbele ya Yehova na kubadilishwa na mikate ingine yenye imetoka tu kutengenezwa, kwa kawaida ni makuhani tu ndio walipaswa kuikula. Hata hivyo, katika hali hiyo, Daudi na watu wake hawakulaumiwa kwa sababu walikula mikate hiyo.—Mambo ya Walawi 24:5-9; 1 Samweli 21:1-6.

      Katika mufano wa pili, Yesu anasema hivi: “Je, hamukusoma katika Sheria kwamba kila siku ya Sabato makuhani katika hekalu wanavunja Sabato na wanabakia bila kosa?” Yesu anapenda kusema kuwa hata siku ya Sabato, makuhani wanachinja wanyama kwa ajili ya toleo na wanafanya kazi zingine kwenye hekalu. Yesu anasema hivi: “Lakini ninawaambia ninyi, hapa kuko mutu mukubwa kuliko hekalu.”—Matayo 12:5, 6; Hesabu 28:9.

      Tena, kwa kutumia Maandiko, Yesu anasema hivi: “Kama mungeelewa maana ya maneno haya, ‘Ninataka rehema hapana zabihu,’ hamungelaumu watu wenye hawana kosa.” Anamalizia kwa kusema hivi: “Kwa maana Mwana wa binadamu ni Bwana wa Sabato.” Yesu iko anazungumuzia wakati wenye atakuwa Mufalme kwa miaka elfu.—Matayo 12:7, 8; Hosea 6:6.

      Wanadamu wameteseka sana katika ulimwengu huu wenye kutawaliwa na Shetani, mwenye jeuri na vita vinaendelea kuongezeka. Mambo yatakuwa tofauti kabisa chini ya utawala wa Sabato kubwa wa Kristo. Katika utawala huo, Yesu atatutolea wakati wa mapumuziko wenye tuko nao lazima na wenye tunangojea kwa hamu!

      • Wafarisayo wanashitaki wanafunzi wa Yesu kuwa wanafanya nini, na sababu gani?

      • Namna gani Yesu anarekebisha mawazo ya Wafarisayo?

      • Ni katika njia gani Yesu ni “Bwana wa Sabato”?

  • Ni Nini Inaruhusiwa Kufanya Siku ya Sabato?
    Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
    • Yesu iko karibu kuponyesha mutu fulani mwenye kuwa na mukono wenye kupooza

      SURA YA 32

      Ni Nini Inaruhusiwa Kufanya Siku Ya Sabato?

      MATAYO 12:9-14 MARKO 3:1-6 LUKA 6:6-11

      • ANAPONYESHA MUKONO WA MWANAUME FULANI SIKU YA SABATO

      Kwenye siku ingine ya Sabato, Yesu anaenda kwenye sinagogi fulani, pengine katika Galilaya. Huko anakuta mwanaume mumoja mwenye kuwa na mukono wenye kukauka. (Luka 6:6) Waandishi na Wafarisayo wako wanaangalia Yesu kwa uangalifu. Sababu gani? Wanaonyesha waziwazi mawazo yao wakati wanauliza hivi: “Je, inaruhusiwa kuponyesha siku ya Sabato?”—Matayo 12:10.

      Viongozi wa dini ya Kiyahudi wanaamini kuwa kuponyesha mutu kunaruhusiwa siku ya Sabato ikiwa tu uzima uko katika hatari. Kwa mufano, hairusiwe siku ya Sabato kuunganisha mufupa ao kufunga sehemu yenye kuteguka, hali zenye hazitie uzima katika hatari. Kwa kweli, waandishi na Wafarisayo hawaulize Yesu maulizo kwa sababu wanahangaikia kabisa mateso ya mwanaume huyo. Wako wanajikaza kupata visababu ili kumuhukumu Yesu.

      Lakini, Yesu anajua mawazo yao ya mubaya. Anatambua kama wamekuwa na mawazo yenye kuvuka mipaka na yenye haitegemee Maandiko kuhusu kuvunja sheria yenye kukataza kufanya kazi siku ya Sabato. (Kutoka 20:8-10) Amekwisha kulaumiwa bila sababu juu ya matendo yake ya muzuri. Sasa Yesu anafanya jambo lenye litatokeza mabishano makubwa kwa kuambia ule mutu mwenye kuwa na mukono wenye kupooza hivi: “Simama na ukuje katikati.”—Marko 3:3.

      Yesu anaangalia waandishi na Wafarisayo, na kuwaambia hivi: “Kama uko na kondoo moja, kisha kondoo huyo anaangukia katika shimo siku ya Sabato, je, kuko mutu yeyote kati yenu mwenye hatamukamata na kumutosha ndani?” (Matayo 12:11) Kwa sababu kuwa na kondoo ni kama vile kuweka feza, sasa hawangeacha kondoo huyo katika shimo mupaka siku yenye kufuata; kondoo huyo angekufa wakati huo na kufanya mutu apoteze. Zaidi ya hilo, Maandiko yanasema hivi: “Mutu mwenye kufanya mambo yenye kuwa sawa anatunza wanyama wake wa kufugwa.”—Methali 12:10.

      Yesu anafanya ulinganisho wenye usawaziko kwa kusema hivi: “Kama ni vile, mwanadamu ni wa maana sana kupita kondoo! Kwa hiyo, inaruhusiwa kufanya jambo la muzuri siku ya Sabato.” (Matayo 12:12) Kwa hiyo, Yesu havunje Sabato kwa kuponyesha mutu huyo. Viongozi hao wa dini wanashindwa kupinga mawazo hayo yenye kufaa, na yenye kuonyesha huruma. Wanabakia kimya.

      Yesu anahuzunishwa na mawazo yao ya mubaya, na anawaangalia kwa kasirani. Kisha anaambia mutu huyo hivi: “Nyoosha mukono wako.” (Matayo 12:13) Wakati mutu huyo ananyoosha mukono wake wenye kupooza, unarudishwa muzima. Hili ni jambo lenye linapaswa kumuletea mutu huyo furaha, lakini hilo linakuwa na matokeo gani kwa wale wenye wanajaribu kumukamata Yesu katika mutego?

      Viongozi Wayahudi wanafanya mukutano ili kumuua Yesu

      Kuliko kufurahi kuwa mukono wa mutu huyo umerudishwa kuwa muzima, Wafarisayo wanatoka inje na mara moja wanaanza kufanya mukutano juu ya Yesu “pamoja na wafuasi wa chama cha Herode, ili kumuua.” (Marko 3:6) Bila shaka, katika chama hicho cha kisiasa ao cha politike, muko pia watu wa kikundi cha dini wenye kuitwa Wasadukayo. Kwa kawaida, Wasadukayo na Wafarisayo wanapingana kati yao, lakini sasa wanajiunga kabisa pamoja ili kumupinga Yesu.

      • Ni hali gani inatokeza mabishano kati ya Yesu na viongozi wa dini ya Kiyahudi?

      • Viongozi wa dini ya Kiyahudi wako na mawazo gani yenye makosa juu ya sheria kuhusu Sabato?

      • Namna gani Yesu anapinga kwa hekima mawazo yenye makosa juu ya Sabato?

Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2026)
Toka
Ingia
  • Kiswahili (Congo)
  • Tumia Wengine
  • Préférences
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Kanuni za Matumizi
  • Kanuni za Kutunza Siri
  • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
  • JW.ORG
  • Ingia
Tumia Wengine