-
Ni Nani Wanaohubiri Habari Njema?Munara wa Mulinzi—2011 | Mwezi wa 3 1
-
-
Ni Nani Wanaohubiri Habari Njema?
“ . . . itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.”—MATHAYO 24:14.
HABARI njema inahubiriwa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova. Wanafanya hivyo katika njia tofauti-tofauti. Njia moja ni kwa . . .
Kuzungumza na Watu. Kama Yesu na wanafunzi wake, Mashahidi wa Yehova wanawatembelea watu ili kuwahubiria habari njema. (Luka 8:1; 10:1) Mashahidi hawangoji watu wawatafute. Kuwahubiria watu kuhusu Ufalme wa Mungu ni kazi inayofanywa na Mashahidi wote, ambao ni zaidi ya milioni saba. Wanahubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, kwa simu, na kwa njia nyingine. Mwaka uliopita, Mashahidi walitumia zaidi ya saa bilioni moja na nusu katika kazi hiyo.
Wanawafundisha wengine kuhusu Ufalme wa Mungu na pia kuhusu ‘mambo yote ambayo Yesu aliwaamuru.’ (Mathayo 28:20) Wanaongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya milioni nane bila malipo.
Mashahidi wanahubiri ulimwenguni pote—katika nchi 236. Wanawahubiria watu wa aina zote. Wanahubiri vijijini na hata mijini, katika misitu ya Amazoni, misitu mikubwa ya Siberia, majangwa ya Afrika, na katika Milima ya Himalaya. Hawalipwi kwa kufanya kazi hiyo, bali wanaifanya kwa kutumia wakati na gharama zao wenyewe. Wanachochewa na upendo wao kwa Mungu na jirani. Pia, wanahubiri habari njema kupitia . . .
Machapisho. Gazeti hili, ambalo jina lake kamili ni Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova, sasa linachapishwa katika lugha 185 likiwa na jumla ya nakala zaidi ya milioni 42 kwa kila toleo. Gazeti la Amkeni!, ambalo pia linatangaza kuhusu Ufalme, linachapishwa katika lugha 83 likiwa na jumla ya nakala milioni 40 hivi kwa kila toleo.
Vitabu, broshua, trakti, CD/MP3, na DVD ambazo zinafafanua mafundisho ya Biblia zinapatikana katika lugha 540 hivi. Katika kipindi cha miaka kumi tu iliyopita, Mashahidi wametayarisha na kugawanya vifaa zaidi ya bilioni 20. Hiyo ni sawa na vifaa vitatu hivi kwa kila mtu anayeishi duniani!
Mashahidi wa Yehova pia wamechapa au kuagiza uchapaji wa tafsiri mbalimbali za Biblia. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ambayo imetafsiriwa, kuchapwa, na kusambazwa na Mashahidi, sasa inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 96. Zaidi ya nakala milioni 166 zimesambazwa. Mashahidi pia wanahubiri habari njema ya Ufalme . . .
Kwenye Mikutano ya Kikristo. Mikutano inayofanywa kila juma katika Majumba ya Ufalme si utaratibu tu wa ibada za kidini; inakusudiwa kuelimisha watu. Hotuba hutolewa kulingana na kichwa fulani cha Biblia, na watu hujifunza Biblia wakitumia gazeti la Mnara wa Mlinzi na machapisho mengine. Katika mikutano hiyo, pia Mashahidi hujifunza jinsi ya kuwa na matokeo zaidi wakiwa watangazaji wa habari njema.
Mashahidi hujifunza habari ileile katika makutaniko zaidi ya 107,000 ulimwenguni pote. Jambo hilo linachangia umoja wao. Watu wote wanakaribishwa kwenye mikutano hiyo. Hakuna sadaka zinazokusanywa. Bila shaka, yote hayo hayangekuwa na maana yoyote ikiwa Mashahidi wangeshindwa kuishi kulingana na yale wanayohubiri. Hivyo basi, wanajaribu kupendekeza habari njema . . .
Kwa Mfano Wao Mzuri. Wanajitahidi kuweka mfano mzuri kuhusiana na mwenendo wao wakiwa Wakristo, wakifanya kadiri wanavyoweza kuwatendea wengine kwa njia ambayo wao wenyewe wangependa watendewe. (Mathayo 7:12) Ingawa hawajakamilika na nyakati nyingine wanakosea, bado wao wanatamani kwa unyofu kuwatendea watu wote kwa upendo, si kwa kuwahubiria habari njema tu, bali pia kwa kuwasaidia katika njia nyingine inapowezekana.
Mashahidi wa Yehova hawajaribu kuugeuza ulimwengu kupitia kazi yao ya kuhubiri. Yehova atakaporidhika kuwa kazi hiyo imefanywa vya kutosha, ndipo mwisho utakapokuja kama Yesu alivyotabiri. Hilo litamaanisha nini kwa dunia na watu?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Habari njema inahubiriwa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote
-
-
“Mwisho” Ni Nini?Munara wa Mulinzi—2011 | Mwezi wa 3 1
-
-
“Mwisho” Ni Nini?
“. . . na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—MATHAYO 24:14.
HIVI karibuni kumekuwa na mazungumzo mengi kuhusu mwisho wa dunia. Katika vitabu, sinema, na magazeti kuna habari zenye kuchekesha na hata za kisayansi zinazoonyesha kwa njia mbalimbali misiba itakayotokea katika siku ya maangamizi. Misiba hiyo inatia ndani uharibifu utakaotokana na vita vya nyuklia, kugongana kwa sayari ndogo, virusi hatari, mabadiliko makubwa ya hali ya hewa, au wavamizi kutoka sayari nyingine.
Maoni ya dini pia yanatofautiana. Dini nyingi zinafundisha kwamba “mwisho” utakomesha uhai wote duniani. Akizungumzia kuhusu Mathayo 24:14, mwanatheolojia mmoja aliandika maneno haya yenye kuogopesha: “Huu ni mmoja kati ya mistari muhimu zaidi katika Neno la Mungu . . . Kizazi chetu kinakabili maangamizi ya kiwango kikubwa sana hivi kwamba ni wachache kati yetu wanaojaribu kuwazia jinsi hali itakavyokuwa.”
Kwa kawaida, wenye maoni hayo hupuuza jambo hili muhimu: Yehova Mungu ‘aliifanya dunia ikiwa imara,’ yeye “hakuiumba tu bila sababu, [bali] aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Hivyo, Yesu alipozungumza kuhusu “mwisho,” hakumaanisha kwamba dunia itaharibiwa; wala hakumaanisha kuwa wanadamu wote wataangamizwa. Alimaanisha kwamba waovu—wale ambao kwa kiburi wanakataa kuishi kulingana na mwongozo wenye upendo wa Yehova—wataharibiwa.
Fikiria mfano huu: Tuseme unamiliki nyumba nzuri na unawaruhusu watu waishi humo bila malipo. Baadhi yao wanaishi na wengine kwa amani na wanaitunza nyumba yako vizuri. Hata hivyo, wengine wanasababisha vurugu, wanapigana, na kuwaonea wale wakaaji wazuri. Wanaharibu nyumba yako na kwa kiburi wanakataa kukusikiliza unapojaribu kuwazuia wasifanye hivyo.
Ungefanya nini ili kurekebisha mambo? Je, ungeibomoa nyumba yako? Yaelekea hungefanya hivyo. Labda ungewaondoa wale wakaaji wabaya na kurekebisha uharibifu ambao umefanywa.
Yehova atafanya vivyo hivyo. Alimwongoza mtunga-zaburi kuandika: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali, bali wale wanaomtumaini Yehova ndio watakaoimiliki dunia. Na bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:9-11.
Mtume Petro alizungumza kuhusu jambo hilohilo. Aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Mbingu zilikuwapo tangu zamani za kale na dunia ikisimama imara kutoka katika maji na katikati ya maji kwa neno la Mungu; na kwa njia hizo ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji.” (2 Petro 3:5, 6) Hapa mtume alikuwa akirejelea Gharika ya siku za Noa. Ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu uliharibiwa, lakini dunia yenyewe haikuharibiwa. Gharika hiyo iliyoikumba dunia nzima ‘iliweka kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja.’—2 Petro 2:6.
Kisha Petro akaongeza: “Mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto.” Ikiwa tungesoma sehemu hiyo tu, huenda tungekosa maana ya mstari mzima. Hata hivyo, ona kwamba mstari huo unaendelea kusema: “Na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” Huo si uharibifu wa dunia, bali wa watu wasiomwogopa Mungu. Ni nini kinachofuata? Petro aliandika: “Kulingana na ahadi yake tunangojea mbingu mpya [Ufalme wa Kimasihi wa Mungu] na dunia mpya [jamii ya wanadamu waadilifu], na humo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:7, 13.
Unabii wa Biblia pia unaonyesha kwamba “mwisho” utafika hivi karibuni. Soma Mathayo 24:3-14 na 2 Timotheo 3:1-5 ili uone mambo yanayothibitisha kwamba maneno hayo ni ya kweli.a
Je, inashangaza kuwa watu wengi wamechanganyikiwa kuhusu Mathayo 24:14, andiko ambalo hata mtoto mdogo anaweza kulielewa? Kuna sababu za kuchanganyikiwa. Shetani amepofusha watu wasielewe kweli zenye thamani zinazopatikana katika Neno la Mungu. (2 Wakorintho 4:4) Pia, Mungu ameficha makusudi yake yasijulikane na watu wenye kiburi lakini ameyafunua kwa watu wanyenyekevu. Kuhusiana na hilo, Yesu alisema: “Ninakusifu wewe hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye akili na umeyafunua kwa watoto.” (Mathayo 11:25) Ni pendeleo kubwa kama nini kuwa miongoni mwa watu wanyenyekevu wanaoelewa vizuri Ufalme wa Mungu ni nini, na wanaoweza kuwa na tazamio la kupata baraka ambazo wale wanaounga mkono Ufalme huo watapata!
-