SURA YA 3
“Mukumbuke Wale Wenye Wanaongoza Kati Yenu”
HII maneno ya mutume Paulo yenye kupatikana mu Waebrania 13:7, inaweza pia kutafsiriwa hivi: “Mukumbuke magavana wenu.” Tangu Pentekoste ya 33 K.K.Y., mitume waaminifu wa Bwana Yesu Kristo njo walitimiza ile daraka. Wao njo walikuwa mu baraza yenye kuongoza ya ile wakati. Walikuwa wanaongoza kutaniko ya Kikristo yenye ilitoka tu kuanzishwa. (Mdo. 6:2-4) Mu mwaka wa 49 K.K.Y., wanaume wengine walianza pia kutumika mu ile baraza yenye kuongoza pamoya na mitume wa Yesu. Wakati tatizo yenye inahusu kutahiriwa ilishugulikiwa, mu ile baraza mulikuwa “mitume na wazee kule Yerusalemu.” (Mdo. 15:1, 2) Walikuwa na daraka ya kuchunguza na kukamata maamuzi juu ya mambo yenye ilihusu Wakristo wa kila fasi. Walikuwa wanatuma mabarua na maagizo yenye ilitia nguvu makutaniko, na yenye ilisaidia wanafunzi waendelee kuwa na umoja mu namna yao ya kuwaza na ya kufanya mambo. Makutaniko ilitii na kufuata kwa unyenyekevu ile maagizo yenye ilikuwa inatoka ku baraza yenye kuongoza. Kwa hiyo, Yehova alibariki makutaniko na kulikuwa ongezeko.—Mdo. 8:1, 14, 15; 15:22-31; 16:4, 5; Ebr. 13:17.
2 Kisha mitume kufa, kulitokea uasi-imani mukubwa sana. (2 Te. 2:3-12) Kama vile Yesu alitabiri mu mufano wake wa ngano na magugu, magugu (Wakristo wa uongo) ilipandwa katika ngano (Wakristo watiwa-mafuta). Kwa miaka mingi, vile vikundi viliachwa vikomalie pamoya mupaka wakati ya mavuno, ni kusema, “umalizio wa mupangilio wa mambo.” (Mt. 13:24-30, 36-43) Mu ile kipindi kulikuwa Wakristo watiwa-mafuta wenye walikubaliwa na Yesu, lakini hakukuwa baraza yenye kuongoza wala njia yenye kujulikana wazi hapa ku dunia yenye Yesu alikuwa natumia ili kuongoza wafuasi wake. (Mt. 28:20) Lakini, Yesu alitabiri kama mambo itabadilika wakati ya mavuno.
3 “Ni nani kwa kweli mutumwa muaminifu na mwenye busara?” Kisha kuuliza ile ulizo, Yesu Kristo alitoa mufano wenye ulikuwa sehemu ya “alama” yenye inahusu “umalizio wa mupangilio wa mambo.” (Mt. 24:3, 42-47) Alionyesha kama ule mutumwa muaminifu atakuwa na kazi mingi ya kupatia watu wa Mungu chakula ya kiroho “kwa wakati wenye kufaa.” Wakati ya mitume, Yesu hakutumia tu mutu moya ili kuongoza, lakini alitumia kikundi ya wanaume. Na leo, mu hii wakati ya umalizio wa mupangilio wa mambo, mutumwa muaminifu mwenye Yesu iko natumia haiko mutu moya.
“MUTUMWA MUAMINIFU NA MWENYE BUSARA” NI NANI?
4 Yesu aliweka nani njo akuwe anapatia wafuasi wake chakula? Ni wazi kwamba iko natumia Wakristo watiwa-mafuta wenye kuwa ku dunia. Biblia inawaita “ukuhani wa kifalme” wenye kuwa na daraka ya “‘kutangaza kotekote sifa za muzuri zaidi’ za Ule mwenye aliwaita kutoka katika giza kuingia katika mwangaza wake wa ajabu.” (1 Pe. 2:9; Mal. 2:7; Ufu. 12:17) Mutumwa muaminifu anafanyizwa na Wakristo wote watiwa-mafuta? Hapana. Kupitia muujiza, Yesu alipatia chakula wanaume 5000 hivi, bila kuhesabia wanamuke na watoto. Kwanza alipatia wanafunzi wake ile chakula, na wanafunzi wakaipatia wale watu wengi. (Mt. 14:19) Alitumia watu kidogo ili kukulisha watu wengi. Na ni vile iko nafanya leo ili kupatia watu chakula ya kiroho.
5 Kwa hiyo, “musimamizi-nyumba muaminifu, mwenye busara,” anafanyizwa na kikundi kidogo ya ndugu watiwa-mafuta wenye wako na daraka ya kutayarisha na kupatia watu chakula ya kiroho wakati ya kuwapo kwa Kristo. (Lu. 12:42) Mu hizi siku za mwisho, ndugu watiwa-mafuta wenye wanafanyiza “mutumwa muaminifu na mwenye busara” wanatumika pamoya ku makao yetu makubwa. Na ni wale ndugu njo wenye wanafanyiza Baraza Yenye Kuongoza ya Mashahidi wa Yehova.
6 Kristo iko natumia ile baraza ili ichapishe habari zenye kuzungumuzia kutimizwa kwa unabii mbalimbali wa Biblia, na ili kutupatia miongozo kwa wakati yenye kufaa juu ya namna ya kutumikisha mu maisha yetu ya kila kila siku kanuni zenye kuwa mu Biblia. Tunapataka ile chakula ya kiroho kupitia makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10; Gal. 6:16) Zamani, mutumwa mwenye kutumainiwa, ao musimamizi-nyumba alikuwa nasimamia mambo mingi ya mu nyumba. Vilevile, mutumwa muaminifu na mwenye busara iko na daraka ya kusimamia nyumba ya imani. Tena, iko nasimamia mali ya kimwili ya tengenezo, kazi ya kuhubiri, programu za mikusanyiko, kuchapisha vichapo vyenye kutegemea Biblia na kuweka waangalizi ili watumikie mu madaraka mbalimbali mu tengenezo. Ile mambo yote ni kwa faida ya ‘watumishi wa nyumbani.’—Mt. 24:45.
7 Sasa, ‘watumishi wa nyumbani’ ni nani? Kwa kifupi, ni wale wote wenye wanakulishwa. Ku mwanzo, watumishi wote wa nyumbani walikuwa watiwa-mafuta. Kisha, kundi kubwa ya “kondoo wengine” ikajiunga nao na kuwa sehemu ya watumishi wa nyumbani. (Yoh. 10:16) Vile vikundi mbili vinakulaka chakula ya kiroho yenye mutumwa muaminifu anatayarishaka.
8 Mu kipindi ya taabu kubwa, wakati Yesu atakuya kutangaza hukumu na kuharibu watu wabaya, atamuweka mutumwa muaminifu “juu ya mali zake zote.” (Mt. 24:46, 47) Wale wote wenye wanafanyiza mutumwa muaminifu watapata zawadi yao mbinguni. Wao pamoya na wenzao wote, ni kusema, watu 144000, watatawala pamoya na Kristo kule mbinguni. Ile wakati hakutakuwa tena mutumwa muaminifu na mwenye busara hapa ku dunia. Lakini, Yehova na Yesu wataongoza wale wenye watatawaliwa na Ufalme wa Kimasiya hapa ku dunia kupitia wanaume wenye watawekwa ili watumike kama “wakubwa.”—Zb. 45:16.
JUU YA NINI ‘TUKUMBUKE WALE WENYE WANAONGOZA’?
9 Kuko sababu mingi zenye zinafanya ‘tukumbuke wale wenye wanaongoza’ na kuonyesha kama tunawatumainia. Juu ya nini kufanya vile ni jambo ya lazima? Mutume Paulo alisema hivi: “Wanaendelea kuwalinda ninyi kama wale wenye watatoa hesabu, ili wafanye vile kwa furaha, hapana kwa kusumbuka, kwa maana jambo hilo lingewaumiza ninyi.” (Ebr. 13:17) Ni lazima tunyenyekee na kutii muongozo wa wale wenye kutuongoza juu wanaendelea kutulinda kiroho na kutusaidia tukuwe mu hali ya muzuri.
10 Mu 1 Wakorinto 16:14, Paulo alisema hivi: “Mambo yote yenye munafanya, yafanywe kwa upendo.” Maamuzi yote yenye inakamatwa kwa ajili ya watu wa Mungu inategemea ile sifa ya maana sana, ni kusema, upendo. Kuhusu upendo, 1 Wakorinto 13:4-8 inasema hivi: “Upendo ni wenye uvumilivu na wenye fazili. Upendo hauna wivu. Haujisifu, haujivune, haujiendeshe bila adabu, hautafute faida zake wenyewe, haukasirike haraka. Hauweke hesabu ya ubaya. Haufurahie ukosefu wa haki, lakini unafurahi pamoja na kweli. Unafunika mambo yote, unaamini mambo yote, unatumaini mambo yote, unavumilia mambo yote. Upendo haushindwe hata kidogo.” Wale wenye kuongoza wanakamataka maamuzi kwa upendo na kwa faida ya watumishi wa Yehova. Njo maana, namna wako natuongoza haipaswe kutuogopesha. Tena, tukumbuke kama ile ni njia yenye Yehova anatumia ili kuonyesha kama anatupenda.
Ni jambo ya maana tujinyenyekeze kwa wale wenye kuongoza, juu wanaendelea kutuhangaikia ili tukuwe na hali ya muzuri ya kiroho
11 Wakati ya mitume, Yehova alitumia watu wenye hawakamilike ili kuongoza watumishi wake. Na njo vile iko nafanya leo. Mu Biblia muko mifano yenye kuonyesha kama, zamani sana Yehova alikuwa natumia watu wenye hawakamilike ili kutimiza mapenzi yake. Kwa mufano, Noa alijenga safina na kuhubiria watu juu ya uharibifu wenye ulitokea mu ile wakati yake. (Mwa. 6:13, 14, 22; 2 Pe. 2:5) Musa alichaguliwa ili kutosha watu wa Yehova kule Misri. (Kut. 3:10) Roho ya Mungu iliongoza wanaume wenye hawakamilike ili waandike Biblia. (2 Ti. 3:16; 2 Pe. 1:21) Hata kama leo Yehova iko natumia wanaume wenye hawakamilike ili kuongoza kazi ya kuhubiri na ya kufanya wanafunzi, ile haipaswe kufanya tukose kutumainia tengenezo yake. Tofauti na ile, tunatiwa moyo juu tunajua kama hakuna kitu inaweza kufanyika mu tengenezo bila Yehova kusaidia. Mambo yenye mutumwa muaminifu anafanyaka wakati ya magumu na mu hali mbalimbali, inatuhakikishia kama ni roho ya Mungu njo iko namuongoza. Leo, sehemu yenye kuonekana ya tengenezo ya Yehova iko napata baraka mingi sana. Njo maana, tunapaswa kuiunga mukono na kuitumainia kwa moyo wote.
NAMNA YA KUONYESHA KAMA TUNATUMAINIA TENGENEZO
12 Wale wenye kuwa na madaraka mu kutaniko, wanaonyesha kama wanatumainia tengenezo ya Yehova, kwa kutimiza kwa uaminifu na kwa furaha mambo yenye wanaombwa kufanya. (Mdo. 20:28) Siye watangazaji wa Ufalme, tunafanyaka kazi ya kuhubiri kwa bidii nyumba kwa nyumba, kurudilia watu, na kuongoza mafunzo ya Biblia. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Juu chakula ya muzuri yenye mutumwa muaminifu iko natoa ituletee faida kabisa, tunapaswa kutayarisha mikutano, kuenda ku mikutano ya kutaniko, mikusanyiko ya muzunguko na pia ya eneo. Tunatianaka moyo sana wakati ya mikutano na mikusanyiko yetu pamoya na ndugu na dada zetu.—Ebr. 10:24, 25.
13 Wakati tunatoa michango kama vile makuta na mambo ingine, tunaonyesha kama tunatumainia tengenezo. (Mez. 3:9, 10) Wakati ndugu zetu wako na lazima ya musaada ya kimwili, tunawasaidia bila kuchelewa. (Gal. 6:10; 1 Ti. 6:18) Tunafanya vile juu tunapenda ndugu na dada zetu, na juu tunapenda kumushukuru Yehova na tengenezo yake kwa mambo yote yenye wako natufanyia.—Yoh. 13:35.
14 Tena, tunaonyesha kama tunatumainia tengenezo ya Yehova kwa kuunga mukono maamuzi yote yenye ile tengenezo inakamata. Tunaweza kufanya vile kwa kufuata kwa unyenyekevu miongozo yenye waangalizi wa mizunguko na wazee wengine wa kutaniko wako natupatia. Wale ndugu wako kati ya “wale wenye wanaongoza.” Kwa hiyo, tunapaswa kuwatii kwa unyenyekevu. (Ebr. 13:7, 17) Hata kama hatuelewe muzuri juu ya nini walikamata maamuzi fulani, tunapaswa kuiunga mukono, juu tunajua kama itatuletea furaha ya wakati murefu. Na Yehova atatubariki kama tunatii Neno yake na tengenezo yake. Kwa kufanya vile, tunaonyesha kama tunatii kabisa Bwana wetu, Yesu Kristo.
15 Tuko na sababu za muzuri za kutumainia mutumwa muaminifu na mwenye busara. Shetani, mungu wa hii mupangilio ya mambo iko anajikaza sana ili kuchafua jina ya Yehova na tengenezo yake. (2 Ko. 4:4) Usiangukie mu mitego ya Shetani! (2 Ko. 2:11) Anajua kama iko tu na “kipindi kifupi cha wakati” mbele atupwe mu abiso. Iko nafanya yake yote ili afanye watumishi wengi wa Yehova waache kumutumikia. (Ufu. 12:12) Hata kama Shetani iko naongeza bidii yake ya kufanya vile, tuendelee kumukaribia Yehova zaidi. Kwa hiyo basi, tumutumainie Yehova na njia yenye anatumia ili kuongoza watu wake leo. Tukifanya vile, familia yetu ya ndugu na dada itakuwa na umoja.