Namna Gani Tunaweza Kuonyesha Kwamba Tunamupenda Yehova?
“Tunaonyesha upendo, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.”—1 YOHANA 4:19.
NYIMBO: 56, 138
1, 2. Namna gani Yehova ametufundisha kumupenda?
NJIA nzuri zaidi yenye muzazi anaweza kutumia ili kufundisha watoto, ni kupitia mufano wake. Wakati anaonyesha kwamba anawapenda watoto wake, anawafundisha namna ya kuonyesha upendo. Hakuna mutu mwingine mwenye ametupenda sana kama Yehova, Baba yetu. Kwa hiyo, tunajua namna ya kuonyesha upendo “kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19.
2 Ni nini inaonyesha kwamba Yehova ‘ametupenda sisi kwanza’? Biblia inasema kwamba wakati tulikuwa ‘tungali watenda-zambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.’ (Waroma 5:8) Yehova, Baba yetu mwenye upendo, alimutoa Mwana wake kuwa zabihu ya ukombozi ili kutukomboa kutoka katika utumwa wa zambi na kifo. Zawadi hiyo yenye bei sana inatusaidia tumukaribie Yehova na kuonyesha kwamba tunamupenda. Yehova alituwekea mufano muzuri wa kuonyesha upendo, wakati alikubali Mwana wake akufe kwa ajili yetu. Kwa kufanya hivyo, alitufundisha kwamba tunapaswa kuonyesha upendo kwa kuhangaikia wengine na kuwaonyesha ukarimu.—1 Yohana 4:10.
3, 4. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tunamupenda Mungu?
3 Upendo ni sifa kubwa ya Yehova. Ndiyo sababu Yesu alisema kwamba amri ya maana zaidi ni: ‘Kumupenda Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.’ (Marko 12:30) Yehova anataka tumupende kwa ‘moyo wetu wote.’ Kwa hiyo, anachukia wakati tunapenda sana mutu ao kitu fulani kuliko yeye. Lakini hatupaswe kujisikia tu kuwa tunamupenda Yehova. Yehova anataka pia tumupende kwa ‘akili yetu yote na kwa nguvu zetu zote.’ Ni kusema, tunapaswa kuonyesha kwamba tunamupenda kupitia namna yetu ya kuwaza na matendo yetu.—Soma Mika 6:8.
4 Kwa hiyo, tunapaswa kutumia uwezo wetu wote na vitu vyote vyenye tuko navyo ili kuonyesha kwamba tunamupenda Yehova. Tunaonyesha kwamba tunamupenda kabisa wakati tunamutia pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu. Katika habari yenye ilitangulia, tulizungumuzia njia ine zenye Yehova anatumia ili kuonyesha kwamba anawapenda sana watoto wake. Tuzungumuzie sasa namna tunaweza kutia nguvu upendo wetu kwa Yehova, na kuonyesha kwamba tunamupenda.
UMUONYESHE YEHOVA SHUKRANI
5. Wakati tunafikiria mambo yote yenye Yehova ametufanyia, hilo linatusukuma tufanye nini?
5 Kwa kawaida wakati mutu fulani anakupatia zawadi, unamuonyesha shukrani. Pia, kwa sababu unaona zawadi hiyo kuwa ya lazima, unaitumia. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: ‘Kila zawadi njema na kila tuzo [zawadi] kamilifu inatoka juu, kwa maana inashuka kutoka kwa Baba wa mianga [nuru] ya mbinguni, naye habadilike, kama kugeuka kwa kivuli.’ (Yakobo 1:17) Tuko wenye shukrani sana kwa sababu Yehova anatupatia kila kitu chenye tuko nacho lazima ili tuishi na tukuwe na furaha. Tunaelewa kwamba anatupenda sana, na tunataka kumuonyesha kwamba sisi pia tunamupenda. Je, unajisikia hivyo?
6. Waisraeli walipaswa kufanya nini ikiwa walipenda Yehova aendelee kuwabariki?
6 Yehova aliwatolea Waisraeli vitu vingi vizuri. Aliwaongoza kwa miaka mingi kupitia sheria zake, na aliwapatia vitu vyote vyenye walikuwa navyo lazima ili kuishi. (Kumbukumbu la Torati 4:7, 8) Kwa hiyo, Waisraeli walipaswa kuonyesha shukrani yao kwa Yehova kwa kutii sheria hizo. Kwa mufano, wakati wa kumutolea Yehova zabihu, walipaswa kumutolea matunda mazuri zaidi “kati ya matunda ya kwanza yaliyoiva ya udongo.” (Kutoka 23:19) Waisraeli walijua kwamba Yehova angeendelea kuwabariki ikiwa tu wangemutii na kumutolea kulingana na uwezo wao wote.—Soma Kumbukumbu la Torati 8:7-11.
7. Namna gani tunaweza kutumia vitu vyetu vya lazima ili kumuonyesha Yehova kwamba tunamupenda?
7 Sisi pia tunaweza kuonyesha kwamba tunamupenda Yehova kwa kumutolea ‘vitu vyetu vyenye samani [vya lazima].’ (Methali 3:9) Tutafanya hivyo wakati tunatumia vitu vyenye tuko navyo ili kumuheshimu. Kwa mufano, tunaweza kutoa michango ili kutegemeza kazi ya Ufalme katika kutaniko letu na katika dunia yote. Iwe tuko na vitu vingi ao hapana, sisi wote tunaweza kutumia vitu vyenye tuko navyo ili kuonyesha kwamba tunamupenda Yehova. (2 Wakorintho 8:12) Lakini, kuna njia zingine zenye tunaweza kutumia ili kuonyesha kwamba tunamupenda Yehova.
Wakati tunamutegemea Yehova kabisa, tunamuonyesha kwamba tunamupenda sana
8, 9. Tunatumia njia ingine gani ili kumuonyesha Yehova kwamba tunamupenda? Ndugu Mike na familia yake walifanya nini?
8 Yesu alitufundisha tuendelee kutafuta kwanza Ufalme wa Mungu, na tusihangaikie chakula na mavazi. Baba yetu anaahidi kwamba atatimiza mahitaji yetu. (Mathayo 6:31-33) Tunamutegemea Yehova na tunajua kwamba atatimiza ahadi yake. Kwa kawaida, wakati tunapenda mutu sana, tunamutumainia pia. Kwa kweli, wakati tunamutegemea Yehova kabisa, tunamuonyesha kwamba tunamupenda sana. (Zaburi 143:8) Kwa hiyo, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Mipango yangu na namna ninatumia wakati na nguvu zangu, inaonyesha kwamba ninamupenda kabisa Yehova? Ninamutegemea Yehova kila siku ili atimize mahitaji yangu?’
9 Ndugu Mike na familia yake walimutegemea Yehova. Wakati ndugu Mike alikuwa kijana, alikuwa na tamaa ya kuenda kuhubiri katika inchi ingine. Aliendelea kuwa na tamaa hiyo hata kisha kuoa na kuzaa watoto wawili. Wakati yeye na familia yake walisoma habari za ndugu na dada fulani wenye walitumikia mahali penye kuwa lazima kubwa ya wahubiri, waliamua kuishi maisha mepesi. Waliuzisha nyumba yao na kuhamia katika nyumba ndogo. Ndugu Mike aliamua pia kupunguza kazi yake. Mwishowe, yeye na familia yake walihamia katika inchi ingine, na walifurahia sana kazi ya kuhubiri. Ndugu Mike alisema hivi: “Tulijionea kwamba maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:33 ni ya kweli.”
UFIKIRI SANA JUU YA MAMBO YENYE YEHOVA ANAKUFUNDISHA
10. Kama Mufalme Daudi, sababu gani tunapaswa kufikiri sana juu ya mambo yenye tunajifunza juu ya Yehova?
10 Mufalme Daudi aliandika hivi: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu; nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.” Kisha aliongeza hivi: ‘Sheria ya Yehova ni kamilifu, inarudisha nafsi. Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, kinamufanya asiye na uzoefu akuwe na hekima.’ Wakati Daudi aliendelea kufikiri sana juu ya sheria za Yehova zenye hekima na juu ya vitu vya ajabu vyenye aliumba, hilo lilimusaidia amukaribie Yehova zaidi na kumuonyesha kwamba anamupenda. Daudi alisema hivi: ‘Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yakuwe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova Mwamba wangu na Mukombozi wangu.’—Zaburi 19:1, 7, 14.
11. Tunaweza kutumikisha namna gani ujuzi wenye Yehova anatupatia ili kuonyesha kwamba tunamupenda? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)
11 Leo, Yehova anatufundisha mambo mengi juu yake, mipango yake, vitu vyenye aliumba, na Neno lake. Ulimwengu huu unachochea watu waendelee kusoma, lakini mara nyingi masomo ya juu inafanya watu wasimupende Mungu. Tofauti na hilo, Yehova yeye anapenda tupate ujuzi, na anatusaidia tukuwe na hekima. Anapenda tutumikishe mambo yenye tunajifunza ili ituletee faida sisi wenyewe na pia watu wengine. (Methali 4:5-7) Kwa mufano, anapenda tusaidie wengine wapate “ujuzi sahihi wa kweli” ili waokolewe. (1 Timotheo 2:4) Wakati tunajikaza kufundisha watu juu ya Ufalme wa Mungu na mambo yenye Ufalme huo utafanyia wanadamu, tunaonyesha kwamba tunamupenda Yehova na tunapenda watu wengine.—Soma Zaburi 66:16, 17.
12. Dada moja kijana alisema nini juu ya zawadi yenye Yehova alimutolea?
12 Vijana pia wanaweza kufikiri sana juu ya mambo yote yenye Yehova amewapatia na kuwafundisha. Dada Shannon anaendelea kukumbuka namna alijisikia kwenye mukusanyiko fulani wenye alihuzuria pamoja na mudogo yake mwanamuke; wakati huo yeye alikuwa na miaka 11, na mudogo yake miaka 10. Kwenye Mukusanyiko huo wa Wilaya wenye kichwa “Ujitoaji wa Kimungu,” dada Shannon, mudogo yake, na vijana wengine wote waliombwa kukaa nafasi fulani ya pekee. Mwanzoni, alikuwa na wasiwasi. Kisha akashangaa kuona kwamba vijana wote walipewa kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Zawadi hiyo nzuri ilimufanya ajisikie namna gani juu ya Yehova? Anasema hivi: “Ni wakati huo ndio nilitambua kwamba Yehova iko kabisa na kwamba ananipenda sana. Tunafurahi sana kwa sababu Yehova, Mungu wetu mukubwa, iko tayari kututolea zawadi nzuri zaidi na kamilifu kama hizo!”
UKUBALI NIZAMU YA YEHOVA
13, 14. Tunapaswa kutenda namna gani wakati Yehova anatupatia nizamu, na sababu gani?
13 Biblia inatukumbusha kwamba wale ‘ambao Yehova anawapenda, anawakaripia, kama vile baba anamukaripia mwana anayemufurahia.’ (Methali 3:12) Wakati tunakubali nizamu ya Yehova na kumuacha atuzoeze, tunajifunza kufanya mambo mema na tunapata amani. Lakini, ‘hakuna nizamu inayoonekana kwa sasa kuwa yenye shangwe, bali [lakini] ni yenye kuhuzunisha.’ (Waebrania 12:11) Hata hivyo, tunapaswa kutenda namna gani wakati Yehova anatupatia nizamu? Tusizarau hata kidogo mashauri yenye Yehova anatutolea ao kuendelea kukasirika wakati hatufurahie mashauri yenye tunapewa. Tunamusikiliza Yehova na kufanya mabadiliko yenye anatuomba tufanye kwa sababu tunamupenda.
Wakati tunakuwa tayari kufanya mabadiliko ili kumufurahisha Yehova, tunaonyesha kwamba tunamupenda kabisa
14 Wayahudi wengi hawakumusikiliza Yehova katika siku za nabii Malaki. Hawakuhangaikia kujua ikiwa Yehova atakubali zabihu zao ao hapana. Kwa hiyo, Yehova aliwatolea mashauri mazito juu ya zabihu hizo. (Soma Malaki 1:12, 13.) Yehova aliwashauria mara nyingi, lakini walikataa kumusikiliza. Kwa hiyo, aliwaambia hivi: ‘Nitaleta juu yenu laana, na mimi nitazilaani baraka zenu.’ (Malaki 2:1, 2) Hilo linaonyesha wazi kwamba ikiwa tunaendelea kukataa mashauri ya Yehova ao kuizarau, tutapoteza urafiki wetu pamoja naye.
Fikiria mambo yenye Yehova anapenda kuliko kufikiria ile yenye kupendwa na watu wengi wa ulimwengu (Ona fungu la 15)
15. Tunapaswa kuepuka mawazo gani?
15 Ulimwengu wa Shetani unachochea watu wakuwe na kiburi na kujipenda wenyewe. Watu wengi hawapendi kushauriwa ao kuambiwa mambo yenye wanapaswa kufanya. Na wengine wanasikiliza mashauri kwa sababu tu wanapaswa kufanya hivyo. Hatupaswe kuwa kama watu hao. Biblia inatushauri ‘tuache kufanyizwa kulingana na mufumo huu wa mambo.’ Lakini, tunapaswa kuelewa mambo yenye Yehova anatuomba na kufanya mambo yenye kumufurahisha. (Waroma 12:2) Anatumia tengenezo lake ili kututolea mashauri kwa wakati wenye kufaa. Kwa mufano, tunapata mashauri juu ya namna wanaume na wanawake wanapaswa kutendeana, namna ya kuchagua marafiki, na namna ya kuamua mambo ya kufanya wakati tunapumuzika ao kujifurahisha. Wakati tunakuwa tayari kukubali nizamu ya Yehova na kufanya mabadiliko yenye anatuomba ili kumufurahisha, tunaonyesha kwamba tunapendezwa na muongozo wake na kwamba tunamupenda kabisa.—Yohana 14:31; Waroma 6:17.
UTEGEMEE MUSAADA NA ULINZI WA YEHOVA
16, 17. (a) Sababu gani tunapaswa kutafuta kujua mawazo ya Yehova mbele ya kuchukua maamuzi? (b) Kuliko kumutegemea Yehova, Waisraeli walifanya nini?
16 Watoto wadogo wanategemea wazazi wao ili wawasaidie na kuwalinda. Hata watu wakubwa wanaweza kuomba wazazi wao musaada. Wanajua kwamba, hata kama wanapaswa kuchukua maamuzi yao wenyewe, wazazi wao wanaweza kuwatolea mashauri mazuri. Yehova, Baba yetu, anatuacha tuchukue maamuzi yetu sisi wenyewe. Lakini, kwa sababu tunamutegemea na kumupenda kabisa, kila mara tunamuomba musaada na kujikaza kujua mawazo yake mbele ya kuchukua maamuzi yoyote. Ikiwa tunamutegemea Yehova, atatupatia roho yake takatifu ili itusaidie kufanya mambo mema.—Wafilipi 2:13.
17 Katika siku za nabii Samweli, Waisraeli walipigana vita na Wafilisti, lakini Waisraeli walishindwa. Kuliko kutafuta mashauri ya Yehova, walisema hivi: ‘Tujichukulie kutoka Shilo sanduku la agano la Yehova, ili likuje katikati yetu na kutuokoa kutoka mukononi mwa adui zetu.’ Matokeo ilikuwa nini? Biblia inasema hivi: ‘Mauaji hayo ikakuwa makubwa sana, hivi kwamba katika Israeli wakaanguka watu 30000 wenye kuenda kwa miguu. Nalo Sanduku la Mungu likatekwa [likanyanganywa].’ (1 Samweli 4:2-4, 10, 11) Waisraeli waliwaza kwamba ikiwa wanabeba tu sanduku la agano kwenye vita, Yehova angewasaidia na kuwalinda. Lakini hawakuomba musaada wa Yehova ao kujaribu kutafuta mashauri yake. Walifanya mambo yenye waliwaza kuwa ni sawa, na walipatwa na matokeo mabaya sana.—Soma Methali 14:12.
18. Kuhusu kumutegemea Yehova, Biblia inakufundisha nini?
18 Muandikaji mumoja wa zaburi mwenye alimupenda sana Yehova na kumutegemea aliandika hivi: ‘Mungojee Mungu, kwa maana bado nitamusifu kuwa ndiye Wokovu wangu Mukubwa. Mungu wangu, nimekata tamaa. Ndiyo sababu ninakukumbuka.’ (Zaburi 42:5, 6) Je, wewe pia unajisikia hivyo juu ya Yehova? Je, unajisikia kuwa karibu naye na unamutegemea? Kufanya hivyo, kutakusaidia ujifunze kumutegemea zaidi. Biblia inatuambia hivi: ‘Umutegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Umutambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.’—Methali 3:5, 6.
19. Utafanya nini ili kumuonyesha Yehova kwamba unamupenda?
19 Yehova ametufundisha namna ya kumupenda kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza. Tuendelee basi kufikiri sana juu ya mambo mengi yenye ametufanyia na juu ya namna anaonyesha kwamba anatupenda sana. Na tuendelee kumuonyesha kwamba tunamupenda kwa moyo wetu wote, kwa nafsi yetu yote, kwa akili yetu yote, na kwa nguvu zetu zote.—Marko 12:30.