SURA YA 44
Yesu Ananyamazisha Upepo Mukali Kwenye Bahari
MATAYO 8:18, 23-27 MARKO 4:35-41 LUKA 8:22-25
YESU ANANYAMAZISHA UPEPO MUKALI KWENYE BAHARI YA GALILAYA
Yesu amekuwa na siku yenye mambo mengi na yenye kuchokesha. Wakati inakuwa mangaribi, anaambia wanafunzi wake hivi: “Tuvuke na kuenda upande mwingine wa bahari,” wenye kuwa ngambo ya bahari kutoka Kapernaumu.—Marko 4:35.
Pembeni ya Bahari ya Galilaya upande wa mashariki, kunapatikana eneo la Wagerasene. Eneo hilo linajulikana pia kwa jina la Dekapoli. Hata kama Wayahudi wengi wanaishi pia katika eneo hilo, miji ya Dekapoli inatawaliwa na desturi ya Kigiriki.
Watu wanajua kama Yesu anaondoka katika Kapernaumu. Inaonekana mashua zingine ziko karibu kuvuka bahari. (Marko 4:36) Kwa kweli, kule kwenye wanaenda haiko mbali. Bahari ya Galilaya iko kama ziwa (lac) kubwa yenye maji ambayo haina chumvi; iko na urefu wa kilometre 21 na upana wa kilometre 12. Lakini ni ya murefu kushuka chini.
Hata kama Yesu ni mwanaume mukamilifu, haishangaze kuona vile anachoka kwa sababu ya kazi yake yenye bidii. Kwa hiyo kisha kuondoka, analala sehemu ya nyuma ya mashua, anatia kichwa chake kwenye muto (oreiller), na kulala usingizi.
Wengi kati ya mitume wanajua muzuri kuendesha mashua, lakini safari yao haitakuwa mwepesi. Milima inawazunguka, na mara nyingi kunakuwa joto kwenye Bahari ya Galilaya. Wakati fulani, hewa yenye baridi sana yenye kutoka kwenye milima inashuka na nguvu yote mupaka kwenye bahari, na wakati inakutana na hewa yenye joto, inatokeza upepo mukali kwenye bahari. Na ni hivyo mambo yanakuwa. Kisha tu wakati kidogo, zoruba inaanza kupiga mashua. Na mashua “ikaanza kujaa maji na kuwa katika hatari.” (Luka 8:23) Lakini, Yesu anaendelea kulala!
Wanaume hao wenye kuongoza mashua wanatumika kwa bidii sana ili kuiongoza, wakitumia ufundi wao wa zamani wa kuongoza mashua wakati kuko upepo mukali. Lakini wakati huu mambo yako tofauti. Wanaogopa kufa, kwa hiyo wanamuamusha Yesu na kusema hivi: “Bwana, utuokoe, tuko karibu kufa!” (Matayo 8:25) Sasa wanafunzi wanaogopa kwamba watazama!
Wakati Yesu anaamuka, anaambia mitume hivi: “Sababu gani munaogopa sana, ninyi wenye imani kidogo?” (Matayo 8:26) Kisha Yesu anakemea upepo na bahari kwa kusema: “Nyamaza! Tulia!” (Marko 4:39) Upepo huo mukali unanyamaza na bahari inatulia. (Wakati Marko na Luka wanazungumuzia muujiza huu wenye kushangaza, wanaonyesha kwanza kama Yesu alituliza kimuujiza upepo, na kisha wanazungumuzia kukosa imani kwa wanafunzi wake.)
Wazia matokeo ya muujiza huo juu wanafunzi! Wametoka tu kuona namna bahari yenye upepo mukali inatulia kabisa. Hilo linawaogopesha sana. Wanaambiana hivi: “Kwa kweli huyu ni nani? Hata upepo na bahari vinamutii.” Na wanafika upande mwengine wa bahari kwa usalama. (Marko 4:41–5:1) Inawezekana mashua zingine zenye zilikuwa zinasafiri pia kwenye bahari hiyo ziliweza kurudia upande wa mangaribi mwa bahari.
Inatia moyo sana kujua kama Mwana wa Mungu iko na uwezo juu hali ya hewa! Wakati atakazia uangalifu wake wote juu ya dunia wakati wa utawala wake katika Ufalme wa mbinguni, watu wote wataishi katika usalama, kwa sababu hakutakuwa misiba ya asili yenye kuogopesha!