Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • lv sura 15 uku. 171-182
  • ‘Ona Mema kwa Ajili ya Kazi Yako Ngumu’

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • ‘Ona Mema kwa Ajili ya Kazi Yako Ngumu’
  • Mubaki “Katika Upendo wa Mungu”
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • MUFANYAKAZI MUKUBWA ZAIDI NA FUNDI WAKE WA KAZI
  • NAMNA YA KUONA MEMA KWA AJILI YA KAZI YETU NGUMU
  • KUTUMIA AKILI TUNAPOTAFUTA KAZI
  • TUWE NA MAONI YANAYOFAA KUHUSU KAZI
  • KUFANYA KAZI YA KUHUBIRI KWA BIDII
  • Ufurahie Kazi Yako
    Namna ya Kubakia Katika Upendo wa Mungu
  • Namna ya Kufurahia Kazi Ngumu
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Furahia Kazi Yako Ngumu
    Buku ya Mukutano Utumishi na Maisha ya Mukristo—2016
  • Kazi
    Amuka!—2015
Ona Habari Zaidi
Mubaki “Katika Upendo wa Mungu”
lv sura 15 uku. 171-182
Wanawake wenye kutumika sana katika inchi fulani ya Afrika

SURA YA 15

‘Ona Mema kwa Ajili ya Kazi Yako Ngumu’

‘Kila mutu aone mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu.’​—MHUBIRI 3:13.

1-3. (a) Watu wengi wanajisikia namna gani juu ya kazi wanayofanya? (b) Bibia inatutia moyo tuwe na mawazo ya namna gani juu ya kazi, na ni maulizo gani tutachunguza katika sura hii?

WATU wengi leo wanaona kazi kuwa muzigo. Kazi wanayofanya inawachukua saa nyingi na hawaifurahie, kwa hiyo, hawataki kuenda kazini kila siku. Kwa kuwa wanajisikia hivyo, ni vigumu kwao kujitoa kabisa ili kufanya kazi na pia ni vigumu kabisa kwao kupata furaha kutokana na kazi yao!

2 Biblia inatutia moyo tuwe na mawazo yanayofaa juu ya kazi ngumu. Inasema kama kazi na matunda yake ni zawadi. Sulemani aliandika hivi: ‘Kila mutu akule, ndiyo, akunywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndio zawadi ya Mungu.’ (Mhubiri 3:13) Yehova anatupenda na kila siku anatutakia mema, kwa hiyo, anataka tufurahie kazi yetu na tufaidike na matunda ya nguvu tulizotumia kufanya kazi. Ili tubaki katika upendo wake, tunapaswa kuona kazi kama anavyoiona na kufanya kazi kulingana na kanuni zake.—Mhubiri 2:24; 5:18.

3 Katika sura hii, tutapata majibu ya maulizo ine yafuatayo: Namna gani tunaweza kuona mema kwa ajili ya kazi yetu ngumu? Ni kazi za namna gani Wakristo hawawezi kufanya? Namna gani tunaweza kuonyesha usawaziko kati ya kazi ya kimwili na mambo ya kiroho? Na ni kazi gani iliyo ya maana zaidi ambayo tunapaswa kufanya? Mbele ya kuchunguza mambo hayo, tuzungumuzie kwanza mufano wa wafanyakazi wakubwa zaidi ya wote, ni kusema, Yehova Mungu na Yesu Kristo.

MUFANYAKAZI MUKUBWA ZAIDI NA FUNDI WAKE WA KAZI

4, 5. Namna gani Biblia inaonyesha kwamba Yehova ni mufanyakazi mwenye bidii?

4 Yehova ndiye Mufanyakazi Mukubwa zaidi. Andiko la Mwanzo 1:1 linasema hivi: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Wakati Mungu alimaliza kazi yake ya kuumba dunia na vitu vyote vilivyo ndani yake, alisema juu ya kazi hiyo kwamba ilikuwa nzuri sana. (Mwanzo 1:31) Hiyo inamaanisha alifurahia kabisa kazi yote aliyofanya kuhusu dunia. Bila shaka, Yehova, “Mungu mwenye furaha,” alifurahi sana kufanya kazi na kupata matokeo mazuri katika kazi yake.—1 Timotheo 1:11.

5 Mungu wetu ni mufanyakazi mwenye bidii; na bado anaendelea kufanya kazi. Miaka mingi sana kisha kumaliza kazi ya kuumba dunia na vitu vyote vilivyo ndani yake, Yesu alisema: ‘Baba yangu anaendelea kufanya kazi mupaka sasa’ (Yohana 5:17) Baba anaendelea kufanya kazi gani? Bila shaka, Yehova, ameendelea kufanya kazi ya kuwaongoza wanadamu na kuwatunza. Ametokeza “kiumbe kipya,” ni kusema, Wakristo waliozaliwa kwa roho takatifu ambao watatawala pamoja na Yesu mbinguni. (2 Wakorintho 5:17) Ameendelea kutumika ili kusudi lake kuelekea wanadamu litimizwe; kusudi hilo ni kwamba wale wanaomupenda wapate uzima wa milele katika dunia mupya. (Waroma 6:23) Bila shaka, Yehova anafurahi sana anapoona matunda ya kazi yake. Mamilioni ya watu wamekubali ujumbe wa Ufalme; wamevutwa na Mungu, na wamebadilisha maisha yao ili waendelee kubaki katika upendo wake.—Yohana 6:44.

6, 7. Ni nini inayoonyesha kama Yesu ni mufanyakazi mwenye bidii tangu zamani?

6 Yesu pia ni mufanyakazi mwenye bidii tangu zamani. Kabla ya kuja duniani, alikuwa “stadi [ao fundi] wa kazi” wa Mungu; wakati wa kuumbwa kwa vitu vyote “mbinguni na duniani.” (Methali 8:22-31; Wakolosai 1:15-17) Yesu aliendelea kufanya kazi kwa bidii alipokuwa hapa duniani. Katika ujana wake, alijifunza kazi ya ujenzi, na akajulikana kuwa “seremala.”a (Marko 6:3) Useremala ni kazi inayoomba kuwa na nguvu na ufundi mbalimbali, na iliomba hivyo kwa sababu wakati huo hawakuwa na mashini za kupasua mbao, mahali pa kununulia vitu vya kazi hiyo kama leo, ao mashini zinazotumia umeme (kura). Wazia sasa namna Yesu alivyokuwa anaenda kutafuta mbao; labda alikuwa akikata miti na kuiburuta mupaka mahali pa kazi! Wazia namna alikuwa akijenga nyumba; alikuwa akitayarisha mbao na kuzipandisha ili kujenga paa ya nyumba, alikuwa akitengeneza milango, na vifaa vingine vya kutia ndani ya nyumba! Bila shaka, Yesu alisikia furaha ambayo mutu anasikia anapofanya kazi nzuri kwa bidii na kwa ufundi.

7 Bidii ya Yesu juu ya kazi ilijulikana sana katika kazi ya kuhubiri. Kwa miaka mitatu na nusu, alijitoa sana kwa kazi hiyo ya maana sana. Kwa kuwa alitaka watu wengi wasikie habari aliyokuwa anahubiri, hakupoteza wakati; alikuwa anaamuka mapema na kuendelea kufanya kazi mupaka usiku sana. (Luka 21:37, 38; Yohana 3:2) Alikuwa anatembea ‘kutoka jiji mupaka jiji na kutoka kijiji mupaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Luka 8:1) Yesu alitembea kwa miguu maelfu ya kilometre, katika barabara zenye mavumbi ili kuwapelekea watu habari njema.

8, 9. Namna gani Yesu aliona mema kwa ajili ya kazi yake ngumu?

8 Je, Yesu aliona mema kwa ajili ya kazi yake ngumu katika mahubiri? Ndiyo! Alipanda mbegu za kweli ya Ufalme, na kuacha mashamba yenye kuwa tayari kwa mavuno. Kufanya kazi ya Mungu kulimutia nguvu na kulimutegemeza hivi kwamba alikubali kujinyima kula chakula ili atimize kazi hiyo. (Yohana 4:31-38) Wazia furaha aliyokuwa nayo mwishoni mwa kazi yake hapa duniani, wakati alipomuambia Baba yake hivi: ‘Nimekutukuza katika dunia, nimemaliza kazi ambayo umenipata niifanye.’—Yohana 17:4.

9 Ni wazi kwamba Yehova na Yesu ndio mifano mizuri kabisa ya watu wanaoona mema kwa ajili ya kazi yao ngumu. Upendo tulio nao kwa Yehova utatusukuma tuwe “waigaji wa Mungu.” (Waefeso 5:1) Upendo tulio nao kwa Yesu utatusukuma ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Petro 2:21) Sasa, namna gani sisi pia tunaweza kuona mema kwa ajili ya kazi yetu ngumu?

NAMNA YA KUONA MEMA KWA AJILI YA KAZI YETU NGUMU

Mwanaume anasafisha madirisha na mwanamuke anatumika katika biro

Kutumikisha kanuni za Biblia kunaweza kukusaidia kuona mema katika kazi yako nguvu

10, 11. Ni nini inayoweza kutusaidia kuwa na mawazo mazuri juu ya kazi yetu ya kimwili?

10 Wakristo wa kweli wanafanya pia kazi za kimwili. Tunapenda kazi yetu ituletee furaha na kutosheka, lakini inaweza kuwa vigumu ikiwa tunafanya kazi fulani ambayo haitupendeze. Kwa hiyo, inafaa kufanya nini ili kuona mema kwa ajili ya kazi yetu?

11 Inafaa kuwa na mawazo mazuri. Labda hatuna uwezo wa kubadilisha hali yetu, lakini tunaweza kubadilisha mawazo yetu. Kufikiria sana mawazo ya Mungu juu ya kazi kunaweza kutusaidia kuwa na mawazo mazuri kuhusu kazi. Kwa mufano, ikiwa wewe ni baba wa familia, kumbuka kwamba kazi yako, hata ikiwa ni ya hali ya chini namna gani, ndio inayokusaidia kutimizia familia yako mahitaji ya kimwili. Kutunza familia yako hivyo si jambo ndogo machoni pa Mungu. Neno lake linasema kwamba mutu ambaye hatimizie watu wa familia yake mahitaji yao ‘ni mubaya kuliko mutu asiye na imani,’ ao mutu ambaye amemukana Yehova (1 Timotheo 5:8) Ikiwa unatambua kama kazi yako inakusaidia kutimiza daraka hilo ulilopewa na Mungu, jambo hilo linaweza kukusaidia ufurahie kazi yako na utosheke, hayo ni mambo ambayo wafanyakazi wenzako hawana.

12. Sababu gani tunaweza kusema kama kufanya kazi kwa bidii na kuwa mwenye kuaminika kunaleta faida?

12 Inafaa kuwa na bidii na kuwa mutu mwenye kuaminika. Tunaweza kuwa na matokeo mazuri katika kazi yetu ikiwa tunafanya kazi kwa bidii na kujifunza kuifanya vizuri. Mara nyingi, wafanyakazi wenye bidii na wanaojua kazi vizuri wanapendwa na mabwana wao wa kazi. (Methali 12:24; 22:29) Kwa kuwa sisi ni Wakristo wa kweli, tunapaswa pia kuwa watu wenye kuaminika katika kazi yetu; hatupaswe kuiba feza, vyombo vya kazi, ao kuiba saa za kutumika tulizosikilizana na bwana wa kazi. (Waefeso 4:28) Kama vile tulivyojifunza katika Sura ya 14, kuwa mutu mwenye kuaminika kunaleta faida nyingi. Mara nyingi, watu wanamuaminia mufanyakazi anayejulikana kuwa si mudanganyifu. Na iwe bwana wa kazi anatambua ao hatambue kama sisi ni wafanyakazi wa bidii, hata hivyo, tunaweza kufurahi kwa sababu tuna ‘zamiri nyoofu [ao safi]’ na tunajua kama tunamupendeza Mungu tunayemupenda.—Waebrania 13:18; Wakolosai 3:22-24.

13. Mwenendo wetu muzuri kwenye kazi unaweza kuwa na matokeo gani?

13 Inafaa kujua kwamba mwenendo wetu unaweza kumutukuza Mungu. Tunapokuwa na mwenendo muzuri wa Kikristo mahali pa kazi, bila shaka, wengine wanaona jambo hilo. Matokeo yanaweza kuwa nini? Kwa kufanya hivyo, tunaweza ‘kulipamba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu.’ (Tito 2:9, 10) Ndiyo, mwenendo wetu muzuri unaweza kuwasaidia wengine waone uzuri wa ibada yetu, na hivyo wavutiwe nayo. Wazia furaha ambayo unaweza kusikia ikiwa mufanyakazi mwenzako anakubali kweli kwa sababu ya mufano wako muzuri kwenye kazi! Na jambo la maana zaidi ni hili: Je, kuna jambo lolote linaloweza kukufurahisha zaidi kuliko kujua kama mwenendo wako muzuri unamutukuza Yehova na kufanya moyo wake ufurahi?—Methali 27:11; 1 Petro 2:12.

KUTUMIA AKILI TUNAPOTAFUTA KAZI

14-16. Mbele ya kukubali kazi fulani, ni maulizo gani mawili ya maana tunapaswa kujiuliza?

14 Biblia haitupatie oroza (liste) ya kazi za kimwili ambazo Wakristo wanapaswa kukubali ao kukataa. Lakini hiyo haimaanishe kwamba tunaweza kukubali kazi yoyote, hata iwe ya namna gani. Maandiko yanaweza kutusaidia kuchagua kazi nzuri na iliyo sawa, inayomupendeza Mungu na kuepuka ile isiyomupendeza. (Methali 2:6) Mbele ya kukubali kazi fulani, kuna maulizo mawili ya lazima tunayopaswa kujiuliza.

15 Je, kazi yenyewe inahusu mambo yanayokatazwa na Biblia? Neno la Mungu linakataza waziwazi kuiba, kusema uongo, na kutengeneza sanamu za kuabudu. (Kutoka 20:4; Matendo 15:29; Waefeso 4:28; Ufunuo 21:8) Tunapaswa kukataa kazi yoyote inayotuomba tufanye mambo kama hayo. Kwa kuwa tunamupenda Yehova, hatuwezi kukubali kazi inayotuomba kufanya mambo yanayovunja amri zake.—1 Yohana 5:3.

16 Je, kazi hiyo inanifanya nionekane kuwa ninawatia wengine moyo waziwazi ili wafanye jambo lisilofaa ao ninaliunga mukono? Tuchukue mufano. Kuwa mwandishi katika biro fulani si vibaya. Lakini, itakuwa namna gani ikiwa Mukristo angepewa kazi hiyo katika biro ya muchezo wa tombola? Ni kweli, kazi yake haitamuomba kuuzisha moja kwa moja tikiti kwa ajili ya muchezo huo. Hata hivyo, je, hatuwezi kusema kwamba kazi yake hiyo inaunga mukono muchezo wa tombola ambao unachochea watu kuwa na pupa ao tamaa, jambo ambalo linakatazwa na Neno la Mungu? (Waefeso 5:3-5) Kwa kuwa tunamupenda Yehova, hatutaki kushiriki katika mazoea yasiyopatana na Biblia.

17. (a) Ni mambo gani mengine tunapaswa kufikiria kwa uzito mbele ya kukubali kazi fulani? (Soma kisanduku “ Niikubali Kazi Hii?”) (b) Kusudi zamiri yetu itusaidie kufanya maamuzi yanayomupendeza Mungu, inaomba kufanya nini?

17 Maulizo mengi juu ya kazi yoyote yanaweza kujibiwa kwa kufikiria sana majibu ya maulizo mawili tuliyochunguza katika fungu la 15 na 16. Lakini kuna mambo mengine ambayo tunapaswa kufikiria kwa uzito mbele ya kukubali kazi fulani.b Hatuwezi kutazamia mutumwa mwaminifu atuwekee sheria juu ya kila hali inayoweza kutokea. Kwa hiyo, inaomba sisi wenyewe tutumie akili. Kama tulivyojifunza katika Sura ya 2, tunapaswa kufundisha zamiri yetu na kuizoeza kwa kujifunza namna ya kutumia Neno la Mungu katika maisha yetu ya kila siku. Ikiwa tunazoeza ‘nguvu zetu za ufahamu kwa kuzitumia,’ zamiri yetu inaweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayomupendeza Mungu na kutuwezesha kubaki katika upendo wake.—Waebrania 5:14.

NIIKUBALI KAZI HII?

Mwanaume anatafuta kazi yenye kwenye gazeti la kutangaza habari

Kanuni: “Fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.

Ujiulize

  • Kazi hii inaomba mutu afanye moja kwa moja mambo ambayo Neno la Mungu linakataza?—Kutoka 20:13-15.

  • Nikifanya kazi hii, je, nitaonekana kuwa ninaunga mukono watu wanaofanya mambo ambayo Biblia inakataza?—Ufunuo 18:4.

  • Kazi hii ni kazi tu ya kuwasaidia watu wengine, na haivunje kanuni ya Biblia?—Matendo 14:16, 17.

  • Matokeo ya kufanya kazi hii ni nini; je, itawakwaza wengine?—Waroma 14:19-22.

  • Nikiiacha familia yangu na kuenda kufanya kazi katika inchi nyingine, hilo linaweza kuharibu amani na hali ya kiroho ya familia yangu?—Waefeso 5:28–6:4.

TUWE NA MAONI YANAYOFAA KUHUSU KAZI

18. Sababu gani inaweza kuwa vigumu mutu kutimiza mambo ya kiroho?

18 Si rahisi kufanya maamuzi mazuri wakati wetu; kwa kuwa tunaishi katika “siku za mwisho” ambazo ni ‘nyakati za hatari zilizo ngumu kushugulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1) Kupata kazi na kuichunga inaweza kuwa vigumu sana. Kwa kuwa sisi ni Wakristo wa kweli, tunajua kwamba ni jambo la lazima sana kufanya kazi kwa bidii ili kulisha familia yetu. Lakini, ikiwa hatufanye angalisho, kushawishiwa na mambo mbalimbali mahali pa kazi ao roho ya ulimwengu ya kufuatia mali za kimwili, vinaweza kutuzuia tusitimize mambo ya kiroho. (1 Timotheo 6:9, 10) Acha tuone namna tunaweza kuwa wenye kusawazika, ni kusema, kuhakikisha “mambo yaliyo ya maana zaidi.”—Wafilipi 1:10.

19. Sababu gani tunapaswa kumutegemea Yehova kwa moyo wetu wote, na kufanya hivyo kutatusaidia tuepuke kufanya nini?

19 Umutegemee Yehova kwa moyo wako wote. (Methali 3:5, 6) Tunapaswa kumutegemea kwa kuwa anatuhangaikia, sivyo? (1 Petro 5:7) Yeye anajua mambo tunayohitaji kuliko sisi wenyewe, na mukono wake si mufupi hata kidogo. (Zaburi 37:25) Kwa hiyo, ni vizuri tufuate shauri la Neno lake linalosema: ‘Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa feza, huku mukirizika na vitu vya sasa. Kwa maana Mungu amesema hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”’ (Waebrania 13:5) Watumishi wengi wa wakati wote wamejionea kwamba Mungu anaweza kuwatimizia mahitaji yao ya kimwili. Tukiamini kwa moyo wetu wote kwamba Yehova anaweza kututunza, tutaepuka kuhangaikia kupita kiasi mahitaji ya kimwili ya familia yetu. (Mathayo 6:25-32) Hatutaruhusu kazi yetu ya kimwili itufanye tupuuze mambo ya kiroho, kama vile kuhubiri habari njema na kuhuzuria mikutano.—Mathayo 24:14; Waebrania 10:24, 25.

20. Kuwa na jicho rahisi maana yake nini, na unaweza kufanya nini ili uwe na jicho kama hilo?

20 Uwe na jicho rahisi. (Mathayo 6:22, 23) Kuwa na jicho rahisi kunamaanisha kuishi maisha rahisi ao mepesi. Mukristo akiwa na jicho rahisi, atakazia mawazo yake kwenye kusudi moja: kufanya mapenzi ya Mungu. Ikiwa kweli jicho letu linakazia vizuri kusudi hilo, hatutatafuta juu chini kazi ya mushahara munono na maisha ya hali ya juu sana. Wala hatutaangukia katika mutego wa kutafuta sana vitu vya kisasa na vya hali ya juu zaidi ambavyo watangazaji wa biashara wanapenda kusadikisha watu kuwa wana lazima ya vitu hivyo ili wawe wenye furaha. Basi, unaweza kufanya nini ili uendelee kuwa na jicho rahisi? Epuka kujiingiza katika madeni yasiyo ya lazima. Usiwe na vitu vingi sana ambavyo vitakuchukua wakati mwingi sana ili kuvitunza. Tii shauri la Biblia linalosema kwamba turizike na “chakula na kitu cha kujifunika.” (1 Timotheo 6:8) Fanya yote inayowezekana ili kufanya maisha yako yawe mepesi.

21. Sababu gani ni lazima kuchagua mambo ya kutia pa nafasi ya kwanza, na ni nini tunayopaswa kutia pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu?

21 Tia mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza, na ushikamane kabisa nayo. Kwa kuwa katika maisha mutu hawezi kufanya kila kitu, ni lazima kuchagua mambo ya kutia pa nafasi ya kwanza. Ikiwa hatufanye hivyo, mambo yasiyo ya maana yanaweza kuchukua wakati wetu, na tutakosa wakati wa kufanya mambo ya lazima. Katika maisha yetu, ni nini tunapaswa kutia pa nafasi ya kwanza? Katika ulimwengu, watu wengi wanakazia kabisa jambo la kusoma sana ili kupata kazi ya mushahara munono. Lakini, Yesu aliwashauri wafuasi wake “waendelee kuutafuta kwanza ufalme.” (Mathayo 6:33) Ndiyo, kwa kuwa sisi ni Wakristo wa kweli, katika maisha yetu tunatia Ufalme wa Mungu pa nafasi ya kwanza. Maisha yetu yote, ni kusema, maamuzi tunayofanya, miradi yetu, na shuguli zetu, mambo hayo yanapaswa kuonyesha kwamba tunaona faida za Ufalme na mapenzi ya Mungu kuwa ya lazima zaidi kuliko vitu vya kimwili na miradi ya ulimwengu huu.

“UAMUZI WANGU UMENILETEA FURAHA NA KUTOSHEKA KATIKA MAISHA”

Dada Zenaida anasema hivi: “Nilikuwa mwanafunzi mwenye akili na kwa hiyo nililipiwa garama za masomo katika masomo yenye kuheshimiwa sana huko New York, City. Washauri wangu wengi wa masomo walinitia moyo sana niombe kuingia kwenye masomo ya juu mbalimbali (université) nyingi zenye kujulikana sana. Nilikubaliwa na kuitwa na masomo ya juu fulani kati ya hayo na hata moja yenye kujulikana sana huko États-Unis, ilikubali kunilipia garama ili niweze kusoma. Lakini, nilikataa musaada huo kwa sababu mbili. Nilifikiria hatari zinazoweza kunipata kwa sababu ya mwenendo mubaya wa wanafunzi ikiwa ninaenda kuishi huko mbali na wazazi, na pia nilikuwa na tamaa sana ya kufanya kazi ya upainia.

“Leo hii, nimeeneza zaidi ya miaka 20 katika kazi ya upainia wa kawaida. Nimejitoa katika utumishi wa namna mbalimbali: kuenda kusaidia mahali ambapo kuna lazima ya wahubiri, kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme, na kusaidia wakati wa misiba mbalimbali kama vile wakati wa matetemeko ya inchi. Kwa sasa, ninafurahia kutumika katika kikundi cha luga ya kigeni huko New York City.

“Ninapofikiria miaka ambayo nimepitisha katika utumishi wa wakati wote, ninatambua kwamba nimebarikiwa sana. Uamuzi wangu umeniletea furaha na kutosheka katika maisha. Hakuna kitu kinachoweza kulinganishwa na furaha pia na marafiki ambao nimepata.”

KUFANYA KAZI YA KUHUBIRI KWA BIDII

Bibi na bwana wanahubiri

Tunaweza kuonyesha upendo wetu kwa Yehova kwa kutia kazi ya kuhubiri pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu

22, 23. (a) Kazi ya lazima sana ya Wakristo wa kweli ni gani, na namna gani tunaweza kuonyesha kwamba kazi hiyo ni ya maana sana kwetu? (Soma kisanduku “Uamuzi Wangu Umeniletea Furaha na Kutosheka Katika Maisha”.) (b) Umeazimia kufanya nini kuhusu kazi ya kimwili?

22 Kwa kuwa tunajua kwamba tunaishi katika siku za mwisho, tunapaswa kutia mawazo yetu kwenye kazi ya maana sana ya Wakristo wa kweli: kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kama Yesu, aliye Mufano wetu, tunapaswa kujitoa sana katika kazi hiyo ya kuokoa uzima. Namna gani tunaweza kuonyesha kwamba kazi hiyo ni ya maana sana kwetu? Watumishi wengi wa Mungu ni wahubiri katika makutaniko na wanajitoa kwa moyo wao wote katika kazi ya kuhubiri. Wengine wamepanga mambo yao ili wawe mapainia na wamisionere. Kwa sababu wazazi wengi wametambua faida ya kuwa na miradi ya kiroho, wamewatia watoto wao moyo wawe watumishi wa wakati wote. Je, wahubiri wa Ufalme wenye bidii wanaona mema kwa ajili ya kazi yao ngumu katika mahubiri? Bila shaka! Kumutumikia Yehova kwa nafsi yote ndio njia hakika ya kupata maisha yenye furaha, kutosheka, na baraka zingine zisizohesabika.​—Methali 10:22.

23 Wengi kati yetu wanafanya kazi ya kimwili ili kupatia familia zao mahitaji ya kimwili, na kazi hiyo inawachukua wakati mwingi. Usisahau kwamba Yehova anataka tuone mema kwa ajili ya kazi yetu ngumu. Kwa hiyo, ikiwa tunapatanisha mawazo yetu na matendo yetu na mawazo yake na kanuni zake, tunaweza kufurahia kazi tunayofanya. Hata hivyo, tufanye yote tunayoweza ili tusiruhusu hata kidogo kazi yetu ya kimwili itufanye tusahau kazi yetu ya lazima sana, ni kusema, kazi ya kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Tunapotia kazi hiyo pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu, tunaonyesha kwamba tunamupenda Yehova na tunataka kabisa kubaki katika upendo wake.

a Inasemekana kuwa neno la Kigiriki linalotafsiriwa “seremala” ni “neno la ujumla lililotumiwa juu ya mutu yeyote aliyekuwa anatumia mbao ili kujenga nyumba, kutengeneza meza na viti, na vitu vingine vya mbao.”

b Unaweza kupata habari zaidi kuhusu mambo ya kufikiria mbele ya kukubali kazi fulani katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 4, 1999, ukurasa wa 28-30, na wa tarehe 15 Mwezi wa 7, 1982, ukurasa wa 26.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine