Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • bt sura 18 uku. 140-147
  • “Wamutafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wamupate”

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • “Wamutafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wamupate”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili” juu ya Ufalme wa Mungu
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • Kuhubiri “Katika Soko” (Mdo. 17:16-21)
  • “Wanaume wa Atene, Ninaona” (Mdo. 17:22, 23)
  • Mungu “Haiko Mbali Sana na Kila Mumoja Wetu” (Mdo. 17:24-28)
  • “Wanadamu Wote Kila Mahali . . . Wanapaswa Kutubu” (Mdo. 17:29-31)
  • “Wamoja . . . Wakakuwa Waamini” (Mdo. 17:32-34)
  • Sitawisha Uwezo wa Kufikiri Pamoja na Wengine
    Huduma Yetu ya Ufalme—2005
  • Uko na Mawazo Gani Juu ya Watu wa Eneo Lako?
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2020
  • Busara
    Penda Watu—Juu Ufanye Wanafunzi
“Kutoa Ushahidi Kamili” juu ya Ufalme wa Mungu
bt sura 18 uku. 140-147

SURA YA 18

“Wamutafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wamupate”

Paulo anazungumuzia jambo yenye wote wanakubaliana na anajipatanisha na wasikilizaji wake

Inategemea Matendo 17:16-34

1-3. (a) Juu ya nini Paulo anauzika sana kule Atene? (b) Kujifunza mufano wa Paulo kutatusaidia namna gani?

PAULO anauzika sana. Iko Atene, muji wa maana sana katika mambo ya elimu mu Ugiriki. Wanafilozofia Socrates, Platon, na Aristote walifundisha mu ule muji. Watu wa Atene wanapenda sana mambo ya dini. Fasi yote, ikuwe mu hekalu, pembeni ya barabara, ao fasi kwenye kuwa watu wengi, Paulo anaona sanamu za mingi, juu Waatene walikuwa naabudu miungu ya mingi. Paulo anajua mawazo ya Yehova Mungu wa kweli juu ya sanamu. (Kut. 20:4, 5) Na kama Yehova, ule mutume muaminifu anachukia sanamu!

2 Mambo yenye Paulo anaona wakati tu anaingia mu soko ni yenye kuchukiza sana. Sanamu mingi za mungu Herme zenye umbo ya kiungo ya uzazi ya mwanaume zimepangwa kaskazini-mangaribi karibu na mulango mukubwa wa soko. Mu soko, munayala mazabahu. Namna gani ule mutume mwenye bidii atahubiria watu hawa wenye kuabudu sanamu za mingi? Ataweza kujizuia na kupata habari ya kuzungumuzia yenye yeye na wasikilizaji wake wanakubaliana? Ataweza kusaidia mutu yeyote kutafuta Mungu wa kweli na kumuabudu?

3 Mu Matendo 17:22-31, tunasoma hotuba ya Paulo kwa watu wenye elimu wa Atene. Paulo alikuwa mwenye kusadikisha, alizungumuza kwa busara, na alitumia utambuzi. Kujifunza mufano wa Paulo kutatusaidia tujue namna ya kuchagua habari yenye siye na wasikilizaji wetu tunakubaliana na kuwasaidia kufikiri.

Kuhubiri “Katika Soko” (Mdo. 17:16-21)

4, 5. Paulo iko nahubiri wapi mu Atene, na ni watu wa namna gani njo wako pale?

4 Paulo alitembelea Atene mu safari yake ya pili ya umisionere mu mwaka wa 50 hivi K.K.Y.a Wakati alikuwa nachunga Sila na Timoteo wafike kutoka Beroya, Paulo ‘alianza kufikiri katika sinagogi pamoja na Wayahudi,’ kama vile alizoea kufanya. Alitafuta pia eneo ingine kwenye angeenda kuhubiria watu wa Atene wenye hawakukuwa Wayahudi, ni kusema, “katika soko.” (Mdo. 17:17) Soko ilikuwa kaskazini-mangaribi mwa Atene na ilikuwa kubwa sana. Ile soko haikukuwa tu fasi ya kuuza na kuuzisha vitu, lakini ilikuwa pia fasi ya maana sana kwenye watu walikutana. Kulingana na kitabu moya, “ile soko ilikuwa fasi kwenye wafanyabiashara, watu wenye walikuwa nafanya mambo ya politike, na wanafilozofia walikuwa wanakutana.” Watu wa Atene walipenda kukutana pale ili kuzungumuzia mambo mbalimbali.

ATENE​—MUJI WA MAANA SANA WA WAKATI WA ZAMANI

Muji wa Atene ulikuwa muji wenye ngome miaka mingi hata mbele historia yake ianze kuandikwa mu karne ya 7 M.K.Y. Atene ilifikia kuwa muji mukubwa wa wilaya ya Atika na ilikuwa na ukubwa wa kilometre 2500 hivi muraba (km2), na ilizungukwa na milima na bahari. Inaonekana kuwa jina ya ule muji ilitokana na jina ya mungu wao mwanamuke Atena.

Mu karne ya 6 M.K.Y., mutawala fulani wa Atene mwenye aliitwa Solon alifanya mabadiliko makubwa kuhusu serikali, sheria, na mambo ya makuta mu ule muji. Ile ilisaidia sana watu wenye walikuwa maskini na ilianzisha demokrasia. Ile demokrasia ilikuwa tu kwa ajili ya watu huru. Lakini watu wengi wenye walikuwa mu ule muji walikuwa watumwa.

Kisha Wagiriki kupata ushindi juu ya Waajemi mu karne ya 5 M.K.Y., Atene ikakuwa muji mukubwa wa utawala mudogo. Mashua za biashara zilikuwa natoka Atene na kuenda mupaka Italia na Sisili ku upande wa mangaribi na mupaka Kipro na Siria ku upande wa mashariki. Wakati Atene ilikuwa muji wenye kuendelea sana, mulikuwa mafundi wazuri zaidi, majumba ya maonyesho, wanafilozofia, wasemaji, waandikaji, na wanasayansi wazuri zaidi mu dunia ile wakati. Mu ile muji mulikuwa majengo mingi na mahekalu yenye watu wangeweza kutembelea. Sehemu yenye kuinuka zaidi mu Atene ilikuwa mulima Acropolis. Ku ile mulima kulikuwa hekalu kubwa yenye iliitwa Parthenon. Mu ile hekalu mulikuwa sanamu ya Atena yenye ilifanyizwa kwa zahabu na pembe za tembo. Na ilikuwa na urefu wa metre 12.

Atene ilikamatwa kwanza na Wasparta, kisha Wamakedonia, na ku mwisho Waroma, wenye walikamata mali yake yote. Lakini wakati wa mutume Paulo, Atene ilikuwa ingali muji wa maana kwa sababu ya historia yake. Na hata, hakuna siku yenye Atene ilikuwa sehemu ya wilaya yoyote ya Roma. Ilipewa mamlaka ya kutawala raia wake na haikulazimika kulipa Waroma ushuru. Hata kama Atene haikukuwa tena muji wenye kuendelea sana, mu ule muji mulikuwa masomo za juu za mingi, na matajiri walikuwa natuma watoto wao kule ili wasome.

5 Haingekuwa mwepesi kwa Paulo kusadikisha watu wenye walikuwa mu ile soko. Kati yao kulikuwa Waepikurea na Wastoa, wanafilozofia wenye waliamini mambo tofauti kabisa.b Waepikurea waliamini kwamba uzima ulijitokeza wenyewe. Hii njo mambo yenye waliamini: “Hakuna sababu ya kumuogopa Mungu; Hakuna mateso katika kifo; Mutu anaweza kufikia mambo ya muzuri; Mutu anaweza kuvumilia mambo ya mubaya.” Wastoa waliamini kama ilikuwa jambo ya maana kupata ujuzi na uelewaji. Lakini hawakuamini kuwa Mungu ni Mutu wa kweli kabisa. Waepikurea na Wastoa hawakuamini ufufuo wenye wanafunzi wa Kristo walikuwa wanafundisha. Ni wazi kwamba mawazo ya filozofia ya vile vikundi mbili haikupatana kabisa na kweli zenye Wakristo wa kweli waliamini zenye Paulo alikuwa anafundisha.

6, 7. Wanafilozofia fulani Wagiriki walitenda namna gani kisha kusikia mafundisho ya Paulo, na watu fulani leo wanatenda namna gani?

6 Wanafilozofia Wagiriki wanatenda namna gani kisha kusikiliza mafundisho ya Paulo? Wamoja wanatumia neno yenye inamaanisha “musema-mingi,” ao “kasuku.” Kuhusu ile neno ya Kigiriki, mutu mumoja mwenye elimu alisema: “Ku mwanzo watu walitumia ile neno ili kuzungumuzia ndege mudogo mwenye anaruka na kuokota-okota mbegu. Pia walitumia ile neno ili kuzungumuzia mutu mwenye alikuwa anaokota masalio na vitu vingine vyenye vilianguka mu soko. Kisha walianza kutumia ile neno kwa njia ya mufano ili kuzungumuzia mutu mwenye anaokota-okota habari huku na huku, na zaidi sana mutu mwenye haelewe hata zile habari.” Wale watu wenye elimu walipenda kuonyesha kama Paulo hakujua kitu, na alikuwa tu anarudilia mambo yenye alisikia kwa wengine. Lakini sawa vile tutaona, ile neno ya kumuzarau haikumuvunja moyo.

7 Mambo inakuwaka vile leo pia. Watu wanatupatiaka majina ya kutuzarau juu tuko Mashahidi wa Yehova, na juu tunaamini mambo yenye Biblia inasema. Kwa mufano, walimu fulani wanafundisha kama mageuzi ni mambo ya kweli. Na wanakazia kama kila mutu mwenye akili anapaswa kukubali ile mafundisho, na kama mwenye haikubali hana akili. Watu wa vile wanaweza kufanya watu wawaze kama tuko ‘wasema mingi’ wakati tuko natetea mambo yenye Biblia inafundisha na kutoa ushuhuda wenye kuonyesha kama kuko Muumbaji. Lakini ile haituogopeshe. Tunasema kwa uhodari wakati tunatetea mambo yenye tunaamini: kama uzima unatokana na Muumbaji mwenye akili, ni kusema, Yehova Mungu.​—Ufu. 4:11.

8. (a) Watu fulani walitenda namna gani wakati walisikia mahubiri ya Paulo? (b) Pengine Areopago kwenye Paulo alipelekwa ilikuwa wapi? (Ona maelezo ya chini.)

8 Wengine wenye walisikia mafundisho ya Paulo mu soko walitenda mu njia tofauti. Walisema hivi: “Anaonekana kuwa mutangazaji wa miungu ya kigeni.” (Mdo. 17:18) Ni kweli kwamba Paulo alikuwa nafundisha Waatene miungu ya mupya? Kufanya vile ilikuwa kosa kubwa sana, kwa sababu ilikuwa kati ya mambo yenye ilifanya Socrate ashitakiwe na ahukumiwe kifo miaka mingi mbele ya pale. Haishangaze kuona kama Paulo alipelekwa Areopago ili afasirie mafundisho yenye ilionekana kuwa ya mupya kwa watu wa Atene.c Paulo angetetea namna gani ujumbe wake mbele ya watu wenye hawakujua Maandiko?

WAEPIKUREA NA WASTOA

Waepikurea na Wastoa walikuwa vikundi mbili tofauti vya wanafilozofia. Wote hawakuamini ufufuo.

Waepikurea waliamini kama kulikuwa miungu, lakini ile miungu haikuhangaikia watu na haingewabariki ao kuwapatia malipizi. Kwa hiyo kusali na kutoa zabihu ilikuwa kuchokea bure. Waliamini kama kufurahia maisha njo ilikuwa jambo ya maana zaidi. Mu mawazo na matendo yao, hawakuhangaikia kanuni za mema na mabaya. Lakini waliamini kama watu walipaswa kuwa na usawaziko juu waepuke matokeo yoyote ya mubaya. Waliamini kama ilikuwa jambo ya maana sana kuwa na ujuzi. Lakini kusudi tu ya ile ujuzi ilikuwa kusaidia watu waachane na mafundisho ya kidini na mambo ya uchawi yenye kuogopesha.

Kwa upande mwingine, Wastoa waliamini kama vitu vyote vilitokana na mungu fulani mwenye hana mawazo wala hisia, na kama nafsi za wanadamu zilitokana na uleule mungu. Wastoa fulani waliamini kama nafsi ingefikia kuharibiwa pamoya na ulimwengu. Wastoa wengine waliamini kama nafsi ingefikia tena kuwa sehemu ya ule mungu, ao ile nguvu. Kulingana na wanafilozofia Wastoa, mutu angeweza kupata furaha kama anafuata sheria za asili za ulimwengu.

“Wanaume wa Atene, Ninaona” (Mdo. 17:22, 23)

9-11. (a) Paulo alianza mazungumuzo yake namna gani? (b) Namna gani tunaweza kuiga mufano wa Paulo mu mahubiri?

9 Kumbuka kama Paulo aliuzika sana wakati aliona zile sanamu zote. Lakini, kuliko kusema moja kwa moja mambo ya mubaya kuhusu ibada ya sanamu, alibakia mwenye kutulia. Kwa busara, alijikaza kuvuta uangalifu wa wasikilizaji wake kwa kuzungumuzia jambo yenye wote walikubaliana. Alianza kwa kusema hivi: “Wanaume wa Atene, ninaona kwamba katika mambo yote munaonekana kuwa munaogopa sana miungu kuliko watu wengine.” (Mdo. 17:22) Mu maneno ingine Paulo alikuwa anasema hivi: ‘Ninaona kama munapenda sana mambo ya dini.’ Kwa hekima, Paulo aliwapongeza kwa sababu walipenda mambo ya dini. Paulo alijua kama watu fulani wenye walipofushwa na mafundisho ya uongo wanaweza kukubali kweli. Alijua vile juu wakati fulani yeye mwenyewe ‘alitenda bila kujua na kwa kukosa imani.’​—1 Ti. 1:13.

10 Ili kuzungumuzia jambo yenye wote walikubaliana, Paulo alisema kama ameona jambo yenye kuhakikisha kama Waatene wanapenda mambo ya dini, ni kusema, mazabahu “Kwa Mungu Mwenye Hajulikane.” Kulingana na kitabu fulani, “Wagiriki walikuwa na zoea ya kufanya mazabahu kwa ajili ya ‘miungu yenye haijulikane.’ Walifanya vile juu waliogopa kama pengine walisahau mungu fulani na ile ingekasirisha ule mungu.” Kwa kufanya mazabahu ya vile, Waatene walikubali kama kulikuwa Mungu mwenye hawakujua. Paulo alitumia ile mazabahu ili kuanza kuzungumuza kuhusu habari njema. Alisema hivi: “Kile munaabudu bila kukijua, ni kile ninawatangazia ninyi.” (Mdo. 17:23) Paulo alifikiri nao mu njia ya chini-chini lakini yenye kuwa na nguvu sana. Hakukuwa nafundisha kuhusu mungu mupya sawa vile watu fulani walimushitaki. Alikuwa anafundisha kuhusu Mungu mwenye hawakujua, ni kusema, Mungu wa kweli.

11 Namna gani tunaweza kuiga mufano wa Paulo mu mahubiri? Kama tunafungua macho, tunaweza kuona mambo yenye inaonyesha kama mutu anapenda mambo ya Mungu. Pengine tunaweza kuona vitu fulani vya kidini vyenye anavala ao vyenye viko mu nyumba yake ao vyenye viko inje ya nyumba yake. Tunaweza kusema: ‘Ninaona kama unapenda mambo ya Mungu. Na nilikuwa napenda kuzungumuza na mutu mwenye anafurahia mambo ya Mungu.’ Wakati tunaitika kama mutu anapenda mambo ya Mungu, tunapata jambo yenye siye wote tunakubaliana, yenye inaweza kutusaidia kuanzisha mazungumuzo. Kumbuka kama kusudi yetu haiko kubagua watu kwa sababu ya mambo yenye wanaamini, juu kati ya ndugu na dada zetu kuko wengi wenye zamani walikuwaka wanaamini mafundisho ya uongo.

Kijana mwanaume iko nazungumuza na mwalimu wake na wanafunzi wenzake wakati wa somo ya sayansi.

Ili kuanzisha mazungumuzo, zungumuzia jambo yenye weye na wasikilizaji wako munakubaliana

Mungu “Haiko Mbali Sana na Kila Mumoja Wetu” (Mdo. 17:24-28)

12. Namna gani Paulo alipatanisha mafundisho yake na hali ya wasikilizaji wake?

12 Paulo alianza kwa kuzungumuzia mambo yenye wote walikubaliana. Angeendelea kufanya vile? Juu alijua kama wasikilizaji wake walijua sana filozofia ya Wagiriki na hawakujua Maandiko, alipatanisha mahubiri yake na hali yao mu njia mbalimbali. Kwanza, alizungumuzia mafundisho ya Biblia bila kutaya moja kwa moja Maandiko. Pili, alionyesha kama haiko tofauti na wasikilizaji wake. Wakati fulani alitumia maneno sawa vile “siye” ao “sisi.” Tatu, alitaya mambo fulani yenye kuwa mu vitabu vya Wagiriki ili kuonyesha kama mambo fulani yenye iko nafundisha inapatikana mu maandishi yao wenyewe. Tuchunguze sasa hotuba ya Paulo yenye kuchochea. Alifundisha kweli gani za maana kuhusu Mungu mwenye watu wa Atene hawakujua?

13. Paulo alisema nini kuhusu namna ulimwengu ulianza, na maneno yake ilipenda kumaanisha nini?

13 Mungu aliumba ulimwengu. Paulo alisema hivi: “Mungu mwenye alifanya ulimwengu na vitu vyote vyenye kuwa ndani, akiwa, kama vile iko, Bwana wa mbingu na dunia, hakae katika mahekalu yenye yalitengenezwa kwa mikono.”d (Mdo. 17:24) Ulimwengu haukujitokeza tu wenyewe. Mungu wa kweli njo Muumbaji wa kila kitu. (Zb. 146:6) Tofauti na Atena ao miungu ingine yenye ilikuwa na lazima ya mazabahu na hekalu ili kusifiwa, Mungu wa mbingu na dunia, mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi hawezi kuenea mu hekalu yenye kujengwa na mikono ya wanadamu. (1 Fa. 8:27) Maneno ya Paulo iko wazi. Ilipenda kumaanisha hivi: Mungu wa kweli ni mukubwa zaidi kuliko sanamu zenye kutengenezwa na wanadamu zenye kupatikana mu mahekalu yenye kufanywa na wanadamu.​—Isa. 40:18-26.

14. Namna gani Paulo alionyesha kama Mungu hana lazima ya kitu yoyote kutoka kwa wanadamu?

14 Mungu hana lazima ya kutegemezwa na wanadamu. Waabudu-sanamu walizoea kuvalisha sanamu zao manguo ya bei, kuzitolea zawadi za bei, ao kuziletea chakula na vinywaji. Ni sawa vile zile sanamu zilikuwa na lazima ya vile vitu! Lakini, pengine wanafilozofia fulani wenye walikuwa wanamusikiliza Paulo waliamini kama Mungu hakukuwa na lazima ya kitu chochote kutoka kwa wanadamu. Kama ni vile, bila shaka walikubaliana na maneno ya Paulo wakati alisema “haiko mikono ya mwanadamu ndiyo inamutumikia.” Mungu, Muumbaji, hana lazima ya kitu yoyote kutoka kwa wanadamu! Lakini, yeye njo anapatia wanadamu mambo yenye wako nayo lazima, ni kusema, “uzima na pumuzi na vitu vyote,” kutia ndani jua, mvua, na udongo wenye kuzaa matunda. (Mdo. 17:25; Mwa. 2:7) Kwa hiyo, Mungu mwenye anatupatia kila kitu hana lazima ya kitu yoyote kutoka kwetu.

15. Paulo alirekebisha namna gani mawazo ya Waatene wenye walijiona kuwa wa maana sana, na mufano wake unatufundisha jambo gani ya maana?

15 Mungu aliumba watu. Waatene waliamini kama walikuwa wa maana zaidi kuliko watu wenye hawakukuwa Wagiriki. Lakini kujivunia taifa ao rangi ya ngozi haipatane na mafundisho ya Biblia. (Kum. 10:17) Paulo alizungumuzia kwa busara na kwa ufundi ile jambo yenye ingewagusa sana. Alisema hivi: “Kutoka kwa mutu mumoja, [Mungu] alifanya kila taifa la watu.” Bila shaka maneno ya Paulo ilifanya wasikilizaji wake wafikiri. (Mdo. 17:26) Alikuwa nazungumuzia habari yenye kuwa mu kitabu ya Mwanzo kuhusu Adamu, baba ya wanadamu wote. (Mwa. 1:26-28) Juu wanadamu wote walitoka kwa mutu mumoya, hakuna rangi ya ngozi ao taifa yenye iko ya maana kupita ingine. Bila shaka wasikilizaji wa Paulo walielewa alimaanisha nini. Mufano wake unatufundisha jambo ya maana. Tunapaswa kuwa na usawaziko na busara wakati tuko nahubiri, lakini hatupendi kuregeza mafundisho ya Biblia juu ya kufanya watu wengine waikubali.

16. Kusudi ya Mungu kwa ajili ya wanadamu ni nini?

16 Mungu anapenda wanadamu wamukaribie. Hata kama wanafilozofia wenye walikuwa namusikiliza Paulo walikuwa wamebishana kwa miaka mingi kuhusu kusudi ya maisha ya wanadamu, hawangeweza kufasiria ile jambo mu njia yenye ingefanya watu watosheke. Lakini, Paulo alionyesha waziwazi kusudi ya Muumbaji kwa ajili ya wanadamu, ni kusema, “wamutafute Mungu, kama watapapasa-papasa wakimutafuta na kwa kweli wamupate, ijapokuwa, kweli, haiko mbali sana na kila mumoja wetu.” (Mdo. 17:27) Inawezekana kabisa kujua Mungu mwenye Waatene hawakujua. Kwa kweli, haiko mbali na watu wenye wanapenda kumupata na kujifunza juu yake. (Zb. 145:18) Kwa kutumia maneno kila mumoja “wetu,” Paulo anaonyesha kama iko kati ya wale wenye wanapaswa ‘kutafuta’ na ‘kupapasa-papasa’ ili kumupata Mungu.

17, 18. Juu ya nini wanadamu wanapaswa kumukaribia Mungu, na namna Paulo aligusa mioyo ya wasikilizaji wake inaweza kutufundisha nini?

17 Wanadamu wanapaswa kumukaribia Mungu. Paulo alisema kama ni kwa sababu ya Mungu njo “tuko na uzima na tunatembea na tuko.” Watu fulani wenye elimu wanasema kama Paulo alikuwa anataya maneno ya Epimenides, mwandikaji wa mashairi wa Krete wa mu karne ya 6 M.K.Y., mwenye “Waatene waliheshimia sana.” Paulo alizungumuzia sababu ingine ya kuchochea wanadamu wamukaribie Mungu. Alisema hivi: “Wamoja kati ya watunga-mashairi wenu wenyewe wamesema, ‘Kwa maana sisi pia tuko watoto wake.’” (Mdo. 17:28) Wanadamu wanapaswa kumukaribia Mungu juu aliumba mwanadamu wa kwanza mwenye ni baba yetu siye wote. Ili kugusa mioyo ya wasikilizaji wake, kwa hekima Paulo alitaya maneno yenye kuwa mu maandishi ya Wagiriki yenye bila shaka wasikilizaji wake waliheshimia.e Kama Paulo, na siye wakati fulani tunaweza kutumia maneno yenye kuwa mu vitabu vya historia, encyclopedia, ao maandishi ingine yenye kuheshimiwa. Kwa mufano, kutumia mu njia yenye kufaa maneno ya kitabu fulani yenye kuheshimiwa kunaweza kusaidia musikilizaji aelewe namna desturi fulani za dini ya uongo zilianza.

18 Mupaka hapa, Paulo amezungumuzia kweli za maana kuhusu Mungu, na kwa ufundi amepatanisha maneno yake na hali ya wasikilizaji wake. Paulo alipenda Waatene watende namna gani kisha kusikiliza zile habari za maana? Bila kukawia, aliwaambia mambo yenye wanapaswa kufanya.

“Wanadamu Wote Kila Mahali . . . Wanapaswa Kutubu” (Mdo. 17:29-31)

19, 20. (a) Namna gani Paulo alionyesha kwa busara kama kuabudu sanamu zenye kutengenezwa na wanadamu ni upumbavu? (b) Watu wenye walikuwa namusikiliza Paulo walipaswa kufanya nini?

19 Sasa Paulo alikuwa tayari kuchochea wasikilizaji wake watende. Alikuwa nafikiria mawazo yenye ilikuwa mu maandishi ya Wagiriki yenye alikuwa alishataya wakati alisema hivi: “Kwa hiyo, kwa kuwa sisi tuko watoto wa Mungu, hatupaswe kufikiri kwamba Mungu ni kama zahabu ao feza ao jiwe, kama kitu chenye kilichongwa kwa ufundi na utungaji wa mwanadamu.” (Mdo. 17:29) Kwa kweli, kama Mungu njo aliumba wanadamu, namna gani angekuwa kama sanamu zenye kufanywa na wanadamu? Namna Paulo alifikiri nao kwa busara, ilionyesha kama kuabudu sanamu ni upumbavu. (Zb. 115:4-8; Isa. 44:9-20) Juu Paulo alijitia ndani kwa kusema “hatupaswe,” ile ilifanya ikuwe mwepesi kwa wasikilizaji wake kukubali mashauri yake.

20 Paulo alionyesha wazi jambo yenye walipaswa kufanya. Alisema hivi: “Mungu ameachilia nyakati hizo za kukosa kujua [za kuwaza kama Mungu anaweza kukubali wanadamu wenye kuabudu sanamu]; lakini sasa anatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.” (Mdo. 17:30) Inawezekana wasikilizaji fulani wa Paulo walishangala sana wakati alisema kuwa wanapaswa kutubu. Lakini hotuba ya Paulo yenye kuchochea ilionyesha kama Mungu njo aliwapatia uzima na kwamba watatoa hesabu mbele yake. Walipaswa kumutafuta Mungu, kujifunza juu yake, na kuishi kulingana na mapenzi yake. Kwa Waatene, ile ilimaanisha kama walipaswa kuelewa kuwa kuabudu sanamu ilikuwa zambi na walipaswa kuacha kufanya vile.

21, 22. Paulo alimalizia hotuba yake na maneno gani yenye kuchochea, na ile maneno iko na maana gani kwetu leo?

21 Paulo alimaliza hotuba yake na hii maneno yenye kuchochea: “[Mungu] ameweka siku yenye anakusudia kuhukumu kwa haki dunia yenye kuikaliwa na watu kupitia mwanaume mwenye ameweka, na ametoa uhakikisho kwa watu wote kwa kuwa amemufufua kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:31) Juu sasa walijua kama Siku ya Hukumu iko nakuya, walipaswa kumutafuta Mungu wa kweli na kumupata! Paulo hakutaya jina ya Ule mwenye Mungu atatumia ili kuhukumu. Lakini alisema jambo fulani ya maana juu yake: Aliishi akiwa mwanadamu, alikufa, na Mungu alikuwa amemufufua!

22 Ile maneno yenye kuchochea yenye Paulo alimalizia nayo iko na maana kubwa kwetu. Tunajua kama Muamuzi mwenye Mungu ameweka ni Yesu Kristo mwenye alifufuliwa. (Yoh. 5:22) Tunajua pia kama Siku ya Hukumu itakuwa na urefu wa miaka 1000 na kama inakaribia sana. (Ufu. 20:4, 6) Hatuogope Siku ya Hukumu juu tunajua kama italeta baraka mingi za muzuri kwa watu wenye watahukumiwa kuwa waaminifu. Tuko hakika kama tumaini yetu ya kuwa na maisha ya muzuri mu siku zenye ziko nakuya itatimia kwa sababu ya muujiza wa ajabu sana wenye ulifanyika, ni kusema, kufufuliwa kwa Yesu Kristo!

“Wamoja . . . Wakakuwa Waamini” (Mdo. 17:32-34)

23. Watu walitenda mu njia gani tofauti-tofauti kisha kusikia hotuba ya Paulo?

23 Kisha kusikiliza hotuba ya Paulo, watu walitenda kwa njia tofauti. ‘Wamoja kati yao walianza kumuchekelea’ wakati walisikia kuhusu ufufuo. Wengine walionyesha heshima lakini hawakugeuka na kuwa waamini. Walisema hivi: “Tutakusikiliza juu ya jambo hili wakati mwingine.” (Mdo. 17:32) Lakini watu fulani walifanya jambo fulani ya muzuri: “Wanaume fulani wakajiunga naye na wakakuwa waamini. Kati yao kulikuwa Dionisio, mwenye alikuwa muamuzi wa tribinali ya Areopago, na mwanamuke mwenye aliitwa Damari, na wengine pamoja nao.” (Mdo. 17:34) Na siye wakati tunahubiri, watu wanatendaka mu njia tofauti-tofauti. Watu fulani wanatuchekelea, wengine wanatuonyesha heshima hata kama hawapendezwe. Lakini tunafurahi wakati watu fulani wanakubali ujumbe wa Ufalme na kuwa waamini.

24. Hotuba yenye Paulo alitoa Areopago inaweza kutufundisha nini?

24 Wakati tunafikiria juu ya hotuba ya Paulo, tunajifunza mambo ya mingi kuhusu namna ya kufasiria mambo mu njia yenye kusadikisha na pia namna ya kujipatanisha na hali ya wasikilizaji wetu. Zaidi ya ile tunaweza kujifunza juu ya nini ni jambo ya lazima kuwa wavumilivu na wenye busara wakati tuko nahubiria watu wenye wamepofushwa na mafundisho ya uongo. Tunaweza pia kujifunza hii somo ya maana: Hatupaswe kuregeza kweli ya Biblia juu tu ya kufurahisha wasikilizaji wetu. Lakini kama tunamuiga mutume Paulo, tunaweza kuwa walimu wazuri wakati tuko nahubiri. Tena, waangalizi wanaweza kuwa walimu wazuri zaidi katika kutaniko. Kama tunafanya vile tutakuwa na uwezo kamili wa kusaidia wengine “wamutafute Mungu . . . na kwa kweli wamupate.”​—Mdo. 17:27.

a Ona kisanduku “Atene​—Muji wa Maana Sana wa Wakati wa Zamani.”

b Ona kisanduku “Waepikurea na Wastoa.”

c Areopago ilikuwa mulima kwenye watawala wa Atene walikuwa wanakutana. Neno “Areopago” inaweza kumaanisha watawala ao ile mulima. Kwa hiyo, watu wenye elimu wako na mawazo tofauti kuhusu kwenye Paulo alipelekwa. Wamoja wanawaza kama alipelekwa ku ile mulima ao karibu na ile mulima ao tena ku mukutano wa watawala fasi ingine, pengine mu soko.

d Neno ya Kigiriki yenye kutafsiriwa “ulimwengu” ni neno koʹsmos. Mara mingi inatumiwa mu Biblia ili kumaanisha watu. Lakini Wagiriki walikuwa naitumia ili kumaanisha ulimwengu wenye kuonekana. Na inaonekana kama juu Paulo alipenda kuzungumuzia mambo yenye yeye na wasikilizaji wake Wagiriki wanakubaliana, alitumia ile neno mu ile maana yenye Wagiriki walielewa.

e Paulo alitumia maneno yenye kuwa mu shairi yenye kuitwa Phaenomena, yenye iliandikwa na Mustoa mwenye kuitwa Aratus. Maneno ya kufanana na ile inapatikana pia mu maandishi ingine ya Wagiriki, kutia ndani wimbo wenye kuitwa Wimbo kwa Zeu, wenye ulitungwa na mwandikaji Mustoa mwenye kuitwa Cleanthes.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine