SURA YA 4
“Watu Wenye Hawana Elimu na Watu wa Kawaida”
Mitume wanatenda kwa uhodari na Yehova anawabariki
Inategemea Matendo 3:1–5:11
1, 2. Petro na Yohana walifanya muujiza gani karibu na mulango wa hekalu?
JUA ya kisha midi inaangaza, kuko mukutano mukubwa wa watu wengi. Wayahudi wengi wenye kumuogopa Mungu na wanafunzi wa Yesu wanaingia mu uwanja wa hekalu. “Saa ya sala” inakaribia.a (Mdo. 2:46; 3:1) Petro na Yohana wanajikaza kupita kati ya wale watu na kuingia mu hekalu kupitia mulango wenye kuitwa Muzuri. Kuko makelele mingi juu watu wengi wako natembea na kuongea wakati uleule. Kuko pia mwanaume wa kukomala mwenye alizaliwa kilema, mwenye alikuwa anaomba-omba. Ule mwanaume anaomba zawadi za rehema.—Mdo. 3:2; 4:22.
2 Wakati Petro na Yohana wanakaribia, ule mutu wa kuomba-omba anawaomba makuta vile alikuwa anazoea kufanya. Wale mitume wanasimama, ile inafanya ule mutu akuwe na tumaini. Petro anamuambia: “Sina feza wala zahabu, lakini kile niko nacho ni kile ninakupatia. Katika jina la Yesu Kristo Munazareti, tembea!” Wazia namna watu wanashangala sana wakati Petro anamukamata mukono, na kwa mara ya kwanza mu maisha yake, anasimama! (Mdo. 3:6, 7) Wazia namna ule mutu iko naangalia miguu yake na kupima kutembea kwa mara ya kwanza mu maisha yake! Ile inafanya aanze kuruka-ruka na kumusifu Mungu kwa sauti kubwa!
3. Ni zawadi gani ya muzuri zaidi yenye wale watu wengi na ule mutu mwenye aliponyeshwa wangeweza kupata?
3 Wale watu wengi wanakimbilia kwenye Petro na Yohana wako mu eneo yenye mistari za nguzo za Sulemani. Wakati wako pale kwenye, wakati fulani Yesu alisimamaka na kufundisha, Petro anawaambia maana ya mambo yenye wamejionea. (Yoh. 10:23) Anasema kama wale watu wengi, kutia ndani ule mutu mwenye aliponyeshwa, wanaweza kupata zawadi ya bei sana kupita feza na zahabu. Ile zawadi haiko tu afya ya muzuri, inatia ndani mambo mingi zaidi. Inawapatia nafasi ya kutubu juu zambi zao zisamehewe na wakuwe wafuasi wa Yesu Kristo, “Kiongozi Mukubwa wa uzima,” mwenye alichaguliwa na Yehova.—Mdo. 3:15.
4. (a) Muujiza wa kuponyesha ulileta fujo gani? (b) Tutazungumuzia maulizo gani mbili?
4 Ni siku ya pekee kabisa! Mutu mumoja ameponyeshwa kimwili na sasa anaweza kutembea. Maelfu ya watu wamepewa nafasi ya kuponyeshwa kiroho, juu waweze kumufurahisha Mungu. (Kol. 1:9, 10) Tena, mambo yenye ilitokea ile siku ilileta fujo kati ya wafuasi waaminifu wa Kristo na watu wenye mamlaka wenye walipenda kuwazuia wasitimize amri ya Yesu ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme. (Mdo. 1:8) Namna Petro na Yohana, “watu wenye hawana elimu na watu wa kawaida” walitenda, na njia yenye walitumia wakati walikuwa wanahubiria wale watu wengi, inaweza kutufundisha nini?b (Mdo. 4:13) Na namna gani tunaweza kuwaiga wao na wanafunzi wengine wakati tunapambana na upinzani?
Haiko “Kupitia Nguvu Zetu” (Mdo. 3:11-26)
5. Namna Petro alihubiria watu wengi, inatufundisha nini?
5 Petro na Yohana walisimama mbele ya watu wengi. Walijua kama pengine wamoja kati yao walikuwa kati ya watu wenye waliomba Yesu auawe. (Mk. 15:8-15; Mdo. 3:13-15) Wazia uhodari wa Petro wakati alitangaza kama ule mutu mwenye alikuwa kilema ameponyeshwa katika jina ya Yesu. Petro hakujaribu kuficha ukweli. Aliwalaumu waziwazi na kuonyesha kama walichangia kumuua Kristo. Hata vile, Petro hakuwawekea kinyongo hata kidogo, juu ‘walitenda bila kujua.’ (Mdo. 3:17) Aliwaita “ndugu,” na kukazia mambo yenye kupendeza juu ya ujumbe wa Ufalme. Kama wangetubu na kumuamini Kristo, wangepata “vipindi vya kutuliza” kutoka kwa Yehova. (Mdo. 3:19) Na siye tunapaswa kuwa na uhodari na kusema mambo waziwazi wakati tunatangaza hukumu ya Mungu yenye inakaribia. Lakini, hatupaswe kuwa wakali, tunapaswa kuhangaikia hali ya wengine na kuepuka kuwahukumu. Tunaona watu wenye tunahubiria kuwa ndugu zetu wa kesho ao kesho yake, na vile Petro alifanya, tunakazia zaidi sana mambo yenye kufurahisha ya ujumbe wa Ufalme.
6. Namna gani Petro na Yohana walionyesha unyenyekevu na kiasi?
6 Wale mitume walikuwa na kiasi. Hawakusema kama walifanya ule muujiza kwa uwezo wao. Petro aliuliza wale watu hivi: “Sababu gani munashangazwa sana na jambo hili, na sababu gani munatuangalia kama vile ni kupitia nguvu zetu ao ni kupitia ushikamanifu wetu kwa Mungu?” (Mdo. 3:12) Petro na wale mitume wengine walijua kama kazi yao ilikuwa na matokeo ya muzuri, haiko juu ya nguvu zao wenyewe, lakini juu ya nguvu za Mungu. Walionyesha kiasi kwa kupatia Yehova na Yesu sifa kwa sababu ya matokeo ya muzuri yenye walipata.
7, 8. (a) Ni zawadi gani yenye tunaweza kutolea watu? (b) Ahadi ya “kurudishwa kwa mambo yote” inatimizwa namna gani leo?
7 Na siye tunapaswa kuonyesha kiasi wakati tunatangaza Ufalme. Ni kweli kama leo roho ya Mungu haipatie Wakristo nguvu ya kuponyesha watu kwa njia ya muujiza. Hata vile, tunaweza kusaidia watu waamini Mungu na Kristo na kupokea zawadi ileile yenye Petro aliahidi, ni kusema, kusamehewa zambi na kutulizwa na Yehova. Kila mwaka, mamia ya maelfu wanapokea ile zawadi, na kuwa wanafunzi wenye kubatizwa wa Kristo.
8 Kwa kweli tunaishi wakati wenye Petro aliita “wakati wa kurudishwa kwa mambo yote.” Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mbinguni mu mwaka wa 1914. Ile ilitimiza mambo yenye “Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu wa zamani.” (Mdo. 3:21; Zb. 110:1-3; Da. 4:16, 17) Wakati kidogo kisha pale, Yesu alianza kuongoza kazi ya kurudisha ao kuponyesha watu kiroho ku dunia. Mamilioni ya watu wameingizwa mu paradiso ya kiroho, na ile inafanya wakuwe raia wa Ufalme wa Mungu. Wamevua utu wa zamani na “kuvaa utu mupya wenye uliumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu.” (Efe. 4:22-24) Vile tu ilikuwa kuhusu kuponyeshwa kwa ule kilema, ile kazi imetimizwa kwa nguvu ya roho ya Mungu, hapana nguvu za wanadamu. Sawa Petro, tunapaswa kutumia Neno ya Mungu kwa uhodari na mu njia yenye kufaa wakati tunafundisha wengine. Matokeo yenye tunapata wakati tunasaidia watu wakuwe wanafunzi wa Kristo inatokana na nguvu ya Mungu, hapana nguvu zetu wenyewe.
“Hatuwezi Kuacha Kusema” (Mdo. 4:1-22)
9-11. (a) Viongozi wa Wayahudi walitenda namna gani wakati walisikia ujumbe wa Petro na Yohana? (b) Mitume waliazimia kufanya nini?
9 Hotuba ya Petro, na ile makelele ya kuruka-ruka ya ule mutu mwenye aliponyeshwa, ilitokeza fujo. Kapiteni wa hekalu mwenye alikuwa na kazi ya kuhakikisha usalama ku hekalu pamoya na wakubwa wa makuhani, wakakuya mbio juu ya kuona jambo yenye ilitokea. Inawezekana walikuwa Wasadukayo. Wasadukayo walikuwa kikundi ya matajiri wenye walikuwa na uvutano mu mambo ya politike; walijikaza kulinda uhusiano muzuri na Waroma, walikatala desturi zenye zilipendwa sana na Wafarisayo, na walipinga fundisho ya ufufuo.c Walikasirika kabisa wakati walikuta Petro na Yohana mu hekalu na wako wanafundisha bila woga kama Yesu alifufuliwa!
10 Wale wapinzani wenye kasirani walitupa Petro na Yohana mu gereza. Kisha siku yenye ilifuata wakawapeleka mbele ya tribinali kubwa ya Wayahudi. Wale watawala wenye kutafuta utukufu, waliona Petro na Yohana kuwa “watu wenye hawana elimu na watu wa kawaida” wenye hawakukuwa na haki ya kufundisha mu hekalu. Hawakusomea ku masomo ya kidini yenye kujulikana sana. Hata vile, maneno yao yenye kuwa wazi na yenye kusadikisha, ilishangaza sana watu. Nini njo ilisaidia Petro na Yohana? Jambo moya ni juu ‘walikuwaka pamoja na Yesu.’ (Mdo. 4:13) Tofauti kabisa na waandishi, Bwana wao alikuwa anafundisha kama mutu mwenye mamlaka.—Mt. 7:28, 29.
11 Ile tribinali ililazimisha wale mitume waache kuhubiri. Ile wakati, amri za ile tribinali ziliheshimiwa sana. Majuma fulani tu mbele ya pale, wakati Yesu alisamba mbele ya ileile tribinali, wenye kuifanyiza walisema hivi: “Anastahili kufa.” (Mt. 26:59-66) Hata vile, Petro na Yohana hawaogope. Wakiwa wenye kusimama mbele ya wale wanaume matajiri, wenye elimu, na wenye uvutano mukubwa, Petro na Yohana wanajibia hivi kwa heshima lakini bila woga: “Kama ni jambo lenye kuwa sawa mbele ya macho ya Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko kumusikiliza Mungu, muamue ninyi wenyewe. Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo yenye tumeona na kusikia.”—Mdo. 4:19, 20.
12. Nini inaweza kutusaidia tukuwe hodari na tuzungumuze kwa usadikisho zaidi?
12 Na weye unaweza kuonyesha uhodari wa vile? Unajisikiaka namna gani wakati unapata nafasi ya kuhubiria matajiri, watu wenye walisomaka sana, ao wenye kujulikana sana? Unafanyaka nini kama watu wa familia yako, wanafunzi wenzako, ao wafanyakazi wenzako wanakuchekelea juu ya imani yako? Unaogopaka? Kama ni vile, usivunjike moyo. Wakati Yesu alikuwa ku dunia, alifundisha mitume wake namna ya kutetea imani yao bila woga na kwa heshima. (Mt. 10:11-18) Kisha kufufuliwa, Yesu aliahidi wanafunzi wake kama angeendelea kuwa pamoya nao “mupaka umalizio wa mupangilio wa mambo.” (Mt. 28:20) Chini ya uongozi wa Yesu, “mutumwa muaminifu na mwenye busara” anatufundisha namna ya kutetea imani yetu. (Mt. 24:45-47; 1 Pe. 3:15) Anafanya vile kupitia mikutano, kama vile Utumishi na Maisha ya Mukristo, na kupitia vichapo vyenye kutegemea Biblia, sawa vile habari zenye kuwa ku sehemu “Majibu ya Maulizo juu ya Biblia,” yenye inapatikana ku jw.org. Uko unatumia muzuri vile vifaa? Ukifanya vile, utakuwa hodari na utazungumuza kwa usadikisho zaidi. Na sawa vile mitume walifanya, hautaacha kitu yoyote ikuzuie kuzungumuzia mambo ya muzuri ya kiroho yenye umeona na kusikia.
Usiache kitu yoyote ikuzuie kuzungumuzia mambo ya muzuri ya kiroho yenye umejifunza
“Wakapandisha Sauti Zao kwa Mungu” (Mdo. 4:23-31)
13, 14. Tukipata upinzani, tunapaswa kufanya nini, na juu ya nini?
13 Kisha tu kuachiliwa, Petro na Yohana walikutana na wengine mu kutaniko. Wote pamoja, “wakapandisha sauti zao kwa Mungu” na kumuomba awapatie uhodari wa kuendelea kuhubiri. (Mdo. 4:24) Petro alijua muzuri kama ni kukosa akili kujaribu kufanya mapenzi ya Mungu kwa kutegemea nguvu yake mwenyewe. Majuma fulani yenye ilikuwa imepita, Petro alijitumainia kupita kiasi na kuambia hivi Yesu: “Hata kama wengine wote wanakwazika kwa sababu ya mambo yenye yatakupata, mimi sitakwazika hata kidogo!” Lakini vile tu Yesu alitabiri, Petro aliogopa wanadamu na kumukana rafiki na mwalimu wake. Lakini, Petro aliacha makosa yake imufundishe.—Mt. 26:33, 34, 69-75.
14 Kama unapenda kuendelea kutoa ushahidi juu ya Kristo, haitoshe tu kuazimia kuhubiri. Wakati wapinzani wanajaribu kuvunja imani yako, ao kukuzuia usihubiri, fuata mufano wa Petro na Yohana. Umuombe Yehova akupatie nguvu. Tafuta musaada wa kutaniko. Ambia wazee na ndugu na dada wengine wenye kukomala kiroho magumu yenye uko nayo. Sala za wengine zinaweza kabisa kukutia nguvu.—Efe. 6:18; Yak. 5:16.
15. Kama uliacha kuhubiri kwa muda fulani, ni mufano gani unaweza kukutia moyo?
15 Kama wakati fulani uliacha kuhubiri juu ya upinzani, usivunjike moyo. Kumbuka kama, wakati Yesu alikufa, mitume wote waliacha kuhubiri kwa muda, lakini bila kukawia walianza tena kutenda. (Mt. 26:56; 28:10, 16-20) Kuliko kuendelea kujihukumu kwa sababu ya makosa yako ya zamani, uache ikufundishe. Na utumie mambo yenye umejifunza ili kutia wengine nguvu.
16, 17. Sala yenye wanafunzi wa Kristo walitoa kule Yerusalemu inaweza kutufundisha nini?
16 Wakati wenye mamlaka wanatutesa, tunapaswa kusali kuhusu nini? Kumbuka kama wanafunzi hawakuomba waepushwe na majaribu. Walikumbuka muzuri hii maneno ya Yesu: “Kama wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yoh. 15:20) Lakini wale wanafunzi washikamanifu waliomba Yehova ‘asikilize’ namna wapinzani wao waliwaogopesha. (Mdo. 4:29) Ni wazi kama wale wanafunzi walijua kama mapenzi ya Mungu njo jambo ya maana zaidi. Walitambua kama mateso yenye walikuwa wanapata ilikuwa utimizo wa unabii. Walijua kama, sawa vile Yesu aliwafundisha kusali, mapenzi ya Mungu ‘yangefanyika duniani,’ hata watawala wanadamu waseme nini.—Mt. 6:9, 10.
17 Juu ya kufanya mapenzi ya Mungu, wanafunzi waliomba Yehova hivi: ‘Uwawezeshe watumwa wako waendelee kutangaza neno lako bila woga wowote.’ Namna gani Yehova alijibia sala yao? “Mahali walikuwa wamekusanyika pamoja pakatetemeshwa, na wote wakajazwa roho takatifu na walikuwa wanasema neno la Mungu bila woga.” (Mdo. 4:29-31) Hakuna kitu yenye inaweza kuzuia mapenzi ya Mungu kufanyika. (Isa. 55:11) Hata hali zikuwe nguvu namna gani, ao adui akuwe nguvu namna gani, tukisali kwa Mungu, tunaweza kuwa hakika kama atatupatia nguvu ya kuendelea kusema neno yake bila woga.
Hawakutoa Hesabu ‘kwa Wanadamu, Lakini kwa Mungu’ (Mdo. 4:32–5:11)
18. Ndugu na dada wa kutaniko ya Yerusalemu walisaidiana namna gani?
18 Ndugu na dada wa ile kutaniko ya mupya yenye ilikuwa Yerusalemu waliongezeka na kuwa zaidi ya 5000.d Hata kama walikuwa watu wa kutokea fasi tofauti-tofauti, wanafunzi walikuwa na “moyo mumoja na nafsi moja.” Walikuwa wameunganishwa katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri. (Mdo. 4:32; 1 Ko. 1:10) Kisha wale wanafunzi kumuomba Yehova abariki bidii yao hawakufunga mikono. Walitegemezana kiroho na hata kimwili pia, wakati ilikuwa lazima. (1 Yo. 3:16-18) Kwa mufano, mwanafunzi Yosefu, mwenye mitume walikuwa wanaita Barnaba, aliuzisha shamba yake. Na kwa moyo wote akapatia mitume makuta yote. Mitume walitumia ile makuta juu ya kusaidia wale wenye walitoka mbali ili wakae Yerusalemu kwa muda murefu zaidi kusudi wajifunze mambo mingi zaidi kuhusu imani yao ya mupya.
19. Juu ya nini Yehova aliua Anania na Safira?
19 Anania na Safira pia waliuzisha mali yao na kutoa muchango. Walipenda kuonyesha kama wametoa makuta yote, kumbe walikuwa ‘wameficha kiasi fulani cha feza.’ (Mdo. 5:2) Yehova aliwaua, haiko juu muchango yenye walitoa ilikuwa kidogo, lakini ni juu nia yao ya kutoa ilikuwa mubaya na tena walidanganya. ‘Hawakudanganya wanadamu, lakini walimudanganya Mungu.’ (Mdo. 5:4) Sawa tu wanafiki wenye Yesu alilaumu, Anania na Safira walitaka sana kusifiwa na wanadamu kuliko kutafuta kukubaliwa na Mungu.—Mt. 6:1-3.
20. Tunajifunza nini kuhusu michango yenye tunatoa?
20 Kama vile wanafunzi waaminifu wa karne ya kwanza walifanyaka kule Yerusalemu, leo, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wanaonyesha roho ya ukarimu kwa kutegemeza kazi ya kuhubiri mu dunia yote kupitia michango yao ya kujipendea. Hakuna mwenye anawalazimisha watumie wakati wao ao makuta yao juu ya kutegemeza kazi ya Ufalme. Kwa kweli, Yehova hapendi tumutumikie “kwa kutokupenda wala kwa kulazimishwa.” (2 Ko. 9:7) Wakati tunatoa michango yetu, Yehova haangaliake wingi wa makuta yenye tunatoa, lakini nia yetu. (Mk. 12:41-44) Hatupendi kuwa kama Anania na Safira hata kidogo kwa kumutumikia Mungu ili kujitafutia faida na kujitafutia sifa. Lakini, kama Petro, Yohana, na Barnaba, upendo wa kweli kwa Mungu na kwa wanadamu wenzetu njo utuchochee kumutumikia Yehova.—Mt. 22:37-40.
a Mu hekalu, sala zilikuwa zinatolewa wakati wa zabihu ya asubui na ya mangaribi. Zabihu ya mangaribi ilikuwa inatolewa “saa ya kenda (15h00 hivi).”
b Ona kisanduku “Petro—Muvuaji wa Samaki Anakuwa Mutume Mwenye Bidii,” na pia “Yohana—Mwanafunzi Mwenye Yesu Alipenda.”
c Ona kisanduku yenye kichwa “Kuhani Mukubwa na Wakubwa wa Makuhani.”
d Mu mwaka wa 33 K.K.Y., pengine kulikuwa Wafarisayo karibu 6000 na hesabu kidogo ya Wasadukayo mu muji wa Yerusalemu. Vile vikundi mbili vilipenda kulinda mamlaka yao. Pengine ile ni sababu ingine yenye ilifanya wajaribu kuzuia wanafunzi kufundisha juu ya Yesu.