Tuwe Tayari Kusameheana
“Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.”—KOL. 3:13.
UTAJIBU NAMNA GANI?
Sababu gani tunapaswa kuwa tayari kusamehe?
Yesu alitumia mufano gani ili kuonyesha kwamba tunapaswa kusamehe?
Tutapata baraka gani kwa kuwa tayari kusameheana?
1, 2. Sababu gani tuchunguze ikiwa tuko tayari kuwasamehe wengine?
NENO la Mungu linatufundisha namna anavyoona zambi na jambo analofanya tunapotenda zambi. Neno lake linatufundisha mengi kuhusu kuwasamehe wengine. Katika habari iliyotangulia, tulijifunza kwa nini Yehova aliwasamehe Daudi na Manase. Kwa kuwa walihuzunika sana kwa sababu ya makosa yao na kutubu, ni kusema, kuacha matendo yao mabaya, Yehova aliwakubali tena.
2 Acheni tuzungumuzie namna sisi pia tunavyoweza kuwasamehe wengine. Ungejisikia namna gani ikiwa mutu fulani wa jamaa yako alikufa kwa sababu ya mambo ambayo Manase alifanya? Je, ungemusamehe Manase? Si vyepesi kujibu ulizo hilo kwa sababu tunaishi katika ulimwengu muovu, wenye jeuri, na wenye kujaa watu wanaotafuta faida zao wenyewe. Sababu gani basi Mukristo anapaswa kuwa na roho ya kuwasamehe wengine? Ikiwa unatendewa vibaya, ni nini itakusaidia utulizane, utende namna Yehova anavyotaka, na kuwa tayari kusamehe?
SABABU GANI TUNAPASWA KUWASAMEHE WENGINE?
3-5. (a) Yesu alitoa mufano gani ili kuwasaidia wasikilizaji wake waone ulazima wa kuwasamehe wengine? (b) Yesu alipenda kufundisha nini katika mufano wake unaopatikana katika Mathayo 18:21-35?
3 Ikiwa tunataka kuendelea kuishi kwa amani na ndugu na dada zetu katika kutaniko, watu wa familia yetu, marafiki zetu, na pia Yehova, tunapaswa kuwa tayari kuwasamehe wale wanaotukosea. Maandiko yanatutia moyo sisi Wakristo kuwasamehe wengine hata ikiwa wanatukosea mara nyingi. Ili tujue sababu gani tunapaswa kuwasamehe wengine, acheni tuzungumuzie mufano wa mutumwa aliye kuwa na deni kubwa la bwana wake.
4 Mutumwa huyo alikuwa na deni kubwa la bwana wake, ili kulipa deni hilo alipaswa kumutumikia bwana wake siku milioni 60; hata hivyo, bwana wake alizima deni hilo. Baadaye, mutumwa huyo alimufuata mutumwa mwenzake aliyekuwa na deni lake; ili mutumwa mwenzake alipe deni hilo alipaswa kutumika siku 100 tu. Mutumwa mwenzake alimuomba amuvumilie, lakini yeye alikataa na akamufungisha ijapokuwa alikuwa amesamehewa deni kubwa. Bwana wake aliposikia habari hiyo alikasirika sana. Kwa hiyo, aliuliza hivi ‘Haikukupasa wewe, nawe, kuwa na rehema juu ya mutumwa mwenzako, kama mimi pia nilivyokuwa na rehema juu yako?’ ‘Ndipo bwana wake, akiwa na gazabu, akamutia [mutumwa huyo asiyesamehe] mikononi mwa walinzi wa jela, mupaka alipe deni lake lote.’—Mt. 18:21-34.
5 Yesu alipenda kufundisha nini kupitia mufano huu? Alimalizia kusema hivi: ‘Vivyo hivyo Baba yangu wa mbinguni atashughulika nanyi pia ikiwa kila mumoja wenu hatamusamehe ndugu yake kutoka moyoni mwake.’ (Mt. 18:35) Mufano huo wa Yesu unafaa kabisa. Kwa sababu sisi ni wanadamu wasio wakamilifu, zambi tunazofanya kila siku zinaonyesha kama ni vigumu kwetu kumutii Mungu kwa ukamilifu. Hata hivyo, Yehova iko tayari kutusamehe na kusahau makosa yetu. Kwa hiyo, kila mutu anayetaka kuwa rafiki ya Yehova anapaswa kuwasamehe wengine. Kama vile Yesu alivyosema katika Mahubiri yake ya Mulimani: ‘Ikiwa munawasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia; lakini ikiwa hamutawasamehe watu makosa yao, Baba yenu naye hatawasamehe makosa yenu.’—Mt. 6:14, 15.
6. Sababu gani siku zote si vyepesi kuwasamehe wengine?
6 Ni vyepesi kusema ‘nitamusamehe,’ lakini kusamehe si jambo jepesi. Si vyepesi kwa sababu wakati mutu anatukosea hilo linaweza kusumbua sana. Jambo hilo linaweza kutukasirisha, kutufanya tufikiri kama wengine wametusaliti, na tunaweza kutaka yule aliyetukosea aazibiwe, ao hata tunaweza kutaka kulipiza kisasi. Kwa hiyo, watu fulani wanafikiri kama hawaweze kumusamehe hata kidogo yule aliyewakosea. Ikiwa unajisikia hivyo, namna gani unaweza kumuiga Yehova kwa kuonyesha roho ya kuwasamehe wengine?
TAFUTA KUJUA KWA NINI UNAKASIRIKA
7, 8. Ikiwa umeumizwa na matendo ya wengine, ni nini itakayokusaidia uonyeshe roho ya kusamehe?
7 Mutu anaweza kukasirika kwa sababu ametendewa vibaya ao anawazia kama wamemutendea hivyo. Fikiria namna kijana mumoja alivyojisikia alipokuwa na hasira. Yeye alieleza hivi: “Wakati mumoja . . . kwa sababu ya hasira, niliondoka nyumbani nikiapa kama sitarudi tena. Ilikuwa siku nzuri wakati wa joto, na nilitembea safari ndefu katika barabara ndogo zenye kupendeza, mupaka wakati utulivu ulio katika barabara hizo na vitu vizuri nilivyoona vilinituliza, kisha saa fulani hasira yangu ilipunguka, nami nilirudi nyumbani.” Mufano wa kijana huyo unatufundisha kwamba kisha kutulizana tunapaswa kuchunguza sababu zilizotufanya tukasirike. Kufanya hivyo kutatusaidia tuepuke kutenda mambo yatakayokufanya tujute baadaye.—Zab. 4:4; Met. 14:29; Yak. 1:19, 20.
8 Lakini, unaweza kufanya nini ikiwa hasira inaendelea? Jaribu kujua sababu gani umekasirika. Unaweza kujiuliza: Je, mutu huyo hakunitendea kwa haki, ao alinikosea adabu? Ao, je, ninafikiri kwamba alinikosea kwa makusudi? Je, jambo alilonitendea ni kosa kabisa? Kuchunguza sababu zilizokufanya ukasirike kutakusaidia umutendee yule aliyekukosea kwa njia inayofaa zaidi na inayolingana na Maandiko. (Soma Methali 15:28; 17:27.) Kujichunguza hivyo kutakusaidia uelewe mambo waziwazi na kuwa tayari kusamehe. Ni kweli kwamba si rahisi, lakini unapofanya hivyo unaruhusu Neno la Mungu likusaidie kuchunguza “fikira na makusudio ya moyo [wako]” na hilo litakusaidia umuige Mungu kwa kuwasamehe wengine.—Ebr. 4:12.
JE, UNA SABABU YA KUKASIRIKA?
9, 10. (a) Utatenda namna gani unapofikiri kama una sababu ya kukasirika? (b) Kuwa na maoni mazuri na kuwasamehe wengine kutakusaidia namna gani maishani?
9 Katika maisha kuna mambo mengi yanayoweza kutukasirisha. Kwa mufano, unapotembeza motokari, labda unaweza kugongwa na motokari ingine. Utafanya nini? Labda umekwisha kusikia ao kujionea namna washofere walivyogombana kwa sababu ya jambo hilo. Lakini, kwa sababu wewe ni Mukristo, haupaswe kufanya hivyo.
10 Ni vizuri kuchukua wakati ili kufikiria mambo yaliyotokea. Labda wewe pia haukuwa mwangalifu kwa njia fulani. Ao labda shofere mwenzako alikugonga kwa sababu gari lake lilikuwa na tatizo fulani. Kupitia mufano huu tunajifunza kwamba ili tutulizane tunapokasirishwa, tunapaswa kuelewa kwa nini mutu fulani alitukosea, kwamba hatuweze kuelewa kila jambo lilitokeza aksida hiyo na tunapaswa kuwa tayari kusamehe. Andiko la Mhubiri 7:9 linasema hivi: ‘Usiwe na haraka kuuzika katika roho yako kwa maana kuuzika hukaa katika kifua cha wajinga.’ Kwa hiyo, jiulize ikiwa una sababu ya kukasirika. Mara nyingi tunaweza kufikiri kama wale waliotukosea walifanya hivyo kwa makusudi, lakini labda wamefanya hivyo kwa sababu tu ya kutokamilika. Tafuta kuelewa vizuri mambo waliyofanya ao maneno waliyosema yaliyokukasirisha na uwe tayari kusamehe kwa upendo. Ukifanya hivyo, utakuwa mwenye furaha zaidi.—Soma 1 Petro 4:8.
‘ACHA AMANI YAKO IKURUDILIE’
11. Tunapaswa kutenda namna gani wakati watu wanakataa kusikiliza ujumbe wetu?
11 Namna gani unaweza kujizuia ikiwa mutu fulani anakukosea adabu katika mahubiri? Mbele ya kuwatuma wanafunzi 70 kuhubiri, Yesu aliwaambia kwamba wanapaswa kutakia amani kila nyumba wanayotembelea. Yesu alisema hivi: ‘Ikiwa rafiki wa amani yumo, amani yenu itakaa juu yake. Lakini ikiwa hayumo, itawarudilia ninyi.’ (Lu. 10:1, 5, 6) Tunafurahi wakati watu wanakubali ujumbe wetu kwa sababu unaweza kuwaletea faida. Lakini wakati fulani watu hawatusikilize. Tunapaswa kufanya nini basi? Yesu alisema kama amani tuliyotakia nyumba hiyo inapaswa kuturudilia. Katika hali yoyote, tunapaswa kuachana na watu kwa amani hata ikiwa hawakutusikiliza. Kukasirika wakati watu wanapinga ujumbe wetu hakuweze kutusaidia kulinda amani yetu.
12. Tunapaswa kutenda namna gani kulingana na maneno ya Paulo kwenye Waefeso 4:31, 32?
12 Jikaze kulinda amani yako si katika mahubiri tu lakini pia katika hali zingine. Kwa kawaida, unapowasamehe wengine hiyo haimaanishe kama ulifurahia mambo mabaya waliyofanya ao hayakukuumiza. Lakini kusamehe wengine kunamaanisha kutowawekea hasira na kutulizana. Kuendelea kukasirika na kuendelea kufikiria namna walivyotukosea kunaweza kutuondolea furaha yetu. Tusiache hasira itutawale. Kumbuka kwamba hatuweze kuwa na furaha ikiwa tunaendelea kuwawekea wengine hasira. Kwa hiyo, tuwe wenye kusamehe!—Soma Waefeso 4:31, 32.
TENDA KWA NJIA INAYOMUPENDEZA YEHOVA
13. (a) Namna gani Mukristo anaweza ‘kukusanya makaa yenye moto’ juu ya kichwa cha adui yake? (b) Kutenda kwa upole kunaweza kuleta matokeo gani?
13 Wakati fulani unaweza kupenda kumusaidia mutu aliyekukosea ili apendezwe na kanuni za Kikristo. Mutume Paulo aliandika hivi: “‘Ikiwa adui yako ana njaa, mulishe; ikiwa ana kiu, mupe kitu anywe; kwa maana kwa kufanya hivyo utakusanya makaa yenye moto juu ya kichwa chake.’ Usiache ushindwe na uovu, bali endelea kuushinda uovu kwa wema.” (Rom. 12:20, 21) Ikiwa unatenda kwa adabu wakati watu wanakukosea adabu, unaweza kusaidia hata watu wakali zaidi kubadilika na kuanza kutenda mambo mazuri. Ikiwa unamuelewa mutu aliyekukosea na kujitia pa nafasi yake, unaweza kumusaidia ajifunze Biblia. Katika hali yoyote, ukitenda kwa upole unaweza kumufanya yule aliyekukosea apendezwe na mwenendo wako muzuri.—1 Pet. 2:12; 3:16.
14. Hata ikiwa tumeumizwa sana na zambi ya mutu fulani, sababu gani hatupaswe kumuwekea hasira?
14 Katika hali fulani, haingefaa kufanya urafiki na watu fulani. Watu hao wanatia ndani mutu ambaye zamani alikuwa Shahidi wa Yehova lakini alitengwa kwa sababu hakutubu. Ikiwa uliumizwa kwa sababu alifanya zambi nzito, labda inaweza kuwa vigumu kwako kumusamehe. Hata kama anatubu unaweza kuendelea kuumizwa moyoni kwa sababu ya zambi aliyofanya. Katika hali kama hizo, unaweza kuendelea kumuomba Yehova akusaidie ili umusamehe mukosaji huyo ambaye ametubu. Haujue mambo yaliyo katika moyo wake, lakini Yehova anajua. Anachunguza mawazo ya ndani ya mutu na anawavumilia wakosaji. (Zab. 7:9; Met. 17:3) Hiyo ndiyo sababu Biblia inasema hivi: “Musimulipe yeyote uovu kwa uovu. Fanyeni mambo mema machoni pa watu wote. Ikiwezekana, kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, musijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi gazabu; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’” (Rom. 12:17-19) Je, una haki ya kumuhukumu mutu mwengine? Hapana. (Mt. 7:1, 2) Lakini uwe hakika kwamba Yehova ndiye anayehukumu kwa haki.
15. Ni nini itatusaidia tusimuwekee hasira yule ambaye ametukosea?
15 Ikiwa unafikiri kama mutu fulani amekukosea sana na kama hautaweza kumusamehe hata kama ametubu, unapaswa kukumbuka kwamba yeye pia anapambana na tatizo fulani kubwa. Yeye pia ameriti kutokamilika. (Rom. 3:23) Yehova anawasikilia huruma wanadamu wote wasio wakamilifu. Kwa hiyo, tunapaswa kumuombea yule aliyetukosea. Ni wazi kwamba hatutaendelea kumuwekea hasira mutu tunayeombea. Pia maneno ya Yesu yanatuonyesha waziwazi kwamba hatupaswe kuendelea kuwawekea wengine hasira. Yeye alisema hivi: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.”—Mt. 5:44.
16, 17. Unapaswa kufanya nini wakati wazee wanaamua kwamba mukosaji ametubu, na sababu gani?
16 Yehova amewapa wazee Wakristo daraka la kushugulikia mambo katika kutaniko. Ndugu hao hawawezi kuelewa waziwazi mambo yote kama Mungu anayejua kila jambo, lakini wanajikaza kuchukua uamuzi unaopatana na Neno la Mungu na wanatafuta uongozi wa roho takatifu. Kwa hiyo, uamuzi wanaochukua kisha kutafuta musaada wa Yehova katika sala, utapatana na maoni yake.—Mt. 18:18.
17 Katika hali kama hii, tunapaswa kuwa waaminifu. Je, utamusamehe mukosaji anayetubu na kumuonyesha kama unamupenda? (2 Kor. 2:5-8) Labda haitakuwa rahisi kufanya hivyo, zaidi sana ikiwa kosa lake lilikuumiza wewe ao mushiriki wa familia yako. Hata hivyo, kumutumaini Yehova na namna anavyoshugulikia mambo, kutakusaidia kutenda kwa hekima na kuwa tayari kusamehe kabisa.—Met. 3:5, 6.
18. Utapata faida gani ukiwa tayari kusamehe?
18 Waganga wanaotunza magonjwa ya akili wanajua faida ya kuwa tayari kusamehe wengine. Kusamehe kunatusaidia tutulizane, tuwe na afya nzuri kwa sababu kunaondoa mambo yanayoharibu afya kama vile huzuni na hasira, na kunatusaidia kufurahia uhusiano muzuri pamoja na wengine. Lakini kukataa kusamehe kunaharibu afya, urafiki, kunaleta huzuni na kutoelewana. Baraka kubwa sana unayoweza kufurahia kwa sababu ya kuwa tayari kusamehe ni uhusiano muzuri pamoja na Baba yetu wa mbinguni, Yehova.—Soma Wakolosai 3:12-14.
[Picha katika ukurasa wa 27]
Mufano huu wa Yesu unatufundisha nini?
[Picha katika ukurasa wa 30]
Wakristo wanaombwa kuwa tayari kusamehe