Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • bt sura 27 uku. 211-217
  • “Kutoa Ushahidi Kamili”

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • “Kutoa Ushahidi Kamili”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili” juu ya Ufalme wa Mungu
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • “Akamushukuru Mungu na Akajipa Uhodari” (Mdo. 28:14, 15)
  • “Linasemwa Mubaya Kila Mahali” (Mdo. 28:16-22)
  • Paulo Anatuachia Mufano kwa “Kutoa Ushahidi Kamili” (Mdo. 28:23-29)
  • ‘Kuhubiri Ufalme wa Mungu’ (Mdo. 28:30, 31)
  • Ukuwe Hodari​—Yehova Ni Musaidizi Wako
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2020
  • “Niko Safi Kutokana Na Damu ya Watu Wote”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” juu ya Ufalme wa Mungu
  • “Musikilize . . . Namna Ninajitetea”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” juu ya Ufalme wa Mungu
  • Paulo Anapelekwa Roma
    Mambo yenye unaweza kujifunza katika Biblia
“Kutoa Ushahidi Kamili” juu ya Ufalme wa Mungu
bt sura 27 uku. 211-217

SURA YA 27

“Kutoa Ushahidi Kamili”

Paulo mwenye amefungwa katika Roma anaendelea kuhubiri

Inategemea Matendo 28:11-31

1. Paulo na wenzake walikuwa hakika juu ya jambo gani, na juu ya nini?

MASHUA yenye kuwa na sanamu ya “Wana wa Zeu,” yenye inawezekana ni mashua kubwa yenye kubeba mbegu, iko natoka mu kisiwa ya Malta mu Mediterania na iko naenda Italia. Ni mwaka wa 59 hivi K.K.Y. Mu ile mashua muko Paulo, mufungwa mwenye anasindikizwa na maaskari, na muko pia Wakristo wenzake, Luka na Aristarko. (Mdo. 27:2) Tofauti na watu wenye kutumika mu ile mashua, wale waeneza-injili hawatafute ulinzi wa Castor na Pollux, wana wa Zeu, mungu wa Wagiriki. Lakini, Paulo na wenzake wanamutumikia Yehova, mwenye alimuambia Paulo kama atatoa ushahidi katika Roma na atasimama mbele ya Kaisari.​—Mdo. 23:11; 27:24.

2, 3. Mashua yenye Paulo iko ndani inapitia wapi, na ni nani alimutegemeza mu safari yote?

2 Siku tatu kisha kusimama Sirakusi, muji wa Sisili wenye kupendeza na wenye ulikuwa wa maana sawa vile Atene na Roma, mashua iliondoka na kuelekea Regiamu, kusini mwa Italia. Kisha ilisukumwa na upepo wa kutoka kusini na kufanya safari ya kilometre 320 mupaka ku bandari ya Italia ya Puteoli (karibu na Naple ya leo). Mu ile safari mashua ilienda haraka sana na ikafika Puteoli siku ya pili kwa sababu ya ule upepo muzuri.​—Mdo. 28:12, 13.

3 Sasa Paulo iko mu sehemu ya mwisho ya safari yake ya kuenda Roma, kwenye atasamba mbele ya Mutawala Nero. Mu safari, “Mungu wa faraja yote” alikuwa pamoya na Paulo. (2 Ko. 1:3) Sawa vile tutaona, Yehova aliendelea kumutegemeza, na Paulo aliendelea kuwa na bidii mu kazi yake ya umisionere.

“Akamushukuru Mungu na Akajipa Uhodari” (Mdo. 28:14, 15)

4, 5. (a) Namna gani Paulo na wenzake walionyeshwa ukaribishaji-wageni wakati walifika Puteoli, na juu ya nini pengine Paulo alipewa uhuru mwingi? (b) Mwenendo muzuri wa Wakristo unawasaidia namna gani hata kama wako mu gereza?

4 Wakati walifika Puteoli, Paulo na wenzake ‘walikuta pale ndugu na wakawaomba kwa mukazo wakae pamoja nao kwa siku saba (7).’ (Mdo. 28:14) Ule ni mufano muzuri kabisa wenye Wakristo wanapaswa kuiga kuhusu kuonyesha ukaribishaji-wageni! Bila shaka wale ndugu wenye walionyesha ile sifa, walibarikiwa zaidi kwa kutiwa moyo na Paulo na wenzake. Lakini juu ya nini mufungwa alipewa ile uhuru yote? Pengine ni juu matendo ya Paulo ilifanya walinzi Waroma wamutumainie.

5 Leo pia, watumishi wa Yehova, hata kama wako mu gereza ao mu kambi za mateso, wanapewa uhuru ao nafasi ya kufanya mambo fulani kwa sababu ya mwenendo wao muzuri. Kwa mufano katika Romania, mwanaume mwenye alihukumiwa miaka 75 kwa sababu ya wizi, alianza kujifunza Biblia na akabadilisha sana maisha yake. Kwa hiyo, wenye kusimamia gereza walimutuma aende mu muji yeye peke ili kuuza vitu kwa ajili ya gereza. Zaidi ya yote. Mwenendo wetu muzuri unamutukuza Yehova.​—1 Pe. 2:12.

6, 7. Namna gani ndugu wa Roma walionyesha upendo mukubwa?

6 Inawezekana Paulo na wenzake walitembea kilometre 50 hivi kutoka Puteoli mupaka Kapua mu Njia ya Apio yenye ilikuwa inapeleka Roma. Ile barabara yenye kujulikana ilitengenezwa kwa majiwe makubwa-makubwa. Mutu mwenye kusafiri mu ile barabara angeweza kuona maeneo yenye kupendeza ya vijiji vya Italia na angeweza hata kuona Bahari ya Mediterania. Ile barabara ilipita pia mu eneo ya tingi-tingi yenye kuitwa Pontine Marshes, yenye ilikuwa ku kilometre 60 hivi kutoka Roma na kutoka kwenye Soko ya Apio ilikuwa. Luka aliandika kama wakati ndugu katika Roma “walisikia habari zetu,” wamoja walikuja mupaka ku ile soko, na wengine walingojea fasi ya kupumuzikia yenye iliitwa Mikahawa Tatu yenye ilikuwa ku kilometre 50 hivi kutoka Roma. Bila shaka walionyesha upendo mukubwa sana!​—Mdo. 28:15.

7 Soko ya Apio haikukuwa fasi ya muzuri ya kupumuzikia kisha kufanya safari ya kuchokesha sana. Horace, mwandikaji Muroma wa mashairi, alisema kama ile soko “iliyala watu wenye kutumika mu mashua. Na watu wenye kutumika fasi za kupumuzikia hawakuheshimia watu.” Aliandika pia kama “maji ya mu ile soko haikukuwa ya muzuri.” Na hata alikatala kukula pale! Hata kama hali haikukuwa muzuri mu ile soko, ndugu kutoka Roma walingoya Paulo na wenzake kwa furaha ili wawasindikize kwa usalama mu sehemu ya mwisho ya safari yao.

8. Juu ya nini Paulo alimushukuru Mungu wakati aliona ndugu zake?

8 Biblia inasema kama ‘wakati Paulo aliona’ ndugu zake, “akamushukuru Mungu na akajipa uhodari.” (Mdo. 28:15) Kwa kweli, wakati tu Paulo aliona ndugu zake, pengine alijua wamoja kati yao, alitiwa nguvu na kufarijiwa. Juu ya nini Paulo alimushukuru Mungu? Ni juu alijua kama upendo wa kweli ni sehemu ya tunda la roho. (Gal. 5:22) Leo pia, roho takatifu inachochea Wakristo wajitoe kwa ajili ya wengine na kufariji wale wenye kuwa na lazima ya musaada.​—1 Te. 5:11, 14.

9. Namna gani tunaweza kuiga ndugu wa Roma wenye walikuya kukutana na Paulo?

9 Kwa mufano, roho takatifu inachochea ndugu wakaribishe waangalizi wa muzunguko, wamisionere, na watumishi wengine wa wakati wote. Wengi kati yao wamejitoa na kujiima mambo mingi ili kumutumikia Yehova zaidi. Ujiulize hivi: ‘Ninaweza kufanya mambo mingi zaidi ili kutegemeza ziara ya mwangalizi wa muzunguko, pengine kwa kumukaribisha yeye na bibi yake kama alishaoa? Ninaweza kufanya mipango ili kuhubiri pamoja nao?’ Ukifanya vile unaweza kupata baraka mingi. Kwa mufano wazia furaha yenye ndugu wa Roma walikuwa nayo wakati Paulo na wenzake waliwaelezea mambo fulani yenye kutia moyo yenye walikutana nayo.​—Mdo. 15:3, 4.

“Linasemwa Mubaya Kila Mahali” (Mdo. 28:16-22)

10. Paulo alikuwa mu hali gani katika Roma, na alifanya nini muda kidogo kisha tu kufika?

10 Mwishowe wakati Paulo na wenye walikuwa naye walifika Roma, “Paulo aliruhusiwa kukaa peke yake akiwa na askari wa kumulinda.” (Mdo. 28:16) Kwa kawaida ili wafungwa wenye walifungiwa ku nyumba wasikimbie walifunga mufungwa munyororo na waliifunga pia ku mulinzi. Lakini juu Paulo alikuwa muhubiri wa Ufalme, ile munyororo haikumunyamazisha. Kisha kupumuzika kwa siku tatu kwa sababu ya ile safari yenye kuchokesha, aliita pamoja wanaume wenye vyeo wa Wayahudi katika Roma ili kujitambulisha na kuwatolea ushahidi.

11, 12. Wakati Paulo alikuwa nazungumuza na Wayahudi wenzake, alisema nini ili wamusikilize bila kumubagua?

11 Paulo akasema hivi: “Wanaume, ndugu, hata kama sikufanya jambo lolote kinyume na watu ao desturi za mababu zetu, nilitolewa nikiwa mufungwa kutoka Yerusalemu na nikatiwa katika mikono ya Waroma. Na kisha kufanya uchunguzi, walitaka kuniacha huru, kwa maana hapakukuwa sababu yoyote ya kuniua. Hata hivyo, wakati Wayahudi walipinga, nililazimika kuomba kesi yangu ya hukumu isikilizwe na Kaisari, lakini haiko kwa sababu nilikuwa na jambo fulani la kushitaki taifa langu.”​—Mdo. 28:17-19.

12 Kwa kuita Wayahudi wenye walikuwa wanamusikiliza “ndugu,” Paulo alipenda kuonyesha kama alikuwa mumoja wao na alipenda wasimubague juu ya mambo yenye pengine walikuwa wamesikia juu yake. (1 Ko. 9:20) Pia, Paulo alionyesha wazi kama hakukuya Roma ili kushitaki Wayahudi wenzake, lakini ili kusikilizwa na Kaisari. Lakini Wayahudi wenye walikuwa Roma hawakukuwa wamepata habari kuhusu ombi ya Paulo ya kusikilizwa na Kaisari. (Mdo. 28:21) Juu ya nini Wayahudi wa Yudea hawakukuwa wamefikishia wenzao ile habari? Kitabu fulani inasema hivi: “Inawezekana mashua yenye Paulo alisafiri ndani njo ilikuwa kati ya mashua za kwanza kufika Italia kisha kipindi ya baridi. Pengine juu mashua hazikuzoea kusafiri mu ile kipindi, wakubwa wa Wayahudi walikuwa hawayatuma mutu ao barua ili kuelezea wenzao kesi ya Paulo.”

13, 14. Paulo alisema nini ili kuzungumuzia Ufalme, na namna gani tunaweza kuiga mufano wake?

13 Ili kuzungumuzia habari ya Ufalme, Paulo anataja jambo fulani yenye ingefanya wale Wayahudi wapende kumusikiliza. Anasema hivi: “Kwa sababu hii niliomba kuwaona ninyi na kuzungumuza na ninyi, kwa maana nimefungwa munyororo huu kwa sababu ya tumaini la Israeli.” (Mdo. 28:20) Tumaini yenye Wakristo walikuwa wanahubiri ilikuwa kuhusu Masiya na Ufalme wake. Kisha wazee Wayahudi wakajibia hivi: “Lakini tunaona inafaa kukusikia wewe ili kujua mawazo yako, kwa maana kwa kweli juu ya zehebu hili, tunajua linasemwa mubaya kila mahali.”​—Mdo. 28:22.

14 Wakati tuko na nafasi ya kuhubiria wengine habari njema, tunaweza kumuiga Paulo kwa kutumia maneno ao maulizo yenye itachochea watu watusikilize. Tunaweza kupata mapendekezo ya kutusaidia kufanya vile mu kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na broshua Fanya Bidii Katika Kusoma na Kufundisha. Uko natumikisha muzuri vile vichapo?

Paulo Anatuachia Mufano kwa “Kutoa Ushahidi Kamili” (Mdo. 28:23-29)

15. Namna Paulo alitoa ushahidi inatufundisha mambo gani ine?

15 Paulo alipanga kukutana siku ingine na Wayahudi wenye ‘walikuja wakiwa wengi zaidi’ fasi kwenye Paulo alikuwa anaishi. Paulo aliwafasiria maandiko “kuanzia asubui mupaka mangaribi . . . kwa kutoa ushahidi kamili juu ya Ufalme wa Mungu, akiwasadikisha juu ya Yesu kwa kutumia Sheria ya Musa na pia Manabii.” (Mdo. 28:23) Namna Paulo alitoa ushahidi inaweza kutufundisha mambo ine. Kwanza, alikazia Ufalme wa Mungu. Pili, alizungumuza mu namna yenye kusadikisha wasikilizaji wake. Tatu, alifikiri nao kupitia Maandiko. Ine, alitia mahitaji ya wasikilizaji wake pa nafasi ya kwanza kwa kuhubiri “kuanzia asubui mupaka mangaribi.” Alituachia mufano muzuri kabisa! Matokeo ilikuwa nini? “Wamoja wakaanza kuamini,” lakini wengine hawakuamini. Luka anasema kama mugawanyiko ukatokea na watu “wakaanza kuondoka.”​—Mdo. 28:24, 25a.

16-18. Juu ya nini Paulo hakushangala kuona Wayahudi fulani wanakatala kumusikiliza, na tunapaswa kutenda namna gani wakati watu wanakatala kutusikiliza?

16 Namna watu walitenda, haikumushangaza Paulo kwa sababu ilipatana na unabii wa Biblia. Tena haikukuwa mara ya kwanza kwa Paulo kuona mambo ya vile. (Mdo. 13:42-47; 18:5, 6; 19:8, 9) Wakati wale wenye walikatala kumusikiliza walikuwa wanaondoka, Paulo aliwaambia hivi: “Roho takatifu ilisema kwa kufaa kupitia nabii Isaya kwa mababu zenu, ikisema, ‘Uende kwa watu hawa na useme: “Kwa kweli mutasikia lakini hamutaelewa hata kidogo, na kwa kweli mutaangalia lakini hamutaona hata kidogo. Kwa maana moyo wa watu hawa umekuwa mugumu.”’” (Mdo. 28:25b-27) Neno ya mu luga ya kwanza-kwanza yenye kutafsiriwa “mugumu,” inaonyesha kama moyo umekuwa “nguvu-nguvu” ao “umeyala mafuta” mupaka ujumbe wa Ufalme unashindwa kuingia ndani. (Mdo. 28:27) Ilihuzunisha kabisa!

17 Kwa kumalizia Paulo alisema kama tofauti na Wayahudi wenye walikatala kumusikiliza, watu wa ‘mataifa . . . hakika wao watasikiliza.’ (Mdo. 28:28; Zb. 67:2; Isa. 11:10) Kwa kweli Paulo alizungumuzia ile jambo kwa uhakika kwa sababu yeye mwenyewe alijionea namna Watu wa Mataifa walikubali ujumbe wa Ufalme!​—Mdo. 13:48; 14:27.

18 Kama Paulo, tusikwazike wakati watu wanakatala kusikiliza habari njema. Tunajua muzuri kama ni watu kidogo tu njo watapata barabara yenye kuongoza kwenye uzima. (Mt. 7:13, 14) Zaidi ya ile wakati watu wenye mutazamo muzuri wanakubali kweli, tufurahi na tuwakaribishe kwa moyo wote.​—Lu. 15:7.

‘Kuhubiri Ufalme wa Mungu’ (Mdo. 28:30, 31)

19. Paulo alifanya nini wakati alikuwa mufungwa?

19 Luka anamalizia habari yake kwa kusema hii maneno yenye kugusa moyo: “[Paulo] akakaa kule kwa miaka mbili ya kuenea katika nyumba yake ya kupanga, na alikuwa anapokea kwa fazili wale wote wenye walikuwa wanakuja kwake, na alikuwa anawahubiria Ufalme wa Mungu na kuwafundisha juu ya Bwana Yesu Kristo kwa uhuru mwingi wa kusema, bila kizuizi.” (Mdo. 28:30, 31) Paulo alikuwa mukaribishaji-wageni, alikuwa na imani, na alikuwa na bidii. Bila shaka alikuwa mufano muzuri!

20, 21. Zungumuzia mifano ya watu wenye utumishi wa Paulo katika Roma uliletea faida.

20 Kati ya watu wenye Paulo alipokea kwa upendo, kulikuwa mwanaume mwenye kuitwa Onesimo; alikuwa mutumwa mwenye alikimbia kutoka Kolosai. Paulo alisaidia Onesimo kuwa Mukristo na Onesimo akakuwa ‘ndugu muaminifu na mupendwa’ kwa Paulo. Na hata Paulo alimuita, “mutoto wangu . . . mwenye nimekuwa baba yake.” (Kol. 4:9; Flm. 10-12) Bila shaka alimutia Paulo moyo sana!a

21 Watu wengine pia walifaidika na mufano muzuri wa Paulo. Aliandikia hivi Wafilipi: “Hali yangu kwa kweli imesaidia kuendeleza habari njema, hivi kwamba vifungo vyangu vya gereza kwa ajili ya Kristo vimejulikana waziwazi kati ya Walinzi wote wa Mufalme na wengine wote. Sasa ndugu wengi katika Bwana wamekuwa na uhakika kwa sababu ya vifungo vyangu vya gereza, na wanaonyesha uhodari mwingi wa kusema neno la Mungu bila woga.”​—Flp. 1:12-14.

22. Wakati Paulo alikuwa mufungwa Roma alitumia namna gani wakati wake?

22 Wakati Paulo alikuwa mufungwa katika Roma alitumia ile wakati ili kuandika barua za maana zenye zinapatikana leo mu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.b Zile barua zilisaidia Wakristo wa karne ya kwanza wenye aliziandikia. Na siye ziko natusaidia juu mashauri yenye kuongozwa na roho ya Mungu yenye aliandika ingali na faida leo.​—2 Ti. 3:16, 17.

BARUA TANO ZENYE PAULO ALIANDIKA WAKATI ALIKUWA MUFUNGWA ROMA KWA MARA YA KWANZA

Barua tano kati ya barua zenye Paulo aliandika ziliandikwa mu mwaka wa 60 hivi mupaka 61 K.K.Y., wakati alifungwa kwa mara ya kwanza katika Roma. Mu barua kwa Mukristo mwenzake Filemoni, Paulo anafasiria kama Onesimo, mutumwa wa Filemoni mwenye alikimbia, amekuwa sasa Mukristo. Paulo alikuwa baba wa kiroho wa Onesimo na alikuwa anatuma ule mutumwa mwenye “zamani hakukuwa na faida,” arudie kwa bwana wake akiwa sasa ndugu Mukristo.​—Flm. 10-12, 16.

Mu barua yake kwa Wakolosai, Paulo anaonyesha kama Onesimo alikuwa mumoja wao. (Kol. 4:9) Onesimo na Mukristo mwenzake Tikiko walikuwa na pendeleo ya kupeleka barua ya Paulo kwa Filemoni, barua yake kwa Wakolosai, na barua yake kwa Waefeso.

Wakati Paulo alikuwa anaandikia Wafilipi, alizungumuzia “vifungo [vyake] vya gereza,” na alizungumuzia hali ya mwenye aliwapelekea ile barua, ni kusema Epafrodito. Wafilipi walikuwa wametuma Epafrodito ili amusaidie Paulo, lakini Epafrodito aligonjwa na kukaribia kufa. Pia Epafrodito alihuzunika sana kwa sababu Wafilipi ‘walisikia [kama] alikuwa mugonjwa.’ Kwa hiyo, Paulo aliwaambia wasamini “watu wa namna hiyo.”​—Flp. 1:7; 2:25-30.

Barua kwa Waebrania iliandikwa kwa ajili ya Wakristo Waebrania wenye walikuwa naishi katika Yudea. Hata kama ile barua haionyeshe waziwazi ni nani aliiandika, ushuhuda unaonyesha kama iliandikwa na Paulo. Kwa sababu namna ile barua iliandikwa inafanana na namna ya kuandika ya Paulo. Paulo anatuma salamu kutoka Italia na anataya Timoteo mwenye alikuwa naye katika Roma.​—Flp. 1:1; Kol. 1:1; Flm. 1; Ebr. 13:23, 24.

23, 24. Kama Paulo namna gani Wakristo wa leo wanaendelea kuwa na furaha hata wakati wanafungwa bila haki?

23 Kitabu ya Matendo haizungumuzie wakati wenye Paulo aliachiliwa. Lakini kulikuwa kulishapita miaka ine hivi tangu afungwe, ni kusema alifanya miaka mbili katika Kaisaria na miaka mbili katika Roma.c (Mdo. 23:35; 24:27) Lakini aliendelea kuwa na furaha na alifanya yote yenye aliweza mu kazi ya Yehova. Sawa Paulo leo watumishi wengi wa Yehova wanaendelea kuwa na furaha na wanaendelea kuhubiri hata kama wanafungwa kwa sababu ya imani yao. Fikiria mufano wa Adolfo, mwenye alifungwa mu inchi ya Uhispania kwa sababu alikatala kuingia mu jeshi. Ofisa fulani alimuambia hivi: “Unatushangaza sana. Tumefanya maisha yako ikuwe nguvu sana mu gereza. Lakini kadiri tunaendelea kufanya vile, njo unakuwa na furaha zaidi na unazungumuza na siye kwa upole zaidi.”

24 Kisha wakati fulani, walimutumainia sana Adolfo mupaka hawakufunga tena mulango wa chumba yake ya gereza. Wakati fulani maaskari walikuwa wanamutembelea ili kumuuliza maulizo kuhusu Biblia. Na hata mulinzi mumoja alikuwa anaenda mu chumba ya gereza ya Adolfo ili kusoma Biblia, na Adolfo alikuwa namuchunga ili wasimuone. Kwa hiyo mufungwa alikuwa nachunga mulinzi. Basi, mufano muzuri wa Mashahidi kama hao ukuchochee pia ukuwe na “uhodari mwingi wa kusema neno la Mungu bila woga,” hata wakati wa magumu.

25, 26. Paulo aliona utimizo wa unabii gani mbele hata miaka 30 ienee kisha ule unabii kutolewa, na ule unabii uko natimia namna gani leo?

25 Kitabu ya Matendo inamalizia na habari yenye kuchochea ya mutume wa Kristo mwenye amefungwa mu nyumba, lakini mwenye ‘alikuwa anahubiri Ufalme wa Mungu’ kwa wote wenye walikuwa nakuya kumutembelea. Mu sura ya kwanza tulisoma kuhusu mugao wenye Yesu alipatia wafuasi wake wakati alisema: “Mutapokea nguvu wakati roho takatifu itakuja juu yenu, na mutakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mupaka kwenye sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Miaka 30 ilikuwa haiyaenea, lakini ujumbe wa Ufalme ulikuwa ‘umehubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.’d (Kol. 1:23) Ile ilionyesha kama roho ya Mungu iko na nguvu kabisa!​—Zek. 4:6.

26 Leo pia roho ya Mungu inatia nguvu Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine,” ili waendelee “kutoa ushahidi kamili juu ya Ufalme wa Mungu” mu inchi 240! (Yoh. 10:16; Mdo. 28:23) Uko nafanya ile kazi kwa nguvu yako yote?

MAISHA YA PAULO KISHA MWAKA WA 61 K.K.Y.

Inaonekana ni mu mwaka wa 61 hivi K.K.Y. njo Paulo alisikilizwa na Mutawala Nero mwenye inaonekana aliamua kama Paulo hakukuwa na kosa. Hatujue habari mingi kuhusu mambo yenye Paulo alifanya kisha Pale. Kama alienda Uhispania sawa vile alikuwa amepanga, inawezekana ni mu ile wakati njo alienda. (Ro. 15:28) Mu mwaka wa 95 hivi K.K.Y., muandikaji Clement wa Roma, aliandika kama Paulo alisafiri “mupaka sehemu za mbali sana za mangaribi,” pengine ile ilitia ndani Uhispania.

Barua tatu zenye Paulo aliandika kisha kuachiliwa, ni kusema Timoteo wa Kwanza, Timoteo wa Pili, na Tito, zinatusaidia kujua kama Paulo alitembelea Krete, Makedonia, Nikopoli, na Troa. (1 Ti. 1:3; 2 Ti. 4:13; Tit. 1:5; 3:12) Pengine ilikuwa katika Nikopoli mu Ugiriki njo Paulo alifungwa tena. Ikuwe ni vile ao hapana, mu mwaka wa 65 hivi K.K.Y., alikuwa tena mu gereza katika Roma. Lakini mara hii Nero hakumuonyesha huruma. Na hata, kulingana na mwanahistoria Muroma Tacitus, wakati moto mukubwa uliharibu muji wa Roma mu mwaka wa 64 K.K.Y., Nero alisingizia Wakristo kama ni wao njo walianzisha ule moto na akaanza kuwatesa sana.

Mu barua yake ya pili kwa Timoteo Paulo mwenye alijua kama kifo yake inakaribia, aliomba Marko na Timoteo wakuye haraka kumuona. Tusisahau kama Luka na Onesiforo waliweka maisha yao mu hatari ili kumufariji Paulo. (2 Ti. 1:16, 17; 4:6-9, 11) Mu ile wakati mutu mwenye angesema waziwazi kama iko Mukristo, angefungwa na kuteswa sana mupaka kifo. Inawezekana Paulo aliuawa kwa sababu ya imani yake muda mufupi kisha kuandika barua yake ya pili kwa Timoteo mu mwaka wa 65 hivi K.K.Y. Inasemekana kama Nero naye alikufa kifo ya mubaya miaka tatu hivi kisha Paulo kuuawa.

HABARI NJEMA ‘ILIHUBIRIWA KATIKA UUMBAJI WOTE CHINI YA MBINGU’

Mu mwaka wa 61 hivi K.K.Y., wakati Paulo alikuwa mu gereza katika Roma aliandika kama “habari njema” ilikuwa ‘imehubiriwa katika uumbaji wote chini ya mbingu.’ (Kol. 1:23) Ile maneno inamaanisha nini?

Inaonekana kama Paulo alipenda kuonyesha kama watu wa mu inchi za mingi walikuwa wamesikia “habari njema.” Lakini kulikuwa inchi zingine kwenye habari njema ilikuwa haiyahubiriwa. Kwa mufano, mu karne ya ine M.K.Y., Aleksanda Mukubwa alifika India kisha kukamata sehemu kubwa ya Asia. Kaisari Yulio alishambulia Uingereza mu mwaka wa 55 M.K.Y., na Klaudio alikamata sehemu ya kusini ya ile kisiwa na kuifanya kuwa sehemu ya Utawala wa Roma mu mwaka wa 43 K.K.Y. Watu walijua pia inchi za mashariki mwa Asia juu njo kwenye kulitoka hariri za muzuri (aina fulani za nyuzi).

Habari njema ilihubiriwa mu Uingereza, China, na mu inchi za mashariki mwa Asia? Inawezekana hapana. Paulo mwenye aliandikia Wakolosai alikuwa hayafikia muradi wake wenye alizungumuzia mu mwaka wa 56 hivi K.K.Y. wa kuhubiri katika “eneo lenye halijaguswa” la Uhispania. (Ro. 15:20, 23, 24) Lakini kufikia mwaka wa 61 hivi K.K.Y., habari njema ya Ufalme ilikuwa imefika fasi za mingi. Hata kama habari njema ilikuwa haiyafika mu maeneo ingine, ilikuwa imefika mu maeneo ya Wayahudi na wageuzwa-imani wenye walibatizwa kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33 K.K.Y., na pia mu maeneo yenye mitume wa Yesu walitembelea.​—Mdo. 2:1, 8-11, 41, 42.

a Paulo alipenda kubakia na Onesimo lakini kufanya vile ingekuwa kuvunja sheria ya Waroma juu Onesimo alikuwa mutumwa wa mutu mwingine. Alikuwa mutumwa wa Filemoni mwenye naye alikuwa Mukristo. Kwa hiyo Onesimo alirudia kwa Filemoni. Alipeleka barua ya Paulo kwa Filemoni na mu ile barua Paulo alimuomba Filemoni akaribishe mutumwa wake Onesimo kwa upendo kama ndugu yake wa kiroho.​—Flm. 13-19.

b Ona kisanduku “Barua Tano Zenye Paulo Aliandika Wakati Alikuwa Mufungwa Roma kwa Mara ya Kwanza.”

c Ona kisanduku “Maisha ya Paulo Kisha Mwaka wa 61 K.K.Y.”

d Ona kisanduku “Habari Njema ‘Ilihubiriwa Katika Uumbaji Wote Chini ya Mbingu.’”

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine