Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w12 15/8 uku. 20-24
  • Fanya Angalisho na Mitego ya Shetani!

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Fanya Angalisho na Mitego ya Shetani!
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • ZUIA ULIMI WAKO ILI USIWASHE MOTO
  • EPUKA MUTEGO WA KAMBA: KUOGOPA WATU NA MIKAZO YA WENGINE
  • EPUKA MUTEGO UNAOGANDAMIZA: KUJISIKIA KAMA HAUWEZI KUSAMEHEWA
  • TUNAJUA VIZURI UJANJA WA SHETANI
  • Unaweza Kuepuka ao Kutoka Katika Mitego ya Shetani!
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2021
  • Simama Imara na Epuka Mitego ya Shetani!
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Pilato na Herode Wanaona Kuwa Yesu Hana Kosa
    Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
  • Uendelee “Kuangalia Mbele”
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Funzo)—2020
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
w12 15/8 uku. 20-24

Fanya Angalisho na Mitego ya Shetani!

‘Toka katika mutego wa Ibilisi.’​—2 TIM. 2:26.

UNGEJIBU NAMNA GANI?

Inafaa ufanye nini ikiwa una tabia ya kuwasema wengine vibaya?

Mifano ya Pilato na Petro inatufundisha nini juu ya woga na mikazo ya wengine?

Namna gani unaweza kuepuka mutego wa kujisikia kama hauwezi kusamehewa?

1, 2. Ni mitego gani ya Shetani ambayo tutazungumuzia katika habari hii?

SHETANI anawawinda watumishi wa Yehova. Lakini kusudi lake si kutuua kabisa, kama vile muwindaji anavyoua wanyama anaonasa. Kusudi kubwa la Ibilisi ni kuwanasa watu wakiwa bado wangali wazima na kuwatumia watu hao kufanya mapenzi yake.​—Soma 2 Timotheo 2:24-26.

2 Ili muwindaji awanase wanyama wakiwa bado wangali wazima anaweza kutumia aina fulani ya mutego. Anaweza kujaribu kumufanya munyama atoke mahali anapojificha ili kumunasa kupitia mutego wa kamba. Ao anaweza kutumia mutego uliofichwa ambao unaweza kufyatuka mara moja na kushika munyama kwa gafula. Ibilisi anatumia mitego ya namna hiyo ili kuwanasa watumishi wa Mungu wakiwa bado wangali wazima. Ili tusinaswe na mitego yake, tunapaswa kufungua macho na kutii maonyo yanayotuonyesha kama mahali fulani karibu kuna mutego moja wa Shetani. Habari hii itazungumuzia namna tunaweza kufanya angalisho ili tusinaswe na mitego tatu ambayo Shetani ametumia kuwanasa watu wengi wa Mungu. Mitego hiyo ni (1) kushindwa kuzuia ulimi, (2) kuogopa watu na mikazo ya wengine, na (3) mutu kujisikia kama Mungu hawezi kumusamehe. Habari itakayofuata itazungumuzia mitego mingine miwili ya Shetani.

ZUIA ULIMI WAKO ILI USIWASHE MOTO

3, 4. Kushindwa kuzuia ulimi wetu kunaweza kuleta magumu gani? Toa mufano.

3 Ili kuwinda wanyama wanaojificha, muwindaji anaweza kuchoma pori ili kuwakamata wanyama wanaojaribu kukimbia moto. Ibilisi anatenda kama muwindaji huyo, anaweza kuwasha moto katika kutaniko la Kikristo. Anapowasha moto huo, anaweza kuwafanya ndugu na dada fulani wakimbie kutaniko ambapo ni mahali salama na kuingia katika makucha yake. Namna gani bila kujua tunaweza kumusaidia Shetani kuwasha moto na hivyo sisi wenyewe kunaswa naye?

4 Mwanafunzi Yakobo alifananisha ulimi na moto. (Soma Yakobo 3:6-8.) Tukishindwa kuzuia ulimi wetu, tunaweza kuwasha moto katika kutaniko. Hilo linaweza kutokea namna gani? Tuchukue hali fulani inayoweza kutokea: Kwenye mukutano, tangazo linatolewa kama dada mumoja amekubaliwa kuwa painia wa kawaida. Kisha mukutano, dada wawili wanaanza kuzungumuzia tangazo hilo. Mumoja anaonyesha furaha yake na anamutakia painia huyo mupya kazi njema. Mwengine anasema kama ikiwa dada huyo ameomba kazi ya upainia ni kwa sababu anatafuta tu kujionyesha ao ajulikane katika kutaniko. Ni nani ungependa awe rafiki yako kati ya dada hao wawili? Ni rahisi kuona ni nani kati ya dada hao anatumia ulimi wake ili kuwasha moto katika kutaniko, sivyo?

5. Ili kuzuia ulimi wetu usiwashe moto katika kutaniko, tunapaswa kufanya nini?

5 Namna gani tunaweza kuzuia ulimi wetu ili usiwashe moto? Yesu alisema hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mt. 12:34) Kwa hiyo, jambo la kwanza ni kuchunguza moyo wetu. Je, tunaepuka kuwa na mawazo mabaya juu ya wengine, yanayoweza kutuchochea tuseme vibaya juu yao? Kwa mufano, tunaposikia kama ndugu fulani anajikaza kufikia mapendeleo fulani, je tunaanza kumuwazia vibaya, ao tunaanza kusema kama anatafuta tu sifa? Ikiwa tuna tabia ya kuwazia wengine vibaya, ni vizuri tukumbuke kwamba Shetani naye alimuwazia Ayubu mutumishi mwaminifu wa Mungu vibaya. (Ayu. 1:9-11) Kuliko kutilia shaka nia ya ndugu na dada yetu, ni vizuri tujiulize kwa nini tunamuwazia vibaya. Je, kweli tuna sababu ya kumuwazia hivyo? Ao je, moyo wetu umetiwa sumu na roho ya kukosa upendo, roho ambayo imeenea sana katika siku hizi za mwisho?​—2 Tim. 3:1-4.

6, 7. (a) Ni sababu gani fulani zinazoweza kutufanya tuwaseme wengine vibaya? (b) Tunapaswa kufanya nini ikiwa wengine wanatutukana?

6 Tuzungumuzie sababu zingine zinazoweza kutufanya tuanze kuwasema wengine vibaya. Labda tunafanya hivyo kwa sababu tunapenda kuonyesha mambo tuliyotimiza katika maisha ao kujionyesha ili kuwashusha wengine. Tunaweza pia kuwasema wengine vibaya ili kutetea sababu zilizotufanya tushindwe kufikia miradi yetu kama wao. Iwe tunawasema wengine vibaya kwa sababu tunachochewa na kiburi, wivu ao hatujitumainie, tujue kama kufanya hivyo kuna matokeo mabaya sana.

7 Wakati fulani, tunaweza kufikiri kama tuna haki ya kumusema ndugu ao dada fulani vibaya. Labda kwa sababu siku fulani yeye pia alitusema vibaya. Tujue kama kurudisha kisasi hakutatengeneza mambo. Kufanya hivyo ni kuwakisha tena moto na pia ni kufanya mapenzi ya Shetani. (2 Tim. 2:26) Tunapaswa kumuiga Yesu. Walipomutukana, “hakujibu kwa matukano.” Lakini, ‘aliendelea kujiweka mikononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.’ (1 Pet. 2:21-23) Yesu alitumaini kabisa kama siku fulani na pa wakati, Yehova atashugulikia jambo hilo kwa namna yake. Tunapaswa kutumainia Mungu kama Yesu alivyofanya. Tunaposema maneno ya kutia moyo, tunasaidia kuendeleza “kifungo chenye kuunganisha cha amani” katika kutaniko.​—Soma Waefeso 4:1-3.

EPUKA MUTEGO WA KAMBA: KUOGOPA WATU NA MIKAZO YA WENGINE

8, 9. Sababu gani Pilato alimukatia Yesu hukumu ya kifo?

8 Munyama anaponaswa katika mutego hana tena nguvu na hawezi tena kufanya jambo lolote. Vilevile, mutu mwenye kuogopa watu anawaacha wamusukume kufanya mambo fulani na watawale maisha yake. (Soma Methali 29:25.) Tuzungumuzie mifano ya wanaume wawili ambao walinaswa katika mutego wa Shetani kwa sababu ya woga na mikazo ya wengine na tuone somo tunalopata.

9 Guvernere Muroma, Pontio Pilato, alijua kama Yesu hakuwa na kosa na inaonekana hakutaka kumutesa. Kwa mufano, Pilato alisema kama Yesu hakufanya jambo “lolote linalostahili kifo.” Lakini, Pilato alimukatia Yesu hukumu ya kifo. Sababu gani? Kwa sababu ya mikazo ya watu wengi. (Lu. 23:15, 21-25) Wapinzani hao wa Yesu walimukaza Pilato na kuanza kumulalamikia hivi: ‘Ukimufungua mutu huyu, wewe si rafiki ya Kaisari.’ (Yoh. 19:12) Labda Pilato aliogopa na kuanza kufikiri kama akiwa upande wa Yesu atapoteza cheo chake ao hata maisha yake. Kwa hiyo, alijiacha mwenyewe hata kufikia kufanya mapenzi ya Shetani.

10. Kwa nini Petro alimukana Yesu?

10 Mutume Petro alikuwa mumoja kati ya marafiki wa sana wa Yesu. Ni yeye aliyesema waziwazi kama Yesu ndiye Masiya. (Mt. 16:16) Wakati Yesu alisema maneno fulani ambayo wanafunzi wengine hawakuelewa, wanafunzi hao walimuacha Yesu, lakini Petro aliendelea kuwa mwaminifu. (Yoh. 6:66-69) Pia wakati maadui walikuja kumukamata Yesu, Petro alitumia upanga ili kumupigania Bwana wake. (Yoh. 18:10, 11) Lakini, wakati fulani, kwa sababu ya kuogopa watu Petro alimukana Yesu Kristo na kusema kama hamujue hata kidogo. Kwa wakati kidogo tu, mutume Petro alinaswa katika mutego wa kuwaogopa watu na woga huo ulimufanya apoteze ujasiri wake wa kutenda yaliyo haki.​—Mt. 26:74, 75.

11. Ni mikazo gani tunayopaswa kupiganisha?

11 Sisi Wakristo hatupaswe kuruhusu mikazo ya wengine ituchochee kufanya mambo yatakayomuchukiza Mungu. Wakubwa wa kazi ao watu wengine wanaweza kutukaza ili tuseme uwongo na kuiba ao wanaweza kutuchochea tufanye uasherati. Wanafunzi wenzetu wanaweza kutuchochea kufanya mambo kama vile kuiba majibu tunapofanya mashindano, kutazama picha za uasherati, kuvuta tumbako, kutumia dawa za kulewesha, ao kufanya uasherati. Ni nini basi inayoweza kutusaidia ili woga na mikazo ya wengine visituchochee kufanya mambo yatakayomuchukiza Yehova?

12. Mifano ya Pilato na Petro inatufundisha nini?

12 Tuzungumuzie mambo tunayoweza kujifunza kupitia mifano ya Pilato na Petro. Pilato hakujua mambo mengi juu ya Kristo. Hata hivyo, alijua kama Yesu hakuwa na kosa na kama hakuwa mutu wa kawaida. Lakini, Pilato alikosa unyenyekevu na hakumupenda Mungu wa kweli. Shetani alimunasa bado angali muzima. Petro yeye alikuwa na ujuzi wa kweli na alimupenda Mungu. Lakini, tunajua kama wakati fulani, alikosa kiasi ao alikosa kujua mipaka yake, akawa mwenye kuogopa na kujiacha kuongozwa na mikazo ya wengine. Mbele Yesu akamatwe, Petro alisema hivi kwa majivuno: “Hata ikiwa wengine wote watakwazika, hata hivyo mimi sitakwazika.” (Mk. 14:29) Ili kujitayarisha kupambana na majaribu ya wakati ujao, ilifaa Petro amutumaini Yehova kama Daudi ambaye aliimba hivi: ‘Yehova yuko upande wangu; sitaogopa. Mutu wa udongo anaweza kunitenda nini?’ (Zab. 118:6) Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alichukua Petro na mitume wengine wawili na kuenda nao katika bustani ya Gethsemane. Kuliko kukesha, Petro na wenzake walilala. Yesu aliwalamusha na kuwaambia hivi: ‘Endeleeni kukesha na kusali, ili musiingie katika jaribu.’ (Mk. 14:38) Lakini, Petro alilala tena na baadaye akaanguka katika mutego wa kuogopa watu na mikazo.

13. Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia ili tupambane na mikazo ya wengine?

13 Mifano ya Pilato na Petro inatufundisha somo lingine la maana: Ikiwa tunapenda kushinda mikazo ya wengine ni lazima tuwe na ujuzi, unyenyekevu, kiasi, tumupende Yehova, na kumuogopa kuliko kuwaogopa watu. Ikiwa imani yetu inajengwa juu ya ujuzi wa kweli, tutakuwa tayari kuwatangazia wengine waziwazi mambo tunayoamini bila kuogopa. Hilo litatusaidia tushinde mikazo ya wengine na woga. Hatupaswe kujiaminia sana. Lakini, tunapaswa kukubali kwa unyenyekevu kama tuna lazima ya musaada wa Mungu ili kushinda mikazo ya wengine. Ni lazima tumuombe Yehova roho yake na kuacha upendo utuchochee kutetea jina lake na kushikamana na sheria zake. Tena, tunapaswa kujitayarisha mbele ya jaribu kutokea. Kwa mufano, kuwatayarisha watoto wetu mbele ya wakati na kusali pamoja nao kunaweza kuwasaidia ili mikazo ya wenzao isiwaongoze kufanya mambo mabaya.​—2 Kor. 13:7.a

EPUKA MUTEGO UNAOGANDAMIZA: KUJISIKIA KAMA HAUWEZI KUSAMEHEWA

14. Shetani anataka tufikiri nini kuhusu makosa tuliyofanya hapo zamani?

14 Mutegaji anaweza kutia muti mukubwa ao jiwe kubwa lenye kuninginia juu mahali munyama anazoea kupita. Munyama asiye mwangalifu anaweza kutikisa kamba inayoshikilia muti huo ao jiwe hilo na muti huo ao jiwe hilo linamuangukia na kumugandamiza. Kujisikia kama Mungu hawezi kukusamehe kisha kufanya kosa fulani, kunaweza kuwa kama muzigo muzito unaogandamiza. Tunapofikiria makosa yetu ya zamani, tunaweza kujisikia kuwa wenye ‘kupondwa kupita kiasi.’ (Soma Zaburi 38:3-5, 8.) Shetani anapenda tufikiri kama Yehova hawezi kusamehe makosa yetu na kwamba hatuwezi kushika sheria Zake.

15, 16. Namna gani unaweza kuepuka mutego wa kujisikia kama hauwezi kusamehewa?

15 Namna gani tunaweza kuepuka mutego huo unaogandamiza? Ikiwa umefanya zambi nzito, tengeneza uhusiano wako na Yehova. Julisha wazee, na uwaombe musaada. (Yak. 5:14-16) Fanya yako yote ili kutengeneza mwenendo wako. (2 Kor. 7:11) Ikiwa umekaripiwa, usivunjike moyo. Malipizi yanaonyesha kama Yehova anakupenda. (Ebr. 12:6) Epuka mambo yaliyokuongoza kwenye zambi hiyo, na uazimie kufanya yaliyo mema. Kisha kutubu na kubadilika, imani katika zabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo inaweza kufunika makosa yako.​—1 Yoh. 4:9, 14.

16 Watu wengi wanaendelea kujisikia kama zambi walizofanya haziwezi kusamehewa hata ikiwa zimekwisha kusamehewa. Ikiwa unajisikia hivyo, kumbuka kama Yehova alisamehe Petro na mitume wengine, hata ikiwa walimuacha Yesu wakati ambapo alikuwa na lazima yao sana. Yehova alimusamehe mwanaume aliyefukuzwa katika kutaniko la Korintho kwa sababu ya uasherati wenye kuhuzunisha, lakini alitubu. (1 Kor. 5:1-5; 2 Kor. 2:6-8) Biblia inataja watu waliofanya makosa makubwa ambao walitubu na Mungu akawasamehe.​—2 Nya. 33:2, 10-13; 1 Kor. 6:9-11.

17. Zabihu ya ukombozi inaweza kutufanyia nini?

17 Yehova atakusamehe na kusahau makosa yako ya zamani ikiwa unatubu kweli kweli na kukubali rehema yake. Usifikiri kama zabihu ya ukombozi ya Yesu haiwezi kufunika zambi zako. Tukijisikia kuwa hatuwezi kusamehewa, tutaangukia katika mitego ya Shetani. Ibilisi anataka ufikiri kama hauwezi kusamehewa, lakini kumbuka kama zabihu ya ukombozi ya Yesu inaweza kufunika zambi za wale ambao wametubu. (Met. 24:16) Kuamini zabihu ya ukombozi kunaweza kutusaidia tusiwe na mawazo hayo yasiyofaa na kunaweza kutupatia nguvu ya kutumikia Mungu kwa moyo wetu wote, akili yetu yote, na nafsi yetu yote.​—Mt. 22:37.

TUNAJUA VIZURI UJANJA WA SHETANI

18. Namna gani tunaweza kuepuka mitego ya Ibilisi?

18 Shetani anatumia mutego ni mutego, jambo la lazima kwake ni kutunasa tu. Kwa kuwa tunajua vizuri ujanja wake, tunaweza kuuepuka. (2 Kor. 2:10, 11) Tukimuomba Mungu hekima ya kupambana na majaribu yetu, hatutanaswa na mitego yake. ‘Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumuomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.’ (Yak. 1:5) Tunapaswa kutenda kulingana na sala zetu kwa kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kutumia mashauri yake. Vitabu vya kutusaidia kuelewa Biblia ambavyo mutumwa mwaminifu anatutolea, vinatuonyesha mitego ya Ibilisi na namna ya kuiepuka.

19, 20. Sababu gani inafaa kuchukia mabaya?

19 Sala na funzo la Biblia vinatusaidia kupenda mema. Lakini, ni lazima tuendelee kuchukia mabaya. (Zab. 97:10) Kufikiria magumu tunayoweza kupata sababu ya kufuata tamaa mbaya kunaweza kutusaidia kuepuka mitego ya Shetani. (Yak. 1:14, 15) Tukijifunza kupenda mema na kuchukia kabisa mabaya, mambo ambayo Shetani anatumia ili kutunasa hayatatuvutia; tutayachukia.

20 Tunamushukuru sana Yehova kwa sababu anatusaidia ili Shetani asitushinde akili! Kupitia roho Yake, Neno Lake, na tengenezo Lake, Yehova anatukomboa ‘kutokana na yule muovu.’ (Mt. 6:13) Katika habari inayofuata, tutazungumuzia mitego mingine miwili ambayo Shetani ametumia ili kuwanasa watumishi wa Mungu wakiwa bado wangali wazima.

[Maelezo ya chini]

a Wazazi wanaweza kuzungumuza na watoto wao habari yenye kichwa “Kukabiliana na mkazo” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, ukurasa wa 132-133. Munaweza kutumia habari hiyo wakati wa Ibada ya Familia ya mangaribi.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kutokuzuia ulimi kunaweza kuwasha moto katika kutaniko

[Picha katika ukurasa wa 24]

Unaweza kuondoa muzigo wa kujisikia kama hauwezi kusamehewa

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine