Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • w14 1/2 uku. 5-7
  • Ni Nani Kabisa Anayeleta Vita na Mateso?

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Ni Nani Kabisa Anayeleta Vita na Mateso?
  • Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Vichwa Vidogo
  • Habari za Kufanana na Zile
  • ISHARA YA SIKU ZA MWISHO
  • KUZIVUNJA KAZI ZA IBILISI
  • Wale Wapanda-Farasi Ine Ni Nani?
    Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Gazeti la Watu Wote)—2017
  • Vita Imemaliza Makuta Mingi Sana—Iko Na Matokeo Gani Ingine?
    Habari Zingine
Munara wa Mulinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
w14 1/2 uku. 5-7

KICHWA | VITA ILIYOBADILISHA ULIMWENGU

Ni Nani Kabisa Anayeleta Vita na Mateso?

Tarehe 11/11/1918, Vita ya Kwanza ya Ulimwengu iliisha. Biashara zilifungwa, na watu walicheza katika barabara mbalimbali. Lakini furaha yao haikuendelea. Mateso mengine yalitokea kisha vita hiyo kuisha, mateso hayo yalikuwa yenye kuua zaidi kuliko bunduki kubwa ya kumwanga masasi.

Katika Mwezi wa 6, mwaka wa 1918, ugonjwa wenye kuua unaoitwa Homa ya Kihispania ulishambulia maaskari waliokuwa wanapigana katika inchi ya Ufaransa. Ugonjwa huo ulionekana haraka kuwa ni wenye kuua sana. Kwa mufano, katika miezi michache, uliua maaskari wengi wa Amerika waliokuwa katika inchi ya Ufaransa kuliko wale waliouawa na maadui wao. Na ugonjwa huo ukaenea haraka katika dunia yote wakati maaskari walianza kurudia katika inchi zao kisha vita kuisha.

Kisha vita kuisha, miaka iliyofuata pia ilikuwa ya njaa na ukosefu wa feza. Sehemu kubwa ya Ulaya iliteseka na njaa kisha mapigano kuisha katika mwaka wa 1918. Kufikia mwaka wa 1923, feza za inchi ya Ujerumani hazikuwa tena na faida yoyote. Miaka sita baadaye, feza zilikosekana duniani pote. Na mwishowe, katika mwaka wa 1939, vita ya pili ya ulimwengu ilianza, kwa njia fulani ilikuwa ni kuendelezwa kwa vita iliyotangulia. Ni nini iliyoleta mateso hayo yote yenye kufuatana?

ISHARA YA SIKU ZA MWISHO

Unabii wa Biblia unatuwezesha kujua ni nini kinachofanya matukio fulani ya kihistoria yatokee na hilo linahusu hasa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Yesu Kristo alitabiri kwamba kuna wakati ‘taifa litasimama kupigana na taifa’ na kwamba njaa na magonjwa ya kuambukiza yatajaa duniani pote. (Mathayo 24:3, 7; Luka 21:10, 11) Aliwaambia wanafunzi wake kwamba mateso hayo yangefanyiza ishara ya siku za mwisho. Maelezo mengine yanaonyeshwa katika kitabu cha Ufunuo. Kitabu hicho kinaambatanisha taabu za duniani na vita iliyotokea mbinguni.​—Soma kisanduku “Vita Duniani na Vita Mbinguni.”

Kitabu kile kile cha Biblia kinazungumuzia wapandaji ine wa farasi, ambao wakati fulani wanaitwa wapandaji ine wa farasi wa Ufunuo. Watatu kati ya wapandaji hao wa farasi wanafananisha mateso yaleyale ambayo Yesu alitabiri zamani, ni kusema vita, njaa, na magonjwa ya kuambukiza. (Soma kisanduku “Je, Kweli Wale Wapandaji Ine wa Farasi Wako Katika Mwendo?”) Ni wazi kwamba Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilianzisha wakati wa taabu ambao ulikuwa haujapata kutokea. Na Biblia inafunua kwamba, kwa njia fulani, Shetani ndiye alianzisha taabu hizo. (1 Yohana 5:19) Je, uwezo wake utamalizwa wakati fulani?

Kitabu cha Ufunuo kinatuhakikishia pia kwamba Shetani ana “kipindi kifupi cha wakati.” (Ufunuo 12:12) Ndiyo sababu ana hasira nyingi na analeta taabu nyingi hapa duniani. Hata hivyo, mateso tunayoona yanaonyesha pia kwamba wakati wa Shetani unakaribia kuisha.

KUZIVUNJA KAZI ZA IBILISI

Vita ya Kwanza ya Ulimwengu lilikuwa pia tukio kubwa katika historia. Ilitokeza kipindi cha vita kati ya mataifa yote na ilichochea mapinduzi na kutoaminiana kati ya viongozi wa wanadamu. Ilionyesha waziwazi kwamba Shetani amefukuzwa mbinguni. (Ufunuo 12:9) Na mutawala huyo wa dunia asiyeonekana alitenda kama dikteta mubaya sana anayejua kwamba anabaki na siku chache tu za kutawala. Wakati siku hizo zitaisha, wakati wa taabu ulioanzishwa na Vita ya Kwanza ya Ulimwengu utaisha pia.

Kupitia unabii wa Biblia, una sababu nzuri ya kuamini kwamba Yesu Kristo, Mufalme wetu wa mbinguni, karibuni ‘atavunja kazi za Ibilisi.’ (1 Yohana 3:8) Watu wengi sana wanasali Ufalme wa Mungu uje. Wewe pia unasali hivyo? Kupitia Ufalme huo, watu waaminifu wataona mapenzi ya Mungu yakifanywa duniani wala si mapenzi ya Shetani. (Mathayo 6:9, 10) Wakati wa utawala wa Ufalme wa Mungu, hakutakuwa tena vita ya ulimwengu ao vita yoyote! (Zaburi 46:9) Jifunze juu ya Ufalme huo ili uone wakati amani itajaa duniani!​—Isaya 9:6, 7.

Vita Duniani na Vita Mbinguni

Miaka 1 900 hivi mbele Vita ya Kwanza ya Ulimwengu kuanza, Shetani alimutolea Yesu “falme zote za ulimwengu.” (Mathayo 4:8, 9) Yesu alipinga jaribu hilo, lakini kisha hapo alimuita Ibilisi kuwa ‘mutawala wa ulimwengu.’ (Yohana 14:30) Zaidi ya hiyo, mutume Yohana aliandika kwamba ‘ulimwengu muzima unakaa katika nguvu za yule muovu.’​—1 Yohana 5:19.

Kwa sababu Shetani Ibilisi ana uwezo mukubwa juu ya ulimwengu, ni jambo lenye kueleweka kusema kwamba alichangia kuleta vita ya ulimwengu na matokeo ya vita hiyo. Kwa kweli, kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba Shetani ndiye anatokeza taabu ambazo zinaonekana duniani tangu mwaka wa 1914. Ona kwa kifupi matukio yanayoelezwa katika Ufunuo sura ya 12:

  • Mustari wa 7: Vita inatokea mbinguni kati ya Mikaeli (Yesu Kristo) na joka mukubwa (Shetani).

  • Mustari wa 9: Ibilisi, “anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa,” anatupwa duniani.

  • Mustari wa 12: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”

Namna matukio yanavyofuatana katika Biblia na mambo yanayotendeka katika ulimwengu, yote hayo yanaonyesha kwamba vita hiyo ya mbinguni ilitokea kisha Ufalme wa Mungu kuanza kutawala mbinguni katika mwaka wa 1914.a Kwa hiyo, katika mwaka huohuo wa maana, vita ilitokea duniani na mbinguni.

a Soma sura ya 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Kweli Wale Wapandaji Ine wa Farasi Wako Katika Mwendo?

Farasi mweupe na mufalme wa mbinguni anayepanda juu yake

Farasi mweupe, ambaye mupandaji wake ni mufalme wa mbinguni. Mufalme, Yesu Kristo mwenyewe, ni yule anayepanda farasi ili kutetea uadilifu. (Zaburi 45:4) Kazi yake ya kwanza ni kumutosha Shetani mbinguni pamoja na mashetani wake.—Ufunuo 6:2; 12:9.

Farasi mwenye rangi ya moto na maaskari kwenye uwanja wa vita

Farasi wa rangi ya moto, ambaye mupandaji wake ana mamlaka “ya kuondoa amani duniani.” (Ufunuo 6:4) Kuanzia mwaka wa 1914, vita inaendelea kuwasumbua wanadamu. Miaka 21 kisha Vita ya Kwanza ya Ulimwengu kuisha, Vita ya Pili ya Ulimwengu ilianza na ikaua watu wengine wengi. Uchunguzi moja unasema kwamba Vita ya Pili ya Ulimwengu iliua watu milioni 60 hivi. Kuanzia mwaka wa 1945, vita ya ulimwengu haijatokea tena lakini vita zinazotokea zinaua pia watu wengi sana. Wanahistoria fulani wanakadiria kwamba watu zaidi ya milioni mia moja wamekufa kwa sababu ya vita katika miaka kati ya 1901 na 2000.

Farasi mweusi na watoto wengi wanaoteseka kwa sababu ya njaa

Farasi mweusi, ambaye mupandaji wake ana kipimo katika mukono wake anafananisha njaa. (Ufunuo 6:5, 6) Katika Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, Majeshi ya Muungano ya inchi mbalimbali yalifunga mipaka ya inchi ya Ujerumani na kutokeza mauaji ya watu karibu 750 000 katika inchi hiyo kwa sababu ya njaa. Warusi zaidi ya milioni mbili walikufa kwa sababu ya njaa katika mwaka wa 1921, na kisha hapo taabu zingine zenye kufanana hiyo zilitokea katika inchi zingine. Kwa ujumla, watu milioni 70 hivi walikufa kwa sababu ya njaa katika miaka kati ya 1901 na 2000. Kila mwaka, watoto zaidi ya milioni tatu walio na miaka chini ya tano wanakufa kwa sababu ya kula vibaya.

Farasi wa rangi ya majivu na watu waliokufa na magonjwa

Farasi wa rangi ya majivu, ambaye mupandaji wake analeta kifo kupitia pigo lenye kuua. (Ufunuo 6:8) Pigo kubwa la kwanza katika miaka kati ya 1901 na 2000 lilikuwa Homa ya Kihispania. Hesabu zinazotolewa zinatofautiana sana, lakini uchunguzi moja unasema kwamba homa hiyo iliua watu milioni 50 hivi. Kitabu kimoja kinasema kwamba “ugonjwa huo ulikuwa moja kati ya misiba mibaya zaidi katika historia. Ugonjwa wa kuambukiza wa majipu haukuua watu wengi kwa uharaka hivyo.” (Man and Microbes) Ugonjwa wa ndui, malaria, na kifua kikuu ni magonjwa mengine yaliyoua mamia ya mamilioni ya watu katika miaka kati ya 1901 na 2000.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine