Gusa Moyo wa Mwanafunzi Wako
1 Kabla ya kupaa mbinguni, Yesu aliambia wanafunzi wake wafundishe wengine “kushika” mambo yote aliyokuwa ameamuru. (Mt. 28:19, 20) Ili mtu ‘ashike’ amri za Kristo, habari hizo zinapaswa kugusa moyo wake. (Zab. 119:112) Unawezaje kugusa moyo wa mtu fulani unayejifunza naye Biblia?
2 Sali Upate Mwongozo wa Yehova: Kufanya wanafunzi ni kazi ya Mungu. Baraka yake, si uwezo wetu mbalimbali, ni ya lazima ili kufanikiwa. (Mdo. 16:14; 1 Kor. 3:7) Hivyo, kusali ili kupata msaada wa Yehova katika kufundisha wengine kweli ni kwa maana sana.—Isa. 50:4.
3 Tambua Yale Ambayo Mwanafunzi Anaamini: Kujua yale ambayo watu wanaamini na sababu zinazofanya wayaamini kunaweza kutupatia ufahamu wenye kina kuhusu yale tunayopaswa kusema ili kugusa moyo wao. Kwa nini mwanafunzi anaona fundisho fulani hasa kuwa lenye kuvutia? Ni nini kilichomsadikisha kwamba hilo linaweza kuaminiwa? Ujuzi kama huo unaweza kutusaidia tuseme kwa ufahamu.—Mdo. 17:22, 23.
4 Jenga Hoja Yenye Akili, ya Kimaandiko: Kweli inapaswa kuwa na maana fulani kwa mwanafunzi. (Mdo. 17:24-31) Tunapaswa kutoa sababu iliyo timamu kuhusu tumaini letu. (1 Pet. 3:15) Lakini, fanyeni hivyo sikuzote kwa wema na uvumilivu.
5 Imarisha Fundisho Kupitia Mifano: Si kwamba tu mifano inafanya mwanafunzi aelewe kwa vyepesi zaidi, lakini pia inachochea hisia-moyo. Inahusisha akili na moyo. Yesu aliitumia mara nyingi. (Mk. 4:33, 34) Bila shaka, ili uwe wenye matokeo, mfano unaotumiwa unapaswa kupatana na nukta inayozungumziwa, nao unapaswa kuhusiana na maisha ya mwanafunzi.
6 Onyesha Faida Zinazotokana na Kukubali Kweli: Watu hutaka kujua faida zinazotokana na kutumikisha yale wanayojifunza. Saidia mwanafunzi wako aone hekima ya maneno ya Paulo kwenye 2 Timotheo 3:14-17.
7 Usivunjike moyo ikiwa watu fulani hawaitikii fundisho lako. Si mioyo yote inayoitikia vizuri. (Mt. 13:15) Hata hivyo, watu fulani hupata kuwa waamini. (Mdo. 17:32-34) Jitihada zako za kufanya habari njema iguse mioyo na zisaidie wengine wengi wakubali na “kushika” yale ambayo Yesu aliamuru.