Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • mwbr19 Mwezi wa 10 uku. 1-7
  • Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha
  • Vichapo Vyenye Kutajwa mu Buku ya Mukutano Utumishi na Maisha (2019)
  • Vichwa Vidogo
  • TAREHE 7-13/10
  • TAREHE 14-20/10
  • TAREHE 21-27/10
  • TAREHE 28/10–3/11
Vichapo Vyenye Kutajwa mu Buku ya Mukutano Utumishi na Maisha (2019)
mwbr19 Mwezi wa 10 uku. 1-7

Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha

TAREHE 7-13/10

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | YAKOBO 3-5

“Onyesha Hekima Yenye Kutoka kwa Mungu”

cl uku. 221-222 fu. 9-10

Je, “Hekima Yenye Inatoka Juu” Inakuongoza mu Maisha Yako?

9 “Kwanza kabisa ni safi.” Kuwa safi maana yake kutakata na kuwa bila uchafu, haiko tu kwa inje lakini pia mu moyo. Biblia inapatanisha hekima na moyo, lakini hekima yenye kutoka mbinguni haiwezi kuingia mu moyo wenye umechafuliwa na tamaa na mawazo ya mubaya, na nia za mubaya. (Mezali 2:10; Matayo 15:19, 20) Lakini, kama moyo wetu uko safi, ni kusema, kwa kadiri yenye inawezekana mwanadamu mwenye hakamilike akuwe safi, ‘tutageuka na kuacha mambo ya mubaya na kutenda mambo ya muzuri.’ (Zaburi 37:27; Mezali 3:7) Njo maana inafaa kabisa kuona kama usafi unatajwa kwanza katika liste ya sifa za hekima. Kama hatuko safi kiroho, na hatuna mwenendo safi, haitawezekana tukuwe na sifa zingine za hekima yenye kutoka juu.

10 “Kisha yenye kufanya amani.” Hekima yenye kutoka mbinguni inatuchochea kufuatia amani, sifa yenye kuwa sehemu ya tunda la roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Tunajikaza sana ili tusiharibu ‘kifungo cha amani’ chenye kinaunganisha watu wa Yehova. (Waefeso 4:3) Pia, tunajikaza kabisa kurudisha amani wakati inavurugika. Juu ya nini ni jambo la maana kufanya vile? Biblia inasema: “Muendelee . . . kuishi kwa amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja na ninyi.” (2 Wakorinto 13:11) Mungu wa amani atakuwa pamoja na sisi kama tunaendelea kuishi kwa amani. Uhusiano wetu na Yehova unategemea namna tunawatendea waabudu wenzetu. Namna gani tunaweza kuwa watu wenye kufanya amani? Fikiria mufano wenye kufuata.

cl uku. 223-224 fu. 12

Je, “Hekima Yenye Inatoka Juu” Inakuongoza mu Maisha Yako?

12 “Yenye usawaziko.” Kuwa na usawaziko, maana yake nini? Watu wenye elimu ya Biblia wanasema kama haiko mwepesi kutafsiri neno la zamani la Kigiriki lenye kutafsiriwa “yenye usawaziko” lenye kuwa mu Yakobo 3:17. Watafsiri wametumia maneno kama vile “upole,” “uvumulivu,” na “mwenye kuhangaikia.” Maana ya kwanza ya neno hilo la Kigiriki ni, “mwenye kukubali mawazo ya wengine.” Tunaweza kufanya nini ili tuonyeshe kama tunaongozwa na ile sifa ya hekima yenye kutoka juu?

cl uku. 224-225 fu. 14-15

Je, “Hekima Yenye Inatoka Juu” Inakuongoza mu Maisha Yako?

14 “Tayari kutii.” Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “tayari kutii” linapatikana mara moja tu mu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Mutu mumoja mwenye elimu ya Biblia anasema kama neno hilo “linatumiwa mara mingi juu ya kuzungumuzia nizamu ya kijeshi.” Linaweza kumaanisha “mwenye anashawishiwa kwa vyepesi” na “mwenye kujitiisha.” Mutu mwenye anaongozwa na hekima yenye kutoka juu anakuwaka tayari kutii mambo yenye Maandiko inasema. Hashikilie sana mawazo yake na kukataa mawazo yoyote yenye inapinga mawazo yake. Lakini, anabadilishaka mawazo yake mara moja wakati anahakikishiwa kupitia Maandiko kama amekamata uamuzi mubaya ao mawazo yake iko na makosa. Je, vile njo wengine wanakuona?

“Yenye Kujaa Rehema na Matunda ya Muzuri”

15 “Yenye kujaa rehema na matunda ya muzuri.” Rehema ni sifa ya maana ya hekima yenye kutoka juu, kwa sababu Biblia inasema kama hekima hiyo ‘imejaa rehema.’ Ona kwamba “rehema” inatajwa pamoja na “matunda ya muzuri.” Jambo hilo linafaa kwa sababu mu Biblia, mara mingi rehema inamaanishaka kuhangaikia sana wengine na kuwatendea kwa huruma mambo mingi ya muzuri. Kichapo kimoja chenye kuzungumuzia Biblia kinafasiria kama rehema ni “kuhuzunishwa na hali ya mubaya ya mutu mwingine na kujaribu kumusaidia.” Kwa hiyo, hekima yenye kutoka kwa Mungu haiko baridi wala haitegemee akili tu. Lakini, ni yenye upendo na yenye kutoka mu moyo, na inawahangaikia wengine. Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha kama tunajaa rehema?

cl uku. 226-227 fu. 18-19

Je, “Hekima Yenye Inatoka Juu” Inakuongoza mu Maisha Yako?

18 “Haibague.” Hekima ya Mungu haina ubaguzi wa kabila na wa taifa. Kama tunaongozwa na hekima hiyo, tunapaswa kujikaza kutosha kabisa mu moyo wetu mwelekeo wowote wa kuonyesha upendeleo. (Yakobo 2:9) Hatupendelee watu fulani kwa sababu ya masomo fulani yenye walisoma, kwa sababu ni matajiri, ao kwa sababu ya madaraka yao mu kutaniko; wala hatumuzarau mwabudu mwenzetu, hata kama anaonekana kuwa wa hali ya chini sana. Kama Yehova anawapenda wale watu, bila shaka sisi pia tunapaswa kuwapenda.

19 “Haiko ya kinafiki.” Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “munafiki” linaweza kumaanisha “mutu mwenye kucheza teatre.” Wakati wa zamani, wachezaji Wagiriki na Waroma wenye walikuwa wanacheza teatre, walikuwa wanavaa vitu fulani vikubwa kwenye uso ili kufunika uso wao. Kwa hiyo, neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “munafiki” likaanza kutumiwa ili kumaanisha mutu mwenye anajifanya vile haiko, ao mutu mwenye anajisingizia. Hekima yenye kutoka kwa Mungu inapaswa kuongoza namna tunatendea waabudu wenzetu na pia namna tunawaona.

Chimba ili Kupata Mali ya Kiroho

w08 15/11 uku. 20 fu. 6

Mambo Makubwa Katika Barua ya Yakobo na ya Petro

4:5​—Hapa Yakobo anarudilia maneno ya andiko gani? Yakobo harudilie maneno ya andiko fulani. Lakini, inawezekana kama ile maneno yenye iliongozwa na roho ya Mungu inategemea mawazo ya maandiko kama vile Mwanzo 6:5; 8:21; Mezali 21:10; na Wagalatia 5:17.

w97 15/11 uku. 20-21 fu. 8

Imani Inafanya Tukuwe Wavumilivu na Tuendelee Kusali

8 Ni zambi kusema mubaya juu ya Mukristo mwenzetu. (Yakobo 4:11, 12) Lakini Wakristo fulani wanachambua Wakristo wenzao, pengine kwa sababu wanajiona wao wenyewe kuwa wenye haki ao kwa sababu wanapenda kujipandisha na kushusha wengine. (Zaburi 50:20; Mezali 3:29) Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa ‘kusema mubaya’ linamaanisha chuki na linatia ndani kufanya shitaka lenye kutiwa chumvi ao la uongo. Kufanya vile ni kumuhukumu ndugu mubaya. Namna gani kufanya vile kunalingana na ‘kusema mubaya juu ya sheria na kuhukumu sheria?’ Waandishi na Wafarisayo ‘walizarau amri ya Mungu kwa werevu’ na kuanza kuhukumu kwa kutumia kanuni zao wenyewe. (Marko 7:1-13) Vilevile, kama tunahukumu ndugu mwenye Yehova hahukumu, je, hatutakuwa ‘tunahukumu sheria ya Mungu’ na kuonyesha kwa makosa kama ile sheria haifae? Na kama tunachambua ndugu yetu bila haki, hatutakuwa tunatimiza sheria ya upendo.​—Waroma 13:8-10.

Hotuba

w10 1/9 uku. 23-24

Hata kama kila zambi ni kosa mbele ya Mungu, yeye anaelewa kama tuko wazaifu na anatuonyesha rehema kwa sababu tuko wanadamu wenye hawakamilike. Muandikaji mumoja wa zaburi alisema hivi: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, basi ni nani, Ee Yehova, angeweza kusimama? Kwa maana wewe unatoa musamaha wa kweli, ili wakuogope sana.” (Zaburi 130:3, 4) Kwa hiyo, tunapaswa kufanya nini wakati tunakosea wengine, pengine bila kukusudia? Kumbuka kama sala ya mufano ya Yesu yenye alifundisha wafuasi wake inatia ndani ombi hili: “Utusamehe zambi zetu, kwa maana sisi pia tunasamehe kila mutu mwenye kuwa na deni letu.” (Luka 11:4) Ndiyo, Mungu atatusamehe kama tunamuomba musamaha katika jina la Yesu.​—Yohana 14:13, 14.

Ona kwamba Yesu alionyesha kama ni lazima sisi pia tuwasamehe watu “wenye kuwa na deni letu.” Mutume Paulo aliwakumbusha waamini wenzake: “Mukuwe wenye fazili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyingi, na musameheane kwa kupenda kama vile Mungu kupitia Kristo aliwasamehe ninyi kwa kupenda.” (Waefeso 4:32) Wakati tunawasamehe wengine makosa yao, tunakuwa na sababu ya muzuri ya kutazamia kama Mungu atatusamehe makosa yetu pia.

Lakini, tuseme nini juu ya zambi nzito kama vile kuiba, kudanganya kimakusudi, uasherati, ulevi, na zambi zingine? Kila mutu mwenye anafanya zile zambi anavunja sheria za Mungu na anamutendea Mungu zambi. Kwa hiyo, anapaswa kufanya nini?

Tunapaswa Kuungama Zambi kwa Nani?

Mungu hajawapatia wanadamu mamlaka ya kusamehe zambi zenye watu wanamutendea. Ni yeye tu njo anaweza kufanya vile. Biblia inatuambia waziwazi hivi: “Kama tunaungama zambi zetu, yeye ni muaminifu na mwenye haki na atatusamehe zambi zetu na kutusafisha na kila namna ya ukosefu wa haki.” (1 Yohana 1:9) Lakini, tunapaswa kuungama zile zambi kwa nani?

Kwa sababu Mungu tu njo anaweza kusamehe zambi, basi tunapaswa kuungama kwake. Sawa vile tuliona, ni vile Daudi alifanya. Lakini, musamaha unaweza kutolewa kwa musingi gani? Biblia inatuambia: “Mutubu na mugeuke ili zambi zenu zipate kufutwa, ili vipindi vya kutuliza vikuje kutoka kwa Yehova mwenyewe.” (Matendo 3:19) Ndiyo, haiko tu kukubali na kuungama zambi njo kutafanya mutu asamehewe, lakini anapaswa pia kuwa tayari kuacha mwenendo wake mubaya. Mara mingi inakuwaka nguvu kuacha mwenendo mubaya. Lakini kuko musaada.

Kumbuka hii maneno ya mwanafunzi Yakobo yenye imekwisha kutajwa: “Muungame waziwazi zambi zenu kwa mutu na mwenzake na kusali kwa ajili ya mutu na mwenzake, ili muponyeshwe.” Yakobo aliendelea kusema: “Sala ya kumulilia Mungu ya mwenye haki iko na nguvu nyingi.” (Yakobo 5:16) “Mwenye haki” anaweza kuwa mumoja wa “wazee wa kutaniko,” wenye Yakobo anataja mu mustari wa 14. Katika kutaniko la Kikristo, kuko “wazee” kiroho wenye wamewekwa ili kusaidia wale wenye wanatafuta musamaha wa Mungu. Wale “wazee” hawawezi kusamehe zambi, kwa sababu hakuna mwanadamu mwenye amepewa mamlaka ya kumusamehe mutu mwenye amemutendea Mungu zambi. Lakini, wale wanaume wazee wako na sifa za kiroho zenye zinawafanya wastahili kukaripia na kumurekebisha mutu mwenye alifanya zambi nzito, kwa kumusaidia atambue kama alifanya zambi nzito na kama iko na lazima ya kutubu.​—Wagalatia 6:1.

Juu ya Nini Tunapaswa Kuungama Zambi?

Mutu mwenye alifanya zambi, ikuwe nzito ao hapana, ameharibu uhusiano wake pamoja na Mungu na mwanadamu mwenzake. Kwa hiyo, anaweza kuhangaika ao kuteseka mu moyo. Zamiri yenye Muumbaji wetu alitupatia njo inafanya mutu ajisikie vile. (Waroma 2:14, 15) Inaomba kufanya nini?

Tukirudilia tena kitabu cha Yakobo, tunapata hii maneno yenye kutia moyo: “Je, kuko mutu yeyote mwenye kuwa mugonjwa [kiroho] kati yenu? Aite wazee wa kutaniko, na wasali kwa ajili yake, wakimupakaa mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itaponyesha ule mugonjwa, na Yehova atamuinua. Pia, kama amefanya zambi, atasamehewa.”​—Yakobo 5:14, 15.

Kwa mara ingine tena, wazee wanaombwa washugulikie mahitaji ya kondoo. Namna gani? Haiko kwa kumusikiliza tu mutu wakati anaungama. Lakini, kwa sababu mutu ni mugonjwa kiroho, wazee wanapaswa kufanya mambo fulani ili ‘kumuponyesha ule mutu mwenye hajisikie muzuri.’ Kuko mambo mbili yenye Yakobo alitaja yenye wanaweza kufanya.

Kwanza, Yakobo anataja ‘kupaka mafuta.’ Ile inahusiana na nguvu ya kuponyesha ya Neno la Mungu. Mutume Paulo alisema kama “neno la Mungu liko na uzima na liko na nguvu . . . na linaweza kutambua mawazo na makusudio ya moyo,” kwa sababu linaingia ndani kabisa katika akili na moyo wa mutu. (Waebrania 4:12) Kwa kutumia Biblia kwa ufundi, wazee wanaweza kumusaidia mugonjwa kiroho aone ni jambo gani lilifanya afanye kosa na kumusaidia achukue hatua zenye zinafaa ili akuwe tena na uhusiano muzuri pamoja na Mungu.

Kisha, anataja “sala ya imani.” Hata kama sala za wanaume wazee haziwezi kumufanya Mungu asifuate haki, sala hizo ni za maana kwa Mungu, mwenye anatamani kusamehe zambi kwa musingi wa zabihu ya bei ya ukombozi ya Kristo. (1 Yohana 2:2) Mungu iko tayari kumusaidia mutenda-zambi yeyote mwenye anatubu kutoka mu moyo na kufanya “matendo yenye yanastahili toba.”​—Matendo 26:20.

Sababu kubwa zaidi yenye inatuchochea kuungama zambi yetu​—ikuwe tumemutendea zambi mwanadamu mwenzetu ao Mungu​—ni juu tukuwe tena na uhusiano muzuri pamoja na Mungu. Yesu Kristo alionyesha kama tunapaswa kwanza kumaliza tatizo lolote lenye kuwa kati yetu na wanadamu wenzetu na kufanya amani pamoja nao ili tuweze kumuabudu Mungu na tuko na zamiri safi. (Matayo 5:23, 24) Andiko la Mezali 28:13 linasema: “Mwenye anafunika makosa yake hatafanikiwa, lakini kila mutu mwenye anayaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” Wakati tunajinyenyekeza mbele ya Yehova Mungu na kuomba musamaha, anatukubali na atatuinua katika wakati wenye kufaa.​—1 Petro 5:6.

TAREHE 14-20/10

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | 1 PETRO 1-2

“Munapaswa Kuwa Watakatifu”

w17.02 uku. 9 fu. 5

Zabihu ya Ukombozi Zawadi “Kamilifu” Kutoka kwa Baba

5 Namna gani tunaweza kuonyesha kuwa tunapenda jina la Yehova? Kupitia mwenendo wetu. Yehova anatuomba tukuwe watakatifu. (Soma 1 Petro 1:15, 16.) Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kumuabudu yeye tu na kumutii kwa moyo wetu wote. Hata wakati tunateswa, tunajikaza kuishi kulingana na mambo yenye Yehova anatufundisha. Wakati tunaishi kulingana na kanuni za Yehova, tunaletea jina lake utukufu. (Mathayo 5:14-16) Tunaonyesha wazi kuwa kanuni zake ni za muzuri na kama Shetani ni muongo. Hatukamilike, kwa hiyo tunafanya makosa. Lakini wakati tunafanya makosa, tunatubu na tunajikaza sana kuacha kufanya mambo yenye kuchafua jina la Yehova.​—Zaburi 79:9.

lvs uku. 77 fu. 6

Namna Tunaweza Kuchagua Mambo ya Kujifurahisha

6 Yehova anatuambia hivi: “Munapaswa kuwa watakatifu, kwa sababu mimi ni mutakatifu.” (1 Petro 1:14-16; 2 Petro 3:11) Yehova atakubali ibada yetu ikiwa tu iko takatifu, ao safi. (Kumbukumbu la Torati 15:21) Ibada yetu haiwezi kuwa safi kama tunafanya mambo yenye Yehova anachukia, kama vile mambo machafu, yenye jeuri, ao yenye kuwa na uhusiano na pepo wachafu. (Waroma 6:12-14; 8:13) Lakini Yehova anaweza kuchukizwa pia kama tunatumia mambo ya vile ili kujifurahisha. Ile inaweza kufanya ibada yetu isikuwe safi na Yehova hawezi kuikubali. Tena, ile mambo inaweza kuharibu kabisa uhusiano wetu pamoja naye.

Chimba ili Kupata Mali ya Kiroho

w08 15/11 uku. 21 fu. 9

Mambo Makubwa Katika Barua ya Yakobo na ya Petro

1:10-12. Malaika walitamani sana kuchunguza na kuelewa kweli nzito za kiroho zenye manabii wa Mungu wa zamani waliandika juu ya kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta. Lakini, ile mambo ilieleweka waziwazi wakati Yehova alianza kushugulika na kutaniko. (Efe. 3:10) Je, hatupaswe kufuata mufano wa malaika na kujikaza kuchunguza ndani ya “mambo mazito ya Mungu”?​—1 Ko. 2:10.

it-2-F uku. 1021 fu. 4

Mwangalizi

Mwangalizi Mukubwa Zaidi. 1 Petro 2:25 inataja maneno ya Isaya 53:6. Mu ile andiko, Petro anazungumuzia wale wenye kuwa ‘kama kondoo wenye walipotea njia’ kisha anasema: “Lakini sasa mumerudia kwa muchungaji na mwangalizi wa nafsi zenu.” Hapa Petro iko anazungumuzia Yehova Mungu, juu wale wenye aliandikia hawakukuwa wamepotea mbali na Yesu, lakini ni kupitia Yesu njo walikuwa wamerudishwa kwa Yehova Mungu, Muchungaji Mukubwa wa watu wake. (Zb 23:1; 80:1; Yer 23:3; Eze 34:12) Tena Yehova ni mwangalizi, mwenye anafanya uchunguzi. (Zb 17:3) Uchunguzi (Gr., e·pi·sko· peʹ) wake unaweza kupatanishwa na uamuzi wake wa kutoa hukumu ya kuharibu, kama vile ilikuwa mu wakati wa mitume, wakati Yerusalemu haikutambua wakati wa ‘kuchunguzwa kwake [Gr., e·pi·sko·pesʹ].’ (Lu 19:44) Ule uchunguzi unaweza kuleta matokeo ya muzuri na faida, kama vile itakuwa kwa wale wenye kumutukuza Mungu katika siku ya “uchunguzi wake [Gr., e·pi·sko·pesʹ].”​—1Pe 2:12.

TAREHE 21-27/10

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | 1 PETRO 3-5

“Mwisho wa Mambo Yote Umekaribia”

w13 15/11 uku. 3 fu. 1

‘Kesha Kuhusiana na Sala’

“MWANAUME mumoja aliyekuwa akifanya kazi usiku hapo zamani alisema hivi: “Kipindi cha usiku ambacho ni vigumu sana kuendelea kuwa macho ni kile kipindi cha mbele ya usiku kucha.” Bila shaka, wengine wanaofanya kazi usiku wanaweza kukubaliana na maneno yake. Sisi pia tuko katika kipindi ambacho ni rahisi sana kusinzia kiroho kwa sababu ulimwengu muovu wa Shetani unakaribia sana mwisho wake. (Rom. 13:12) Ni hatari kabisa ikiwa tunalala usingizi katika kipindi hiki cha mwisho-mwisho! Tunapaswa ‘kuwa na utimamu wa akili’ na kufuata shauri la Maandiko linalotuchochea ‘tukeshe kuhusiana na sala.’​—1 Pet. 4:7.

w99 15/4 uku. 22 fu. 3

Namna ya Kutambua na Kuushinda Uzaifu Wowote wa Kiroho

Basi, kamata kwa uzito onyo hili la upole la mutume Petro: “Mwisho wa mambo yote umekaribia. Kwa hiyo, mukuwe na akili ya muzuri, na mukeshe kuhusiana na sala. Zaidi ya mambo yote, mukuwe na upendo mwingi ninyi kwa ninyi, kwa sababu upendo unafunika zambi nyingi.” (1 Petro 4:7, 8) Ni mwepesi sana kuruhusu uzaifu wetu mbalimbali​—na wa watu wengine​—uingie mu mioyo yetu na akili zetu na kuwa kizuizi ao kitu cha kukwaza. Shetani anajua muzuri ule uzaifu wa wanadamu. Moja kati ya njia zake za ujanja ni kugawanya watu juu awashinde. Kwa hiyo, lazima tufanye haraka kufunika zambi za aina hiyo kwa kuonyeshana upendo mwingi na ‘tusimupatie Ibilisi nafasi.’​—Waefeso 4:25-27.

w18.03 uku. 14-15 fu. 2-3

Kukaribisha Wageni Kunaleta Furaha na Ni Jambo la Maana Sana!

2 Zaidi ya hilo, Petro alitia moyo ndugu zake hivi: ‘Mukaribishane.’ (1 Pet. 4:9) Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “kukaribisha” linamaanisha “kupendezwa na, ao kuonyesha wema kwa wageni.” Hata hivyo, ona kwamba Petro anatia moyo ndugu na dada zake ‘wakaribishane,’ hata kama tayari walikuwa wanajuana na kufanya mambo pamoja. Namna gani kukaribisha wengine kungewasaidia?

3 Kungefanya wakaribiane zaidi. Fikiria mufano wako mwenyewe. Ulifurahi wakati mutu fulani alikualika katika nyumba yake? Uko na mambo ya muzuri yenye unaendelea kukumbuka juu ya tukio hilo? Wakati ulialika ndugu ao dada fulani wa kutaniko lenu, urafiki wenu ulikomaa tena zaidi? Wakati tunakaribisha ndugu na dada zetu, tunafikia kuwajua muzuri zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Katika siku za Petro, kadiri hali ziliendelea kuharibika, Wakristo walipaswa kukaribiana zaidi. Mambo yako hivyo pia kwa Wakristo katika “siku [hizi] za mwisho.”​—2 Tim. 3:1.

Chimba ili Kupata Mali ya Kiroho

w13 15/6 uku. 23

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Biblia inasema kwamba Yesu ‘aliwahubiria roho walio katika gereza.’ (1 Pet. 3:19) Maneno hayo yanamaanisha nini?

▪ Mutume Petro anaonyesha kwamba roho hao walikuwa wale ambao “hawakuwa watiifu wakati subira ya Mungu ilipokuwa ikingoja katika siku za Noa.” (1 Pet. 3:20) Bila shaka, Petro alikuwa akizungumuzia malaika waliochagua kujiunga na Shetani katika uasi. Yuda anataja malaika ambao “hawakubaki mahali pao pa kwanza bali wakaacha makao yao wenyewe yanayofaa,” anaposema kwamba Mungu ‘amewaweka akiba wakiwa na vifungo vya milele chini ya giza nzito kwa ajili ya hukumu ya ile siku kubwa.’​—Yuda 6.

Ni katika njia gani viumbe hao wa kiroho hawakutii katika siku za Noa? Mbele ya Garika, roho waovu hao walivaa miili ya kibinadamu​—jambo ambalo Mungu hakuwapangia. (Mwa. 6:2, 4) Zaidi ya hilo, malaika hao waliolala na wanawake walikuwa wakifanya jambo lisilo la asili. Mungu hakuwaumba malaika ili wafanye ngono pamoja na wanawake. (Mwa. 5:2) Mungu atawaharibu malaika hao waovu na wasiotii kwa wakati ambao ameweka. Lakini kwa sasa, kama vile Yuda anavyosema, malaika hao wako katika hali ya ‘giza nzito,’ ni kusema, gereza la kiroho.

Ni wakati gani na namna gani Yesu aliwahubiria hao “roho walio katika gereza”? Petro aliandika kwamba jambo hilo lilitukia kisha “Yesu kufanywa kuwa hai katika roho.” (1 Pet. 3:18, 19) Petro anasema tena kwamba Yesu ‘aliwahubiria.’ Petro anatumia wakati uliopita ili kuonyesha kwamba mahubiri hayo yalifanyika mbele aandike barua yake ya kwanza. Kwa hiyo, inaonekana kwamba, wakati fulani kisha kufufuliwa, Yesu aliwatangazia roho hao waovu hukumu ya haki ambayo wanastahili kupewa. Yesu hakuwatolea tumaini lolote. Mahubiri hayo yalikuwa ya hukumu. (Yona 1:1, 2) Kwa kuwa Yesu alikuwa ameonyesha imani na uaminifu mupaka kifo na baadaye alifufuliwa​—na kuonyesha hivyo kwamba Ibilisi hakuwa na uwezo juu yake, Yesu alikuwa na musingi muzuri wa kutangaza hukumu hiyo.​—Yoh. 14:30; 16:8-11.

Kwa wakati unaokuja, Yesu atamutupa Shetani na malaika hao katika abiso. (Lu. 8:30, 31; Ufu. 20:1-3) Mupaka wakati huo, roho hao wasiotii wataendelea kuwa katika giza nzito la kiroho, na mwishowe wataharibiwa bila shaka.​—Ufu. 20:7-10.

w08 15/11 uku. 21 fu. 7

Mambo Makubwa Katika Barua ya Yakobo na ya Petro

4:6​—“Wafu” wenye walitangaziwa “habari njema” ni nani? Ni wale wenye walikuwa ‘wafu katika makosa yao na zambi zao,’ ao wale wenye walikuwa wafu kiroho, mbele ya kusikia habari njema. (Efe. 2:1) Lakini, kisha kuamini habari njema, walianza kuwa “wazima” kiroho.

TAREHE 28/10–3/11

UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | 2 PETRO 1-3

‘Weka Karibu Katika Akili Kuwapo kwa Siku ya Yehova’

w06 15/12 uku. 27 fu. 11

Yehova ‘Atahakikisha Kuwa Haki Imefanywa’

11 Lakini, namna gani tunapaswa kuelewa maneno ya Yesu kwamba Yehova atahakikisha kuwa haki imefanywa “haraka”? Neno la Mungu linaonyesha kuwa, hata kama “yeye [Yehova] ni muvumilivu,” atatimiza haki haraka kwa wakati wenye kufaa. (Luka 18:7, 8; 2 Petro 3:9, 10) Katika siku za Noa, wakati Garika ilifika, waovu waliharibiwa bila kukawia. Vilevile, katika siku za Loti, wakati moto ulishuka kutoka mbinguni, waovu waliangamia. Yesu alisema: “Itakuwa vilevile ile siku yenye Mwana wa binadamu atafunuliwa.” (Luka 17:27-30) Kwa mara ingine tena, waovu watapatwa na “uharibifu wa kushitukia.” (1 Watesalonike 5:2, 3) Kwa kweli, tunaweza kuwa hakika kabisa kama Yehova hataruhusu ulimwengu wa Shetani uendelee kwa siku moja zaidi kulingana na vile haki inaomba.

w06 15/12 uku. 19 fu. 18

“Siku Kubwa ya Yehova Iko Karibu”

18 Haishangaze kama mutume Petro anatuonya tuweke karibu katika akili “kuwapo kwa siku ya Yehova”! Namna gani tunaweza kufanya vile? Njia moja ni kuwa na “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ushikamanifu kwa Mungu.” (2 Petro 3:11, 12) Kuendelea kuwa na ile matendo kutatusaidia kutazamia kwa hamu kuja kwa “siku ya Yehova.” Maana ya kwanza ya neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “kuweka karibu katika akili” ni “kuharakisha.” Kwa kweli, hatuwezi kuharakisha wakati wenye unabakia wa kuja kwa siku ya Yehova. Lakini, wakati tunangojea ile siku, tutaona kama wakati unapita haraka kama tuko na mambo mingi ya kufanya katika utumishi wa Mungu.​—1 Wakorinto 15:58.

Chimba ili Kupata Mali ya Kiroho

w08 15/11 uku. 22 fu. 2

Mambo Makubwa Katika Barua ya Yakobo na ya Petro

1:19​—“Nyota ya muchana” ni nani, na ni wakati gani alitokea, na tunajua namna gani kama jambo hilo limekwisha kufanyika? “Nyota ya muchana” ni Yesu Kristo katika mamlaka ya Ufalme. (Ufu. 22:16) Mu mwaka wa 1914, Yesu alitokea mbele ya uumbaji wote akiwa Mufalme wa Kimasiya, na kutangaza mapambazuko ya siku mupya. Kugeuka sura kulionyesha mbele ya wakati utukufu wa Yesu na mamlaka ya Ufalme, na kukazia kwamba unabii wa neno la Mungu ni wenye kutegemeka. Kukazia akili neno hilo kunatia mwangaza katika mioyo yetu, na hivyo tunajua kama Nyota ya Muchana ametokea.

w08 15/11 uku. 22 fu. 3

Mambo Makubwa Katika Barua ya Yakobo na ya Petro

2:4​—“Tartaro” ni nini, na malaika waasi walitupwa ndani wakati gani? Tartaro ni hali fulani kama vile hali ya mufungwa katika gereza, na ni viumbe wa roho tu njo wanazuiliwa, hapana wanadamu. Ni hali ya giza nzito sana la kiakili kuhusiana na makusudi yenye kungaa ya Mungu. Wale wenye kuwa mu Tartaro hawana tumaini lolote la wakati wenye kuja. Mungu aliwatupa malaika waasi ndani ya Tartaro katika siku za Noa, na watabakia mu ile hali ya kushushwa mupaka wakati wataharibiwa.

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2026)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine