Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha
TAREHE 1-7/03
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 7-8
“Mambo Yenye Kambi ya Waisraeli Inatufundisha”
it-1-F uku. 508 fu. 5
Kutaniko
Zamani mu Israeli, mara mingi wakubwa ao wawakilishi njo walikuwa wanashugulikia mambo kwa ajili ya watu wengine. (Ezr 10:14) Kwa hiyo, kisha kusimamisha tabenakulo, “wakubwa wa makabila” walileta matoleo yao. (Hes 7:1-11) Mu siku za Nehemia pia, makuhani, Walawi na “vichwa vya watu” njo wenye walikuwa wanashuhudia kwa muhuri “mapatano yenye kutegemeka.” (Ne 9:38–10:27) Wakati Waisraeli walikuwa mu jangwa, watu 250 “kutoka kati ya wakubwa wa mukusanyiko, wanaume wenye kuchaguliwa wa kutaniko, watu wa maana,” walijiunga na Kora, Datani, Abiramu na Oni na wakakusanyika ili kumupinga Musa na Haruni. (Hes 16:1-3) Mungu alimungoza Musa achague wanaume 70 kati ya wanaume wazee Waisraeli wenye walikuwa maofisa ili wamusaidie kubeba “muzigo wa watu” wenye hangeweza kubeba yeye peke. (Hes 11:16, 17, 24, 25) Walawi 4:15 inazungumuzia “wazee wa mukusanyiko,” na inaonekana kama wawakilisha wa watu walikuwa wanaume wazee wenye walikuwa mu taifa la Israeli, vichwa vya watu, waamuzi na maofisa wao.—Hes 1:4, 16; Yos 23:2; 24:1.
it-2-F uku. 835-836
Rubeni
Mu kambi ya Waisraeli, Warubeni walikuwa upande wa kusini wa tabenakulo. Karibu yao kulikuwa wazao wa Simeoni na wazao wa Gadi. Wakati wa kuhama, ule mugawanyo wa makabila tatu wenye uliongozwa na Rubeni, ulifuata mugawanyo wa makabila ingine tatu, ni kusema, kabila la Yuda, Isakari na Zabuloni. (Hes 2:10-16; 10:14-20) Na ni vile pia makabila ilifuatana ili kutoa matoleo yao siku yenye tabenakulo ilizinduliwa.—Hes 7:1, 2, 10-47.
w04-SW 1/8 uku. 25 fu. 1
Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hesabu
8:25, 26. Ili kuhakikisha kwamba wanaume wenye uwezo ndio waliochaguliwa kufanya kazi za Walawi, wanaume wazee waliagizwa wastaafu kutoka katika utumishi wa lazima. Hata hivyo, wangeweza kujitolea kuwasaidia Walawi wengine. Ingawa leo wahubiri wa Ufalme hawastaafu, kanuni ya sheria hiyo hutufunza jambo muhimu. Ikiwa kwa sababu ya umri mkubwa Mkristo hawezi kutimiza wajibu fulani, huenda akafanya aina ya utumishi ambao ana uwezo wa kutimiza.
Mali ya Kiroho
it-2-F uku. 637
Muzaliwa wa Kwanza
Juu wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli njo walikuwa wanachaguliwa kuwa vichwa vya nyumba mbalimbali, ni wao njo waliwakilisha taifa lote. Mu Biblia, Yehova anasema kama taifa lote la Israeli ni “muzaliwa [wake] wa kwanza,” maana yake taifa lake la kwanza kwa sababu ya agano lenye alifanya na Abrahamu. (Kut 4:22) Juu ya kulinda uzima wa Waisraeli, Yehova alitoa amri ya kusema ‘kila muzaliwa wa kwanza mwanaume kati ya Waisraeli; muzaliwa wa kwanza mwanaume, wa mwanadamu na wa munyama,’ atakaswe kwa ajili yake. (Kut 13:2) Kwa hiyo, wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli walikuwa mali yake.
TAREHE 8-14/03
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 9-10
“Namna Yehova Anaongoza Watu Wake”
it-1-F uku. 386 fu. 5
Kambi
Namna Kambi ilikuwa inahamishwa kutoka fasi moja kuenda fasi ingine, ilikuwa pia kati ya mambo ya kushangaza ya tengenezo (mu Hesabu sura ya 33, Musa anaonyesha kama kambi ilihamishwa karibu mara 40). Wakati wingu lilifunika tabenakulo, kambi ilibakia palepale. Lakini wakati liliinuka, na kambi ilihamishwa. “Kwa agizo la Yehova Waisraeli walikuwa wanaondoka, na kwa agizo la Yehova walikuwa wanapiga kambi.” (Hes 9:15-23) Walitumia tarumbeta mbili za feza ili kupatia watu wenye walikuwa mu kambi ile maagizo ya Yehova. (Hes 10:2, 5, 6) Milio ya pekee yenye kubadilika badilika ya zile tarumbeta ilionyesha kama kambi ilipaswa kuhamishwa. Ile ilifanyika kwa mara ya kwanza mu “mwaka wa pili [1512 M.K.Y.], mwezi wa pili, siku ya makumi mbili.” Mugawanyo wa kwanza wa makabila tatu wenye uliongozwa na Yuda na wenye ulifuatwa na Isakari, kisha Zabuloni njo uliondoka wa kwanza na ulikuwa mbele pamoja na sanduku la agano. Wenye waliwafuata ilikuwa Wagershoni na Wamerari wenye walibeba tabenakulo. Kisha, mugawanyo wa makabila tatu wenye uliongozwa na Rubeni na wenye ulifuatwa na Simeoni na Gadi ulifuata. Kisha tena, wenye walifuata ilikuwa Wakohati wenye walibeba vyombo vya patakatifu, na kisha mugawanyo wa tatu wa makabila tatu wenye uliongozwa na Efraimu na wenye ulifuatwa na Manase na Benyamini. Na ku mwisho, ilikuwa kikundi cha nyuma cha kulinda kambi, ni kusema, mugawanyo wa makabila tatu wenye uliongozwa na Dani na wenye ulisindikizwa na Asheri na Naftali. Migawanyo mbili yenye ilikuwa na nguvu sana na watu mingi sana njo ilikuwa, moja mbele na ingine moja nyuma.—Hes 10:11-28.
w11-SW 15/4 uku. 4-5
Je, Unatambua Uthibitisho wa Mwongozo wa Mungu?
Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunathamini mwongozo wa Mungu? Mtume Paulo alisema hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee.” (Ebr. 13:17) Huenda nyakati nyingine ikawa vigumu kufanya hivyo. Kwa mfano: Jiweke katika hali ya Mwisraeli aliyeishi katika siku za Musa. Wazia kwamba baada ya wewe kutembea kwa muda fulani, ile nguzo inasimama. Itasimama mahali hapo kwa muda gani? Siku moja? Juma moja? Miezi fulani? Unajiuliza, ‘Je, ninahitaji kufungua mizigo yangu yote?’ Kwanza, huenda ukafungua vitu ambavyo unahitaji zaidi. Hata hivyo, baada ya siku chache, ukiwa umechoka kutafuta-tafuta vitu ndani ya mizigo yako, unaanza kufungua kila kitu. Lakini mara tu unapokaribia kumaliza kufungua kila kitu, unaona nguzo ikiinuka—na hivyo unalazimika kufunga mizigo yako tena! Hilo halingekuwa jambo rahisi wala lenye kupendeza. Ingawa hivyo, bado Waisraeli walipaswa ‘kuondoka mara moja baada ya’ wingu kuinuka.—Hes. 9:17-22.
Hivyo basi, tunatenda jinsi gani tunapopata mwongozo kutoka kwa Mungu? Je tunajaribu kuufuata ‘mara moja baada ya’ kutolewa? Au je, tunaendelea kufanya mambo kama vile tu tulivyozoea kufanya? Je, tunaelewa mwongozo uliorekebishwa, kama vile kuhusu kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani, kuwahubiria watu wanaozungumza lugha ya kigeni, kushiriki katika ibada ya familia kwa ukawaida, kushirikiana na Halmashauri za Uhusiano na Hospitali, na kujiendesha vizuri tunapokuwa katika makusanyiko? Pia, tunaonyesha kwamba tunathamini mwongozo wa Mungu kwa kukubali mashauri. Tunapofanya maamuzi mazito, hatutegemei hekima yetu wenyewe badala yake tunatafuta mwongozo kutoka kwa Yehova na tengenezo lake. Na kama vile tu mtoto anavyotafuta ulinzi kutoka kwa mzazi wake kunapokuwa na dhoruba, tunatafuta ulinzi katika tengenezo la Yehova wakati matatizo ya ulimwengu huu yanayofanana na mvua ya mawe yanapotupata.
Mali ya Kiroho
it-1-F uku. 207 fu. 7
Mukusanyiko
Faida ya kukusanyika. Pasaka ya kila mwaka ilikazia ulazima wa kukusanyika ili kupata faida kutokana na mipango yenye Yehova alikamata ya kukusanya watu wake ili kuwapatia chakula ya kiroho. Kila mutu mwenye alikuwa safi na hakukuwa ameenda safari lakini anakataa kimakusudi kuenda ku Pasaka alipaswa kuuawa. (Hes 9:9-14) Wakati Mufalme Hezekia aliita wakaaji wa Yuda na wakaaji wa Israeli ili kufanya Pasaka, aliwaambia hivi: “Watu wa Israeli . . . musikuwe kichwa-nguvu kama mababu zenu. Mujinyenyekeze mbele ya Yehova na mukuje patakatifu pake penye ametakasa milele na mumutumikie Yehova Mungu wenu, ili kasirani yake yenye kuwaka igeuke kutoka kwenu. . . . Yehova Mungu wenu ni mwenye huruma na rehema, na hatageuza uso wake kutoka kwenu kama munarudia kwake.” (2Ny 30:6-9) Mutu mwenye alikataa kimakusudi kuenda ku Pasaka alionyesha kabisa kama anamuacha Mungu. Hata kama Wakristo hawafanye zile sikukuu, sawa vile Pasaka, mutume Paulo anawatia moyo wasiache kukusanyika kwa ukawaida na anasema hivi: “Tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo ya muzuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama vile wengine wako na desturi, lakini tutiane moyo, na kufanya vile zaidi sana kwa kadiri munaona siku ile kuwa inakaribia.”—Ebr 10:24, 25; ona KUTANIKO.
TAREHE 15-21/03
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 11-12
“Epuka Kunungunika-nungunika”
w01-SW 15/6 uku. 17 fu. 20
Msiwe Wasikiaji Wasahaulifu
20 Wakristo wengi hawashawishiwi kufanya ngono haramu. Hata hivyo, tunahitaji kuwa waangalifu tusijiachilie kufuata mwenendo ambao utatufanya tuwe wanung’unikaji, na ambao waweza kufanya tukataliwe na Mungu. Paulo anatushauri hivi: “Wala tusimtie Yehova kwenye jaribu, kama vile baadhi [ya Waisraeli] walivyomtia yeye kwenye jaribu, ila kuangamia kutokana na wale nyoka. Wala tusiwe wanung’unikaji, kama vile baadhi yao walivyonung’unika, ila kuangamia kutokana na mwangamizi.” (1 Wakorintho 10:9, 10) Waisraeli waliwanung’unikia Musa na Aroni—naam, hata walimnung’unikia Mungu mwenyewe—wakilalamika juu ya mana waliyopewa kimuujiza. (Hesabu 16:41; 21:5) Je, Yehova aliudhiwa zaidi na uasherati wao kuliko kunung’unika kwao? Simulizi la Biblia linaonyesha kwamba wanung’unikaji wengi waliuawa na nyoka. (Hesabu 21:6) Katika kisa kingine kilichotukia hapo awali, wanung’unikaji waasi zaidi ya 14 700 waliuawa. (Hesabu 16:49) Kwa hiyo, na tusiijaribu subira ya Yehova kwa kudharau maandalizi yake.
w06-SW 15/7 uku. 15 fu. 7
‘Epukeni Manung’uniko’
7 Mtazamo wa Waisraeli ulikuwa umebadilika kama nini! Mwanzoni, walipowekwa huru kutoka Misri na kukombolewa kupitia Bahari Nyekundu, uthamini wao uliwachochea kumwimbia Yehova sifa. (Kutoka 15:1-21) Lakini kwa sababu ya matatizo ya nyikani na kuwaogopa Wakanaani, watu wa Mungu walipoteza uthamini wao na kuonyesha mtazamo wa kutoridhika. Badala ya kumshukuru Mungu kwa uhuru aliowapa, walimlaumu kwa sababu walidhani kwamba wamekosa vitu fulani. Hivyo, kunung’unika kulionyesha kwamba hawakuthamini maandalizi ya Yehova. Haishangazi kwamba Yehova alisema hivi: “Kusanyiko hili lenye uovu litaendelea kuwa na manung’uniko haya ambayo linaendeleza juu yangu mpaka wakati gani?”—Hesabu 14:27; 21:5.
it-2-F uku. 715 fu. 1
Ugomvi
Kunungunika. Kunungunika kunavunjaka moyo na kunabomoaka. Wakati kidogo tu kisha Waisraeli kutoka Misri, walianza kumunungunikia Yehova kwa kutafuta-tafuta makosa mu namna aliwaongoza kupitia Musa na Haruni. (Kut 16:2, 7) Ile manunguniko ilivunja Musa moyo na akaomba Yehova amuue. (Hes 11:13-15) Mutu mwenye ananungunika anaweza kujitia mu hatari ya kifo. Yehova aliona manunguniko ya watu juu ya Musa, kuwa manunguniko na uasi juu ya uongozi wake. (Hes 14:26-30) Watu mingi walikufa kwa sababu ya ile tabia ya kutafuta-tafuta makosa.
Mali ya Kiroho
it-2-F uku. 207
Mana
Maelezo. Mana ilikuwa “mweupe kama mbegu za mugiligilani” (coriandre) na “ilikuwa kama” ulimbo wa bedola. Utamu wake ulikuwa sawa vile wa “keki zenye kuwa tambarare na zenye kuwa na asali” ao wa “keki tamu yenye ilitiwa mafuta.” Kisha kuisaga kwenye majiwe ya kusagia ya mukono ao kuitwanga mu kinu, waliitokotesha ao kuitumia ili kutengeneza mikate na kuipika.—Kut 16:23, 31; Hes 11:7, 8.
TAREHE 22-28/03
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 13-14
“Namna Imani Inafanyaka Tukuwe na Uhodari”
w06-SW 1/10 uku. 16-17 fu. 5-6
Kuwa Hodari Kupitia Imani na Kumwogopa Mungu
5 Lakini, wapelelezi wawili Yoshua na Kalebu, walitamani kuingia Nchi ya Ahadi. Walisema hivi: “[Wakanaani] ni mkate kwetu. Ulinzi wao umegeuka kutoka juu yao, na Yehova yuko pamoja nasi. Msiwaogope.” (Hesabu 14:9) Je, uhakika wa Yoshua na Kalebu ulikuwa na msingi? Ndiyo! Wao pamoja na taifa lote, walikuwa wameona Yehova akifedhehesha taifa la Misri lenye nguvu na miungu yao kupitia Mapigo Kumi. Kisha, walimwona Yehova akimzamisha Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu. (Zaburi 136:15) Ni wazi kwamba, wapelelezi kumi na wale walioathiriwa nao hawakupaswa kuogopa. Yehova alisema hivi kwa huzuni nyingi: “Watakosa kuniamini mpaka wakati gani ijapokuwa ishara zote ambazo nilifanya katikati yao?”—Hesabu 14:11.
6 Yehova alitaja chanzo cha tatizo, yaani, woga wa watu hao ulionyesha kwamba hawakuwa na imani. Naam, kuna uhusiano wa karibu sana kati ya imani na uhodari, hivi kwamba mtume Yohana aliandika hivi kuhusu kutaniko la Kikristo na vita vyake vya kiroho: “Huu ndio ushindi ambao umeushinda ulimwengu, imani yetu.” (1 Yohana 5:4) Leo, imani kama ya Yoshua na Kalebu imewezesha habari njema ya Ufalme ihubiriwe ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni sita, vijana kwa wazee, wenye nguvu na walio dhaifu. Hakuna adui ambaye amefaulu kunyamazisha jeshi hilo lenye nguvu na lililo hodari.—Waroma 8:31.
Mali ya Kiroho
it-1-F uku. 740
Inchi Yenye Mungu Alipatia Waisraeli
INCHI yenye Mungu alipatia Waisraeli ilikuwa ya muzuri kabisa. Musa alituma watu fulani ili kupeleleza Inchi ya Ahadi na kuwaambia warudie na matunda fulani ya mu ile inchi. Wakati walirudia, walikuja na tini, makomamanga na kishada kimoja cha zabibu chenye kilibebwa na wanaume wawili kwenye muti! Hata kama waliogopa kwa sababu ya kukosa imani, walisema hivi: Inchi “kwa kweli inatiririka maziwa na asali.”—Hes 13:23, 27.
Hotuba
8 Ninaendelea kuona ahadi za Mungu kuwa ni za kweli kabisa? Kwa mufano, Mungu ameahidi kwamba ataharibu ulimwengu huu wa Shetani. Hata hivyo, je, tunakengeushwa na mambo mbalimbali ya kujifurahisha ya ulimwengu huu? Ikiwa ni hivyo, tunaweza kuanza kufikiri kwamba mwisho ungali mbali sana. (Habakuki 2:3) Tufikirie mufano mwingine. Yehova alitoa zabihu ya ukombozi, na ameahidi kusamehe makosa yetu. Lakini, ikiwa tunaendelea kukumbuka makosa yetu ya zamani, tunaweza kuanza kufikiri kwamba Yehova hajatusamehe kabisa. (Matendo 3:19) Na hilo linaweza kutufanya tukose furaha ya kumutumikia Mungu na kuacha kazi ya kuhubiri.
9 Ningali ninamutumikia Yehova kabisa kwa bidii? Ikiwa tunamutumikia Yehova kwa bidii, hilo litatusaidia tukaze akili yetu juu ya tumaini letu la wakati unaokuja. Lakini, itakuwa namna gani ikiwa tumeanza kukaza sana akili yetu juu ya faida zetu wenyewe? Kwa mufano, tunaweza kukubali kazi fulani yenye kuwa na mushahara muzuri, lakini yenye inafanya tusimutumikie Yehova kwa bidii. Hilo linaweza kufanya imani yetu ipunguke, na kutufanya tukuwe “goigoi” ni kusema, kumutumikia Yehova kwa uvivu.—Waebrania 6:10-12.
10 Niko tayari kusamehe wengine? Wakati wengine wanatukosea, je, tunakasirika na kuacha kuzungumuza nao? Ikiwa tunafanya hivyo, tunaweza kuanza kujifikiria sana sisi wenyewe. Wakati tunasamehe wengine, tunaonyesha kwamba tuko na imani katika Yehova. Namna gani? Wakati watu wanatukosea, wanakuwa na deni letu. Vilevile, wakati tunamukosea Yehova, tunakuwa na deni lake. (Luka 11:4) Kwa hiyo, wakati tunasamehe wengine, tunaonyesha kwamba tunamutumainia Yehova. Tunamutumainia abariki bidii yetu, na baraka zake ni za maana sana kuliko kuomba watu hao walipe deni letu. Wanafunzi wa Yesu walielewa kwamba inaomba kuwa na imani ili kusamehe wengine. Wakati Yesu aliwaambia kwamba wanapaswa kusamehe hata wale wenye wamewakosea mara nyingi, wanafunzi wake walimuambia hivi: ‘Utupatie imani zaidi.’—Luka 17:1-5.
11 Ninakasirika wakati wengine wananipatia mashauri? Tutafute namna ya kutumikisha mashauri yenye tunapewa kuliko kutafuta makosa katika mashauri hayo ao makosa ya mutu mwenye kutupatia mashauri. (Methali 19:20) Kwa hiyo, ujikaze sana ukuwe na maoni kama ya Yehova!
12 Ninanungunikia wale wenye kuongoza katika kutaniko? Wakati Waisraeli walikaza akili yao juu ya habari yenye kuvunja moyo ya wapelelezi kumi, walianza kunungunikia Musa na Haruni. Kisha Yehova akamuuliza Musa hivi: ‘Watakosa kuniamini mupaka wakati gani?’ (Hesabu 14:2-4, 11) Yehova alijua kwamba Waisraeli hawakumutegemea kwa sababu walinungunikia wanaume wenye alichagua ili waongoze, ni kusema, Musa na Haruni. Vilevile, ikiwa kila mara tunanungunikia wale wenye Yehova anatumia ili kuongoza watu wake leo, hilo linaweza kuonyesha kwamba imani yetu katika Mungu imeanza kuwa zaifu.
TAREHE 29/03–4/04
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 15-16
“Epuka Kujivuna na Kujiaminia Kupita Kiasi”
w11-SW 15/9 uku. 27 fu. 12
Je, Yehova Anakujua?
12 Hata hivyo, taifa la Israeli lilipokuwa njiani kuelekea kwenye Nchi ya Ahadi, Kora aliona mambo ambayo alifikiri kwamba yalikuwa makosa katika mpango wa Mungu. Kisha, wanaume wengine 250 walioongoza katika taifa hilo wakajiunga na Kora katika kujaribu kufanya marekebisho. Ni lazima iwe kwamba Kora na wale watu wengine walihisi kwamba uhusiano wao pamoja na Yehova hauwezi kuharibika. Walimwambia Musa hivi: “Imetosha, kwa sababu kusanyiko lote, wote hao ni watakatifu na Yehova yuko katikati yao.” (Hes. 16:1-3) Walikuwa na uhakika kupita kiasi na mtazamo wenye kiburi kama nini! Musa aliwaambia hivi: “Yehova atajulisha ni nani aliye wake.” (Soma Hesabu 16:5.) Kufikia mwisho wa siku iliyofuata, Kora na wote waliokuwa wamemuunga mkono katika kuasi walikuwa wamekufa.—Hes. 16:31-35.
w11-SW 15/9 uku. 27 fu. 11
Je, Yehova Anakujua?
11 Musa na Kora wanatofautiana sana inapohusu kuheshimu mpango wa Yehova na maamuzi yake. Matendo yao yanatusaidia kuelewa maoni ya Yehova kuwahusu. Kora alikuwa Mlawi Mkohathi, na alifurahia mapendeleo mengi, ambayo inaelekea yalitia ndani kuona Yehova akikomboa taifa la Israeli kupitia Bahari Nyekundu, kuunga mkono hatua ya Yehova ya kuwahukumu Waisraeli waliokosa kutii kwenye Mlima Sinai, na kushiriki katika kusafirisha sanduku la agano. (Kut. 32:26-29; Hes. 3:30, 31) Inaonekana kwamba alikuwa mshikamanifu kwa Yehova kwa miaka mingi na hivyo aliheshimiwa na watu wengi katika kambi ya Waisraeli.
Mali ya Kiroho
w98-SW 1/9 uku. 20 fu. 1-2
Hakikisha Unatanguliza Mambo Yanayopasa Kutangulizwa!
Yehova aliona kisa hicho kwa uzito. Biblia yasema, “BWANA akamwambia Musa, Mtu huyo lazima atauawa.” (Hesabu 15:35) Kwa nini Yehova aliona jambo ambalo mwanamume huyo alifanya kuwa zito sana?
Watu walikuwa na siku sita za kukusanya kuni na vilevile kushughulikia mahitaji yao ya chakula, mavazi, na makao. Siku ya saba ilikuwa itengwe kwa ajili ya mahitaji yao ya kiroho. Ingawa kukusanya kuni hakukuwa makosa, ilikuwa makosa kutumia wakati ambao ulipaswa kutengwa kwa ajili ya kumwabudu Yehova kufanya hivyo. Ijapokuwa Wakristo hawako chini ya Sheria ya Kimusa, je, kisa hiki hakitufundishi somo la kutanguliza mambo tunayopasa kutanguliza leo?—Wafilipi 1:10.
Hotuba
5 Kamusi moja inaeleza kwamba kujivuna “ni kujiona kuwa wa maana sana na mwenye kuheshimiwa.” Tena ni “kutosheka kwa sababu wewe ao watu wenye unapenda sana wametimiza jambo fulani nzuri ao wamepata kitu fulani kizuri.” Kujisikia hivyo haiko mubaya. Mutume Paulo aliwaambia Wakristo Wathesalonike hivi: ‘Sisi wenyewe tunajivunia ninyi kati ya makutaniko ya Mungu kwa sababu ya uvumilivu wenu na imani katika mateso yenu yote na ziki munazovumilia.’ (2 Tes. 1:4) Kwa hiyo, kufurahia kazi yenye wengine wametimiza na kujivuna kwa kiasi fulani, kunaweza kutusaidia tujisikie muzuri. Hatuwezi kusikilia haya familia yetu, desturi za kwetu, ao nafasi kwenye tumekomalia.—Mdo. 21:39.
6 Lakini, kuna aina fulani ya majivuno yenye inaweza kubadilika na kuwa kiburi. Aina hiyo ya majivuno inaweza kutufanya tupoteze uhusiano wetu na wengine na kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. Kujivuna kwa namna hiyo kunaweza kutufanya tuchukie wengine na kukataa mashauri mazuri yenye wanatutolea. (Zab. 141:5) Aina hiyo ya majivuno ni “kujitumainia kwa njia isiyofaa” ao kuwa na “kiburi kama watu wenye kujiona kuwa wao ni wa maana sana kuliko wengine.” Yehova anachukia kiburi. (Eze. 33:28; Amo. 6:8) Kwa sababu Shetani ni mwenye kiburi, anafurahi sana wakati anaona wanadamu wanaonyesha kiburi na majivuno. Kwa mufano, alifurahi sana wakati Nimrodi, Farao, na Absalomu walionyesha kiburi. (Mwa. 10:8, 9; Kut. 5:1, 2; 2 Sam. 15:4-6) Mungu alimukataa Kaini kwa sababu ya kiburi. Alimushauria, lakini kwa sababu alikuwa mwenye kiburi sana, alikataa mashauri hayo; na hilo lilimuletea musiba.—Mwa. 4:6-8.
TAREHE 5-11/04
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 17-19
“Mimi Ni . . . Uriti Wako”
w11-SW 15/9 uku. 13 fu. 9
Je, Unamfanya Yehova Awe Fungu Lako?
9 Fikiria Walawi, ambao hawakupata urithi wa nchi. Kwa kuwa walihangaikia hasa ibada safi, ili kupata mahitaji yao walihitaji kumtegemea Yehova, ambaye aliwaambia hivi: “Mimi ni fungu lako.” (Hes. 18:20) Ingawa hatutumikii katika hekalu halisi kama makuhani na Walawi walivyofanya, tunaweza kuiga roho yao, tukiwa na uhakika kwamba Yehova atatuandalia mahitaji yetu. Kadiri tunavyozidi kuingia katika siku za mwisho, ndivyo linavyokuwa jambo la maana zaidi kutegemea nguvu za Mungu za kutuandalia mahitaji yetu.—Ufu. 13:17.
w11-SW 15/9 uku. 7 fu. 4
Yehova Ni Fungu Langu
4 Mgawo huo ulimaanisha nini kwa Walawi? Yehova alisema kwamba angekuwa fungu lao kumaanisha kwamba badala ya kupewa urithi wa nchi, walikabidhiwa pendeleo lenye thamani sana la utumishi. Wangepata urithi wa kuwa “ukuhani wa Yehova.” (Yos. 18:7) Mistari mingine inayozunguka andiko la Hesabu 18:20 inaonyesha kwamba jambo hilo halikufanya wawe maskini kimwili. (Soma Hesabu 18:19, 21, 24.) Walawi walipaswa kupewa “kila sehemu ya kumi katika Israeli iwe urithi wao kwa sababu ya utumishi wao.” Wangepokea asilimia 10 ya mazao yote ya Waisraeli na ya wanyama walioongezeka. Kisha Walawi walipaswa kutoa sehemu ya 10 ya vitu walivyopokea kuwa mchango, “ule ulio bora zaidi,” ili kutegemeza ukuhani. (Hes. 18:25-29) Makuhani walipewa pia “michango yote mitakatifu” ambayo wana wa Israeli walimletea Mungu mahali pake pa Ibada. Hivyo, washiriki wa ukuhani walikuwa na sababu nzuri za kuamini kwamba Yehova angewatunza.
Mali ya Kiroho
g02-SW 6/8 uku. 14 fu. 2
Chumvi Ni Bidhaa Muhimu
Chumvi pia imekuwa alama ya uthabiti na udumifu. Hiyo ndiyo sababu, katika Biblia agano muhimu liliitwa “agano la chumvi,” na wale waliokubaliana mara nyingi walikula mlo pamoja, uliotiwa chumvi ili kuidhinisha agano hilo. (Hesabu 18:19) Chini ya Sheria ya Musa, chumvi ilitiwa kwenye matoleo madhabahuni, bila shaka ikionyesha hali ya kutokuwa na ufisadi au uharibifu wowote.
Hotuba
4 Tunamutolea Yehova kwa sababu tunamupenda na tunapenda kumuonyesha shukrani. Tunaguswa moyo sana wakati tunafikiria mambo yote yenye Yehova ametufanyia. Wakati alizungumuzia mambo yenye walikuwa nayo lazima ili kujenga hekalu, Mufalme Daudi alisema waziwazi kuwa kila kitu chenye tuko nacho kinatoka kwa Yehova na kama kila kitu chenye tunamupatia kinatoka katika vitu vyenye amekwisha kutupatia.—Soma 1 Mambo ya Nyakati 29:11-14.
5 Kutoa pia ni sehemu ya ibada yetu kwa Yehova. Katika maono fulani, mutume Yohana alisikia watumishi wa Yehova huko mbinguni wanasema hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” (Ufu. 4:11) Kwa kweli, unakubali kama Yehova anastahili utukufu wote na nguvu zote na heshima yote yenye tunaweza kumutolea wakati tunamupatia mambo ya muzuri zaidi yenye tuko nayo. Kupitia Musa, Yehova aliamuru Waisraeli wakusanyike mbele za Yehova mara tatu katika mwaka ili kufanya sikukuu. Kwa sababu kutoa ilikuwa sehemu ya ibada yao kwenye sikukuu hizo, Waisraeli hawakupaswa ‘kuonekana mbele za Yehova mikono mitupu.’ (Kum. 16:16) Vilevile leo, kutoa bila uchoyo ili kuonyesha shukrani na kutegemeza sehemu ya duniani ya tengenezo la Yehova, ni sehemu ya maana ya ibada yetu.
6 Kutoa kunatuleta faida. Ni muzuri tukuwe wenye kutolea wengine kwa ukarimu kuliko kuwa tu wenye kupokea. (Soma Methali 29:21.) Kwa mufano, mutoto anaweza kupatia wazazi wake zawadi fulani kwa kutumia feza kidogo zenye wamemupatia. Wazazi wanaweza kufurahia sana zawadi hiyo! Ao, mutoto mwenye kufanya kazi ya upainia na mwenye kuishi nyumbani anaweza kuwapatia wazazi feza fulani ili kuwasaidia kutimiza mahitaji yao. Hata kama wazazi hawamuombe kufanya hivyo, wanaweza kukubali zawadi hizo kwa sababu mutoto anatumia njia hiyo ili kuonyesha shukrani yake kwa ajili ya mambo yote yenye wanamufanyia. Vilevile, Yehova anajua kama wakati tunamutolea vitu vyetu vya lazima hilo linatuletea faida.
TAREHE 12-18
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 20-21
“Endelea Kuwa Mupole Wakati Unakazwa Kufanya Mambo ya Mubaya”
Tafuta Upole ili Kumupendeza Yehova
19 Tutaepuka kufanya makosa. Fikiria tena mufano wa Musa. Kwa miaka mingi aliendelea kuwa mupole na alimupendeza Yehova. Kisha, karibu na mwisho wa safari yenye magumu ya miaka 40 mu jangwa, Musa alishindwa kuonyesha upole. Dada yake, mwenye inawezekana kabisa kuwa alisaidia kuokoa uzima wake katika Misri, alitokea kufa na kuzikwa katika Kadeshi. Na mara ingine tena, Waisraeli walinungunika kama hawakuhangaikiwa muzuri. Wakati huo, ‘walibishana na Musa’ juu ya kukosa maji. Hata kama walikuwa wameona miujiza yote yenye Yehova alikuwa amefanya kupitia Musa, na hata kama Musa alikuwa amewaongoza kwa wakati murefu bila kutafuta faida zake mwenyewe, watu walinungunika. Hawakunungunika tu juu ya kukosa maji lakini pia walimunungunikia Musa; ni kama vile yeye njo alifanya wakose maji.—Hes. 20:1-5, 9-11.
Tafuta Upole ili Kumupendeza Yehova
20 Musa alikasirika sana; kwa hiyo, akakosa kuonyesha sifa yake ya upole. Hata kama Yehova alikuwa amemuamuru azungumuze na mwamba, Musa alisema na watu kwa kasirani na alisema kama yeye njo angefanya muujiza. Kisha, akapiga mwamba mara mbili na maji mingi ikatoka. Kwa sababu ya kiburi na kasirani, alifanya kosa nzito. (Zb. 106:32, 33) Juu Musa alikosa kuonyesha sifa ya upole kwa wakati fulani, hakuruhusiwa kuingia katika Inchi ya Ahadi.—Hes. 20:12.
21 Mufano wa Musa unatufundisha mambo ya maana. Kwanza, tunapaswa kujikaza sikuzote ili tuendelee kuwa na tabia ya upole. Kama tunaacha kuonyesha upole kwa muda fulani, tunaweza kuwa na kiburi bila kukawia na kinaweza kutufanya tuseme na kutenda kwa upumbavu. Pili, wakati tuko na mahangaiko ya akili, inaweza kuwa nguvu kuendelea kuwa wapole. Kwa, hiyo tunapaswa kujikaza kuwa wapole hata wakati tuko na mikazo.
w09-SW 1/9 uku. 19 fu. 5
Mwamuzi Anayehukumu kwa Haki
Kwanza, Mungu hakumwagiza Musa azungumze na watu, sembuse kuwahukumu kuwa waasi. Pili, Musa na Haruni hawakumpa Mungu utukufu. ‘Hamkunitakasa,’ Mungu akasema. (Mstari wa 12) Kwa kusema “tuwatolee ninyi maji,” Musa alizungumza kana kwamba yeye na Haruni—si Mungu—ndio waliokuwa wakiwaandalia maji hayo kimuujiza. Tatu, hukumu hiyo ililingana na hukumu zilizokuwa zimetolewa awali. Mungu hakuwaruhusu waasi wa kizazi kilichotangulia waingie Kanaani, kwa hiyo hakuwaruhusu Musa na Haruni pia waingie. (Hesabu 14:22, 23) Nne, Musa na Haruni walikuwa viongozi wa Israeli. Wale walio na madaraka mengi wanawajibika zaidi kwa Mungu.—Luka 12:48.
Mali ya Kiroho
Maoni ya Yehova Juu ya Uzaifu wa Wanadamu?
12 Katika hali hizo zote, Yehova alipaswa kumupatia Haruni malipizi mara moja. Lakini alielewa kwamba Haruni hakuwa mutu mubaya. Inaonekana kwamba Haruni alifanya makosa kwa sababu alikuwa katika hali ngumu na alichochewa na watu wabaya. Lakini, Haruni alikubali makosa yake na alikuwa tayari kukubali malipizi ya Yehova. (Kut. 32:26; Hes. 12:11; 20:23-27) Yehova alikazia imani ya Haruni na nia yake ya kutubu. Miaka mingi baadaye, Haruni na watoto wake waliendelea kukumbukwa kuwa watu waliomuogopa Yehova.—Zab. 115:10-12; 135:19, 20.
Hotuba
MAMBO UNAWEZA KUFANYA
Jiwekee muradi. Kuliko kusema “Hiyo ndiyo hali yangu,” jikaze kubadilika katika kipindi fulani, labda katika miezi sita. Katika kipindi hicho, andika maendeleo yako nafasi fulani. Kila wakati unapokasirika, andika (1) jambo lenye lilitokea, (2) namna ulitenda, na (3) namna ungetenda kwa njia ya muzuri, na sababu gani ungefanya hivyo. Kisha, ujiwekee muradi wa kutumia namna hiyo ya muzuri ya kutenda wakati utachokozwa tena. Shauri: Andika pia maendeleo yako! Andika juu ya namna unavyojisikia muzuri kisha kuonyesha sifa ya kujizuia.—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 3:8.
Usitende haraka. Wakati mutu fulani ao kitu fulani kinakukasirisha, usiseme neno la kwanza linalokuja katika akili yako. Lakini, ungojee. Vuta pumuzi kabisa ikiwa ni lazima. Erik, aliye na miaka 15, anasema hivi: “Wakati ninavuta pumuzi, hilo linanitolea wakati wa kufikiri mbele nifanye ao kusema jambo fulani lenye nitahuzunikia baadaye.”—Kanuni ya Biblia: Methali 21:23.
Panua mawazo yako. Wakati fulani unaweza kukasirika kwa sababu unaona tu sehemu moja ya hali fulani, ni kusema, sehemu inayokukasirisha. Jaribu kufikiria sehemu ingine ya hali hiyo. Kijana mwanamuke anayeitwa Jessica anasema hivi: “Hata wakati watu wananitendea bila adabu kabisa, kwa kawaida kuna maelezo fulani yanayoweza kunisaidia niwaelewe kidogo.”—Kanuni ya Biblia: Methali 19:11.
Ikiwa ni lazima, ondoka hapo. Biblia inasema hivi: ‘Kabla mabishano hayajalipuka, ujiondokee.’ (Methali 17:14) Kama vile andiko hilo linasema, wakati fulani ni muzuri tu kuondoka katika hali inayochochea hasira. Kwa hiyo, kuliko kuendelea kuwaza juu ya tatizo na kuacha hasira yako ipande zaidi, usibakie bila kufanya jambo lolote. Kijana mwanamuke anayeitwa Danielle anasema hivi: “Ninaona kuwa kufanya mazoezi ya mwili kunaweza kupunguza mahangaiko yangu ya akili na kunisaidia nisipandwe na hasira.”
Jifunze kutofuatilia kila jambo. Biblia inasema hivi: ‘Mufazaike, lakini musitende zambi. Museme moyoni mwenu, . . . na kunyamaza.’ (Zaburi 4:4) Ona kama hakuna ubaya wa kujisikia mwenye kufazaika. Ulizo ni, Ni nini kitatokea kisha hapo? Kijana mwanaume anayeitwa Richard anasema hivi: “Ikiwa unaacha wengine wakukasirishe, hilo linawafanya wakuwe na uwezo juu yako. Sababu gani usijikaze kuwa mutu muzima na kuacha jambo hilo lipite?” Ukifanya hivyo, utatawala hasira yako kuliko kuacha hasira ikutawale.
TAREHE 19-25/04
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 22-24
“Yehova Anageuza Laana Kuwa Baraka”
bt-SW uku. 53 fu. 5
Kutangaza “Habari Njema Juu ya Yesu”
5 Leo, kama vile ilivyokuwa katika karne ya kwanza, kuteswa kwa watu wa Mungu hakujazuia kazi yao ya kuhubiri. Kila mara kuwahamisha Wakristo kwa lazima—iwe kwa kuwatupa gerezani au kuwalazimisha wahamie nchi nyingine—kumefungua maeneo mapya ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Kwa mfano, wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wa Yehova waliwahubiria wafungwa wenzao katika kambi za mateso za Nazi. Myahudi mmoja aliyekutana na Mashahidi katika kambi hizo anasema: “Uimara wa wafungwa waliokuwa Mashahidi wa Yehova ulinihakikishia kwamba imani yao ilikuwa na msingi wa Maandiko—nami mwenyewe nikawa Shahidi.”
it-1-F uku. 909
Wazimu
Wazimu wa Kumupinga Yehova. Kwa upumbavu, nabii Balaamu alipenda kutabiri mambo ya mubaya juu ya Israeli ili Mufalme Balaki wa Wamoabu amupatie feza. Lakini Yehova alibadilisha mambo na akamuzuia kufanya vile. Mutume Petro alisema hivi juu ya Balaamu: “Munyama wa kubeba mizigo mwenye hana sauti alisema kwa sauti ya mwanadamu na kuzuia mwendo wa wazimu wa nabii huyo.” Kuhusu wazimu wa Balaamu, mutume alitumie neno la Kigiriki pa·ra·phro·niʹa, lenye linatoa wazo ya ‘kupoteza akili.’—2Pe 2:15, 16; Hes 22:26-31.
Mali ya Kiroho
w04-SW 1/8 uku. 27 fu. 2
Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hesabu
22:20-22—Kwa nini hasira ya Yehova iliwaka dhidi ya Balaamu? Yehova alikuwa amemwambia nabii Balaamu asiwalaani Waisraeli. (Hesabu 22:12) Hata hivyo, nabii huyo alienda pamoja na watu wa Balaki akiwa amekusudia kabisa kuwalaani Waisraeli. Balaamu alitaka kumpendeza mfalme wa Moabu na kupokea zawadi kutoka kwake. (2 Petro 2:15, 16; Yuda 11) Hata baada ya Balaamu kulazimishwa kuwabariki Waisraeli badala ya kuwalaani, bado alitafuta kibali cha mfalme kwa kupendekeza kwamba waabudu wa kike wa Baali watumiwe ili kuwashawishi wanaume Waisraeli. (Hesabu 31:15, 16) Hivyo, hasira ya Mungu dhidi ya Balaamu iliwaka kwa sababu ya pupa mbaya sana ya nabii huyo.
TAREHE 26/04–2/05
UTAJIRI WA NENO LA MUNGU | HESABU 25-26
“Mutu Moja Anaweza Kufanya Mambo Ibadilike?”
‘Kimbia Uasherati!’
MUVUAJI wa samaki anaenda nafasi kwenye anaweza kupata aina ya samaki yenye anapenda kukamata. Anachagua chambo cha kutumia na anatupa ndoano mu maji. Anangojea kwa uvumilivu, na wakati samaki inakula chambo anaikamata kupitia ndoano na kuileta ku inchi kavu.
2 Vilevile, watu wanaweza kunaswa. Kwa mufano, Waisraeli walikuwa karibu kuingia mu Inchi ya Ahadi wakati walipiga kambi katika maeneo tambarare ya Moabu. Mufalme wa Moabu aliahidi mwanaume mwenye kuitwa Balaamu kama atamupatia feza mingi ikiwa analaani Waisraeli. Mwishowe, Balaamu alipata njia yenye ingefanya Waisraeli wajiletee laana wao wenyewe. Alichagua chambo kwa uangalifu. Alituma vijana wanamuke Wamoabu mu kambi ya Waisraeli ili washawishi wanaume Waisraeli.—Hesabu 22:1-7; 31:15, 16; Ufunuo 2:14.
‘Kimbia Uasherati!’
4 Juu ya nini Waisraeli wengi vile walinaswa mu mutego wa Balaamu? Walikuwa wanafikiria tu kupata furaha yao ya kichoyo, na walisahau mambo yenye Yehova alikuwa amewafanyia. Waisraeli walikuwa na sababu mingi za kuwa washikamanifu kwa Mungu. Alikuwa amewakomboa kutoka mu utumwa wa Misri, aliwapatia chakula mu jangwa, na aliwafikisha kwa usalama ku mupaka wa Inchi ya Ahadi. (Waebrania 3:12) Lakini, walishawishiwa kufanya uasherati. Mutume Paulo aliandika hivi: “Na tusifanye uasherati, kama vile wamoja kati yao walifanya uasherati, . . . wakaanguka.”—1 Wakorinto 10:8.
Mali ya Kiroho
it-1-F uku. 933 fu. 5-6
Mupaka
Kwa hiyo inaonekana kama namna inchi iligawanywa kati ya makabila, ilitegemea mambo mbili: kupiga kura na ukubwa wa kabila. Pengine kura ilikuwa inaonyesha tu fasi yenye ilikuwa karibu na eneo yenye kila kabila ingepata, kwa kuonyesha ni wapi uriti wa kila kabila ungekuwa. Kwa mufano, upande wa kaskazini ao kusini, mashariki ao mangaribi, mu eneo tambarare la pembeni ya bahari ao mu eneo lenye milima. Yehova njo alifanya kukuwe mupango wa kupiga kura, na ile njo ingefanya kusikuwe wivu ao ugomvi kati ya makabila. (Mez 16:33) Kupitia ile mupango, Yehova angeweza pia kuongoza mambo mu njia ya kwamba hali ya kila kabila ipatane na unabii wenye kuwa mu Mwanzo 49:1-33, wenye muzee wa ukoo Yakobo alitoa na iko ku kitanda mbele akufe.
Kisha kura kuonyesha fasi yenye kabila fulani itariti, iliomba sasa kufikiria ukubwa wa kabila ili kujua ukubwa wa eneo yenye ile kabila ilipaswa kupewa. “Munapaswa kugawanya inchi hiyo kwa kura ili kuwa uriti kati ya familia zenu. Kwa kikundi kikubwa mutaongeza uriti wake, na kwa kikundi kidogo mutapunguza uriti wake. Uriti wa kila mutu utakuwa mahali kwenye kura yake itaangukia.” (Hes 33:54) Uamuzi wa kupiga kura ili kuonyesha fasi yenye kabila fulani ilipaswa kuriti haukuwa unabadilika, lakini kulikuwa kunafanywa mabadiliko fulani kuhusu ukubwa wa uriti. Kwa mufano, wakati ilionekana kama eneo ya Yuda ilikuwa kubwa sana, sehemu fulani za ile eneo zilipunguzwa na zikapewa kabila la Simeoni.—Yos 19:9.
Hotuba
w04-SW 1/4 uku. 29
Kuna sababu kadhaa zinazoweza kutusaidia kuelewa tofauti kati ya idadi ya Waisraeli wanaotajwa katika mistari hiyo miwili. Mojawapo ya sababu za msingi zaidi ni kwamba idadi kamili inaweza kuwa kati ya 23 000 na 24 000, na hivyo tunaweza kutumia mojawapo ya idadi hizo kama idadi kamili.
Fikiria uwezekano mwingine. Mtume Paulo alitaja masimulizi hayo kuhusu Waisraeli huko Shitimu kuwa kielelezo cha kuwaonya Wakristo katika Korintho la kale, jiji ambalo lilijulikana sana kwa maisha yaliyopotoka kiadili. Aliandika: “Wala tusifanye uasherati, kama baadhi yao walivyofanya uasherati, na kuanguka, 23 000 kati yao katika siku moja.” Akitaja wale waliouawa na Yehova kwa sababu ya kufanya uasherati, Paulo alisema kwamba idadi yao ilikuwa 23 000.—1 Wakorintho 10:8.
Hata hivyo, kitabu cha Hesabu sura ya 25 kinatuambia kwamba ‘Israeli alijishikamanisha na Baali wa Peori; nayo hasira ya Yehova ikaanza kuwaka juu ya Israeli.’ Ndipo, akamwamuru Musa awaue “wote walio vichwa vya watu.” Musa naye akawaamuru waamuzi watekeleze amri hiyo. Mwishowe, Finehasi alipotenda kwa haraka na kumuua Mwisraeli aliyemwingiza mwanamke Mmidiani katika kambi, “tauni ikakomeshwa.” Masimulizi hayo yanamalizika kwa maneno haya: “Waliokufa kutokana na tauni hiyo walijumlika kuwa 24 000.”—Hesabu 25:1-9.
Yaonekana idadi inayotolewa katika kitabu cha Hesabu inatia ndani wale “walio vichwa vya watu” ambao waliuawa na waamuzi, na wale waliouawa moja kwa moja na Yehova. Huenda ikawa kwamba waamuzi waliwaua vichwa vya watu elfu moja, hivyo kufanya jumla ya wote waliouawa kuwa 24 000. Hata kama wale waliokuwa vichwa vya watu au viongozi wa maasi walifanya uasherati, wakashiriki katika sherehe, au wakakubaliana na wale waliofanya mambo hayo, walikuwa na hatia ya ‘kujishikamanisha na Baali wa Peori.’
Kuhusu neno ‘kujishikamanisha,’ kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinasema kwamba neno hilo linaweza kumaanisha “kuungana na mtu mwingine.” Waisraeli walikuwa watu waliojiweka wakfu kwa Yehova, lakini ‘walipojishikamanisha na Baali wa Peori,’ walivunja uhusiano huo pamoja na Mungu. Miaka 700 hivi baadaye, Yehova alisema hivi kuwahusu Waisraeli kupitia nabii Hosea: “Wao wenyewe waliingia kwa Baali wa Peori, nao wakajiweka wakfu kwa kitu kile cha aibu, wakawa wenye kuchukiza kama kile kitu walichokipenda.” (Hosea 9:10) Wote waliofanya hivyo walistahili hukumu kali ya Mungu. Hivyo, Musa akawakumbusha hivi wana wa Israeli: “Macho yenu wenyewe ndiyo yaliyoona mambo ambayo Yehova alifanya katika kile kisa cha Baali wa Peori, kwamba kila mtu aliyemfuata Baali wa Peori ndiye ambaye Yehova Mungu wako aliangamiza kutoka katikati yako.”—Kumbukumbu la Torati 4:3.