Kazi Inayoomba Unyenyekevu
1 Neno la Mungu linatushauri tuwe ‘wanyenyekevu katika akili, tukiwa hatulipi ubaya kwa ubaya bali, kinyume cha hiyo, tukitoa baraka.’ (1 Pet. 3:8, 9) Bila shaka shauri hilo linatumika katika kazi ya kuhubiri. Kwa kweli, huduma ya Kikristo inaweza kujaribu unyenyekevu wetu.
2 Unyenyekevu ni sifa inayotusaidia tuvumilie hali zisizopendeza. Tunapohubiri, tunakaribia watu tusiowajua bila kualikwa, tukijua kwamba wengine wataitikia katika hali isiyo na fadhili. Kuendelea kuhubiri ijapokuwa hali kama hizo kunaomba unyenyekevu. Katika eneo moja gumu sana, dada wawili mapainia walihubiri mlango kwa mlango kila siku kwa muda wa miaka miwili bila kupata mtu yeyote wa kuwasikiliza! Hata hivyo, walivumilia, na leo kuna makutaniko mawili katika eneo hilo.
3 Kushughulikia Ukosefu wa Adabu: Unyenyekevu utatusaidia kumwiga Yesu wengine wanapokuwa hawana fadhili wala adabu. (1 Pet. 2:21-23) Kwenye nyumba moja, mke na kisha mume wake walimtukana dada mmoja na kumwomba atoke nje ya kiwanja chao. Dada akatabasamu tu na kusema kwamba alitumaini kuzungumza nao wakati mwingine. Jambo hilo liligusa sana mume huyo na mke wake hivi kwamba walisikiliza Shahidi aliyewatembelea wakati uliofuata na wakakubali mwaliko wa kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Yule dada ambaye hapo mwanzoni alidhihakiwa alikuwa hapo ili kuwasalimu na kuwatolea ushahidi zaidi. Sisi pia tunaweza kupunguza upinzani wa wale wanaoitikia vibaya kwa kuonyesha “tabia-pole na staha yenye kina kirefu.”—1 Pet. 3:15; Mez. 25:15.
4 Epuka Majivuno: Ujuzi wetu wa Biblia haututolei sababu ya kuona watu kuwa chini yetu au kusema juu yao kwa kudharau. (Yn. 7:49) Badala yake, Neno la Mungu linatushauri ‘tusiseme kwa ubaya juu ya yeyote.’ (Tito 3:2) Tunapojishusha, kama alivyofanya Yesu, tunaburudisha wengine. (Mt. 11:28, 29) Hali yenye unyenyekevu inaongeza uvutio kwa ujumbe wetu.
5 Ndiyo, unyenyekevu unatusaidia tuvumilie katika eneo gumu. Unaweza kupunguza upinzani wa wale wanaoitikia vibaya, na unafanya wengine wavutiwe na ujumbe wa Ufalme. Zaidi ya yote, unampendeza Yehova, ambaye “huwapa wanyenyekevu fadhili isiyostahiliwa.”—1 Pet. 5:5.