-
Anafundisha Unyenyekevu Kwenye Pasaka ya MwishoYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 116
Anafundisha Unyenyekevu Kwenye Pasaka Ya Mwisho
MATAYO 26:20 MARKO 14:17 LUKA 22:14-18 YOHANA 13:1-17
YESU ANAKULA PASAKA YAKE YA MWISHO PAMOJA NA MITUME
ANAFUNDISHA SOMO FULANI KWA KUNAWISHA MIGUU YA MITUME
Kwa muongozo wa Yesu, Petro na Yohana tayari wamefika Yerusalemu ili kutayarisha Pasaka. Kisha, Yesu na mitume wengine kumi wanawafuata huko. Ni kisha muchana, na jua linaanza kuingia katika mawingu upande wa mangaribi wakati Yesu na mitume wake wanashuka kutoka kwenye Mulima wa Mizeituni. Hii ni siku ya mwisho ya Yesu; ataonekana tena hapa kisha tu kufufuliwa.
Bila kukawia, Yesu pamoja na mitume wake, wanafika Yerusalemu na wanaenda katika nyumba kwenye watakulia chakula cha Pasaka. Wanapanda mupaka kwenye chumba cha juu. Humo wanakuta kwamba mambo yote yamekwisha kuwa tayari kwa ajili ya chakula chao cha pekee. Yesu amekuwa akingojea kwa hamu tukio hili, kwa sababu anasema hivi: “Nimetamani sana kula Pasaka hii pamoja na ninyi mbele niteseke.”—Luka 22:15.
Miaka mingi mbele ya hapo, desturi ya kupitisha vikombe vya divai kati ya watu wenye kula Pasaka ilianzishwa. Sasa, kisha kupokea kikombe cha divai, Yesu anatoa shukrani na kusema: “Mukamate hiki na mukipitishe kwa kila mumoja kati yenu, kwa maana ninawaambia ninyi, kuanzia sasa sitakunywa tena divai ya muzabibu mupaka wakati Ufalme wa Mungu utakuja.” (Luka 22:17, 18) Ni wazi kwamba kifo chake kinakaribia.
Kisha muda fulani wakati wa chakula cha Pasaka, jambo lenye haliko la kawaida linatokea. Yesu anasimama, anaweka pembeni nguo yake ya inje na anakamata nguo ya kupanguza nayo maji. Kisha anatia maji katika beseni yenye kuwa karibu yake. Kwa kawaida ni mwenye nyumba ndiye alipaswa kuhakikisha kwamba miguu ya wageni wake inanawishwa, pengine na mutumwa wake. (Luka 7:44) Wakati huu, mwenye nyumba haiko, kwa hiyo, Yesu anafanya kazi hii. Kazi hiyo ingepaswa kufanywa hata na mumoja wa mitume wake, lakini hakuna hata mumoja mwenye anaifanya. Je, ni kwa sababu ya mabishano fulani yenye yalikuwa kati yao? Hata sababu ikuwe nini, wanasikia haya kuona Yesu akiwanawisha miguu.
Wakati Yesu anataka kumunawisha Petro, anakataa na kusema hivi: “Hautaninawisha miguu hata kidogo.” Yesu anamwambia hivi: “Kama sikunawishe, hauna sehemu pamoja na mimi.” Petro anajibu hivi: “Bwana, usininawishe miguu tu, lakini uninawishe pia mikono na kichwa.” Jibu hili la Yesu linamushangaza: “Kila mutu mwenye ameoga iko na lazima tu ya kunawa miguu, lakini iko safi kabisa. Na ninyi muko safi, lakini hapana ninyi wote.”—Yohana 13:8-10.
Yesu ananawisha miguu ya mitume wote 12, kutia ndani Yuda Iskariote. Kisha kuvaa nguo yake ya inje, Yesu anakaa tena pembeni ya meza, anawauliza: “Je, munaelewa jambo lenye nimewafanyia? Ninyi munaniita, ‘Mwalimu,’ na, ‘Bwana,’ na munasema kweli, kwa maana ni vile niko. Kwa hiyo, kama mimi mwenye ni Bwana na Mwalimu, niliwanawisha ninyi miguu, ninyi pia munapaswa kunawishana miguu. Kwa maana niliwawekea ninyi mufano, ili kama vile niliwafanyia ninyi, ninyi pia mufanye vilevile. Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, mutumwa haiko mukubwa kuliko bwana wake, wala ule mwenye alitumwa haiko mukubwa kuliko ule mwenye alimutuma. Kama munajua mambo haya, ninyi ni wenye furaha ikiwa munayatenda.”—Yohana 13:12-17.
Hilo ni somo la muzuri sana kuhusu unyenyekevu! Wafuasi wa Yesu hawapaswe kujitanguliza, hawapaswe kuwaza kama wako wa maana na kwamba wanapaswa kutumikiwa. Lakini, kuliko kufuata desturi ya kunawisha tu miguu ya watu, wanapaswa kufuata mufano wa Yesu kwa kuwa tayari kutumikia wengine kwa unyenyekevu na bila ubaguzi.
-
-
Chakula cha Mangaribi cha BwanaYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 117
Chakula Cha Mangaribi Cha Bwana
MATAYO 26:21-29 MARKO 14:18-25 LUKA 22:19-23 YOHANA 13:18-30
YUDA ANAONYESHWA KUWA MUSALITI
YESU ANAANZISHA CHAKULA CHA UKUMBUSHO
Kisha tu kuanza kwa mangaribi hii, Yesu alifundisha mitume wake somo la unyenyekevu kwa kuwanawisha miguu. Sasa inaonekana kwamba kisha chakula cha Pasaka, anataja unabii huu wa Daudi: “Mutu mwenye nilikuwa ninaishi naye kwa amani, mwenye nilitumainia, mwenye alikuwa anakula mukate wangu, ameinua kisigino chake juu yangu.” Kisha anaeleza hivi: “Mumoja wenu atanisaliti.”—Zaburi 41:9; Yohana 13:18, 21.
Mitume wanaangaliana, na kila mumoja anauliza: “Bwana, je, ni mimi?” Hata Yuda naye anauliza. Petro anamwambia Yohana, mwenye kukaa pembeni ya Yesu kwenye meza, amuulize. Kisha Yohana anamukaribia Yesu na kumuuliza: “Bwana, ni nani?”—Matayo 26:22; Yohana 13:25.
Yesu anajibu hivi: “Ni ule mwenye nitapatia kipande cha mukate chenye ninaingiza katika bakuli.” Na kisha kuingiza mukate katika bakuli, anamupatia Yuda, na kusema hivi: “Kwa kweli, Mwana wa binadamu anaenda zake, kama vile iliandikwa juu yake, lakini ole kwa ule mutu mwenye anamusaliti Mwana wa binadamu! Ingekuwa muzuri zaidi kwa mutu huyo kama hangezaliwa.” (Yohana 13:26; Matayo 26:24) Kisha Shetani anaingia ndani ya Yuda. Yuda alikuwa tayari muovu, sasa anajiachilia kufanya mapenzi ya Ibilisi na kuwa “mwana wa uharibifu.”—Yohana 6:64, 70; 12:4; 17:12.
Yesu anamuambia Yuda: “Kile unafanya, ukifanye mbio sana.” Mitume wengine wanawaza kama Yesu anamuambia: “‘Nunua vitu vyenye tuko navyo lazima kwa ajili ya sikukuu,’ ao kwamba apatie maskini kitu fulani.” (Yohana 13:27-30) Lakini haiko hivyo, Yuda anaenda kumusaliti Yesu.
Mangaribi hiyohiyo, wakati wa chakula cha Pasaka, Yesu anaanzisha aina mupya ya chakula. Anakamata mukate, anatoa sala ya shukrani, anauvunja, na kuutolea mitume wake ili waukule. Anasema hivi: “Huu unamaanisha mwili wangu wenye utatolewa kwa ajili yenu. Muendelee kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Kipande cha mukate kinapitishwa kati yao, na mitume wanakikula.
Sasa Yesu anakamata kikombe cha divai, anatoa sala ya shukrani, na kisha anakipitishia mitume. Kila mumoja wao anakunywa, kisha Yesu anasema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa musingi wa damu yangu, yenye itamwangwa kwa ajili yenu.”—Luka 22:20.
Kwa kufanya hivyo, Yesu anaanzisha ukumbusho wa kifo chake wenye wafuasi wake wanapaswa kufanya kila mwaka tarehe 14 Mwezi wa Nisani. Itawakumbusha mambo yenye Yesu na Baba yake wamefanya ili kuwezesha wanadamu wenye imani waponyoke hukumu ya zambi na kifo. Ukumbusho unapita mambo yenye Pasaka ililetea Wayahudi kwa sababu unaletea wanadamu wenye imani ukombozi wa kweli.
Yesu anasema kama damu yake “itamwangwa kwa ajili ya wengi kwa musamaha wa zambi.” Mitume wake waaminifu na wengine wengi wako kati ya watu wengi wenye wanapata musamaha huo. Ni wao watakuwa naye katika Ufalme wa Baba yake.—Matayo 26:28, 29.
-
-
Wanabishana ili Kujua Ni Nani Ndiye Mukubwa Zaidi Kati yaoYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 118
Wanabishana Ili Kujua Ni Nani Ndiye Mukubwa Zaidi Kati Yao
MATAYO 26:31-35 MARKO 14:27-31 LUKA 22:24-38 YOHANA 13:31-38
YESU ANATOA MASHAURI KUHUSU KUTAFUTA CHEO
ANATABIRI KWAMBA PETRO ATAMUKANA
UPENDO UNATAMBULISHA WANAFUNZI WA YESU
Mangaribi yake ya mwisho pamoja na mitume wake, Yesu amewatolea somo la muzuri la kutumikia wengine kwa unyenyekevu kwa kuwanawisha miguu. Sababu gani hilo linafaa? Kwa sababu ya uzaifu wenye wameonyesha. Wamejitoa kwa Mungu, lakini wangali wanahangaikia kujua ni nani ndiye mukubwa zaidi kati yao. (Marko 9:33, 34; 10:35-37) Wanaonyesha tena uzaifu huo mangaribi hii.
Mitume wanaanza “bishano kali kati yao juu ya ni nani kati yao alionwa kuwa mukubwa zaidi.” (Luka 22:24) Yesu anapaswa kuwa mwenye huzuni sana kuwaona wakibishana tena. Anafanya nini?
Kuliko kuwafokea mitume wake kwa sababu ya tabia hiyo, Yesu anafikiri nao kwa uvumilivu. Anawaambia hivi: “Wafalme wa mataifa wanapiga ubwana juu yao, na wale wenye kuwa na mamlaka juu yao wanaitwa Watenda-mema. Hata hivyo, ninyi hamupaswe kuwa vile. . . . Kwa maana ni nani mukubwa zaidi, ule mwenye anakula ao ule mwenye anatumikia?” Kisha kuwakumbusha mufano wenye kila mara amewawekea, Yesu anasema: “Lakini mimi ni kama mutu mwenye kutumikia.”—Luka 22:25-27.
Hata kama walikuwa na uzaifu, mitume wamebaki waaminifu kwa Yesu katika majaribu yenye alipata. Kwa hiyo anasema: “Ninafanya agano pamoja na ninyi, kama vile Baba yangu alifanya agano pamoja na mimi, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:29) Wanaume hawa ni wafuasi waaminifu wa Yesu. Anawahakikishia kwamba kupitia agano lenye amefanya pamoja nao, watakuwa katika Ufalme na kutawala pamoja naye.
Hata kama mitume wako na tumaini hili la muzuri sana, bado hawajakamilika. Yesu anawaambia: “Shetani ameomba kuwapata ninyi wote ili awapepue kama ngano,” yenye inasambaa wakati inapepuliwa. (Luka 22:31) Anawaambia hivi: “Ninyi wote mutakwazika usiku huu kwa sababu ya mambo yenye yatanipata, kwa maana imeandikwa: ‘Nitapiga muchungaji, na kondoo wa kundi watatawanyika.’”— Matayo 26:31; Zekaria 13:7.
Petro anasema hivi kwa kujitumainia: “Hata kama wengine wote wanakwazika kwa sababu ya mambo yenye yatakupata, mimi sitakwazika hata kidogo!” (Matayo 26:33) Yesu anamuambia Petro kwamba mbele jogoo iwike mara mbili usiku huo, atamukana. Lakini, Yesu anaongeza: “Nimemulilia Mungu kwa ajili yako ili imani yako isififie; na wewe, wakati utarudia, utie nguvu ndugu zako.” (Luka 22:32) Lakini Petro anasema hivi kwa uhakika: “Hata nikilazimika kufa pamoja na wewe, sitakukana hata kidogo.” (Matayo 26:35) Mitume wengine nao wanasema vile.
Yesu anaambia wanafunzi wake: “Ningali pamoja na ninyi kwa wakati kidogo. Mutanitafuta; na kama vile niliambia Wayahudi, ‘Kwenye ninaenda hamuwezi kuja,’ sasa ninawaambia ninyi pia.” Kisha anaongeza: “Ninawapatia ninyi amri mupya, kwamba mupendane; kama vile nimewapenda ninyi, ninyi pia mupendane vilevile. Kwa jambo hili wote watajua kama ninyi ni wanafunzi wangu—kama muko na upendo kati yenu.”—Yohana 13:33-35.
Wakati Petro anasikia Yesu akisema kwamba angali pamoja nao kwa wakati kidogo, anauliza: “Bwana, unaenda wapi?” Yesu anamujibu: “Kule ninaenda hauwezi kunifuata sasa, lakini utanifuata kisha wakati fulani.” Petro anachanganyikiwa, kwa hiyo anasema: “Bwana, sababu gani siwezi kukufuata sasa? Nitatoa uzima wangu kwa ajili yako.”—Yohana 13:36, 37.
Yesu anawakumbusha sasa jambo lenye lilitokea wakati aliwatuma katika safari ya mahubiri huko Galilaya wakiwa bila mufuko wa feza ao mufuko wa chakula. (Matayo 10:5, 9, 10) Anawauliza: “Je, mulikosa kitu chochote?” Wanajibu: “Hapana!” Sasa watafanya nini katika siku zenye kuwa mbele? Anawatolea muongozo huu: “Lakini sasa ule mwenye kuwa na mufuko wa feza aukamate, akamate vilevile mufuko wa chakula, na ule mwenye hana upanga auzishe nguo yake ya inje na anunue moja. Kwa maana ninawaambia ninyi kwamba mambo yenye yaliandikwa juu yangu yanapaswa kutimia, ni kusema, ‘Alihesabiwa pamoja na watu wenye kuvunja sheria.’ Kwa maana hilo linatimia juu yangu.”—Luka 22:35-37.
Yesu anazungumuzia wakati wenye atapigwa misumari kwenye muti pamoja na watenda maovu, ao watu wenye kuvunja sheria. Kisha hapo wafuasi wake watapata mateso makali. Wanaona kama wako tayari na wanasema: “Bwana, angalia! Hapa kuko panga mbili.” Anajibu: “Inatosha.” (Luka 22:38) Kujua kama wako na panga mbili, kutamutolea Yesu nafasi ya kufundisha somo lingine la maana.
-
-
Yesu—Ni Njia, Kweli, na UzimaYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 119
Yesu—ni Njia, Kweli, Na Uzima
YESU ANAENDA KUTAYARISHA NAFASI
ANAAHIDI WANAFUNZI WAKE KWAMBA WATAPATA MUSAIDIZI
BABA NI MUKUBWA KULIKO YESU
Yesu angali katika chumba cha juu pamoja na wanafunzi wake kisha chakula cha ukumbusho, anawaambia hivi: “Mioyo yenu isivurugike. Mukuwe na imani katika Mungu; mukuwe na imani katika mimi pia.”—Yohana 13:36; 14:1.
Yesu anaelezea mitume wake waaminifu kuwa hawapaswe kutaabika ao kuhangaika kwa sababu anaenda. Anasema hivi: “Katika nyumba ya Baba yangu kuko makao mengi. . . . Kama ninaenda na kuwatayarishia ninyi nafasi, nitakuja tena na nitawapokea ninyi katika nyumba yangu mwenyewe, ili kwenye niko, ninyi pia mukuwe pale.” Lakini, mitume hawaelewe kuwa anazungumuzia juu ya kuenda mbinguni. Tomasi anauliza hivi: “Bwana, sisi hatujue kwenye unaenda. Namna gani tunaweza kujua njia?”—Yohana 14:2-5.
Yesu anajibia hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.” Wale wenye kumukubali na kusikiliza mafundisho yake na kufuata mufano wake, ndio tu wanaweza kuingia katika nyumba ya Baba yake, ni kusema, mbinguni. Yesu anasema hivi: “Hakuna mwenye anakuja kwa Baba isipokuwa kupitia mimi.”—Yohana 14:6.
Filipo mwenye anasikiliza kwa uangalifu, anamuomba hivi: “Bwana, utuonyeshe Baba, na hilo linatutosha.” Pengine Filipo anapenda Mungu afanye mambo fulani ili kujionyesha kama vile alifanya katika maono yenye Musa, Eliya, na Isaya waliona. Lakini, mitume wako na jambo la muzuri zaidi kuliko maono hayo. Yesu anaonyesha jambo hilo, anajibia hivi: “Je, hata kisha mimi kuwa pamoja na ninyi kwa wakati murefu vile, Filipo, bado haujanijua? Kila mutu mwenye ameniona mimi amemuona Baba pia.” Yesu anaonyesha kwa ukamilifu utu ao sifa za Baba yake; kwa hiyo, kuishi na Yesu na kumutazama kwa uangalifu ni kama vile kumuona Baba. Kwa kweli, Baba ni mukubwa kuliko Mwana, kwa sababu Yesu anasema hivi: “Mambo yenye ninawaambia ninyi, siyaseme kwa kujitungia mwenyewe.” (Yohana 14:8-10) Kwa hiyo, mitume wanaona kuwa Yesu anamupatia Baba yake utukufu kwa ajili ya mafundisho yake.
Mitume wa Yesu wameona namna anafanya miujiza na wamesikia namna anatangaza habari njema juu ya Ufalme wa Mungu. Sasa anawaambia hivi: “Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, kila mutu mwenye ananiamini atafanya pia kazi zenye mimi ninafanya; na atafanya kazi kubwa kuliko hizi.” (Yohana 14:12) Yesu hapendi kusema kuwa watafanya miujiza mikubwa kuliko yenye alifanya. Lakini, watafanya kazi ya kuhubiri kwa muda murefu zaidi, katika eneo kubwa zaidi, na watahubiria watu wengi zaidi.
Hawatabakia peke yao wakati Yesu ataenda, kwa sababu anawapatia ahadi hii: “Mukiomba jambo lolote katika jina langu, nitalifanya.” Pia, anasema hivi: “Nitamuomba Baba, na atawapatia ninyi musaidizi mwingine akuwe pamoja na ninyi milele, roho ya ile kweli.” (Yohana 14:14, 16, 17) Anawahakikishia kuwa watapata roho takatifu, ambayo ni musaidizi mwingine. Jambo hilo linatokea siku ya Pentekoste.
Yesu anasema hivi: “Kisha tu wakati kidogo ulimwengu hautaniona tena, lakini ninyi mutaniona, kwa sababu ninaishi na ninyi mutaishi.” (Yohana 14:19) Kisha kufufuliwa kwake, Yesu atawatokea akiwa na mwili wa kibinadamu, lakini pia kisha wakati fulani, atawafufua na kuwa pamoja nao mbinguni wakiwa viumbe wa roho.
Sasa Yesu anasema kweli hii yenye kuwa mwepesi: “Kila mutu mwenye kuwa na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye mwenye ananipenda. Na kila mutu mwenye ananipenda atapendwa na Baba yangu, na mimi nitamupenda na nitajionyesha waziwazi kwake.” Juu ya jambo hilo mutume Yuda, mwenye anaitwa pia Tadayo, anauliza hivi: “Bwana, kumetokea nini ili ukusudie kujionyesha waziwazi kwetu lakini hapana kwa ulimwengu?” Yesu anajibu hivi: “Kama mutu yeyote ananipenda, atashika neno langu, na Baba yangu atamupenda . . . Kila mutu mwenye hanipendi hashike maneno yangu.” (Yohana 14:21-24) Tofauti na mitume wake, ulimwengu haumuone Yesu kuwa njia, kweli, na uzima.
Yesu iko karibu kuenda, sasa namna gani wanafunzi wake wataweza kukumbuka mambo yote yenye aliwafundisha? Yesu anaeleza hivi: “Lakini musaidizi, roho takatifu yenye Baba atatuma katika jina langu, huyo atawafundisha mambo yote na kuwakumbusha mambo yote yenye niliwaambia.” Mitume wameona nguvu ya roho takatifu wakati inatenda, kwa hiyo, maneno hayo yanawatia moyo sana. Yesu anaongeza hivi: “Ninawaachia ninyi amani; ninawapatia amani yangu. . . . Mioyo yenu isivurugike wala kuregea kwa woga.” (Yohana 14:26, 27) Kwa sababu Yehova atawaongoza na kuwalinda, wanafunzi wa Yesu hawana sababu ya kuhangaika.
Hivi karibuni wataona ushuhuda wenye kuonyesha kuwa Mungu atawalinda. Yesu anasema hivi: “Mutawala wa ulimwengu anakuja, na hana uwezo juu yangu.” (Yohana 14:30) Shetani aliweza kuingia katika Yuda na kumuchochea. Lakini Yesu hana uzaifu wowote wa zambi wenye Shetani anaweza kutumia ili kumuchochea aache kumutii Mungu. Na Shetani hataweza kumufanya abakie katika kifo. Sababu gani? Yesu anasema hivi: “Ninafanya kama vile Baba aliniamuru.” Iko hakika kuwa Baba yake atamufufua.—Yohana 14:31.
-
-
Kuzaa Matunda Kama Matawi na Kuwa Marafiki wa YesuYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 120
Kuzaa Matunda Kama Matawi Na Kuwa Marafiki Wa Yesu
MUZABIBU WA KWELI NA MATAWI
NAMNA YA KUBAKIA KATIKA UPENDO WA YESU
Yesu ametoka tu kutia wanafunzi wake moyo kwa kuzungumuza nao kwa moyo wote. Ni usiku sana, pengine katikati ya usiku imekwisha kupita. Sasa Yesu anatoa mufano wenye kuchochea:
Anaanza hivi: “Mimi ndiye muzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mulimaji.” (Yohana 15:1) Mufano wake unafanana na mambo yenye yalikuwa yamesemwa mamia ya miaka mbele ya hapo juu ya taifa la Israeli, taifa lenye liliitwa muzabibu wa Yehova. (Yeremia 2:21; Hosea 10:1, 2) Lakini, Yehova anakaribia kukataa taifa hilo. (Matayo 23:37, 38) Kwa hiyo, Yesu anazungumuzia wazo la mupya. Yeye ndiye muzabibu wenye Baba yake amepanda tangu atiwe mafuta kwa roho takatifu katika mwaka wa 29 wakati wetu. Lakini, Yesu anaonyesha kuwa muzabibu unafananisha mambo mengi zaidi, anasema hivi:
“[Baba yangu] anatosha ndani yangu kila tawi lenye halizae matunda, na anasafisha kila tawi lenye linazaa matunda, ili lizae matunda zaidi. . . . Kama vile tawi likiwa peke yake haliwezi kuzaa matunda ikiwa halikae kwenye muzabibu, vilevile ninyi hamuwezi kuzaa matunda ikiwa hamukae katika umoja na mimi. Mimi ndiye muzabibu; na ninyi ndio matawi.”—Yohana 15:2-5.
Yesu ameahidi wanafunzi wake waaminifu kuwa kisha yeye kuenda, atatuma musaidizi, roho takatifu. Kisha siku makumi tano na moja, mitume na watu wengine walipata roho takatifu, na wakakuwa matawi ya muzabibu huo. Na “matawi” yote yalipaswa kubakia katika muungano na Yesu. Ili kutimiza kazi gani?
Anaeleza hivi: “Kila mutu mwenye anakaa katika umoja na mimi, na mimi katika umoja naye, huyo anazaa matunda mengi; kwa maana bila mimi hamuwezi kufanya jambo lolote hata kidogo.” “Matawi” hayo, ni kusema, wanafunzi wake waaminifu wangezaa matunda mengi, kwa kuiga sifa za Yesu, kwa kuhubiria wengine kwa bidii juu ya Ufalme wa Mungu, na kufanya wanafunzi wengi zaidi. Mambo yatakuwa namna gani ikiwa mutu anakosa kubakia katika muungano pamoja na Yesu na kushindwa kuzaa matunda? Yesu anasema hivi: “Kama mutu yeyote hakae katika umoja na mimi, anatupwa inje.” Kwa upande mwengine, Yesu anasema hivi: “Kama munakaa katika umoja na mimi, na maneno yangu yanakaa ndani yenu, muombe kila kitu chenye munataka na kitatendeka kwenu.”—Yohana 15:5-7.
Sasa Yesu anarudilia jambo lenye alikuwa amezungumuzia mara mbili, ni kusema, kushika amri zake. (Yohana 14:15, 21) Anaeleza ni katika njia gani ya maana wanafunzi wake wanaweza kuonyesha kuwa wanafanya hivyo, anasema hivi: “Kama munashika amri zangu, mutabakia katika upendo wangu, kama vile mimi nilishika amri za Baba na ninabakia katika upendo wake.” Lakini, zaidi ya kumupenda Mungu na Mwana wake, wanapaswa kufanya mambo mengine. Yesu anasema hivi: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mupendane kama vile niliwapenda ninyi. Hakuna mwenye iko na upendo mukubwa kuliko huu, kwamba mutu atoe uzima wake kwa ajili ya marafiki wake. Ninyi ni marafiki wangu kama munafanya mambo yenye ninawaamuru.”—Yohana 15:10-14.
Katika saa kidogo, Yesu ataonyesha upendo wake kwa kutoa uzima wake kwa wale wote wenye kuonyesha imani katika yeye. Mufano wake unapaswa kuchochea wanafunzi wake wakuwe na upendo kama huo wa kujitoa kwa ajili ya mutu na mwenzake. Upendo huo utawatambulisha kama vile Yesu alikuwa amesema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—kama muko na upendo kati yenu.”—Yohana 13:35.
Kwa kweli, mitume wanasikia namna Yesu anawaita “marafiki.” Anaeleza sababu gani anawaita hivyo, anasema hivi: “Lakini nimewaita ninyi marafiki, kwa sababu nimewajulisha mambo yote yenye nilisikia kutoka kwa Baba yangu.” Ni pendeleo kubwa sana kuwa marafiki wa sana wa Yesu na kujua mambo yenye Baba alimuambia! Lakini ili kufurahia urafiki huo, wanapaswa ‘kuendelea kuzaa matunda.’ Ikiwa wanafanya hivyo, Yesu anasema hivi: ‘Jambo lolote lenye munaomba Baba katika jina langu, atawapatia ninyi jambo hilo.’—Yohana 15:15, 16.
Upendo kati ya “matawi” hayo, ni kusema, wanafunzi wake, utawasaidia kuvumilia mambo yenye kuwa mbele. Aliwaonya kuwa ulimwengu utawachukia, lakini aliwatia moyo hivi: “Kama ulimwengu unawachukia ninyi, munajua kwamba umenichukia mimi mbele ya kuwachukia ninyi. Kama mungekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kitu chake. Sasa kwa sababu ninyi hamuko sehemu ya ulimwengu, . . . kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.”—Yohana 15:18, 19.
Yesu anaendelea kueleza sababu gani ulimwengu utawachukia, anasema hivi: “Watawatendea ninyi mambo yote haya kwa sababu ya jina langu, kwa kuwa hawajue Ule mwenye alinituma.” Yesu anasema kuwa kazi zake za miujiza zinahukumu wale wenye kumuchukia. Anasema hivi: “Kama singefanya kati yao kazi zenye hakuna mutu mwingine mwenye alizifanya, hawangekuwa na zambi; lakini sasa wameniona mimi na wamenichukia na wamemutendea Baba yangu vilevile.” Kwa kweli, chuki yao inatimiza unabii.—Yohana 15:21, 24, 25; Zaburi 35:19; 69:4.
Yesu anatoa tena ahadi ya kutuma musaidizi, roho takatifu. Wanafunzi wake wote watapokea roho hiyo yenye kuwa na nguvu na itawasaidia kuzaa matunda, ni kusema, ‘kutoa ushahidi.’—Yohana 15:27.
-
-
“Musiogope! Mimi Nimepata Ushindi juu ya Ulimwengu”Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 121
“Musiogope! Mimi Nimepata Ushindi Juu Ya Ulimwengu”
KARIBUNI MITUME HAWATAMUONA TENA YESU
HUZUNI YA MITUME ITAGEUKA KUWA FURAHA
Yesu na mitume wake wanajitayarisha kuondoka katika chumba cha juu kwenye walikulia chakula cha Pasaka. Kisha kuwaonya sana, Yesu anaongeza hivi: “Nimewaambia ninyi mambo haya ili musikwazike.” Sababu gani maonyo hayo yalikuwa yenye kufaa? Anawaambia hivi: “Watu watawafukuza ninyi katika sinagogi. Kwa kweli, saa inakuja wakati kila mutu mwenye atawaua ninyi atawaza amemutolea Mungu utumishi mutakatifu.”—Yohana 16:1, 2.
Pengine habari hiyo inaogopesha mitume. Hata kama Yesu alikuwa amesema kuwa ulimwengu ungewachukia, hakuwaambia moja kwa moja kuwa wangeuawa. Sababu gani? Anasema hivi: “Sikuwaambia mambo haya mwanzoni, kwa sababu nilikuwa pamoja na ninyi.” (Yohana 16:4) Sasa anawaonya mbele ya kuondoka. Hilo lingeweza kuwasaidia wasikwazike kisha hapo.
Yesu anaendelea kusema hivi: “Ninaenda kwa Ule mwenye alinituma; na bado hakuna hata mumoja wenu mwenye ananiuliza, ‘Unaenda wapi?’” Mangaribi hiyo walikuwa wamemuuliza juu ya mahali kwenye alikuwa anaenda. (Yohana 13:36; 14:5; 16:5) Lakini sasa wanaogopa kwa sababu ya mambo yenye alisema juu ya mateso, na hilo linawaletea huzuni sana. Kwa hiyo, wanashindwa kuuliza maulizo mengine juu ya utukufu wenye atapata ao kumuuliza ikiwa hilo litakuwa na matokeo gani juu ya waabudu wa kweli. Yesu anasema hivi: “Kwa sababu nimewaambia mambo haya, huzuni imejaa katika mioyo yenu.”—Yohana 16:6.
Kisha, Yesu anaeleza hivi: “Ninaenda kwa faida yenu. Kwa maana kama siende, musaidizi hatakuja kwenu; lakini kama ninaenda, nitamutuma kwenu.” (Yohana 16:7) Wanafunzi wanaweza kupata roho takatifu ikiwa tu Yesu anakufa na kuenda mbinguni; anaweza kutuma roho hiyo kama musaidizi kwa watu wake nafasi yoyote katika dunia.
Roho takatifu ‘itatolea ulimwengu uhakikisho wenye kusadikisha juu ya zambi na juu ya mambo yenye kuwa sawa na juu ya hukumu.’ (Yohana 16:8) Ndiyo, kosa la ulimwengu la kushindwa kuonyesha imani katika Mwana wa Mungu litaonyeshwa waziwazi. Wakati Yesu atapanda mbinguni jambo hilo litatoa ushuhuda wa uadilifu wake na kuonyesha kuwa Shetani, “mutawala wa ulimwengu huu,” anastahili kupewa hukumu kali.—Yohana 16:11.
Yesu anaendelea kusema hivi: “Ningali na mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamutaweza kuyabeba sasa.” Wakati atawamwangia roho takatifu, itawasaidia kuelewa “kweli yote,” na wataweza kuishi kulingana na kweli hiyo.—Yohana 16:12, 13.
Mitume wanavurugika kwa sababu ya maneno yenye Yesu anasema kisha hapo, anasema hivi: “Kisha wakati kidogo hamutaniona tena, na tena, kisha wakati kidogo mutaniona.” Wanaulizana ikiwa Yesu anapenda kusema nini. Yesu anatambua kuwa wanapenda kumuuliza juu ya jambo hilo, kwa hiyo anawaambia hivi: “Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, mutalia na kuomboleza, lakini ulimwengu utafurahi; mutahuzunika, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha.” (Yohana 16:16, 20) Wakati Yesu anauawa kisha muchana yenye kufuata, viongozi wa dini wanafurahi sana, lakini wanafunzi wake wanakuwa na huzuni. Kisha huzuni yao inabadilika na kuwa furaha wakati Yesu anafufuliwa! Na furaha yao inaendelea wakati anawamwangia roho takatifu ya Mungu.
Wakati analinganisha hali ya mitume wake na ya mwanamuke mwenye kuwa na maumivu ya kuzaa, Yesu anasema hivi: “Wakati mwanamuke iko anazaa, anakuwa na huzuni kwa sababu saa yake imekuja, lakini kisha kuzaa mutoto, hakumbuke tena taabu kwa sababu anafurahi kwamba mutu amezaliwa katika ulimwengu.” Yesu anatia moyo mitume wake kwa kusema hivi: “Ninyi pia, munahuzunika sasa; lakini nitawaona tena, na mioyo yenu itafurahi, na hakuna mutu mwenye atawanyanganya furaha yenu.”—Yohana 16:21, 22.
Mupaka wakati huu, mitume hawajafanya ombi lolote katika jina la Yesu. Sasa anasema hivi: “Siku hiyo mutamuomba Baba katika jina langu.” Sababu gani watafanya hivyo? Haiko kwa sababu baba hapendi kuwajibia. Kwa kweli, Yesu anasema hivi: “Kwa maana Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mumenipenda . . . nikiwa mwakilishi wa Mungu.”—Yohana 16:26, 27.
Pengine maneno hayo yenye kutia moyo ya Yesu ndiyo yalichochea mitume kusema hivi kwa uhakika: “Kwa jambo hili tunaamini kwamba ulitoka kwa Mungu.” Uhakika huo utajaribiwa hivi karibuni. Kwa kweli, Yesu anaeleza mambo yenye yatatokea. Anasema hivi: “Muangalie! Saa inakuja, kwa kweli, imekuja, wakati kila mumoja wenu atatawanyika na kuenda kwenye nyumba yake mwenyewe na mutaniacha peke yangu.” Lakini anawahakikishia hivi: “Nimewaambia ninyi mambo haya ili kupitia mimi mukuwe na amani. Katika ulimwengu mutapata taabu, lakini musiogope! Mimi nimepata ushindi juu ya ulimwengu.” (Yohana 16:30-33) Yesu hatawaacha peke yao. Iko hakika kuwa wao pia wanaweza kupata ushindi juu ya ulimwengu, kama vile yeye amepata ushindi, kwa kufanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu hata kama Shetani na ulimwengu wake watajaribu kuvunja ushikamanifu wao.
-
-
Sala ya Mwisho ya Yesu Katika Chumba cha JuuYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 122
Sala Ya Mwisho Ya Yesu Katika Chumba Cha Juu
MATOKEO YA KUJUA MUNGU NA MWANA WAKE
UMOJA KATI YA YEHOVA, YESU, NA WANAFUNZI
Kwa sababu anasukumwa na upendo mwingi juu ya mitume wake, Yesu amewatayarisha juu ya kuondoka kwake kwenye kunakaribia sana. Sasa anainua macho yake kuelekea mbinguni na anasali kwa Baba yake hivi: “Tukuza mwana wako ili mwana wako akutukuze, kwa kuwa ulimupatia mamlaka juu ya kila mwili, ili apatie uzima wa milele wale wote wenye umemupatia.”—Yohana 17:1, 2.
Ni wazi kwamba Yesu anaelewa kuwa kumupatia Baba yake utukufu ndilo jambo la maana zaidi. Lakini tumaini lenye Yesu anazungumuzia ni lenye kutia moyo sana, ni kusema, uzima wa milele! Kwa sababu amepewa “mamlaka juu ya kila mwili,” Yesu anaweza kutoa faida ya zabihu yake ya ukombozi kwa wanadamu wote. Lakini, ni hesabu fulani tu ndio watabarikiwa. Sababu gani ni watu fulani tu? Kwa sababu Yesu atatolea faida za zabihu yake ya ukombozi wale tu wenye kutenda kulingana na jambo lenye anazungumuzia sasa. Anasema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, wajifunze ili wafikie kukujua wewe Mungu wa pekee wa kweli, na ule mwenye ulituma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.
Mutu anapaswa kujua muzuri kabisa Baba na Mwana, ni kusema, kuwa na urafiki wa sana pamoja nao. Anapaswa kuona mambo namna wanayaona. Zaidi ya hilo, anapaswa kujikaza kuiga sifa zao za muzuri katika namna yake ya kuwatendea wengine. Na anapaswa kuelewa kuwa, kati ya kumutukuza Mungu na wanadamu kupata uzima wa milele, kumutukuza Mungu ndilo jambo la maana zaidi. Sasa Yesu anarudilia habari hii kubwa:
“Nimekutukuza katika dunia, kwa kuwa nimemaliza kazi yenye ulinipatia nifanye. Basi sasa, Baba, unitukuze pembeni yako kwa utukufu wenye nilikuwa nao pembeni yako mbele ya ulimwengu kuwa.” (Yohana 17:4, 5) Ndiyo, Yesu anaomba arudishwe katika utukufu wa mbinguni kupitia ufufuo.
Hata hivyo, Yesu hasahau mambo yenye ametimiza katika kazi yake ya kuhubiri. Anasali hivi: “Nimejulisha jina lako kwa watu wenye ulinipatia kutoka katika ulimwengu. Walikuwa wako, na ukanipatia, na wameshika neno lako.” (Yohana 17:6) Katika kazi yake ya kuhubiri, Yesu hakutaja tu jina la Mungu, Yehova. Alisaidia mitume wake wajue jina hilo linawakilisha nini, ni kusema, sifa za Mungu na namna yake ya kutendea wanadamu.
Mitume wamefikia kumujua Yehova, daraka la Mwana wake, na mambo yenye Yesu amefundisha. Kwa unyenyekevu, Yesu anasema hivi: “Nimewapatia maneno yenye ulinipatia, na wameyakubali na wamejua kabisa kwamba nilikuja nikiwa mwakilishi wako, na wameamini kwamba ulinituma.”—Yohana 17:8.
Kisha Yesu anazungumuzia waziwazi tofauti kati ya wanafunzi wake na ulimwengu wa wanadamu wote kwa ujumla. Anasema hivi: “Ninaomba kwa ajili yao; siombe kwa ajili ya ulimwengu, lakini ninaomba kwa ajili ya wale wenye wewe ulinipatia, kwa sababu ni wako. . . . Baba Mutakatifu, uwalinde kwa sababu ya jina lako lenye umenipatia, ili wakuwe kitu kimoja kama vile sisi tuko kitu kimoja. . . . Nimewalinda, na hakuna hata mumoja wao mwenye aliharibiwa isipokuwa ule mwana wa uharibifu,” ni kusema, Yuda Iskariote, mwenye alikuwa anatafuta namna ya kumusaliti Yesu.—Yohana 17:9-12.
Yesu anaendelea kusali hivi: “Ulimwengu umewachukia. . . . Siombe kwamba uwatoshe katika ulimwengu, lakini ninaomba kwamba uwalinde kwa sababu ya ule muovu. Wao hawako sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi siko sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14-16) Mitume na wanafunzi wengine wako katika ulimwengu, ni kusema, ulimwengu wa wanadamu wenye kuongozwa na Shetani, lakini wanapaswa kuendelea kujitenga na ulimwengu huo na ubaya wake. Namna gani?
Wanapaswa kuendelea kuwa watakatifu, ni kusema, wenye kuwekwa pembeni ili wamutumikie Mungu, kwa kutumikisha katika maisha yao kweli yenye kupatikana katika Maandiko ya Kiebrania na kweli zenye Yesu alikuwa amefundisha. Yesu anasali hivi: “Uwatakase kwa njia ya ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Kisha wakati fulani, mitume fulani wataandika vitabu vyenye kuongozwa na roho ya Mungu vyenye vitakuwa sehemu ya “ile kweli” yenye inaweza kumutakasa mutu.
Lakini kisha wakati fulani, kutakuwa wengine pia wenye watakubali “ile kweli.” Kwa hiyo, Yesu anasali haiko ‘kwa ajili ya hawa tu [wale wenye kuwa hapo], lakini anaomba pia kwa ajili ya wale wenye wanamuamini kupitia neno lao.’ Yesu anaomba nini kwa ajili yao wote? Anasema hivi: “Ili wote wakuwe kitu kimoja, kama vile wewe, Baba, uko katika umoja na mimi na mimi niko katika umoja na wewe, wao pia wakuwe katika umoja na sisi.” (Yohana 17:20, 21) Hilo halimaanishe kuwa Yesu na Baba yake wako mutu mumoja kwa njia ya moja kwa moja. Wako mumoja katika maana ya kwamba wanapatana katika mambo yote. Yesu anasali kuwa wanafunzi wake pia wakuwe na umoja kama huo.
Muda mufupi mbele ya hapo, Yesu alikuwa amemuambia Petro na wengine kuwa alikuwa anaenda kuwatayarishia nafasi, ni kusema, nafasi huko mbinguni. (Yohana 14:2, 3) Yesu anarudilia wazo hilo katika sala. Anasema hivi: “Baba, ninataka wale wenye umenipatia wakuwe pamoja na mimi kwenye niko, ili waone utukufu wangu wenye umenipatia, kwa sababu ulinipenda mbele ya kuwekwa kwa musingi wa ulimwengu.” (Yohana 17:24) Anahakikisha kuwa zamani sana, mbele Adamu na Eva wazae watoto, Mungu alimupenda Mwana wake muzaliwa wa kwanza, mwenye alifikia kuwa Yesu Kristo.
Ili kumalizia sala yake, Yesu anakazia jina la Mungu na upendo wake kwa mitume na wengine wenye watakubali “ile kweli.” Anasema hivi: “Nimewajulisha jina lako na nitalijulisha, ili upendo wenye ulinipenda ukuwe ndani yao na mimi nikuwe katika umoja nao.”—Yohana 17:26.
-
-
Anasali Wakati Iko na Huzuni NyingiYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 123
Anasali Wakati Iko Na Huzuni Nyingi
MATAYO 26:30, 36-46 MARKO 14:26, 32-42 LUKA 22:39-46 YOHANA 18:1
YESU IKO KATIKA BUSTANI YA GETSEMANE
JASHO LAKE LIKO KAMA MATONE YA DAMU
Yesu anamaliza kusali pamoja na mitume wake waaminifu. ‘Kisha kuimba sifa, wanatoka na kuenda kwenye Mulima wa Mizeituni.’ (Marko 14:26) Wanaenda ngambo ya mashariki katika bustani yenye kuitwa Getsemane, kwenye Yesu alikuwa anazoea kuenda.
Wakati wanafika mahali hapo penye kupendeza, katikati ya miti ya mizeituni, Yesu anaacha nyuma mitume wake munane. Pengine wanabakia kwenye muingilio wa bustani, kwa sababu anawaambia hivi: “Mukae hapa, wakati mimi ninaenda pale kusali.” Yesu anakamata mitume tatu, ni kusema, Petro, Yakobo, na Yohana, na anaenda pamoja nao mbali katika bustani. Anakuwa na huzuni nyingi na anawaambia hivi mitume wake tatu: “Nimehuzunika sana, kiasi cha kufa. Mukae hapa na muendelee kukesha pamoja na mimi.”—Matayo 26:36-38.
Kisha, Yesu anaenda mbali kidogo na nafasi kwenye anawaacha, ‘anaanguka chini na kuanza kusali.’ Anaomba nini kwa Mungu katika wakati huu wa maana sana? Anasali hivi: “Baba, mambo yote yanawezekana kwako; uniondolee kikombe hiki. Hapana vile ninapenda, lakini, vile wewe unapenda.” (Marko 14:35, 36) Anapenda kusema nini? Anajaribu kuepuka daraka lake la kutoa zabihu ya ukombozi? Hapana!
Wakati alikuwa mbinguni alikuwa anaona namna Waroma walikuwa wanatesa sana watu wenye walikuwa wanaua. Kwa sababu sasa yeye ni mwanadamu mwenye anaweza kusikia mambo kama vile maumivu na woga, hangojee kwa hamu mambo yenye yanakaribia kumupata. Hata hivyo, jambo lenye kumuhangaisha zaidi ni kwamba, kufa kama vile mutu mwenye alifanya makosa makubwa kunaweza kuchafua jina la Baba yake. Katika saa kidogo, atatundikwa kwenye muti kama vile mutu mwenye amekufuru.
Kisha kusali kwa muda murefu, Yesu anarudia na kukutana mitume wake wanalala usingizi. Anaambia Petro hivi: “Je, hamungeweza kukesha pamoja na mimi hata kwa saa moja? Muendelee kukesha na kusali bila kuacha, ili musiingie katika jaribu.” Yesu anaelewa kuwa mitume wake pia wamekuwa na mahangaiko na ni usiku sana. Anaongeza hivi: “Kwa kweli, roho inataka lakini mwili ni zaifu.”—Matayo 26:40, 41.
Kisha Yesu anaenda kwa mara ya pili na kumuomba Mungu amuondolee “kikombe hiki.” Wakati anarudia, tena anakutana mitume wake tatu wanalala usingizi, walipaswa kusali wakati huo ili wasiingie katika majaribu. Wakati Yesu anazungumuza nao, “hawakujua wamujibu nini.” (Marko 14:40) Yesu anaenda mara ya tatu, na kupiga magoti ili kusali.
Yesu anahangaika sana kwa sababu kufa kama vile mutu mwenye alifanya makosa makubwa kutachafua jina la Baba yake. Hata hivyo, Yehova anasikiliza sala ya Mwana wake, na wakati fulani anatuma malaika ili kumutia nguvu. Lakini, Yesu haache kumulilia Baba yake katika sala, anaendelea “kusali kwa bidii zaidi.” Anahangaika sana katika moyo wake. Yesu iko na daraka kubwa sana la kutimiza! Uzima wake wa milele na wa wanadamu wenye kumuamini unahusika. Kwa kweli, ‘jasho lake linakuwa kama matone ya damu yenye kuanguka chini.’—Luka 22:44.
Wakati Yesu anarudia mara ya tatu kuona mitume wake, tena anawakuta wanalala usingizi. Anawaambia hivi: “Wakati kama huu, munalala usingizi na kupumuzika! Muangalie! Saa imekaribia ya Mwana wa binadamu kusalitiwa katika mikono ya watenda-zambi. Musimame tuende. Muangalie! Musaliti wangu amekaribia.”—Matayo 26:45, 46.
-
-
Kristo Anasalitiwa na KufungwaYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 124
Kristo Anasalitiwa Na Kufungwa
MATAYO 26:47-56 MARKO 14:43-52 LUKA 22:47-53 YOHANA 18:2-12
YUDA ANAMUSALITI YESU KATIKA BUSTANI
PETRO ANAKATA SIKIO LA MWANAUME FULANI
YESU ANAKAMATWA
Katikati ya usiku imepita kabisa. Makuhani wamekubali kumupatia Yuda vipande 30 vya feza ili amusaliti Yesu. Kwa hiyo, Yuda anaongoza kikundi kikubwa cha makuhani wakubwa na Wafarisayo ili kuenda kumutafuta Yesu. Wanasindikizwa na kikundi fulani cha maaskari Waroma chenye kuwa na silaha na chenye kuongozwa na kamanda.
Inaonekana kuwa wakati Yesu aliambia Yuda aondoke kwenye chakula cha Pasaka, Yuda alienda mara moja kwa wakubwa wa makuhani. (Yohana 13:27) Walikusanya walinzi wao na kikundi cha maaskari. Pengine Yuda aliwapeleka kwanza kwenye chumba ambamo Yesu na mitume wake walifanyia sikukuu ya Pasaka. Lakini sasa kikundi hicho kikubwa kimevuka Bonde la Kidroni na kinaenda kwenye bustani. Zaidi ya silaha, wako pia na mienge na taa, wanapenda kabisa kumupata Yesu.
Wakati Yuda anaongoza kikundi hicho cha watu kwenye Mulima wa Mizeituni, iko hakika kuwa atamupata Yesu huko. Juma lenye lilipita wakati Yesu na mitume wake walikuwa wanafanya safari kati ya Betania na Yerusalemu, mara kwa mara walisimama katika bustani ya Getsemane. Lakini sasa ni usiku, na Yesu anaweza kuwa katika vivuli vya miti ya mizeituni katika bustani. Kwa hiyo, namna gani maaskari wenye pengine walikuwa hawajamuona Yesu hata siku moja wangeweza kumujua? Ili kuwasadia, Yuda atawatolea alama fulani. Anasema hivi: “Kila mutu mwenye nitabusu, ni yeye; mumukamate na kumufunga.”—Marko 14:44.
Wakati Yuda anaongoza kikundi hicho katika bustani, anamuona Yesu na mitume wake na anaenda mara moja nafasi kwenye iko. Yuda anasema hivi: “Jambo Rabi!” na anamubusu Yesu kwa wororo. Yesu anamuambia hivi: “Mwenzangu, umekuja kufanya nini?” (Matayo 26:49, 50) Yesu anajibu ulizo lake mwenyewe, anasema hivi: “Yuda, unamusaliti Mwana wa binadamu kwa busu?” (Luka 22:48) Yesu anaachia pale, hahangaike tena juu ya musaliti wake!
Sasa Yesu anaingia katika mwangaza wa mienge na taa na kuuliza hivi: “Munatafuta nani?” Kikundi hicho kinajibu hivi: “Yesu Munazareti.” Bila kuogopa, Yesu anasema hivi: “Ni mimi.” (Yohana 18:4, 5) Kwa sababu hawakujua mambo yatakuwa namna gani, wanaume hao wanaanguka chini.
Kuliko kuchukua nafasi hiyo ili kukimbilia katika giza, Yesu anauliza tena wanatafuta nani. Wakati wanasema tena, “Yesu Munazareti,” kwa utulivu, anasema hivi: “Niliwaambia ni mimi. Basi, kama munanitafuta, muache hawa waende.” Hata katika wakati huu mugumu sana, Yesu anakumbuka mambo yenye alikuwa amesema, kuwa hatapoteza hata mumoja wao. (Yohana 6:39; 17:12) Yesu amelinda mitume wake waaminifu na hakuna mwenye amepotea, “isipokuwa ule mwana wa uharibifu,” ni kusema, Yuda. (Yohana 18:7-9) Kwa hiyo, anaomba sasa waache mitume wake waaminifu waende.
Wakati maaskari wanasimama na kuanza kumukaribia Yesu, mitume wanaelewa mambo yenye yanafanyika. Wanauliza hivi: “Bwana, tuwapige kwa upanga?” (Luka 22:49) Hata mbele Yesu ajibie, Petro anachukua upanga moja kati ya panga mbili zenye mitume wako nazo. Anamushambulia Malko, mutumishi wa kuhani mukubwa, na kumukata sikio la upande wa kuume.
Yesu anagusa sikio la Malko na kuponyesha kidonda. Kisha anafundisha somo la maana kwa kumuamuru Petro hivi: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wote wenye wanatumikisha upanga watakufa kwa upanga.” Yesu iko tayari kufungwa, kwa sababu anasema hivi: “Maandiko yenye kusema kuwa mambo haya yanapaswa kutendeka, yatatimizwa namna gani?” (Matayo 26:52, 54) Anaongeza hivi: “Je, sipaswe kunywa kikombe chenye Baba amenipatia?” (Yohana 18:11) Yesu alikubali mapenzi ya Mungu yatendeke juu yake, hata kufikia hatua ya kufa.
Yesu anauliza hivi kikundi hicho cha watu: “Je, mumekuja kunikamata mukiwa na mapanga na marungu kama vile munakuja kumukamata munyanganyi? Kila siku nilikuwa ninakaa katika hekalu nikifundisha, lakini hamukunikamata na kunifunga. Lakini yote haya yametokea ili kutimiza mambo yenye manabii waliandika.”—Matayo 26:55, 56.
Kikundi cha maaskari, kamanda wa jeshi, na walinzi wa Wayahudi wanamukamata Yesu na kumufunga. Wakati mitume wanaona jambo hilo, wanakimbia. Hata hivyo, “kijana mumoja,” pengine mwanafunzi Marko anabakia pamoja na kikundi hicho ili kumufuata Yesu. (Marko 14:51) Kijana huyo anatambuliwa, na kikundi hicho cha watu kinajaribu kumukamata, kwa hiyo, anaacha nguo yake ya kitani na kukimbia.
-
-
Yesu Anapelekwa kwa Anasi, Kisha Kwa KayafaYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 125
Yesu Anapelekwa Kwa Anasi, Kisha Kwa Kayafa
MATAYO 26:57-68 MARKO 14:53-65 LUKA 22:54, 63-65 YOHANA 18:13, 14, 19-24
YESU ANAPELEKWA KWA ANASI MWENYE ZAMANI ALIKUWA KUHANI MUKUBWA
SANHEDRINI INAFANYA HUKUMU YENYE HAIPATANE NA SHERIA
Kisha Yesu kufungwa kama mutu mwenye alifanya makosa makubwa, anapelekwa kwa Anasi, mwenye alikuwa kuhani mukubwa wakati kijana Yesu alishangaza walimu kwenye hekalu. (Luka 2:42, 47) Kisha, watoto fulani wa Anasi walitumikia cheo cha kuhani mukubwa, na sasa ni Kayafa, mukwe wake, ndiye kuhani mukubwa.
Wakati Anasi iko anamusambisha Yesu, Kayafa anakusanya watu wote wenye kufanyiza Sanhedrini. Sanhedrini hiyo inafanyizwa na watu 71 kutia ndani kuhani mukubwa na wengine wenye walikuwa wametumikia cheo hicho zamani.
Anasi anauliza Yesu “juu ya wanafunzi wake na juu ya mafundisho yake.” Yesu anajibu kwa kifupi hivi: “Nimesema na ulimwengu waziwazi. Sikuzote nilifundisha katika sinagogi na katika hekalu, mahali penye Wayahudi wote wanakusanyika, na sikusema jambo lolote kwa siri. Sababu gani unaniuliza? Uliza wale wenye walisikia kile niliwaambia.”—Yohana 18:19-21.
Mumoja wa walinzi mwenye alikuwa anasimama pale anamupiga Yesu kofi kwenye uso na kusema hivi kwa ukali: “Je, ni vile unajibu mukubwa wa makuhani?” Lakini kwa sababu Yesu alijua kuwa hakufanya jambo fulani la mubaya, anajibu hivi: “Kama nimesema mubaya, shuhudia ubaya huo; lakini kama yale nilisema yako sawa, sababu gani unanipiga?” (Yohana 18:22, 23) Kisha Anasi anaomba Yesu apelekwe kwa Kayafa, mukwe wake.
Sasa wale wote wenye kufanyiza Sanhedrini, ni kusema, kuhani mukubwa wa sasa, wazee wa watu, na waandishi, wamekusanyika. Wanakusanyika kwenye nyumba ya Kayafa. Sheria inakataza kusambisha mutu katika usiku wa Pasaka, lakini hilo haliwazuie kuendelea na kusudi lao la mubaya.
Kwa kweli, Kikundi hicho hakitende kwa haki hata kidogo. Kisha Yesu kumufufua Lazaro, Sanhedrini iliamua kuwa Yesu anapaswa kufa. (Yohana 11:47-53) Na siku fulani zenye zilikuwa zimepita viongozi wa dini walipanga njama ya kumukamata Yesu na kumuua. (Matayo 26:3, 4) Kwa kweli, hata mbele ya kusambishwa, tayari Yesu amekwisha kuhukumiwa kifo!
Zaidi ya kufanya mukutano wenye haukubaliwe na sheria, wakubwa wa makuhani na wengine wenye kufanyiza Sanhedrini wanajaribu kutafuta mashahidi wa uwongo ili wapate mambo ya kumushitaki Yesu. Wanapata mashahidi wengi, lakini ushuhuda wao ni wenye kupingana. Mwishowe, mashahidi wawili wanakuja na kusema hivi: “Tulimusikia akisema, ‘Nitabomoa hekalu hili lenye lilifanywa kwa mikono, na kwa siku tatu (3) nitajenga lingine lenye halikufanywa kwa mikono.’” (Marko 14:58) Hata hivyo, wanaume hao hawakubaliane kabisa-kabisa.
Kayafa anauliza Yesu: “Haujibu hata neno moja? Watu hawa wanashuhudia nini juu yako?” (Marko 14:60) Yesu anabakia kimya juu ya mashitaka hayo ya uongo yenye kusemwa na mashahidi wenye ushuhuda wao haupatane. Kwa hiyo, Kayafa, Kuhani Mukubwa, anatumikisha ufundi mwingine.
Kayafa anajua kuwa Wayahudi wanachukia mutu yeyote mwenye kujiita kuwa Mwana wa Mungu. Mbele ya hapo, wakati Yesu alimuita Mungu Baba yake, Wayahudi walipenda kumuua kwa sababu walisema “anajifanya kuwa sawa na Mungu.” (Yohana 5:17, 18; 10:31-39) Kwa sababu anajua jambo hilo, Kayafa anamuuliza Yesu kwa ujanja hivi: “Ninakuapisha mbele ya Mungu mwenye kuishi utuambie kama wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu!” (Matayo 26:63) Kwa kweli, Yesu amesema waziwazi kuwa yeye ni Mwana wa Mungu. (Yohana 3:18; 5:25; 11:4) Ikiwa hafanye hivyo sasa, hilo linaweza kuonyesha kuwa anakataa kuwa yeye ni Mwana wa Mungu na kuwa yeye ni Kristo. Yesu anasema hivi: “Mimi ndiye; na mutaona Mwana wa binadamu akiwa amekaa kwenye mukono wa kuume wa nguvu na akikuja pamoja na mawingu ya mbinguni.”—Marko 14:62.
Wakati Kayafa anasikia jambo hilo, anapasua nguo zake na kusema hivi: “Amemutukana Mungu! Je, tuko na lazima ya mashahidi wengine? Muone! Sasa mumesikia matukano juu ya Mungu. Munafikiri nini?” Watu wa Sanhedrini wanafanya hukumu yenye kukosa haki, wanasema hivi: “Anastahili kufa.”—Matayo 26:65, 66.
Kisha wanaanza kumuchekelea Yesu na kumupiga ngumi. Wengine wanamupiga makofi kwenye sura na kumutemea mate. Kisha kufunika sura yake yote na kumupiga makofi, wanamuchekelea kwa kusema hivi: “Toa unabii! Ni nani alikupiga?” (Luka 22:64) Ni hivyo Mwana wa Mungu anatendewa mubaya wakati hasambishwe kulingana na sheria!
-
-
Petro Anamukana Yesu Kwenye Nyumba ya KayafaYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 126
Petro Anamukana Yesu Kwenye Nyumba Ya Kayafa
MATAYO 26:69-75 MARKO 14:66-72 LUKA 22:54-62 YOHANA 18:15-18, 25-27
PETRO ANAMUKANA YESU
Kisha Yesu kukamatwa katika bustani ya Getsemane, mitume wanamuacha, wanakimbia kwa sababu wanaogopa. Hata hivyo, wawili kati yao wanaacha kukimbia. Ni Petro “na vilevile mwanafunzi mwingine,” pengine mutume Yohana. (Yohana 18:15; 19:35; 21:24) Pengine wanamukaribia Yesu wakati anapelekwa kwa Anasi. Wakati Anasi anamutuma Yesu kwa Kuhani Mukubwa Kayafa, Petro na Yohana wanamufuata kwa mbali. Inawezekana kuwa wanaogopea maisha yao wenyewe na wanahangaika kwa sababu ya mambo yenye yatamupata Bwana wao.
Yohana anajulikana kwa kuhani mukubwa na kwa hiyo, anaruhusiwa kuingia katika uwanja wa nyumba ya Kayafa. Petro anabakia inje mupaka wakati Yohana anarudia na kuzungumuza na mutumishi mwanamuke mwenye kuchunga mulango. Kisha Petro anaruhusiwa kuingia
Ni usiku wenye baridi, kwa hiyo, watu wenye kuwa katika uwanja wanawasha moto wa makaa. Petro anakaa pamoja nao ili kuota moto wakati iko anangojea “ili aone mambo yatakuwa namna gani” wakati Yesu iko anasambishwa. (Matayo 26:58) Sasa, kupitia mwangaza wa moto, mwanamuke mwenye alikuwa anachunga mulango mwenye aliingiza Petro anamuangalia muzuri. Anamuuliza hivi: “Wewe pia ni mumoja wa wanafunzi wa mutu huyu, haiko vile?” (Yohana 18:17) Na wengine pia wanamutambua Petro na kusema kuwa alikuwa pamoja na Yesu.—Matayo 26:69, 71-73; Marko 14:70.
Petro anaogopa sana kwa sababu ya jambo hilo. Hapendi watu wamutambue, anajaribu hata kuondoka na kuenda kwenye mulango. Kwa hiyo, Petro anakataa kuwa hakukuwa pamoja na Yesu, kwa kusema hivi: “Simujue na sielewe unataka kusema nini.” (Marko 14:67, 68) Pia anaanza “kulaani na kuapa,” maana yake, iko tayari kufanya kiapo ili kuonyesha kuwa maneno yake ni kweli na kuwa anakubali kupatwa na matokeo ya mubaya ikiwa anasema uongo.—Matayo 26:74.
Wakati huohuo, Yesu anaendelea kusamba, pengine katika sehemu fulani ya nyumba ya Kayafa yenye kuwa juu ya uwanja. Petro na wengine wenye wanangojea chini, pengine wanaona namna mashahidi mbalimbali wako wanaingia ndani na kutoka ili kutoa ushuhuda.
Kwa sababu namna ya kusema ya Petro ni ya Wagalilaya, hilo linaonyesha kuwa anasema uongo kwa kusema kama hamujue Yesu. Zaidi ya hilo, mutu mumoja katika kikundi hicho ni mutu wa familia ya Malko, mwenye Petro alikata sikio. Kwa hiyo, anamuambia Petro hivi: “Mimi nilikuona katika bustani pamoja naye, haiko vile?” Wakati Petro anamukana Yesu kwa mara ya tatu, jogoo anawika kama vile Yesu alikuwa ametabiri.—Yohana 13:38; 18:26, 27.
Wakati huo, inawezekana kuwa Yesu iko kwenye baraza na iko anaangalia kwenye uwanja. Bwana anageuka na kumuangalia Petro mara moja, hilo lilipaswa kumuumiza sana Petro. Anakumbuka mambo yenye Yesu alikuwa amesema saa fulani mbele ya hapo katika chumba cha juu. Wazia namna Petro anajisikia wakati anatambua jambo lenye amefanya! Petro anaenda inje na analia kwa uchungu.—Luka 22:61, 62.
Jambo hilo liliwezekana namna gani? Namna gani Petro mwenye alikuwa hakika kuwa iko nguvu kiroho na mushikamanifu, anakana Bwana wake? Watu hawaseme kweli juu ya Yesu, na wanamushitaki kuwa mutu mwenye alifanya makosa makubwa. Petro alipaswa kumutetea mutu huyo mwenye hana kosa, lakini alimukana mutu huyo mwenye kuwa “na maneno ya uzima wa milele.”—Yohana 6:68.
Mambo ya mubaya yenye yalimupata Petro yanaonyesha kuwa hata mutu mwenye kuwa na imani yenye nguvu na mushikamanifu anaweza kuanguka ikiwa hajitayarishe muzuri juu ya majaribu yenye yanaweza kutokea. Watumishi wote wa Mungu wanapaswa kujifunza somo fulani juu ya mambo yenye yalimupata Petro!
-