-
Sanhedrini Inamusambisha, Kisha Anapelekwa kwa PilatoYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 127
Sanhedrini Inamusambisha, Kisha Anapelekwa Kwa Pilato
MATAYO 27:1-11 MARKO 15:1 LUKA 22:66–23:3 YOHANA 18:28-35
ANASAMBISHWA ASUBUI MBELE YA SANHEDRINI
YUDA ANAJARIBU KUJITUNDIKA
YESU ANATUMWA KWA PILATO ILI AHUKUMIWE
Asubui inakaribia wakati Petro anamukana Yesu mara tatu. Watu wenye kufanyiza Sanhedrini wamemaliza hukumu yao yenye haipatane na sheria na wameondoka. Sasa ni asubui ya Siku ya Tano, wanakusanyika tena pengine ili kufanya ionekane kuwa hukumu yenye walifanya usiku inapatana na sheria. Yesu analetwa mbele yao.
Tena tribinali hiyo inamuuliza hivi: “Kama wewe ndiye Kristo utuambie.” Yesu anawajibu hivi: “Hata kama ningewaambia, hamungeamini hata kidogo. Zaidi ya hayo, kama ningewauliza, hamungenijibu.” Hata hivyo, bila kuogopa Yesu anajitambulisha kuwa ni yeye ndiye alitabiriwa katika andiko la Danieli 7:13. Anasema hivi: “Kuanzia sasa Mwana wa binadamu atakaa kwenye mukono wa kuume wenye nguvu wa Mungu.”—Luka 22:67-69; Matayo 26:63.
Wanaendelea kumuuliza hivi: “Kwa hiyo, je, wewe ndiye Mwana wa Mungu?” Yesu anajibu hivi: “Ninyi wenyewe munasema kwamba mimi ndiye.” Hilo linaonekana kuwa sababu yenye kufaa ya kumuua Yesu kwa kumushitaki kuwa amekufuru. Wanauliza hivi: “Sababu gani tutafute ushahidi zaidi?” (Luka 22:70, 71; Marko 14:64) Kwa hiyo, wanamufunga Yesu na kumupeleka kwa Gavana Muroma, Pontio Pilato.
Pengine Yuda Iskariote anaona namna Yesu anapelekwa kwa Pilato. Wakati Yuda anatambua kuwa Yesu amehukumiwa, anasikia huzuni sana na anapoteza tumaini. Hata hivyo, kuliko kumukaribia Mungu na kutubu kwa moyo wake wote, anaenda kurudisha vipande 30 vya feza. Yuda anaambia wakubwa wa makuhani hivi: “Nilitenda zambi wakati nilisaliti damu yenye haina kosa.” Lakini wanamujibu hivi kwa ukali: “Je, ile inatuangalia? Ile ni mambo yako!”—Matayo 27:4.
Yuda anatupa vipande hivyo 30 vya feza katika hekalu na kisha anaongeza zambi yake kwa kujaribu kujiua. Wakati Yuda anajaribu kujitundika, inawezekana kuwa tawi kwenye anafungia kamba linakatika. Mwili wake unaangukia kwenye majiwe makubwa yenye yalikuwa chini na unapasuka.—Matendo 1:17, 18.
Ingali asubui sana wakati Yesu anapelekwa kwenye nyumba ya Pontio Pilato. Lakini Wayahudi wenye wanamupeleka huko wanakataa kuingia. Wanafikiri kwamba kuwa karibu na watu wa Mataifa kunaweza kuwachafua. Hilo lingewafanya wakose kula chakula cha tarehe 15 ya mwezi wa Nisani, siku ya kwanza ya Sikukuu ya Mikate Yenye Haina Chachu, yenye ilionwa kuwa sehemu ya kipindi cha Pasaka.
Pilato anatoka inje na kuwauliza hivi: “Munaleta shitaka gani juu ya mutu huyu?” Wanajibu hivi: “Kama mutu huyu hangekuwa mukosaji, hatungemutia katika mikono yako.” Pengine Pilato anajisikia kuwa wanajaribu kumulazimisha, kwa hiyo, anasema hivi: “Mumukamate ninyi wenyewe na mumuhukumu kulingana na sheria yenu.” Wayahudi wanafunua nia yao ya kumuua Yesu kwa kujibu hivi: “Sisi haturuhusiwe kumuua mutu yeyote.”—Yohana 18:29-31.
Kwa kweli, ikiwa wanamuua Yesu wakati wa sikukuu ya Pasaka, pengine hilo litaleta muvurugo kati ya watu. Lakini ikiwa wanaweza kuchochea Waroma wamuue Yesu kwa kumushitaki juu ya mambo ya politike, kwa sababu Waroma wanaruhusiwa kufanya hivyo, watu wataona kuwa haiko viongozi hao Wayahudi ndio wanamuhukumu Yesu kifo.
Viongozi hao wa dini hawamuambie Pilato kuwa wanamuhukumu Yesu kwa sababu amekufuru. Sasa wanatunga mashitaka mengine ya uongo. Wanasema hivi: “Tulimukuta mutu huyu [1] akileta muvurugo katika taifa letu na [2] kukataza watu kulipa Kaisari kodi, na [3] kusema kwamba yeye mwenyewe ni Kristo mufalme.”—Luka 23:2.
Kwa sababu Pilato anawakilisha Utawala wa Roma, iko na sababu ya kuhangaikia shitaka la kwamba Yesu anajiita kuwa mufalme. Kwa hiyo, Pilato anaingia tena katika nyumba, anamuita Yesu na kumuuliza hivi: “Wewe ndiye Mufalme wa Wayahudi?” Ni kama vile anasema hivi, ‘Umevunja sheria ya utawala kwa kujitangaza kuwa mufalme na kumupinga Kaisari?’ Pengine, ili kujua ikiwa Pilato alikuwa amesikia mambo mengi juu yake, Yesu anamuambia hivi: “Je, unauliza vile kwa kujitungia wewe mwenyewe, ao watu wengine walikuambia juu yangu?”—Yohana 18:33, 34.
Ili kuonyesha kuwa hajue mambo mengi juu ya Yesu lakini anapenda kujua, Pilato anajibu hivi: “Mimi siko Muyahudi, haiko vile?” Anaongeza hivi: “Taifa lako mwenyewe na wakubwa wa makuhani walikutia katika mikono yangu. Ulifanya nini?”—Yohana 18:35.
Yesu hajaribu kuepuka wazo kubwa, ni kusema, ufalme wake. Anajibu katika njia yenye bila shaka inamushangaza Gavana Pilato.
-
-
Pilato na Herode Wanaona Kuwa Yesu Hana KosaYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 128
Pilato Na Herode Wanaona Kuwa Yesu Hana Kosa
MATAYO 27:12-14, 18, 19 MARKO 15:2-5 LUKA 23:4-16 YOHANA 18:36-38
PILATO NA HERODE WANAULIZA YESU MAULIZO
Yesu hajaribu kumuficha Pilato kuwa yeye ni mufalme kabisa. Lakini, Ufalme wake haulete hatari kwa Utawala wa Roma. Yesu anasema hivi: “Ufalme wangu hauko sehemu ya ulimwengu huu. Kama Ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe katika mikono ya Wayahudi. Lakini, kwa kweli, Ufalme wangu hautoke katika chanzo hiki.” (Yohana 18:36) Ndiyo, Yesu iko na Ufalme, lakini hauko wa ulimwengu huu.
Pilato haachie pale. Anauliza hivi: “Kwa hiyo, basi, wewe ni mufalme?” Yesu anapenda Pilato ajue kama amesema kweli wakati anajibu hivi: “Wewe mwenyewe unasema kwamba mimi ni mufalme. Nimezaliwa kwa ajili ya hili, na kwa ajili ya hili nimekuja katika ulimwengu, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli. Kila mutu mwenye kuwa upande wa ile kweli anasikiliza sauti yangu.”—Yohana 18:37.
Mbele ya hapo Yesu alikuwa amemuambia Tomasi hivi: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima.” Sasa Pilato anasikia kuwa jambo lenye lilifanya Yesu akuje duniani ni kutoa ushahidi juu ya “ile kweli,” zaidi sana kweli juu ya Ufalme wake. Yesu anaazimia kuwa muaminifu kwa ajili ya kweli hiyo hata kama hilo linamuomba kutoa uzima wake. Pilato anauliza hivi: “Kweli ni nini?” Lakini hangojee kupata maelezo zaidi. Anaona kuwa amesikia mambo ya kutosha ili kumuhukumu mutu huyo.—Yohana 14:6; 18:38.
Pilato anarudia ili kuongea na kikundi cha watu wenye wanangojea inje ya nyumba yake. Pengine Yesu iko pembeni yake wakati anaambia hivi wakubwa wa makuhani na wengine wenye kuwa pamoja nao: “Sipate kosa lolote kwa mutu huyu.” Watu hao wanakasirika kwa sababu ya uamuzi huo, kwa hiyo, wanakazia hivi: “Anachochea watu kwa kufundisha katika Yudea yote, kuanzia Galilaya na hata mupaka hapa.”—Luka 23:4, 5.
Pilato anapaswa kushangazwa na Wayahudi hao wenye kushikilia mawazo yenye hayana musingi. Wakati wakubwa wa makuhani na wazee wanaendelea kulalamika, Pilato anauliza Yesu hivi: “Hausikie mambo yote yenye wanashuhudia juu yako?” (Matayo 27:13) Yesu hajibie jambo lolote. Pilato anashangaa kwa sababu Yesu anabakia kimya wakati anashitakiwa mambo ya uongo.
Wayahudi wanasema kuwa Yesu ‘alianzia Galilaya.’ Wakati Pilato anafuatilia jambo hilo, anavumbua kuwa kwa kweli, Yesu ni mutu wa Galilaya. Hilo linamupatia Pilato wazo juu ya namna anaweza kuepuka daraka la kumuhukumu Yesu. Herode Antipa (mwana wa Herode Mukubwa) anatawala Galilaya, na iko katika Yerusalemu katika kipindi hiki cha Pasaka. Kwa hiyo, Pilato anamutuma Yesu kwa Herode. Ni Herode Antipa ndiye alitoa amri ili Yohana Mubatizaji akatwe kichwa. Kisha, wakati alisikia kuwa Yesu iko anafanya miujiza, Herode alikuwa na wasiwasi kuwa pengine Yesu ni Yohana mwenye amefufuka.—Luka 9:7-9.
Sasa Herode anafurahi kwa sababu anatumainia kumuona Yesu. Haiko kwa sababu anapenda kumusaidia Yesu ao anapenda kujua kabisa ikiwa mambo yenye wanamushitakia ni ya kweli. Herode anapenda tu kumuona, na ‘anatamani kumuona anafanya alama fulani.’ (Luka 23:8) Hata hivyo, Yesu hafanye mambo yenye Herode alipenda afanye. Kwa kweli, wakati Herode anamuuliza maulizo, Yesu hajibie jambo lolote. Kwa sababu ya kasirani, Herode na maaskari wake wanamutendea Yesu “kwa zarau.” (Luka 23:11) Wanamuvalisha nguo ya heshima na wanamuchekelea. Kisha Herode anamurudisha Yesu kwa Pilato. Herode na Pilato walikuwa maadui zamani, lakini sasa wanakuwa marafiki.
Wakati Yesu anarudishwa, Pilato anaita wakubwa wa makuhani, viongozi Wayahudi na watu na kusema hivi: “Nilimuuliza mbele yenu lakini sikupata jambo lolote lenye kuhakikisha mashitaka yenye munaleta juu yake. Kwa kweli, hata Herode hakupata jambo lolote, kwa maana alimurudisha kwetu, na muangalie! Mutu huyu hakufanya jambo lolote lenye kustahili kifo. Kwa hiyo nitamupatia azabu na kumufungua.”—Luka 23:14-16.
Pilato anapenda kumuachilia Yesu, kwa sababu anaelewa kuwa ni wivu ndio unachochea makuhani wamulete kwake. Wakati Pilato anajaribu kumuachilia Yesu, anapata jambo lingine ya kumuchochea kufanya hivyo. Wakati anakaa kwenye kiti cha hukumu, bibi yake anamutumia ujumbe huu: “Usiingie katika mambo ya mutu huyo mwenye hana kosa, kwa maana niliteseka sana leo katika ndoto [inawezekana ndoto yenye kutoka kwa Mungu] kwa sababu yake.”—Matayo 27:19.
Pilato anajua kama anapaswa kumuachilia mutu huyo mwenye hana kosa; lakini atafanya hivyo namna gani?
-
-
Pilato Anasema: “Muangalie! Mwanaume!”Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 129
Pilato Anasema: “Muangalie! Mwanaume!”
MATAYO 27:15-17, 20-30 MARKO 15:6-19 LUKA 23:18-25 YOHANA 18:39–19:5
PILATO ANAJARIBU KUMUACHILIA YESU
WAYAHUDI WANAOMBA BARABA AACHILIWE
YESU ANACHEKELEWA NA KUTENDEWA MUBAYA
Pilato anaambia hivi kikundi cha watu wenye wanapenda kumuua Yesu: “Sikupata jambo lolote lenye kuhakikisha mashitaka yenye munaleta juu yake. Kwa kweli, hata Herode hakupata jambo lolote.” (Luka 23:14, 15) Sasa, ili kujaribu kumulinda Yesu, Pilato anatumia njia ingine kwa kuambia watu hivi: “Muko na desturi kwamba niwafungulie mutu mumoja siku ya Pasaka. Basi, munataka niwafungulie Mufalme wa Wayahudi?”—Yohana 18:39.
Pilato anajua kama kuko mufungwa mumoja mwenye anaitwa Baraba, mwenye anajulikana kuwa mwizi, mwenye kuleta muvurugo, na muuaji. Kwa hiyo, Pilato anawaambia hivi: “Munataka niwafungulie nani, Baraba ao Yesu mwenye kuitwa Kristo?” Kwa sababu wanachochewa na wakubwa wa makuhani, watu wanaomba Baraba afunguliwe, hapana Yesu. Pilato anawauliza tena hivi: “Munataka niwafungulie nani kati ya hawa wawili?” Watu hao wanalalamika hivi: “Baraba”!—Matayo 27:17, 21.
Pilato anahuzunika, na anawauliza hivi: “Basi, nifanye nini na Yesu mwenye kuitwa Kristo?” Watu wanalalamika hivi: “Auawe kwenye muti!” (Matayo 27:22) Bila haya, wanaomba mutu mwenye hana kosa auawe. Pilato anawauliza hivi: “Sababu gani? Mutu huyu amefanya jambo gani la mubaya? Mimi sikuona ndani yake jambo lolote lenye linafanya astahili kifo; kwa hiyo nitamupatia azabu kisha nitamufungua.”—Luka 23:22.
Hata kama Pilato anajikaza sana, watu hao wenye hasira wanalalamika hivi kwa sauti moja: “Auawe kwenye muti!” (Matayo 27:23) Viongozi wa dini wamechochea kikundi hicho kikuwe na hasira kali mupaka kinapenda kumwanga damu ya mutu! Na haiko damu ya mutu mwenye alifanya makosa makubwa, ao ya muuaji fulani. Ni damu ya mutu mwenye hana kosa mwenye walikaribisha katika Yerusalemu kama Mufalme siku tano zenye zilikuwa zimepita. Ikiwa wanafunzi wa Yesu wako pale, wanabakia kimya na bila kujionyesha.
Pilato anaona kuwa watu hawakubali maombi yake. Muvurugo unaanza, kwa hiyo, anakamata maji na ananawa mikono yake mbele ya macho ya watu hao. Anawaambia hivi: “Damu ya mutu huyu haiko juu ya kichwa changu. Ile ni mambo yenu wenyewe.” Hata hivyo, hilo halibadilishe mawazo yao. Lakini wanasema hivi: “Damu yake ikuwe juu yetu na juu ya watoto wetu.”—Matayo 27:24, 25.
Gavana anapenda kuwafurahisha watu hao kuliko kufanya jambo lenye anajua kuwa ni sawa. Pilato anakubali ombi la watu, na anamuachilia Baraba. Anaamuru Yesu atoshwe manguo na kupigwa.
Kisha kumupiga mubaya sana, maaskari wanamupeleka Yesu katika nyumba ya gavana. Kikundi cha maaskari kinakusanyika na kumupiga tena kwa mijeledi. Wanatengeneza taji la miiba na kumuvalisha taji hilo kwenye kichwa. Pia maaskari wanatia katika mukono wa kuume wa Yesu utete na kumuvalisha nguo ya murefu ya rangi nyekundu, kama ile yenye wafalme wanavaa. Wanamuambia hivi kwa zarau: “Jambo, wewe Mufalme wa Wayahudi!” (Matayo 27:28, 29) Zaidi ya hilo, wanamutemea Yesu mate na kuendelea kumupiga makofi katika sura. Kisha wanakamata utete wenye uko katika mikono yake, wanautumia ili kumupiga kwenye kichwa, na kufanya “taji” la miiba la kumupatisha haya liingie zaidi katika kichwa chake.
Yesu anajiendesha kwa heshima na anabakia imara wakati wanamufanyia mambo hayo yote, hilo linamushangaza Pilato mupaka anajaribu tena kujionyesha kuwa hana kosa, anasema hivi: “Muone! Ninamuleta inje kwenu ili mujue kwamba sione kosa lolote ndani yake.” Je, Pilato anawaza kuwa kumuleta Yesu sasa akiwa mwenye kuumia na kutokwa damu kunaweza kufanya watu hao wabadilishe mawazo yao? Wakati Yesu anasimama mbele ya watu hao wenye hawana huruma, Pilato anasema hivi: “Muangalie! Mwanaume!”—Yohana 19:4, 5.
Hata kama Yesu ni mwenye kuumia anajiendesha kwa heshima na kwa utulivu mupaka hata Pilato anatambua jambo hilo, kwa sababu maneno yake yanaonekana kuwa yenye heshima na huruma.
-
-
Yesu Anatolewa na Anapelekwa ili AuaweYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 130
Yesu Anatolewa Na Anapelekwa Ili Auawe
MATAYO 27:31, 32 MARKO 15:20, 21 LUKA 23:24-31 YOHANA 19:6-17
PILATO ANAJARIBU KUMUACHILIA YESU
YESU ANAHUKUMIWA NA ANAPELEKWA ILI AUAWE
Hata kama Yesu ametendewa mubaya sana na kuchekelewa, bidii ya Pilato ya kutaka kumufungua haichochee wakubwa wa makuhani na wale wenye kuwaunga mukono. Hawapendi jambo lolote liwazuie kuua Yesu. Wanaendelea kulalamika hivi: “Auawe kwenye muti! Auawe kwenye muti!” Pilato anajibu hivi: “Mumukamate ninyi wenyewe na mumuue, kwa maana mimi sione kosa lolote ndani yake.”—Yohana 19:6.
Wayahudi hawamusadikishe Pilato kuwa Yesu anastahili kifo kwa kutumia mashitaka ya politike, lakini tuseme nini juu ya mashitaka ya mambo ya dini? Wanarudilia shitaka la kuwa Yesu amekufuru, lenye walisema wakati walikuwa wanamusambisha mbele ya Sanhedrini. Wanasema hivi: “Sisi tuko na sheria, na kulingana na sheria anapaswa kufa, kwa sababu alijifanya mwenyewe kuwa mwana wa Mungu.” (Yohana 19:7) Hili ni shitaka la mupya kwa Pilato.
Anarudia ndani ya nyumba yake na kujaribu kutafuta njia ya kufungua mwanaume huyo mwenye ametendewa mubaya sana na mwenye bibi yake aliota ndoto juu yake. (Matayo 27:19) Tuseme nini juu ya shitaka hilo la mupya lenye Wayahudi wanatoa, la kusema kwamba mufungwa huyo ni “mwana wa Mungu”? Pilato anajua kwamba Yesu ni mutu wa Galilaya. (Luka 23:5-7) Lakini, anamuuliza hivi: “Umetoka wapi?” (Yohana 19:9) Je, Pilato alikuwa anajiuliza ikiwa pengine Yesu aliishi zamani, na kwa njia fulani alitoka kwa Mungu?
Pilato alikuwa amesikia moja kwa moja namna Yesu alimuambia kuwa yeye ni mufalme lakini Ufalme wake hauko sehemu ya ulimwengu huu. Yesu hapendi kurudilia mambo yenye alikuwa amesema, kwa hiyo, anabakia kimya. Kwa sababu Yesu anakataa kumujibu, Pilato anakasirika na anamuambia hivi kwa ukali: “Unakataa kusema na mimi? Haujue kama niko na mamlaka ya kukufungua na niko na mamlaka ya kukuua?”—Yohana 19:10.
Yesu anasema tu hivi: “Wewe haungekuwa na mamlaka yoyote juu yangu kama haungepewa kutoka juu. Ndiyo sababu mutu mwenye alinitia katika mikono yako iko na zambi kubwa zaidi.” (Yohana 19:11) Inawezekana kuwa Yesu hafikirie tu mutu mumoja. Lakini anamaanisha kuwa Kayafa, wale wenye kumuunga mukono, na Yuda Iskariote wako na zambi kubwa zaidi kuliko Pilato.
Maneno ya Yesu na namna anajiendesha vinamushangaza Pilato, na anaogopa zaidi kuwa pengine Yesu ametoka kwa Mungu, kwa hiyo, anajaribu tena kumuachilia. Lakini, Wayahudi wanasema mambo mengine yenye yanapaswa kumuogopesha Pilato. Wanamuogopesha hivi: “Kama unamufungua mutu huyu, wewe hauko rafiki ya Kaisari. Kila mutu mwenye anajifanya mwenyewe kuwa mufalme anasema mubaya juu ya Kaisari.”—Yohana 19:12.
Pilato anatosha tena Yesu inje, anakaa kwenye kiti chake cha hukumu na kuambia watu hivi: “Muone! Mufalme wenu!” Lakini, Wayahudi hawabadilishe mawazo yao. Wanalalamika hivi: “Umuondoe! Umuondoe! Auawe kwenye muti!” Pilato anasema hivi: “Niue mufalme wenu?” Kwa muda murefu Wayahudi wameteswa na Utawala wa Roma; hata hivyo, wakubwa wa makuhani wanasema hivi: “Sisi hatuna mufalme isipokuwa Kaisari.”—Yohana 19:14, 15.
Kwa sababu ya kuogopa, Pilato anakubali ombi lenye Wayahudi wamefanya tena na tena, na anawatolea Yesu ili wamuue. Maaskari wanamutosha Yesu nguo ya rangi ya zambarau na wanamuvalisha nguo zake za inje. Wakati Yesu anapelekwa, anapaswa kubeba yeye mwenyewe muti wake wa mateso.
Sasa ni asubui ya Siku ya Tano tarehe 14 mwezi wa Nisani. Yesu amekuwa macho tangu Siku ya Ine asubui na ametendewa matendo mbalimbali ya mubaya yenye kuumiza sana. Yesu anajikaza sana kubeba muti huo muzito, lakini nguvu zinamuisha. Kwa hiyo, maaskari wanakaza mutu mumoja mwenye kupita amusaidie, ni kusema, Simoni wa Kirene ya Afrika abebe muti huo wa mateso mahali penye Yesu atauawa. Watu wengi wanawafuata, wamoja wanajipiga-piga kifua kwa uchungu kwa sababu wanahuzunishwa na mambo yenye yako yanatendeka.
Yesu anaambia hivi wanamuke wenye kulia: “Mabinti wa Yerusalemu, muache kunililia. Lakini mujililie ninyi wenyewe na watoto wenu; kwa maana muangalie! Siku zinakuja wakati watu watasema, ‘Wenye furaha ni wanamuke tasa, na matumbo ya uzazi yenye hayakuzaa, na maziwa yenye hayakunyonyesha!’ Kisha wataanza kuambia milima, ‘Mutuangukie!’ na vilima, ‘Mutufunike!’ Kama wanafanya mambo haya wakati muti ni mubichi, itakuwa namna gani wakati utakuwa umekauka?”—Luka 23:28-31.
Yesu anazungumuzia taifa la Wayahudi. Liko kama muti wenye kukauka wenye ungali na sehemu fulani ya mubichi kwa sababu Yesu angali na pia Wayahudi fulani wenye kumuamini. Wakati hao wataondolewa, kutabakia tu taifa lenye kukauka kiroho, kama muti wenye kufa. Watu watalia sana wakati majeshi ya Roma yataleta hukumu ya Mungu juu ya taifa hilo!
-
-
Mutu Mwenye Hana Kosa Anateseka Kwenye MutiYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 131
Mufalme Mwenye Hana Kosa Anateseka Kwenye Muti
MATAYO 27:33-44 MARKO 15:22-32 LUKA 23:32-43 YOHANA 19:17-24
YESU ANATUNDIKWA KWENYE MUTI WA MATESO
ALAMA YENYE KUWEKWA JUU YA KICHWA CHA YESU INAFANYA WATU WAMUCHEKE
YESU ANATOA TUMAINI LA UZIMA KATIKA PARADISO DUNIANI
Yesu anapelekwa nafasi moja yenye haiko mbali sana na muji, kwenye yeye na wezi wengine wawili wanapaswa kuuawa. Nafasi hiyo inaitwa Golgota, ao Mahali pa Fuvu la kichwa, na ni mahali penye watu wanaweza kuona “kwa mbali.”—Marko 15:40.
Wanaume hao watatu wenye kuhukumiwa wanatoshwa nguo zao. Kisha divai yenye kuwa na manemane na nyongo yenye kuwa chungu inaletwa. Inaonekana kuwa wanamuke wa Yerusalemu wametengeneza divai hiyo yenye kupunguza maumivu. Na Waroma hawakataze kuipatia wale wenye kutundikwa. Lakini, wakati tu Yesu anaionja, anakataa kabisa kuikunywa. Sababu gani? Anapenda kutumia akili yake yote wakati huu wa jaribu kubwa; anapenda kuwa na uwezo wa kufikiri na kuwa muaminifu mupaka kifo.
Yesu ananyoroshwa kwenye muti wa mateso. (Marko 15:25) Maaskari wanapigilia misumari katika mikono yake na miguu yake, wanatoboa minofu na misuli na hilo linaleta maumivu makali. Wakati muti unasimamishwa, maumivu yanakuwa makali hata zaidi wakati uzito wa mwili wa Yesu unapasua vidonda vyake. Lakini, Yesu hatukane maaskari hao. Anasali hivi: “Baba, wasamehe, kwa maana hawajue jambo lenye wanafanya.”—Luka 23:34.
Waroma wako na zoezi la kuweka alama yenye kuonyesha kosa lenye mutu mwenye kuhukumiwa alifanya. Wakati huu Pilato amewaka alama yenye kuwa na maneno haya: “Yesu Munazareti Mufalme wa Wayahudi.” Yameandikwa katika Kiebrania, Kilatini, na Kigiriki, kwa hiyo, karibu watu wote wanaweza kuisoma. Tendo hilo la Pilato linaonyesha kuwa anachukia Wayahudi wenye walikazia sana ili Yesu auawe. Wakubwa wa makuhani hawafurahie jambo hilo, kwa hiyo wanakataa kwa kusema hivi: “Usiandike, ‘Mufalme wa Wayahudi,’ lakini uandike kwamba alisema, ‘Mimi ni Mufalme wa Wayahudi.’” Lakini kwa sababu Pilato hapendi tena wamuchochee, anajibu hivi: “Maneno yenye nimeandika, nimeyaandika.”—Yohana 19:19-22.
Makuhani hao wenye kukasirika wanarudilia mashitaka ya uongo yenye yalikuwa yametolewa wakati Yesu alikuwa anasambishwa katika Sanhedrini. Haiko jambo la kushangaza kuwa watu wenye kupita katika njia wanatingiza vichwa vyao na kusema hivi kwa kumucheka na kwa zarau: “Aha! Wewe mwenye ulitaka kubomoa hekalu na kulijenga kwa siku tatu (3) jiokoe mwenyewe kwa kushuka kutoka kwenye muti wa mateso.” Vilevile wakubwa wa makuhani na waandishi wanaambiana hivi: “Sasa Kristo, Mufalme wa Israeli, ashuke sasa kutoka kwenye muti wa mateso, ili tuone na kuamini.” (Marko 15:29-32) Hata wezi wenye walikuwa wametundikwa kwenye upande wa kuume na wa kushoto wa Yesu wanamusema pia, hata kama ni yeye tu ndiye mwenye hana kosa kabisa.
Maaskari ine Waroma wanamucheka pia Yesu. Pengine walikuwa wanakunywa divai yenye kuwa makali, sasa wanamucheka Yesu kwa kuweka divai hiyo mbele yake, lakini Yesu hawezi kuifikia na kunywa. Kwa zarau Waroma wanatumia maneno yenye kuwa juu ya kichwa cha Yesu na kusema hivi: “Kama wewe ndiye Mufalme wa Wayahudi, jiokoe wewe mwenyewe.” (Luka 23:36, 37) Fikiria jambo hili! Mwanaume mwenye ameonyesha wazi kuwa yeye ndiye njia, kweli, na uzima sasa anatendewa kwa zarau na kuchekelewa bila sababu. Lakini anavumilia mambo hayo yote bila kusema jambo lolote juu ya Wayahudi wenye kuangalia, maaskari Waroma wenye kumucheka, ao watenda zambi wawili wenye wametundikwa pembeni yake.
Maaskari hao ine wamekamata nguo za inje za Yesu na kuzigawanya katika vipande ine. Wanapiga kura ili kuona ni nani mwenye atachukua kila kipande. Lakini nguo ya Yesu ya ndani ni ya hali ya juu, “haikukuwa na mushono, ilikuwa imesukwa kuanzia juu mupaka chini.” Maaskari hao wanawaza hivi: “Tusiipasue, lakini tuipigie kura ili kuamua itakuwa ya nani.” Kwa hiyo, wanatimiza andiko lenye kusema hivi: “Waligawana nguo zangu kati yao wenyewe, na wakapigia nguo yangu kura.”—Yohana 19:23, 24; Zaburi 22:18.
Kisha wakati fulani, mwizi mumoja mwenye kutundikwa karibu na Yesu anatambua kuwa Yesu anapaswa kuwa Mufalme kabisa. Anakaripia ule mwingine kwa kumuambia maneno haya: “Je, wewe haumuogope Mungu hata kidogo, kwa kuwa sasa umepata hukumu ileile? Sisi tunastahili kutendewa hivi, kwa maana tunapewa azabu kupatana na makosa yenye tulifanya; lakini mutu huyu hakufanya jambo lolote la mubaya.” Kisha anamuomba Yesu hivi: “Unikumbuke wakati utaingia katika Ufalme wako.”—Luka 23:40-42.
Yesu anajibu hivi: “Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso,” hapana katika Ufalme lakini “katika Paradiso.” (Luka 23:43) Ahadi hiyo iko tofauti na ahadi yenye Yesu ameambia mitume wake, ni kusema, watakaa kwenye viti vya ufalme katika Ufalme wake. (Matayo 19:28; Luka 22:29, 30) Lakini, pengine mutenda zambi huyo Muyahudi alikuwa amekwisha kusikia juu ya Paradiso yenye Yehova alikuwa ametolea Adamu, Eva na wazao wao. Sasa mwizi huyo anaweza kufa na tumaini hilo.
-
-
“Hakika Huyu Alikuwa Mwana wa Mungu”Yesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 132
“Hakika Huyu Alikuwa Mwana Wa Mungu”
MATAYO 27:45-56 MARKO 15:33-41 LUKA 23:44-49 YOHANA 19:25-30
YESU ANAKUFA KWENYE MUTI
MAMBO YENYE HAYAKO YA KAWAIDA YANATOKEA WAKATI YESU ANAKUFA
Sasa ni “saa sita,” ao katikati ya muchana. Giza lenye haliko la kawaida linatokea “juu ya inchi yote mupaka saa kenda,” kisha muchana. (Marko 15:33) Giza hilo lenye kuogopesha halikutokea kwa sababu mwezi uliingia katikati ya dunia na jua. Hilo linatokea wakati wa mwezi mupya, lakini huu ni wakati wa Pasaka, wakati mwezi wote ni wenye kuenea. Na giza hilo linabakia kwa muda murefu sana kuliko kufanya dakika fulani kama vile inakuwa wakati mwezi unaingia katikati ya dunia na jua. Kwa hiyo, ni Mungu ndiye ameleta giza hilo!
Wazia mambo hayo yalipaswa kuwa na matokeo gani juu ya wale wenye walikuwa wanamuchekelea Yesu. Wakati wa kipindi hicho cha giza, wanamuke ine wanakaribia muti wa mateso. Wanamuke hao ni mama ya Yesu, Salome, Maria Magdalene, na Maria mama ya mutume Yakobo Mudogo.
Mutume Yohana iko pembeni ya “muti wa mateso” pamoja na mama ya Yesu mwenye kuwa na huzuni. Maria anaona namna mutoto mwenye alizaa na kukomalisha anateseka sana kwenye muti wa mateso. Jambo hilo ni kama “upanga murefu” wenye kuingizwa katika mwili wake. (Yohana 19:25; Luka 2:35) Lakini, hata kama Yesu anasikia maumivu makali sana, anahangaikia hali ya mama yake. Anajikaza sana kugeuzia kichwa chake upande wa Yohana na anamuambia mama yake hivi: “Mwanamuke, ona! Mwana wako!” Kisha anamugeukia Maria na kuambia Yohana hivi: “Ona! Mama yako!”—Yohana 19:26, 27.
Yesu anafanya mipango ili mama yake, pengine mwenye kuwa sasa mujane, achungwe na mutume mwenye anapenda sana. Yesu anajua kuwa ndugu zake wadogo, ni kusema, watoto wengine wa Maria, walikuwa hawajamuamini. Kwa hiyo anafanya mipango ili mama yake atimiziwe mahitaji yake ya kimwili na ya kiroho. Huo ni mufano muzuri sana!
Wakati giza linakaribia kuisha, Yesu anasema hivi: “Ninasikia kiu.” Kwa kufanya hivyo anatimiza maandiko. (Yohana 19:28; Zaburi 22:15) Yesu anajisikia kuwa ni kama vile Baba yake ameondoa ulinzi juu yake ili ushikamanifu wake ujaribiwe mupaka mwisho. Kristo anaita hivi pengine katika luga ya Galilaya yenye kutokana na Kiaramu: “Eli, Eli, lama sabaktani?” maana yake ni, “Mungu wangu, Mungu wangu, sababu gani umeniacha?” Watu fulani wenye wanasimama karibu naye hawaelewe maneno yake, kwa hiyo, wanasema hivi: “Munasikia! Anaita Eliya.” Mumoja wao anakimbia, anatia sifongo katika divai yenye kuwa chungu, anaitia kwenye mwisho wa utete, na kumupatia Yesu akunywe. Lakini wengine wanasema hivi: “Mumuache! Tuone kama Eliya atakuja kumushusha.”—Marko 15:34-36.
Kisha Yesu analalamika hivi: “Imetimizwa!” (Yohana 19:30) Ndiyo, ametimiza mambo yote yenye Baba yake alimutuma afanye hapa duniani. Mwishowe, Yesu anasema hivi: “Baba, ninaweka roho yangu katika mikono yako.” (Luka 23:46) Kwa hiyo, Yesu anatia uzima wake katika mikono ya Yehova, na iko hakika kuwa Mungu atamurudishia uzima huo. Yesu anamutegemea kabisa Mungu, kwa hiyo, anainamisha kichwa chake na anakufa.
Wakati huo, tetemeko kubwa la inchi linatokea, linapasua miamba. Tetemeko hilo liko na nguvu sana mupaka makaburi yenye kuwa inje ya Yerusalemu yanafunguka na maiti za watu wenye kufa zinatoka inje. Wapita njia wenye wanaona maiti hizo wanaingia katika “muji mutakatifu” na kusema mambo yenye wametoka tu kujionea.—Matayo 12:11; 27:51-53.
Wakati Yesu anakufa, pazia ndefu na yenye kuwa na uzito sana yenye kutenganisha Mahali Patakatifu na Patakatifu Zaidi inapasuka katika vipande viwili, kutoka juu mupaka chini. Matukio hayo yenye kushangaza yanaonyesha hasira ya Mungu juu ya wale wenye waliua Mwana wake na yanamaanisha kuwa njia ya kuenda Mahali Patakatifu Zaidi, ni kusema, mbinguni, inakuwa sasa wazi.—Waebrania 9:2, 3; 10:19, 20.
Kwa kweli, watu wanaogopa sana. Mukubwa wa jeshi mwenye anasimamia kuuawa kwa Yesu, anasema hivi: “Hakika mutu huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Marko 15:39) Pengine alikuwa hapo wakati Yesu alikuwa anasamba mbele ya Pilato wakati alikuwa anaulizwa ikiwa yeye ni Mwana wa Mungu ao hapana. Sasa iko hakika kuwa Yesu ni mutu mwenye kufanya mambo yenye kuwa sawa na kwa kweli yeye ni Mwana wa Mungu.
Watu wengine wenye waliona matukio hayo yenye kushangaza, wanarudia nyumbani kwao, “wakijipiga-piga kwenye vifua vyao” ili kuonyesha huzuni yao nyingi na haya. (Luka 23:48) Kati ya wale wenye kuangalia kwa mbali ni wanafunzi wanamuke wenye walikuwa wanasafiri pamoja na Yesu kwa wakati fulani. Wao pia wanaguswa sana na matukio hayo makubwa sana.
-
-
Mwili wa Yesu Unatayarishwa na UnazikwaYesu—Ni Njia, Kweli, na Uzima
-
-
SURA YA 133
Mwili Wa Yesu Unatayarishwa Na Kuzikwa
MATAYO 27:57–28:2 MARKO 15:42–16:4 LUKA 23:50–24:3 YOHANA 19:31–20:1
MWILI WA YESU UNAONDOLEWA KWENYE MUTI
MWILI UNATAYARISHWA KWA AJILI YA MAZIKO
WANAMUKE WANAKUTA KABURI LIKO WAZI
Sasa ni mangaribi ya Siku ya Tano tarehe 14 mwezi wa Nisani. Wakati jua litashuka, Sabato ya tarehe 15 ya mwezi wa Nisani itaanza. Yesu amekwisha kufa, lakini wezi wawili wenye kuwa pembeni hawajakufa. Sheria ilisema kuwa miili yenye kufa “isibakie kwenye muti usiku wote” lakini, inapaswa kuzikwa “siku hiyo.”—Kumbukumbu la Torati 21:22, 23.
Zaidi ya hilo, kipindi cha kisha muchana cha Siku ya Tano kinaitwa Matayarisho kwa sababu watu wanatayarisha chakula na kumalizia kazi zenye zinapaswa kufanywa mbele ya Sabato kuanza. Wakati jua litashuka, Sabato “kubwa,” itaanza. (Yohana 19:31) Inaitwa hivyo kwa sababu tarehe 15 ya mwezi wa Nisani itakuwa siku ya kwanza ya siku saba za Sikukuu ya Mikate Yenye Haina Chachu, kwa kawaida siku ya kwanza inakuwa Sabato. (Mambo ya Walawi 23:5, 6) Wakati huu siku ya kwanza inakuwa siku ileile ya Sabato ya kila juma, ni kusema, siku ya saba.
Kwa hiyo, Wayahudi wanaomba Pilato afanye jambo fulani ili Yesu na wezi wenye walikuwa wanatundikwa pembeni yake wakufe haraka. Namna gani? Kwa kuwavunja miguu. Hilo litafanya washindwe kutumia miguu yao ili kuinua mwili wao ili waweze kupumua. Maaskari wanakuja na kuvunja miguu ya wezi hao wawili. Lakini, inaonekana kuwa Yesu amekufa, na kwa hiyo, hawavunje miguu yake. Hilo linatimiza andiko la Zaburi 34:20 lenye kusema hivi: “Analinda mifupa yake yote; hakuna mumoja kati ya mifupa yake wenye umevunjwa.”
Ili wakuwe hakika kuwa Yesu amekufa kabisa, askari mumoja anaingiza mukuki katika mbavu zake, sehemu kwenye moyo wake unapatikana. ‘Mara moja damu na maji vinatoka.’ (Yohana 19:34) Hilo linatimiza andiko lingine lenye kusema hivi: “Wataangalia ule mwenye walitoboa.”— Zekaria 12:10.
Yosefu “mutu mumoja tajiri” kutoka katika muji wa Arimatea, na ambaye ni mutu mwenye kuheshimiwa sana wa Sanhedrini, iko pia nafasi kwenye Yesu anatundikwa. (Matayo 27:57) Biblia inamuita kuwa “mutu mwema na mwenye kufanya mambo yenye kuwa sawa,” mwenye “anangojea Ufalme wa Mungu.” Kwa kweli, kwa sababu yeye ni “mwenye alikuwa mwanafunzi wa Yesu lakini kwa uficho,” hakuunga muko tribinali wakati ilimuhukumu Yesu. (Luka 23:50; Marko 15:43; Yohana 19:38) Yosefu anatenda bila kuogopa na anamuomba Pilato mwili wa Yesu. Pilato anamuita mukubwa wa jeshi mwenye alikuwa anasimamia kuuawa kwa Yesu, na mukubwa huyo anahakikisha kuwa Yesu amekufa. Mara moja, Pilato anakubali ombi la Yosefu.
Yosefu anauza nguo ya kitani safi na kizuri na kushusha mwili wa Yesu kwenye muti. Anafunga mwili huo katika nguo hiyo na kuutayarisha kwa ajili ya maziko. Nikodemo, “mwenye alikuwa amekuja kwake [Yesu] usiku mara ya kwanza,” anasaidia kufanya matayarisho. (Yohana 19:39) Analeta kilo 33 ya muchanganyiko wa bei sana wa manemane na udi. Mwili wa Yesu unafungwa katika vitambaa vyenye kuwa na vikolezo hivyo, kulingana na desturi ya Wayahudi ya maziko.
Yosefu iko na kaburi lenye halijatumiwa lenye kuchimbuliwa katika mwamba wenye kuwa karibu na mahali hapo, na mwili wa Yesu unawekwa katika kaburi hilo. Kisha jiwe kubwa linawekwa kwenye muingilio wa kaburi. Wanafanya hivyo haraka sana, mbele Sabato ianze. Inawezekana kuwa Maria Magdalene na Maria mama ya Yakobo Mudogo walikuwa wanasaidia kutayarisha mwili wa Yesu. Sasa wanaenda haraka nyumbani “kutayarisha manukato na mafuta yenye marashi” yenye watapakaa mwili wa Yesu kisha Sabato.—Luka 23:56.
Siku yenye ilifuata, ni kusema, siku ya Sabato, wakubwa wa makuhani na Wafarisayo wanaenda kwa Pilato na kumuambia hivi: “Tumekumbuka mambo yenye ule mujanja alisema wakati alikuwa angali muzima, ‘Nitafufuliwa kisha siku tatu (3).’ Kwa hiyo, amuru kaburi lilindwe mupaka siku ya tatu (3), ili wanafunzi wake wasikuje na kumuiba na kuambia watu, ‘Amefufuliwa kutoka kwa wafu!’ Halafu uongo huu wa mwisho utakuwa mubaya kuliko ule wa kwanza.” Pilato akawaambia: “Ninyi muko na walinzi. Muende mulilinde vile munajua.”—Matayo 27:63-65.
Siku ya Yenga asubui sana, Maria Magdalene, Maria mama ya Yakobo, na wanamuke wengine wanaleta vikolezo kwenye kaburi ili kupakaa mwili wa Yesu. Wanaambiana hivi: “Ni nani atatuviringishia jiwe kutoka kwenye muingilio wa kaburi?” (Marko 16:3) Lakini tetemeko la inchi limetokea. Zaidi ya hilo, malaika wa Mungu ametosha jiwe hilo, walinzi hawako tena, na kaburi liko wazi!
-