Vichapo Vyenye Kutajwa mu Buku ya Mukutano Utumishi na Maisha
© 2023 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
TAREHE 6-12/11
UTAJIRI WA NENO YA MUNGU | YOBU 13-14
“Kama Mutu Anakufa, je, Anaweza Kuishi Tena?”
w99-SW 15/10 uku. 3 fu. 1-3
Jitihada Yetu ya Kuishi Muda Mrefu Zaidi
HATA leo ni wachache wawezao kupinga maneno hayo kuhusu ufupi wa maisha, ingawa yaliandikwa miaka ipatayo 3,500 iliyopita. Sikuzote watu hawaridhiki kufurahia upeo wa maisha kwa muda mfupi tu, kisha kuzeeka na kufa. Hivyo, njia za kurefusha maisha zimeongezeka katika historia yote.
Wakati wa Yobu Wamisri walikula mapumbu ya wanyama katika jitihada ambazo hazikufua dafu za kurudia ujana wao. Lengo moja kuu la tiba ya kurefusha maisha ya enzi za kati lilikuwa kutokeza dawa ambayo ingeweza kurefusha maisha. Waliofuatia tiba ya kurefusha maisha waliamini kwamba dhahabu iliyotokezwa na wanadamu ingesababisha uhai usioweza kufa na kwamba kulia sahani za dhahabu kungerefusha maisha. Wachina wa kale waliofuata dini ya Tao walifikiri kwamba wangeweza kugeuza maumbile ya mwili kwa kutumia mbinu kama kutafakari, mazoezi ya kupumua, na utaratibu maalum wa kula na hivyo kufikia hali ya kutoweza kufa.
Mvumbuzi Mhispania aitwaye Juan Ponce de León anajulikana kuwa alitafuta kwa udi na uvumba chemchemi ya ujana. Daktari fulani wa karne ya 18 alipendekeza katika kitabu chake, Hermippus Redivivus, kwamba mabikira wachanga wawekwe katika kijumba wakati wa masika na pumzi zao zikusanywe katika chupa na kutumiwa kama dawa ya kurefusha maisha. Ni wazi kwamba hakuna hata moja ya mbinu hizo iliyofanikiwa.
Muti Ukikatwa Unaweza Kuchipuka Tena?
UKILINGANISHA muti wa muzeituni wenye kuzeeka na muti wa mwerezi mukubwa wa Lebanoni, muzeituni unaweza kuonekana kuwa mudogo sana. Hata hivyo, muzeituni uko na uwezo wa ajabu wa kuishi kwa muda murefu sana. Inasemekana kwamba mizeituni fulani imeishi miaka 1000. Muti wa muzeituni unatuma mizizi yake mbali sana katika udongo; kwa hiyo, muti huo uko na uwezo wa kuchipuka tena hata kama umekwisha kukatwa. Kadiri mizizi yake inaendelea kuishi, muti huo utachipuka tena.
Muzee wa ukoo Ayubu alikuwa hakika kwamba hata kama angekufa, angeweza kuishi tena. (Yob 14:13-15) Pengine alitumia mufano wa muti wa muzeituni ili kuonyesha kama anaamini kabisa kwamba Mungu iko na uwezo wa kumufufua. Ayubu alisema hivi: ‘Kwa ajili ya muti kuna tumaini, ukikatwa, utachipuka tena.’ Wakati mvua inaanza kunyesha na kumaliza kipwa kali, shina la muzeituni lenye kukauka linaweza kuotesha sehemu fulani kupitia mizizi yake na kutoa ‘matawi kama mumea mupya.’—Yob 14:7-9.
w11-SW 1/3 uku. 22 fu. 5
“Utaitamani Sana”
Maneno ya Ayubu yanatusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyotupenda: Ana uhusiano wa kipekee na wale ambao kama Ayubu, hujiweka mikononi mwake na kumruhusu awafinyange ili wawe watu wenye kupendeza machoni pake. (Isaya 64:8) Yehova anawathamini sana waabudu wake waaminifu. ‘Anatamani’ washikamanifu wake waliokufa. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “-tamani” pasipo shaka ni “mojawapo ya maneno mazito zaidi ya kuonyesha hamu kubwa,” asema msomi mmoja. Ndiyo, Yehova anawakumbuka waabudu wake na pia anatamani kuwafufua.
Mali ya Kiroho
it-1-F uku. 412
Majivu
Majivu ilitumiwa pia juu ya kufananisha mambo yenye haikukuwa ya maana sana. Kwa mufano, Abrahamu alimuambia Yehova hivi: “Mimi ni mavumbi na majivu.” (Mwa 18:27; ona pia Isa 44:20; Yob 30:19.) Na Yobu alisema kama maneno ya washauri wake wa uongo ilikuwa sawa “mezali za majivu.”—Yob 13:12.
TAREHE 13-19/11
UTAJIRI WA NENO YA MUNGU | YOBU 15-17
“Usifuate Mufano wa Elifazi Wakati Unafariji Wengine”
w05-SW 15/9 uku. 26 fu. 4-5
Kataa Mawazo Yasiyofaa!
Katika hotuba zote tatu, Elifazi alionyesha wazo la kwamba Mungu ni mwenye kudai mengi mno hivi kwamba hakuna jambo watumishi wake wanalofanya linalompendeza. Elifazi alimwambia Ayubu hivi: “Hata watumishi wake, Mungu hana imani nao; na malaika wake huwaona wana kosa.” (Ayubu 4:18, maelezo ya chini) Baadaye Elifazi alisema hivi kumhusu Mungu: “Yeye hana imani na watakatifu wake, na mbingu zenyewe kwa kweli si safi machoni pake.” (Ayubu 15:15) Naye akauliza: “Je, Mweza-Yote anapendezwa kwa vyovyote kwa kuwa wewe ni mwadilifu?” (Ayubu 22:3) Bildadi alikubaliana na maoni hayo kwa kuwa alisema hivi: “Kuna hata mwezi, nao si mwangavu; nazo nyota zenyewe si safi machoni pake [Mungu].”—Ayubu 25:5.
Tunapaswa kujihadhari ili tusiathiriwe na kufikiri kwa namna hiyo. Kunaweza kutufanya tufikiri kwamba Mungu anatudai mambo mengi mno. Kufikiri kwa njia hiyo kunahatarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Isitoshe, tukiathiriwa na kufikiri kwa namna hiyo, tutaitikiaje tunapotiwa nidhamu? Badala ya kukubali rekebisho kwa unyenyekevu, huenda moyo wetu ‘ukawa na ghadhabu juu ya Yehova’ na hata tunaweza kumwekea kinyongo. (Methali 19:3) Hakika hilo linaweza kuharibu uhusiano wetu pamoja na Mungu.
Tufuate Mufano wa Yesu: Tukuwe Wanyenyekevu na Tutendee Wengine kwa Huruma
16 Tutumie maneno ya huruma. Ikiwa tunasikilia wengine huruma, tutachochewa kutumia maneno yenye “kuzifariji nafsi zilizohuzunika.” (1 Tes. 5:14) Tunaweza kusema nini ili kutia moyo wale wenye kuhuzunika? Tunaweza kuwatia moyo ikiwa tunawaonyesha kupitia maneno yetu kwamba tunawahangaikia kabisa. Tunaweza kuwapongeza kutoka moyoni ili kuwasaidia waone sifa zao nzuri na uwezo wao mbalimbali. Tunaweza kuwakumbusha kwamba, ikiwa Yehova aliwavuta kwa Mwana wake, ni kwa sababu Yehova anawaona kuwa watu wa maana sana. (Yoh. 6:44) Tunaweza kuwatia moyo kwa kuwaonyesha kwamba Yehova anawahangaikia sana watumishi wake “waliovunjika moyo” ao “waliopondwa roho.” (Zb. 34:18) Maneno yetu yenye huruma yanaweza kusaidia wale wenye kuwa na lazima ya kufarijiwa.—Met. 16:24.
Mali ya Kiroho
w06-SW 15/3 uku. 14 fu. 11
Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ayubu
7:9, 10; 10:21; 16:22—Je, maneno hayo yanaonyesha kwamba Ayubu hakuamini ufufuo? Ayubu anazungumza mambo ambayo yangetukia ikiwa angekufa. Kwa hiyo, alimaanisha nini? Huenda maneno yake yanamaanisha kwamba iwapo angekufa, watu walioishi katika siku zake hawangemwona tena. Hawangemtambua wala yeye hangeweza kurudi nyumbani kwake wala kutambuliwa tena hadi wakati wa Mungu uliowekwa. Pia, huenda Ayubu alimaanisha kwamba hakuna mtu anayeweza kutoka Sheoli bila kusaidiwa. Maneno ya Ayubu 14:13-15 yanaonyesha wazi kwamba Ayubu aliamini kutakuwa na ufufuo siku zijazo.
TAREHE 20-26/11
UTAJIRI WA NENO YA MUNGU | YOBU 18-19
“Usiache Waamini Wenzako Hata Kidogo”
Machozi ya Yesu Inaweza Kutufundisha Nini?
9 Unaweza kusaidia wale wenye kuwa na huzuni. Yesu hakulia tu pamoja na Marta na Maria lakini pia aliwasikiliza na kuwafariji. Tunaweza pia kufanya vile juu ya wale wenye kuwa na huzuni. Dan, muzee moja mwenye kuishi Australia, anasema hivi: “Kisha kupoteza bibi yangu nilikuwa na lazima ya musaada. Ndugu wengi na bibi zao, mara mingi walikuwa tayari kunisikiliza. Hawakunizuia nionyeshe huzuni yangu na hawakunihukumu wakati nilikuwa nalia. Walinisaidia pia kufanya mambo fulani, sawa vile kusafisha gari yangu, kuuza vitu fulani, na kunisaidia kupika chakula wakati nilijisikia kama siwezi kufanya ile kazi yote miye peke. Na walisali pamoja na miye mara mingi. Walionyesha kabisa kama walikuwa marafiki wa kweli, ndugu wenye ‘wamezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.’”—Mez. 17:17.
Wakati Mupendwa Wako Anamuacha Yehova
16 Endelea kutegemeza familia ya ule mwenye alitengwa. Wako na lazima ya upendo wako na vitia-moyo vyako sana kuliko hata zamani. (Ebr. 10:24, 25) Wakati fulani, watu wa familia ya mwenye alitengwa wanajisikiaka sawa vile nao pia walitengwa na kutaniko. Hatupende wajisikie vile! Zaidi sana vijana wenye wazazi wao walitengwa wako na lazima sana ya vitia-moyo na kupongezwa. Maria, mwenye bwana yake alitengwa na kisha akaacha familia, anasema hivi: “Marafiki wangu fulani walikuya ku nyumba na walipika chakula na walinisaidia kujifunza pamoja na watoto wangu. Walihuzunika pamoja na miye na tulilia pamoja. Walinitetea wakati watu wengine walisema mambo yenye haiko ya kweli juu yangu. Kusema kweli, walinitia moyo sana!”—Ro. 12:13, 15.
w90-SW 1/9 uku. 22 fu. 20
Je! Wewe Wajitahidi Kufikia?
20 Baraza la wazee lapaswa kung’amua kwamba mfuto huenda ukasababisha mkazo kwa aliyekuwa mwangalizi au mtumishi wa huduma, hata ikiwa yeye aacha pendeleo hilo kwa kujitolea. Ikiwa yeye hakutengwa na ushirika, lakini wazee waona kwamba ndugu huyo ameshuka moyo, wao wapaswa kuandaa usaidizi wa kiroho wenye upendo. (1 Wathesalonike 5:14) Wapaswa kumsaidia ang’amue kwamba yuahitajiwa katika kundi. Hata ikiwa shauri limetakiwa, huenda usiwe ni muda mrefu sana kabla mwanamume mnyenyekevu mwenye shukrani hajapokea mapendeleo zaidi ya utumishi katika kundi.
Mali ya Kiroho
w94-SW 1/10 uku. 32
Uwezo wa Neno Lenye Fadhili
Hata hivyo, Ayubu mwenyewe alipohitaji kitia-moyo, Elifazi na waandamani wake hawakutamka maneno yenye fadhili. Wao walimlaumu Ayubu kwa ajili ya taabu yake, wakidokeza kwamba ni lazima alikuwa na kosa fulani la siri. (Ayubu 4:8) The Interpreter’s Bible chaeleza hivi: “Kile Ayubu ahitajicho ni huruma ya moyo wa kibinadamu. Yeye apokea tu mfululizo wa misemo ya kidini ya kurudiwa-rudiwa yaliyo ‘kweli’ kabisa na yanayovutia kabisa na maadili yaleyale.” Ayubu alivunjika moyo sana kwa kusikia hotuba za Elifazi na waandamani wake hivi kwamba alilazimika kupaza sauti hivi: “Je, mtanichukiza nafsi yangu hata lini, na kunivunja-vunja kwa maneno?”—Ayubu 19:2.
Tusimfanye kamwe mtumishi mwenzetu wa Mungu alie kwa dhiki kwa sababu ya maneno yetu yasiyo na maana na yasiyo ya fadhili. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 24:15.) Mithali moja ya Biblia yaonya hivi: “Yale uyasemayo yaweza kuokoa uhai au kuuharibu; kwa hiyo ni lazima ukubali matokeo ya maneno yako.”—Methali 18:21, TEV.
Hotuba: Umutie Moyo Mwanafunzi Wako Ajikaze Kuwa na Marafiki mu Kutaniko
Namna ya Kusaidia Wanafunzi wa Biblia Wafikie Kubatizwa—Sehemu ya Pili
10 Walimu wa Biblia wanapaswa kuhangaikia kabisa wanafunzi wao. Wanapaswa kuwaona kuwa ndugu na dada wa kesho. (Soma 1 Watesalonike 2:7, 8.) Haiko mwepesi kwao kuachana na marafiki wao wa zamani na kufanya mabadiliko ili kumutumikia Yehova. Tunapaswa kuwasaidia wapate marafiki wazuri mu kutaniko. Ujikaze ukuwe rafiki ya mwanafunzi wako kwa kupitisha wakati pamoja naye hata kama haiko saa ya kujifunza. Unaweza kumuita ku telefone, kumuandikia ujumbe ao kumutembelea siku yenye haiko siku yenu ya kujifunza. Ile itaonyesha kama unamuhangaikia kabisa.
11 Mezali moja inasemaka kama, “Kijiji chote njo kinakomalishaka mutoto.” Sisi pia tunaweza kusema kama, “Kutaniko lote njo linasaidiaka mwanafunzi wa Biblia afikie kuwa mwanafunzi wa Yesu.” Njo maana walimu wazuri wanasaidia wanafunzi wao wajuane na ndugu na dada mu kutaniko. Wale ndugu na dada wanaweza kusaidia mwanafunzi amukaribie Yehova zaidi. Kama mwanafunzi anapitisha wakati pamoja nao, wanaweza kumusaidia atie nguvu urafiki wake pamoja na Yehova, na wanaweza kumusaidia wakati wa magumu. Tunapenda kila mwanafunzi wa Biblia aone kama iko wa maana mu kutaniko na kama iko mu familia yetu ya kiroho. Na tunapenda afurahie upendo wenye kuwa kati ya ndugu na dada mu familia yetu ya kiroho. Ile itafanya ikuwe mwepesi kwake kuachana na marafiki wenye hawamusaidie amupende Yehova. (Mez. 13:20) Atajua kama ikiwa marafiki wake wa zamani wanamukataa anaweza kupata marafiki wazuri mu tengenezo la Yehova.—Mk. 10:29, 30; 1 Pe. 4:4.
TAREHE 27/11–3/12
UTAJIRI WA NENO YA MUNGU | YOBU 20-21
“Haiombe Mutu Akuwe Tajiri Juu Akuwe Mwenye Haki”
w07-SW 1/8 uku. 29 fu. 12
Je, Wewe Ni “Tajiri Kwa Mungu”?
12 Yesu alisema kwamba kuwa tajiri kwa Mungu ni tofauti kabisa na kujiwekea hazina za vitu vya kimwili, au kujitafutia utajiri wa kimwili. Hivyo, Yesu alikuwa akisema kwamba hangaiko letu kuu maishani halipaswi kuwa kukusanya utajiri wa kimwili au kufurahia vitu tulivyo navyo. Badala yake, tunapaswa kutumia mali zetu kwa njia ambayo itaboresha, au kujenga, uhusiano wetu pamoja na Yehova. Tukifanya hivyo, bila shaka tutakuwa matajiri kwa Mungu. Kwa nini? Kwa sababu tutaweza kupata baraka nyingi kutoka kwake. Biblia inatuambia hivi: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Methali 10:22.
Mali ya Kiroho
w95-SW 1/1 uku. 9 fu. 19
Kumshinda Shetani na Kazi Zake
19 Ni jambo la kupendeza kwamba mtumishi wa Mungu Ayubu alilazimika kukabili “mawazo yenye usumbufu” ambayo Shetani aliwasilisha kupitia Elifazi na Sofari. (Ayubu 4:13-18, NW; 20:2, 3) Kwa hiyo Ayubu alipatwa na “uchungu,” uliomfanya aseme ‘maneno ya haraka’ kuhusu “vitisho” vinavyopata akili yake. (Ayubu 6:2-4; 30:15, 16) Elihu alimsikiliza Ayubu kwa ukimya na kumsaidia kwa moyo mweupe aone maoni yenye hekima sana ya Yehova kuhusu mambo. Vilevile leo, wazee wenye ufahamu huonyesha kwamba wao hujali waliopatwa na pigo kwa kutowaongezea “mkazo” watu kama hao. Badala ya kufanya hivyo, kama Elihu, wao huwasikiliza kwa saburi na kisha kutumia mafuta yenye kufariji ya Neno la Mungu. (Ayubu 33:1-3, 7, NW; Yakobo 5:13-15) Hivyo mtu yeyote ambaye hisia zake za moyoni husumbuliwa na masumbufu, yaliyo ya kweli au ya kuwaziwa, au ‘atishikaye katika ndoto na kwa maono’ kama Ayubu alivyokuwa, aweza kupata faraja ya Kimaandiko yenye kutuliza katika kutaniko.—Ayubu 7:14; Yakobo 4:7.
Hotuba: Mungu Anapenda Ukuwe Tajiri?
g-SW 5/09 uku. 12-13
Je, Mungu Anataka Uwe Tajiri?
“Mungu amenipa siku nyingine mpya! Nitakuwa tajiri!”
“Ninataka kuwa tajiri sana kwa sababu Mungu na malaika wote wanataka niwe tajiri sana.”
“Mungu anatupa uwezo wa kupata mali.”
“Ninafanikiwa kwa sababu ya kile Kitabu [Biblia].”
MANENO hayo yanaonyesha maoni ya watu wengi wa kidini ambao husema kwamba mtu hupata mali kwa sababu ya kubarikiwa na Mungu. Wao huhubiri Injili ya kwamba ukifanya yale ambayo Mungu anataka, Mungu atakupa mali wakati huu na pia atakubariki baadaye. Injili hiyo imewavutia watu wengi na vitabu vinavyoiendeleza vinauzwa kwa wingi. Lakini je, “Injili ya ufanisi” inapatana na Biblia?
Kwa kweli, Muumba wetu, ambaye Biblia inamtaja kuwa “Mungu mwenye furaha” anataka tuwe wenye furaha na tufanikiwe maishani. (1 Timotheo 1:11; Zaburi 1:1-3) Isitoshe, yeye huwabariki wale wanaompendeza. (Methali 10:22) Lakini, je, leo baraka hizo zinakuja kupitia kupata mali? Jibu linakuwa wazi ikiwa tunaelewa umuhimu wa nyakati zetu kuhusiana na kusudi la Mungu.
Je, Huu Ni Wakati wa Kutafuta Utajiri?
Nyakati za kale, Yehova Mungu aliwabariki baadhi ya watumishi wake kwa kuwapa mali. Kwa mfano, Mungu aliwabariki Ayubu na Mfalme Sulemani kwa mali. (1 Wafalme 10:23; Ayubu 42:12) Hata hivyo, kuna watu wengi wenye kumwogopa Mungu kama vile Yohana Mbatizaji na Yesu Kristo, ambao hawakuwa na mali. (Marko 1:6; Luka 9:58) Tunajifunza nini kutokana na hilo? Biblia inaonyesha kwamba Mungu hushughulika na watumishi wake kupatana na kusudi lake wakati huo. (Mhubiri 3:1) Tunaweza kutumia kanuni hiyo leo namna gani?
Unabii wa Biblia unaonyesha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo,” au “siku za mwisho” za ulimwengu huu. Kipindi hicho kingekuwa na vita, magonjwa, njaa, matetemeko ya nchi, na kuzorota kwa jamii. Mambo hayo yamekumba wanadamu kwa kiwango kikubwa tangu mwaka wa 1914. (Mathayo 24:3; 2 Timotheo 3:1-5; Luka 21:10, 11; Ufunuo 6:3-8) Kwa ufupi, ulimwengu huu ni kama meli iliyo karibu kuzama! Tunapofikiria mambo hayo, je, lingekuwa jambo la akili kwa Mungu kubariki kila mtumishi wake kwa mali, au Mungu angetaka tutangulize mambo mengine muhimu?
Yesu Kristo alilinganisha nyakati zetu na siku za Noa. Yesu alisema: “Kwa maana kama vile walivyokuwa katika siku hizo kabla ya gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:37-39) Yesu pia alilinganisha siku zetu na siku za Loti. Majirani wa Loti huko Sodoma na Gomora walikuwa ‘wakila, wakinywa, wakinunua, wakiuza, wakipanda, na kujenga.’ “Lakini siku ambayo Loti alitoka Sodoma kulinyesha moto na kiberiti kutoka mbinguni na kuwaangamiza wote,” Yesu aliongezea hivi: “Itakuwa vivyo hivyo siku ile ambayo Mwana wa binadamu atafunuliwa.”—Luka 17:28-30.
Kwa kweli, hakuna ubaya wowote kula, kunywa, kufunga ndoa, kununua, na kuuza. Jambo hatari ni kujihusisha sana na mambo hayo hata tusahau umuhimu wa nyakati tunazoishi. Kwa hiyo jiulize, ‘Je, Mungu angekuwa akitufaidi ikiwa angetubariki kwa kutupa vitu ambavyo vingetukengeusha maishani?’ Badala ya kutufaidi, angekuwa akituhatarisha. Mungu mwenye upendo hatendi kwa njia hiyo!—1 Timotheo 6:17; 1 Yohana 4:8.
Wakati wa Kuokoa Uhai!
Wakati huu muhimu katika historia, watu wa Mungu wana kazi inayopaswa kufanywa haraka. Yesu alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Mashahidi wa Yehova wanachukulia maneno hayo kwa uzito sana. Hivyo, wao huwatia moyo majirani wao wajifunze kuhusu Ufalme na matakwa ya Mungu ya kupata uzima wa milele.—Yohana 17:3.
Hata hivyo, Mungu hataki watumishi wake waaminifu wajinyime raha za maisha. Badala yake, anataka waridhike na mahitaji ya lazima maishani ili wakazie fikira kumtumikia. (Mathayo 6:33) Wanapofanya hivyo, Mungu atahakikisha kwamba wamepata vitu vya kimwili wanavyohitaji. Waebrania 13:5 inasema hivi: “Namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu vya sasa. Kwa maana yeye [Mungu] amesema: ‘Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.’”
Mungu atatimiza ahadi hiyo kwa njia kubwa atakapohifadhi hai “umati mkubwa” wa waabudu wa kweli waokoke mwisho wa mfumo huu wa mambo na kuingia katika ulimwengu mpya wenye amani na ufanisi wa kweli. (Ufunuo 7:9, 14) Yesu alisema: “Mimi nimekuja ili [wafuasi wake waaminifu] wapate kuwa na uzima na wapate kuwa nao kwa wingi.” (Yohana 10:10) ‘Uzima huo mwingi’ si kupata mali nyingi maishani sasa, bali ni uzima usio na mwisho katika Paradiso chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu.—Luka 23:43.
Usikubali kudanganywa na Injili ya ufanisi ambayo kwa kweli ni Injili ya kukengeusha. Badala yake, tii himizo hili la dharura ambalo Yesu alitoa kwa upendo: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.”—Luka 21:34, 35.
TAREHE 4-10/12
UTAJIRI WA NENO YA MUNGU | YOBU 22-24
“Mwanadamu Anaweza Kuwa na Faida kwa Mungu?”
w05-SW 15/9 uku. 27 fu. 1-3
Kataa Mawazo Yasiyofaa!
Wazo la kwamba Mungu ni mwenye kudai mengi mno linahusiana sana na maoni ya kwamba Mungu huona wanadamu kuwa bure kabisa. Hotuba ya tatu ya Elifazi ina swali hili: “Je, mwanamume anaweza kuwa na faida kwa Mungu mwenyewe, kwamba mtu mwenye ufahamu awe na faida kwake?” (Ayubu 22:2) Elifazi alikuwa akimaanisha kwamba Mungu huona mwanadamu kuwa bure kabisa. Vivyo hivyo, Bildadi alisema hivi: “Mwanadamu anayeweza kufa anawezaje kuwa upande wa haki mbele za Mungu, au, mtu aliyezaliwa na mwanamke anawezaje kuwa safi?” (Ayubu 25:4) Kulingana na maoni hayo, Ayubu, mwanadamu duni anayeweza kufa, angewezaje kudai kuwa mwadilifu mbele za Mungu?
Watu fulani leo wanajiona kuwa hawafai. Huenda wanahisi hivyo kwa sababu ya malezi yao, matatizo ya maisha, au kwa sababu ya chuki kuelekea jamii au kabila lao. Lakini Shetani na roho wake waovu pia wanafurahia kumfanya mtu ahisi kwamba hafai. Wanapomfanya ahisi kwamba Mungu Mweza-Yote hafurahii chochote anachofanya, inakuwa rahisi sana kwa mtu huyo kuvunjika moyo. Baada ya muda, mtu huyo anaweza kupeperushwa, na hata kujiondoa kwa Mungu aliye hai.—Waebrania 2:1; 3:12.
Uzee na magonjwa hutuwekea vizuizi. Huenda ikaonekana tunatimiza tu sehemu ndogo sana katika utumishi wa Ufalme tukilinganisha na yale tuliyofanya tulipokuwa vijana wenye nguvu na afya nzuri. Ni muhimu kutambua kwamba Shetani na roho wake waovu wanataka tuhisi kwamba Mungu hafurahii yale tunayofanya. Tunapaswa kukataa kufikiri kwa namna hiyo.
w95-SW 15/2 uku. 27 fu. 6
Somo la Jinsi ya Kushughulika na Matatizo
Waandamani wake watatu walimvunja moyo Ayubu hata zaidi kwa kusema mawazo yao ya kibinafsi badala ya hekima ya kimungu. Elifazi hata alifikia hatua ya kusema kwamba ‘Mungu hana imani katika watumishi wake’ na kwamba kwa kweli ilikuwa mamoja kwa Yehova iwe Ayubu alikuwa mwadilifu au la. (Ayubu 4:18; 22:2, 3, NW) Ni vigumu kuwazia maneno yenye kuvunja moyo—au yaliyo ya uongo zaidi—kuliko hayo! Haishangazi kwamba baadaye Yehova aliwakemea Elifazi na waandamani wake kwa ukufuru huo. “Ninyi hamkunena yaliyo sawa katika habari zangu,” yeye akasema. (Ayubu 42:7) Lakini dai lenye madhara zaidi lilikuwa lije bado.
w03-SW 15/4 uku. 14-15 fu. 10-12
Vijana Wanaofurahisha Moyo wa Yehova
10 Kama Biblia inavyoonyesha, Shetani alitilia shaka uaminifu wa Ayubu na pia wengine wote wanaomtumikia Mungu, kutia ndani wewe. Naam, Shetani alimwambia Yehova hivi alipokuwa akizungumza kuwahusu wanadamu kwa ujumla: “Yote aliyo nayo mtu [si Ayubu tu bali mtu yeyote] atayatoa kwa ajili ya uhai wake.” (Ayubu 2:4) Je, unaona jinsi unavyohusika katika suala hilo muhimu? Kama inavyoonyeshwa na Mithali 27:11, Yehova anasema kwamba unaweza kumpa msingi wa kumjibu Shetani anayemlaumu. Wazia Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu anakusihi wewe utoe jibu kuhusiana na suala kuu lililopo. Hilo ni daraka na pendeleo kubwa sana. Je, unaweza kutimiza yale ambayo Yehova anakusihi ufanye? Ayubu aliyatimiza. (Ayubu 2:9, 10) Ndivyo alivyofanya Yesu na vilevile wengine wengi tangu zamani, kutia ndani vijana. (Wafilipi 2:8; Ufunuo 6:9) Unaweza kufanya vivyo hivyo. Hata hivyo, unapaswa kujua kwamba ni lazima uunge mkono upande mmoja katika suala hilo. Kupitia mwenendo wako utaonyesha kwamba unatetea lawama ya Shetani au jibu la Yehova. Utatetea nini?
Yehova Anakujali!
11 Je, uchaguzi wako ni muhimu machoni pa Yehova? Je, uaminifu ambao watu wengi wameonyesha hautoshi kumpa sababu ya kumjibu Shetani? Ibilisi alidai kwamba hakuna mtu anayemtumikia Yehova kwa sababu ya kumpenda, dai ambalo limekwisha thibitishwa kuwa la uwongo. Lakini bado Yehova anataka uunge mkono upande wake katika suala la enzi kuu kwa sababu anakujali. Yesu alisema hivi: “Si jambo la kutamanika kwa Baba yangu aliye mbinguni kwa mmoja wa wadogo hawa kuangamia.”—Mathayo 18:14.
12 Ni wazi kwamba, Yehova anapendezwa na uchaguzi wako. Jambo muhimu zaidi ni kwamba anaathiriwa nao. Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova ana hisia ambazo huchochewa na mwenendo mzuri au mbaya wa binadamu. Kwa mfano, Yehova ‘alihuzunika,’ Waisraeli walipomwasi tena na tena. (Zaburi 78:40, 41) Kabla ya Gharika ya siku za Noa, wakati ‘maovu ya mwanadamu yalipokuwa makubwa,’ Yehova ‘alihuzunika moyo.’ (Mwanzo 6:5, 6) Fikiria maana ya jambo hilo. Ukiamua kuwa na mwenendo mbaya, utamhuzunisha Muumba wako. Hiyo haimaanishi kwamba Mungu ni dhaifu au anaongozwa na hisia tu. Badala yake anakupenda na kukujali. Kwa upande mwingine, unapofanya yanayofaa unafurahisha moyo wa Yehova. Yeye hufurahi kwa sababu anapata sababu nyingine ya kumjibu Shetani, na pia kwa sababu anaweza kukupa thawabu. Ndivyo anavyotaka kufanya. (Waebrania 11:6) Yehova Mungu ni Baba mwenye upendo kama nini!
Mali ya Kiroho
w04-SW 15/7 uku. 21-22
Tumia Miradi ya Kiroho ili Kumtukuza Muumba Wako
Fikiria jinsi Yehova alivyotimiza kazi ya kuumba ulimwengu ambayo inatia ndani kusudi lake la kuumba dunia. Maneno, “ikawa jioni, ikawa asubuhi,” yanaonyesha kwamba Yehova ndiye aliamua urefu wa vipindi vya uumbaji. (Mwanzo 1:5, 8, 13, 19, 23, 31) Mwanzoni mwa kila kipindi cha uumbaji, alijua waziwazi mradi au kusudi lake kwa siku hiyo ya uumbaji. Naye Mungu akatimiza kusudi lake la kuumba vitu. (Ufunuo 4:11) ‘Nafsi ya Yehova mwenyewe ina tamaa, naye ataifanya,’ akasema mzee wa ukoo Ayubu. (Ayubu 23:13) Yehova alifurahi kama nini kuona “kila kitu alichokuwa amefanya” na kukitangaza kuwa “chema sana”!—Mwanzo 1:31.
Ili tutimize miradi yetu, sisi pia tunapaswa kuwa na tamaa kuu ya kuifikia. Ni nini kitakachotusaidia kukuza tamaa hiyo kuu? Hata wakati dunia ilipokuwa bila umbo, na ukiwa, Yehova angeweza kuona kimbele jinsi ambavyo ingekuwa baadaye—johari maridadi katika anga ambayo ingemletea heshima na utukufu. Vivyo hivyo, tamaa yetu ya kutimiza yale ambayo tumeazimia kufanya inaweza kukuzwa kwa kutafakari matokeo na manufaa ya kutimizwa kwa mradi huo. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kuhusiana na Tony, mwenye umri wa miaka 19. Hakusahau kamwe kile kilichomvutia alipotembelea ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Ulaya Magharibi. Tangu wakati huo na kuendelea, Tony alikuwa akifikiria swali hili: ‘Mtu huhisije anapoishi na kutumika mahali kama hapa?’ Tony hakuacha kamwe kufikiria uwezekano wa kutumika Betheli, naye aliendelea kujitahidi kufikia mradi huo. Alifurahi sana wakati miaka kadhaa baadaye ombi lake la kutumika kwenye ofisi ya tawi lilipokubaliwa.
Hotuba: Kama Tuko na Mawazo ya Muzuri Yehova Ataendelea Kututumikisha
Endelea Kuwa na Mawazo ya Muzuri juu ya Mahubiri
17 Yesu aliendelea kuwa na mawazo ya muzuri na aliendelea kuhubiri hata kama watu fulani hawakupenda kusikiliza ujumbe wake. Juu ya nini? Alijua kama watu walikuwa na lazima ya kujifunza kweli, na alipenda kusaidia watu wengi kadiri inawezekana. Alijua pia kama watu fulani wangekatala ujumbe wake ku mwanzo lakini wangefikia kuukubali. Fikiria mambo yenye ilimufikia Yesu mu familia yake. Katika utumishi wake wenye ulifanya miaka tatu na nusu hakuna hata ndugu yake mumoja mwenye alifikia kuwa mwanafunzi wake. (Yoh. 7:5) Lakini kisha ufufuo wake, walifikia kuwa Wakristo.—Mdo. 1:14.
18 Kusema kweli, hatujue ni nani mwenye anaweza kufikia kuwa mutumishi wa Yehova. Kwa watu fulani inaomba wakati mingi ili wajifunze kweli. Hata wale wenye hawapende kutusikiliza wanaweza kuona kama tuko na mwenendo wa muzuri na mawazo ya muzuri, na pengine ile inaweza kuwafanya “wamutukuze Mungu.”—1 Pe. 2:12.
19 Hata kama tunapanda na kutia maji, tunapaswa kukumbuka kama Mungu njo anakomalishaka. (Soma 1 Wakorinto 3:6, 7.) Ndugu Getahun, mwenye anatumikia Etiopia, anasema hivi: “Kwa zaidi ya miaka 20, ni miye tu njo nilikuwa Shahidi wa Yehova mu eneo kwenye niliishi. Lakini sasa kuko wahubiri 14. Wahubiri 13 walibatizwa, kutia ndani bibi yangu na watoto wangu watatu. Ku mikutano tunakuwaka watu 32 hivi.” Getahun anafurahi juu aliendelea kuhubiri na aliendelea kuvumilia ili Yehova avute wale wenye moyo muzuri mu tengenenzo Lake!—Yoh. 6:44.
20 Yehova anaona watu wote kuwa wa maana sana. Anatupatia pendeleo la kutumika pamoja na Mwana wake ili kukusanya watu kutoka mu mataifa yote mbele mwisho ufike. (Hag. 2:7) Kazi yetu ya kuhubiri inafanana na kazi ya kuokoa. Na tuko sawa vile kikundi ya watu wenye kuokoa wale wenye kuwa mu mashua yenye ilishazama. Hata kama wote hawatapata watu wa kuokoa, lakini wote watakuwa wamefanya kazi ya maana sana. Ni vile pia na kazi yetu ya kuhubiri. Hatujue ni watu wangapi wenye wataokoka mu ulimwengu wa Shetani. Lakini Yehova anaweza kutumikisha mutu yeyote kati yetu ili kuwasaidia. Andreas, mwenye kuishi Bolivie, anasema hivi: “Najua kama wakati mutu anajifunza kweli na anafikia kubatizwa ni juu watu wengi walitumika pamoja ili kumusaidia.” Tuendelee basi kuwa na mawazo ya vile kuhusu kazi yetu ya kuhubiri. Tukifanya vile Yehova atatubariki, na kazi yetu ya kuhubiri itatuletea furaha mingi.
TAREHE 11-17/12
UTAJIRI WA NENO YA MUNGU | YOBU 25-27
“Unaweza Kuwa Muaminifu-Mushikamanifu Hata Kama Haukamilike”
it-1-F 1194 fu. 5
Uaminifu-Mushikamanifu
Yobu. Yobu, mwenye bila shaka aliishi mu kipindi yenye ilikuwa kati ya kifo ya Yosefu na wakati wa Musa, anazungumuziwa kuwa mwanaume “mwenye hana lawama [mu kiebrania, tam] na munyoofu, alikuwa anamuogopa Mungu na kuepuka mambo ya mubaya.” (Yob 1:1, na maelezo ya chini; ona YOBU.) Uaminifu-mushikamanifu wa wanadamu ni kati ya mambo yenye Shetani alishakia wakati alipinga haki ya Yehova ya kutawala. Ile inaonekana wazi kupitia maulizo yenye Yehova aliuliza Adui yake Shetani kuhusu Yobu, wakati ule adui aliingia mu mukutano wa malaika mbinguni. Shetani alimusingizia Yobu kama alikuwa anamutumikia Mungu na nia ya mubaya. Alisema kama ikiwa Yobu alimutumikia Mungu haikuwa juu alipenda kabisa kufanya vile, lakini ni juu tu ya faida yake. Kwa kusema vile, alishakia uaminifu-mushikamanifu wa Yobu kwa Mungu. Kisha kuruhusiwa kumupotezea Yobu mali yake na hata watoto wake, Shetani alishindwa kuharibu uaminifu-mushikamanifu wa Yobu. (Yob 1:6–2:3) Kisha, Shetani alisema kama ikiwa Yobu aliendelea kuvumilia, hata kama alipoteza mali na watoto wake, ni juu alikuwa angali na uzima wake. (Yob 2:4, 5) Kisha Shetani akamupiga kwa ugonjwa mubaya sana. Tena, bibi yake akaanza kumuambia amulaani Mungu, na marafiki wake wakaanza kumusema mubaya na kusema mubaya juu ya kanuni za Yehova na makusudi yake. (Yob 2:6-13; 22:1, 5-11) Hata vile, Yobu aliendelea kuwa muaminifu-mushikamanifu. Alisema hivi: “Mupaka wakati nitakufa, sitaacha uaminifu-mushikamanifu wangu! Nitaendelea kutenda haki na sitaiacha hata kidogo; moyo wangu hautanihukumu wakati wote wenye nitakuwa muzima.” (Yob 27:5, 6) Uaminifu-mushikamanifu wa Yobu ulionyesha kama Shetani alisema uongo.
Endelea Kuwa Muaminifu-Mushikamanifu!
3 Wakati neno uaminifu-mushikamanifu linatumiwa juu yetu sisi watumishi wa Mungu, linamaanisha kumupenda Yehova kwa moyo wote na kujitoa kwake kwa moyo wote, na hilo linatuchochea kutia mapenzi yake pa nafasi ya kwanza katika maamuzi yetu yote. Tuchunguze habari fulani juu ya namna neno uaminifu-mushikamanifu linatumiwa mu Biblia. Maana ya kwanza ya neno la Biblia lenye kutafsiriwa “uaminifu-mushikamanifu,” ni kuwa kamili, bila kasoro, ao muzima. Kwa mufano, Waisraeli walikuwa wanamutolea Yehova zabihu za wanyama, na Sheria ilisema kama wanyama hao walipaswa kuwa bila kasoro. (Law. 22:21, 22) Watu wa Mungu hawakuruhusiwa kutoa munyama mwenye alikuwa anakosa muguu, sikio, ao jicho; na hawangepaswa kutoa munyama mwenye kuwa mugonjwa. Yehova aliona kama ni jambo la maana munyama wa zabihu akuwe kamili, bila kasoro, ao muzima. (Mal. 1:6-9) Tunaweza kuelewa juu ya nini Yehova anapendezwa na kitu chenye hakina kasoro ao chenye kuwa kamili. Kwa mufano, wakati tunauza kitu fulani kama vile tunda, kitabu, ao kifaa fulani, hatupendi kile chenye kuwa na matundu ao chenye kukosa sehemu fulani. Tunapenda kitu chenye kuwa kamili, chenye hakina kasoro, ao chenye kuwa kizima. Yehova naye anataka upendo na ushikamanifu wenye tunamuonyesha ukuwe vile; unapaswa kuwa kamili, bila kasoro, ao muzima.
4 Je, tunapaswa kuwaza kama ni lazima tukuwe wakamilifu ili tukuwe waaminifu-washikamanifu? Kwa kweli, tunaweza kuona kama tunafanyaka makosa mingi. Fikiria sababu mbili zenye zinaweza kutufanya tusiwaze kama tunapaswa kuwa wakamilifu ili tukuwe waaminifu-washikamanifu. Kwanza, Yehova hakazie akili makosa yetu. Neno lake linatuambia hivi: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, basi ni nani, Ee Yehova, angeweza kusimama?” (Zb. 130:3) Anajua kama hatuko wakamilifu, tuko wanadamu watenda-zambi, na iko tayari kutusamehe. (Zb. 86:5) Pili, Yehova anajua mipaka yetu, na hatuombe tufanye mambo yenye kupita uwezo wetu. (Soma Zaburi 103:12-14.) Kwa hiyo, ni katika maana gani tunaweza kuwa kamili, bila kasoro, ao wazima mu macho yake?
5 Upendo unasaidia watumishi wa Yehova wakuwe waaminifu-washikamanifu. Upendo wetu na ushikamanifu wetu kwa Mungu, Baba yetu wa mbinguni, unapaswa kuendelea kuwa kamili, bila kasoro, ao muzima. Kama upendo wetu unabakia vile hata wakati tunajaribiwa, hilo linaonyesha kama tuko waaminifu-washikamanifu. (1 Ny. 28:9; Mt. 22:37) Tufikirie tena wale Mashahidi tatu wenye tulizungumuzia ku mwanzo wa habari hii. Juu ya nini walitenda vile? Je, ule kijana mwanamuke hapendake kujifurahisha ku masomo? Ao ule kijana mwanaume anapenda kupatishwa haya ku mulango? Ao ule mwanaume mwenye kuwa na familia anapenda kupoteza kazi yake? Hapana. Lakini, wanajua kama kanuni za Yehova ni za haki, na wanakaza akili yao juu ya mambo yenye kumufurahisha Baba yao wa mbinguni. Upendo wao kwake unawachochea kumutia pa nafasi ya kwanza katika maamuzi yenye wanakamata. Kwa kufanya vile, wanaonyesha kama wako waaminifu-washikamanifu.
Mali ya Kiroho
Tumepangwa Kupatana na Neno la Mungu
3 Wakati tunaangalia vitu vyenye Yehova aliumba, tunaona wazi kuwa yeye ni Mungu mwenye kupanga mambo muzuri. ‘Aliuweka musingi wa dunia. Aliziweka mbingu imara kwa utambuzi.’ (Methali 3:19) Kuko mambo mengi yenye hatujue juu ya vitu vyenye Yehova aliumba. Kwa kweli, ni ‘munongono [mambo madogo sana] ulioje wa jambo lililosikiwa juu yake.’ (Ayubu 26:14) Lakini mambo madogo yenye tunajua juu ya ulimwengu yanaonyesha wazi kama ni wenye kupangwa muzuri sana. (Zaburi 8:3, 4) Mamilioni ya nyota zinatembea katika anga kwa njia yenye kupangwa muzuri. Pia, fikiria namna sayari (planètes) zenye kuwa katika mufumo wa jua zinazunguka-zunguka jua. Utaratibu huo unawezekana tu kwa sababu Yehova amepanga namna sayari na nyota zinazunguka. Wakati tunafikiria namna ‘amezifanya mbingu kwa uelewaji’ na dunia pia, tunapenda kumusifu, kumuabudu, na kuwa washikamanifu kwake.—Zaburi 136:1, 5-9.
TAREHE 18-24/12
UTAJIRI WA NENO YA MUNGU | YOBU 28-29
“Unajulikana Kuwa Mutu Muzuri Sawa Vile Yobu?”
w02-SW 15/5 uku. 22 fu. 19
Waonyeshe Fadhili-upendo Wenye Uhitaji
19 Masimulizi ya Biblia tuliyozungumzia pia yanakazia kwamba fadhili-upendo zinapaswa kuonyeshwa wale ambao hawawezi kujitimizia mahitaji yao. Abrahamu alihitaji msaada wa Bethueli ili kuendeleza ukoo wake. Naye Yakobo alihitaji msaada wa Yosefu ili mwili wake upelekwe Kanaani. Naomi pia alihitaji msaada wa Ruthu ili kupata mrithi. Abrahamu, Yakobo, na Naomi hawangeweza kutimiza mahitaji yao bila kusaidiwa. Vivyo hivyo leo, fadhili-upendo zinapaswa hasa kuonyeshwa wale wenye uhitaji. (Mithali 19:17) Tunapaswa kumwiga mzee wa ukoo Yobu, ambaye alijali ‘maskini aliyelilia msaada, yatima asiyekuwa na wa kumsaidia’ na pia wale “waliokuwa karibu kuangamia.” Yobu pia ‘aliwafanya wajane waone tena furaha moyoni’ na akawa ‘macho kwa kipofu na miguu kwa viwete.’—Ayubu 29:12-15, BHN.
it-2 uku. 1144 fu. 10
Manguo
Manguo inatumiwa juu ya kufananisha mambo ingine mingi mbalimbali. Vile uniforme ao nguo fulani ya pekee inatambulishaka mwenye kuivala, ni vile pia mu Biblia manguo inatumiwa mu njia ya mufano juu ya kutambulisha mutu ao kuonyesha musimamo wake na mambo yenye iko anafanya yenye inapatana na ule musimamo. Ni vile njo mufano wa Yesu wa nguo ya ndoa unaonyesha. (Mt 22:11, 12; ona NGUO YA KICHWA; VIATU.) Mu Ufunuo 16:14, 15, Bwana Yesu, alionya wanafunzi wake wasilale kiroho na kufikia kupoteza utambulisho wao wa Kikristo. Ile inaweza kuwa mubaya sana juu “siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote” inakaribia sana.
w09-SW 1/2 uku. 15 fu. 3-4
Majina Yana Maana
Hatukujichagulia majina tuliyopewa tulipozaliwa. Hata hivyo, sisi wenyewe ndio tunaoamua tutakuwa na sifa gani. (Methali 20:11) Hebu jiulize: ‘Yesu na mitume wangenichagulia jina gani ikiwa wangepewa nafasi ya kufanya hivyo? Ni jina gani ambalo lingeeleza vizuri sifa yangu kuu?’
Tunapaswa kufikiria swali hilo kwa uzito. Kwa nini? “Ni afadhali kuchagua jina badala ya utajiri mwingi,” akaandika Mfalme Sulemani mwenye hekima. (Methali 22:1) Kwa kweli, tukijipatia jina zuri, au sifa nzuri katika jamii, tumepata kitu cha thamani. Hata hivyo, jambo muhimu zaidi ni kwamba tukijifanyia jina zuri mbele za Mungu, tutapata hazina ya kudumu. Jinsi gani? Mungu anaahidi kwamba ataandika katika “kitabu cha kumbukumbu” majina ya wale wanaomwogopa, na atawapa uzima wa milele.—Malaki 3:16; Ufunuo 3:5; 20:12-15.
Mali ya Kiroho
g00-SW 8/7 uku. 11 fu. 3
Tabasamu Ni Yenye Manufaa Kwako!
Je, kweli kutabasamu hubadili hali ya mambo? Je, wakumbuka wakati tabasamu ya mtu fulani ilipokufanya uhisi kitulizo au kukufanya uhisi umestarehe? Au mtu alipokosa kutabasamu kukakufanya uwe na wasiwasi au hata kuhisi umepuuzwa? Naam, tabasamu hubadili hali ya mambo. Huwa na matokeo kwa yule anayetabasamu na yule ambaye ameonyeshwa tabasamu. Yobu, anayetajwa katika Biblia alisema hivi kuhusu adui zake: “Kama nikiwacheka [“nikatabasamu nao,” NW] hawakuamini; wala hawakuangusha nuru ya uso wangu.” (Ayubu 29:24, Zaire Swahili Bible) “Nuru” ya uso wa Yobu huenda ilirejezea furaha au uchangamfu.
TAREHE 25-31/12
UTAJIRI WA NENO YA MUNGU | YOBU 30-31
“Namna Yobu Aliendelea Kuwa na Mwenendo Safi”
w10-SW 15/4 uku. 21 fu. 8
Usiruhusu Macho Yako Yaone Mambo Yasiyofaa!
8 Tamaa ya macho na ya mwili inaweza pia kuwa na uvutano mbaya juu ya Wakristo wa kweli. Kwa hiyo, Neno la Mungu linatutia moyo tujitie nidhamu kuhusu mambo tunayoona na kutamani. (1 Kor. 9:25, 27; soma 1 Yohana 2:15-17.) Mwanamume mwadilifu Ayubu alitambua kwamba kuna uhusiano wenye nguvu kati ya kuona na kutamani. Alisema hivi: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu. Basi nawezaje kukaza fikira kwa bikira?” (Ayu. 31:1) Ayubu hakukataa tu kumgusa mwanamke kwa njia potovu lakini hangeruhusu hata akili yake ifikirie jambo kama hilo. Yesu alikazia kwamba ni lazima tulinde akili zetu kutokana na mawazo mapotovu aliposema hivi: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mt. 5:28.
w08-SW 1/9 uku. 11 fu. 4
Fikiria ‘Mwisho Baadaye’
Kabla ya kuchukua hatua ya kwanza kufuata barabara yenye ishara “Usiingie,” jiulize, ‘Inanielekeza wapi?’ Kufikiria jinsi ‘mwisho baadaye’ unavyoweza kuwa kunatosha kukuzuia usifuate njia inayoweza kuwa na matokeo mabaya. UKIMWI na magonjwa mengine ya zinaa, mimba zisizotakikana, utoaji-mimba, mahusiano yaliyoharibika, na dhamiri zilizochafuka ni matokeo mabaya yanayowapata wale wanaopuuza ishara hizo. Mwisho wa barabara kwa wanaojihusisha katika ukosefu wa maadili unaelezwa waziwazi na mtume Paulo. “Hawataurithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10.
w10-SW 15/11 uku. 6 fu. 15-16
Vijana—Mwongozwe na Neno la Mungu
15 Unafikiri ushikamanifu wako kwa Mungu utajaribiwa zaidi wakati gani—je, ni wakati unapokuwa na wengine au unapokuwa peke yako? Ni kweli kwamba unapokuwa shuleni au kazini, inaelekea kwamba ulinzi wako wa kiroho unakuwa imara. Unakuwa macho kuona hatari yoyote ya kiroho. Lakini unapostarehe na kuacha kujilinda ndipo unapokuwa katika hatari kubwa zaidi ya kushambuliwa kiadili.
16 Kwa nini unapaswa kumtii Yehova hata unapokuwa peke yako? Kumbuka jambo hili: Unaweza kuumiza hisia za Yehova au kuufanya moyo wake ushangilie. (Mwa. 6:5, 6; Met. 27:11) Yehova anafurahishwa au kuumizwa na matendo yako kwa sababu ‘anakujali.’ (1 Pet. 5:7) Anataka umsikilize ili ujifaidi mwenyewe. (Isa. 48:17, 18) Watumishi fulani wa Yehova katika Israeli la kale walipopuuza mashauri yake, walimfanya ahisi uchungu. (Zab. 78:40, 41) Kwa upande mwingine, Yehova alimpenda sana nabii Danieli, kwa kuwa malaika alimwita “mtu mwenye kutamanika sana.” (Dan. 10:11) Kwa nini? Kwa sababu Danieli aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu si mbele ya watu tu bali pia akiwa peke yake.—Soma Danieli 6:10.
Mali ya Kiroho
w05-SW 15/11 uku. 11 fu. 3
Ustadi wa Kusikiliza kwa Upendo
Waandamani wa Ayubu walisikiliza angalau hotuba zake kumi. Na bado, Ayubu alisema hivi: “Laiti ningekuwa na mtu wa kunisikiliza!” (Ayubu 31:35) Kwa nini alisema hivyo? Kwa sababu kusikiliza kwao hakukumfariji. Hawakumjali Ayubu wala hawakutaka kuelewa hisia zake. Kwa kweli, hawakuwa na hisia-mwenzi kama wasikilizaji wenye huruma. Mtume Petro anashauri hivi: “Ninyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo, wanyenyekevu katika akili.” (1 Petro 3:8) Tunaweza kuonyeshaje hisia-mwenzi? Njia moja ni kwa kujali hisia za yule mtu mwingine na kujitahidi kumwelewa. Tunaweza kuonyesha kwamba tunajali kwa kusema maneno yenye huruma kama vile “haikosi kuwa uliumia sana” au “haikosi ulihisi kwamba hukueleweka.” Njia nyingine ni kusema kwa maneno yako mwenyewe mambo ambayo mtu huyo anakwambia. Hilo linaonyesha kwamba umeelewa yale anayosema. Kusikiliza kwa upendo kunamaanisha kusikiliza maneno na hata hisia zinazowasilishwa.
Hotuba: Kichwa: Namna Gani Naweza Kufasiria Mawazo ya Biblia Kuhusu Homosexualité?
Biblia Inasema Nini Juu ya Mwanaume Kulala na Mwanaume ao Mwanamuke Kulala na Mwanamuke?
Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?
Mashahidi wa Yehova waamini kwamba kanuni za Biblia kuhusu mwenendo ni za maana zaidi katika maisha, na wako tayari kuishi kulingana na kanuni hizo. (Isaya 48:17) Hilo linamaanisha kwamba Mashahidi wa Yehova wanakataa matendo yote mabaya kuhusu ngono, kama vile wanaume kulala na wanaume ao wanawake kulala na wanawake. (1 Wakorintho 6:18) Mashahidi wa Yehova wamechagua kuishi maisha ya namna hiyo, na wako na haki ya kufanya hivyo.
Lakini, Mashahidi wa Yehova wanajikaza pia ‘kufuatilia amani pamoja na watu wote.’ (Waebrania 12:14) Hata kama Mashahidi wa Yehova wanakataa kabisa matendo ya mwanaume kulala na mwanaume ao mwanamuke kulala na mwanamuke, hawakaze wengine wakuwe na mawazo yao. Tena hawajiunge na watu wenye kutesa na kuchukia watu hao ao kufurahi wakati watu hao wanatendewa hivyo. Mashahidi wa Yehova wanajikaza kutendea wengine namna wanapenda wawatendee pia.—Mathayo 7:12.
Biblia Inaunga Mukono Ubaguzi?
Watu fulani wanaweza kusema kwamba Biblia inaunga mukono kuonyesha ubaguzi wanaume wenye kulala na wanaume ao kuonyesha ubaguzi wanawake wenye kulala na wanawake, na kwamba watu wenye wanafuata mambo yenye Biblia inasema hawavumilie wengine. Wanaweza kufikiri hivi: ‘Biblia iliandikwa wakati watu walikuwa hawajafunguka akili. Leo, tunakubali watu wa kila rangi ya ngozi, watu wa kila inchi, na maamuzi ya watu kuhusu ngono.’ Watu hao wanawaza kama kuchukia tendo la wanaume kulala na wanaume ao wanawake kulala na wanawake ni kama kuchukia watu wa rangi ingine ya ngozi. Mawazo yao ni yenye kufaa? Hapana. Sababu gani?
Kwa sababu kuchukia tendo la wanaume kulala na wanaume ao wanawake kulala na wanawake ni tofauti na kuchukia watu wenye kufanya hivyo. Biblia inaomba Wakristo waheshimie watu wa namna zote. (1 Petro 2:17) Lakini, hilo halimaanishe kwamba Wakristo wanapaswa kukubali mwenendo wowote.
Tufikirie mufano huu: Wazia kama unaona kuvuta tumbako ni hatari kwa afya na hata kwamba ni tendo lenye kuchukiza. Utafanya nini kama mufanyakazi mwenzako anavutaka tumbako? Atakuona kuwa hauna akili yenye kufunguka kwa sababu tu mawazo yako juu ya tumbako ni tofauti na yake? Kuwa na mawazo tofauti na yake juu ya kuvuta tumbako kunamaanisha mara moja tu kwamba unamuonyesha ubaguzi? Kama mufanyakazi mwenzako anakuomba ubadilishe mawazo yako juu ya tumbako, hauone kwamba hilo litamufanya akuwe na akili yenye haifunguke na mwenye havumilie wengine?
Mashahidi wa Yehova wanachagua kuishi kulingana na kanuni zenye kuwa katika Biblia. Hawakubali matendo yenye Biblia inakataza. Lakini, hawazarau ao kutendea mubaya watu wenye kuwa na matendo tofauti na yao.
Mawazo ya Biblia Ni Yenye Kupita Mipaka?
Tuseme nini juu ya wanaume wenye kuwa na tamaa ya kulala na wanaume ao wanawake wenye kuwa na tamaa ya kulala na wanawake? Walizaliwa hivyo? Kama walizaliwa hivyo, haitakuwa kuvuka mipaka kusema kwamba wanafanya mubaya kwa sababu wanatenda kulingana na tamaa yao?
Biblia haiseme kwamba wanaume wenye kulala na wanaume ao wanawake wenye kulala na wanawake walizaliwa na tabia hiyo ao hapana, lakini inakubali kwamba tabia fulani za watu zimetia mizizi ndani yao. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba tunapaswa kuepuka matendo fulani, kama vile mwanaume kulala na mwanaume ao mwanamuke kulala na mwanamuke, ikiwa tunataka kumupendeza Mungu.—2 Wakorintho 10:4, 5.
Watu fulani wanaweza kusema kama mawazo ya Biblia yanapita mipaka. Wanawaza kama tunapaswa kutenda kupatana na tamaa zetu ao kama tamaa zetu za kufanya kitendo cha ndoa ni zenye nguvu sana, na kwa hiyo hatupaswe kuzizuia na hata hatuwezi kuzizuia. Lakini, Biblia inawasifu watu kwa kusema kwamba wako na uwezo wa kuzuia tamaa yao. Tofauti na wanyama, watu wanaweza kuchagua kama watatenda kulingana na tamaa yao ao hapana.—Wakolosai 3:5.
Fikiria mufano huu: Watu fulani wenye elimu wanasema kwamba watu wanaweza kuzaliwa na tabia fulani kama vile kuonyesha hasira. Biblia haionyeshe kama watu wenye kuwa na tabia ya kuonyesha hasira walizaliwa hivyo ao hapana, lakini inaonyesha kwamba watu fulani ni ‘wenye hasira’ na kwamba wako na ‘mwelekeo wa gazabu.’ (Methali 22:24; 29:22) Lakini, Biblia inasema pia hivi: ‘Acha hasira na uache gazabu.’ —Zaburi 37:8; Waefeso 4:31.
Ni watu kidogo tu ndio wanaweza kukataa shauri hilo ao kusema kwamba shauri hilo linavuka mipaka kuhusu watu wenye kuwa na mwelekeo wa kuonyesha hasira. Lakini, hata watu wenye elimu wenye wanawaza kwamba hasira imetia mizizi ndani ya chembe za uriti za mutu fulani, wanajikaza sana ili kumusaidia azuie tabia hiyo.
Mashahidi wa Yehova wanafanya hivyo pia kuhusu mwenendo wowote wenye kupingana na kanuni za Biblia, kama vile mwanaume kulala na mwanamuke bila kuoana. Katika hali hizo zote, shauri hili la Biblia linafaa: ‘Kila mumoja wenu ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono.’—1 Wathesalonike 4:4, 5.
‘Wengine Wenu Mulikuwa Hivyo’
Wakati wa mitume, watu wenye walitaka kuwa Wakristo walikuwa na tabia na hali mbalimbali za maisha, na watu fulani kati yao walifanya mabadiliko makubwa katika maisha yao. Kwa mufano, kisha kuzungumuzia ‘waasherati, waabudu-sanamu, wazinzi, wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili,’ Biblia inasema tena hivi: ‘Wengine wenu mulikuwa hivyo.’—1 Wakorintho 6:9-11.
Wakati Biblia inasema ‘wengine wenu mulikuwa hivyo,’ inamaanisha kwamba wanaume wenye waliacha kulala na wanaume ao wanawake wenye waliacha kulala na wanawake hawakusikia tena tamaa ya kufanya hivyo? Inaweza kuwa nguvu kuwaza hivyo, kwa sababu Biblia inasema hivi: ‘Muendelee kutembea kwa roho nanyi hamutatenda tamaa ya kimwili hata kidogo.’—Wagalatia 5:16.
Biblia haiseme kama Mukristo haiwezi kusikia tamaa ya mubaya hata kidogo. Lakini, inasema kama Mukristo hapaswe kutenda kulingana na tamaa hiyo. Wakristo wanajifunza kuzuia tamaa kama hiyo; hawaendelee kuwaza juu ya tamaa hiyo mupaka kufikia kuitimiza.—Yakobo 1:14, 15.
Biblia inaonyesha tofauti kati ya mwelekeo ao tamaa ya kufanya jambo fulani na kufanya jambo hilo. (Waroma 7:16-25) Mwanaume mwenye kuwa na mwelekeo wa kulala na mwanaume ao mwanamuke mwenye kuwa na mwelekeo wa kulala na mwanamuke anaweza kuzuia jambo lenye akili yake inafikiria sana, kama vile tu anaweza kuzuia kila tamaa ya mubaya, kutia ndani mwelekeo wa kukasirika, kufanya uzinifu, na kuwa na pupa.—1 Wakorintho 9:27; 2 Petro 2:14, 15.
Hata kama Mashahidi wa Yehova wanaunga mukono kanuni za Biblia, hawakaze wengine wakuwe na mawazo yao. Tena hawajaribu kubadilisha sheria zenye kulinda haki ya watu wenye kuwa na mawazo tofauti na yao. Mashahidi wa Yehova wanatangaza ujumbe muzuri, na wako na tamaa ya kutangazia kila mutu mwenye kuwa tayari kusikiliza ujumbe huo.—Matendo 20:20.