-
Wazee, Munaona Namna Gani Kazi ya Kuzoeza Wengine?Munara wa Mulinzi—2015 | Mwezi wa 4 15
-
-
Wazee, Munaona Namna Gani Kazi ya Kuzoeza Wengine?
“Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.” —MHU. 3:1.
1, 2. Waangalizi wengi wa muzunguko wameona hali gani katika makutaniko mengi?
MWANGALIZI wa muzunguko anakaribia kumaliza mukutano wake pamoja na baraza la wazee. Wakati anawaangalia, anaonyesha kwamba anawapenda sana wazee hao wenye bidii. Wamoja kati yao walikuwa wamekomaa sana, wangeweza kuwa hata na miaka ya baba yake. Lakini, jambo fulani linamuhangaisha; kwa hiyo anawauliza hivi: “Ndugu, mumefanya nini ili kuzoeza wengine wakuwe na mengi zaidi ya kufanya katika kutaniko?” Wakakumbuka kwamba wakati mwangalizi huyo alitembelea kutaniko lao wakati uliopita, aliwaomba wajikaze sana ili kuzoeza wengine. Mwishowe, muzee mumoja akasema hivi: “Kusema kweli, hatukufanya kabisa vile ulituambia.” Wazee wengine wakakubaliana naye.
2 Ikiwa uko muzee wa kutaniko, pengine wewe pia ungejibu kama muzee huyo. Katika dunia yote, waangalizi wa muzunguko wameona kwamba, katika makutaniko mengi, kuna lazima kubwa ya kuzoeza ndugu, iwe ni vijana ao wenye kukomaa, ili walichunge kundi. Lakini kufanya hivyo kuna magumu fulani. Sababu gani?
3. (a) Namna gani Maandiko yanaonyesha kwamba ni lazima kuzoeza wengine, na sababu gani kila mumoja wetu anapaswa kufikiria jambo hilo? (Ona maelezo ya chini.) (b) Sababu gani wazee fulani wanaweza kuona kwamba ni vigumu kuzoeza wengine?
3 Ikiwa wewe ni muchungaji, bila shaka umetambua kwamba ni jambo la lazima sana kuzoeza wengine.a Unajua kwamba ndugu wengi wanahitajiwa ili wasaidie makutaniko yaendelee kuwa nguvu kiroho na kuanzisha makutaniko mengine. (Soma Isaya 60:22.) Pia, unajua kwamba, Neno la Mungu linakuomba ‘uwafundishe wengine.’ (Soma 2 Timotheo 2:2.) Hata hivyo, kama wazee wenye tumezungumuzia kwenye mwanzo wa habari hii, unaweza kuona kwamba ni vigumu kuzoeza wengine. Kisha kutimiza mahitaji ya familia, mambo ya kazi, madaraka mbalimbali katika kutaniko, na mambo mengine yenye inaomba kufanywa haraka, unaweza kuona kwamba hauna tena wakati wa kuzoeza wengine. Hata hivyo, tuone sababu gani ni jambo la lazima kuzoeza wengine.
UTIE KAZI YA KUZOEZA WENGINE PA NAFASI YA KWANZA
4. Toa sababu moja yenye inaweza kufanya wazee fulani waache kwanza kuzoeza wengine.
4 Sababu gani wazee fulani wanaweza kuona kwamba ni vigumu kupata wakati wa kuzoeza wengine? Wanaweza kufikiri hivi: ‘Ni jambo la lazima kuzoeza wengine, lakini haiko jambo la haraka sana kama mambo mengine ya kutaniko. Ikiwa ninaacha kwanza kuzoeza wengine, kutaniko litaendelea tu vizuri.’ Ni kweli, mambo mengi inaomba kushugulikiwa haraka. Lakini kuacha kwanza kuzoeza wengine kunaweza kuharibu hali ya kiroho ya kutaniko.
5, 6. Mufano wa mutembezaji wa motokari na namna anaona kazi ya kutunza motere, unaweza kutufundisha nini, na namna gani hilo linaweza kuhusu mazoezi yenye ndugu wanapokea katika kutaniko?
5 Fikiria mufano huu: Mutembezaji wa motokari anajua kwamba, ili motokari yake iendelee kutumika muzuri, anapaswa kubadilisha mafuta kwa ukawaida. Lakini anaweza kufikiri kwamba kubadilisha mafuta ya motere haiko jambo la haraka sana sawa vile kujaza mazuti ao esanse katika motokari. Bila shaka, ikiwa hatie mazuti ao esanse katika motokari yake, itazimika na kuacha kutembea. Anaweza kufikiri hivi: ‘Hata kama sina wakati wa kubadilisha mafuta, motokari yangu itaendelea kutembea kwa wakati fulani.’ Lakini kufanya hivyo kunaweza kuleta hatari gani? Ikiwa mutembezaji wa motokari anaendelea kusema kwamba atatunza motokari yake wakati mwingine, siku moja motokari hiyo itaharibika sana. Na ikiwa motokari hiyo inaharibika sana, atatumia wakati na feza nyingi ili kuitengeneza. Mufano huo unatufundisha nini?
6 Wazee wanafanya kazi nyingi za lazima zenye zinaombwa kushugulikiwa haraka; ikiwa hawafanye hivyo, kutaniko linaweza kuwa katika hali mbaya. Kwa hiyo, kama vile tu mutembezaji anahakikisha kwamba tanki ya motokari yake inajaa mazuti ao esanse, wazee pia wanapaswa ‘kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Flp. 1:10) Hata hivyo, wazee fulani wanahangaikia sana mambo yenye inahitaji kushugulikiwa haraka, mupaka wanafikia kukosa wakati wa kuzoeza wengine; kufanya hivyo, ni kama vile kukosa kutunza motere ya motokari. Lakini, ikiwa kila mara wazee wanaacha kwanza kuzoeza wengine, mwishowe kutaniko litakosa ndugu wenye kustahili ili kushugulikia mambo mbalimbali.
7. Tunapaswa kuona namna gani wazee wenye wanachukua wakati ili kuzoeza wengine?
7 Ndiyo sababu wazee wanapaswa kuwa waangalifu ili wasifikiri kwamba kuzoeza wengine haiko jambo la lazima sana. Wazee wenye kufikiria wakati unaokuja na kutumia wakati wao ili kuzoeza ndugu wenye hawana uzoefu mwingi ni wasimamizi-nyumba wenye hekima na ni baraka kabisa kwa kutaniko lote. (Soma 1 Petro 4:10.) Kutaniko linafaidika namna gani?
UTUMIE WAKATI KWA HEKIMA
8. (a) Sababu gani wazee wanapaswa kuzoeza wengine? (b) Wazee wenye kutumikia mahali penye kuwa lazima kubwa wako na daraka gani la haraka? (Ona kisanduku “Daraka Kubwa Sana.”)
8 Hata wazee wenye uzoefu mwingi zaidi wanapaswa kuwa wanyenyekevu na kuelewa kwamba kadiri wanaendelea kukomaa, hawatakuwa tena na uwezo wa kutimiza kabisa mambo yenye wanafanya sasa katika kutaniko. (Mika 6:8) Pia, wanapaswa kujua kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” linaweza kuleta mabadiliko ya bila kutazamia na kufanya ikuwe vigumu kwao kutimiza madaraka yao katika kutaniko. (Mhu. 9:11, 12; Yak. 4:13, 14) Wazee wenye kuhangaikia hali nzuri ya kondoo za Yehova, wanaelezea vijana Wakristo kwa wakati unaofaa mambo yenye wamejifunza kwa miaka mingi.—Soma Zaburi 71:17, 18.
9. Ni tukio gani la wakati unaokuja linafanya ikuwe jambo la lazima sana kuzoeza wengine?
9 Ni jambo gani lingine linaonyesha kwamba wazee wenye kuzoeza wengine ni baraka kwa kundi? Wanasaidia ndugu na dada katika kutaniko waendelee kuwa nguvu kiroho. Namna gani? Bidii yenye wazee wanafanya ili kuzoeza wengine inafanya ndugu wengi zaidi wakuwe tayari kusaidia kutaniko likuwe nguvu kiroho na lenye umoja tangu sasa, na zaidi sana wakati wa muvurugo mukubwa, ni kusema, wakati wa ziki kubwa. (Eze. 38:10-12; Mika 5:5, 6) Kwa hiyo, wazee wapendwa, tafazali, tunawaomba kuanzia leo mufanye kwa ukawaida kazi ya kuzoeza wengine.
10. Muzee anapaswa kufanya nini ili apate wakati wa kuzoeza wengine?
10 Bila shaka, tunaelewa kwamba munatumia wakati mwingi sana ili kushugulikia kazi mbalimbali za lazima katika kutaniko, na hilo linaweza kuwafanya mujisikie kuwa wenye kuchoka sana. Lakini, ni jambo la lazima mutumie sehemu fulani ya wakati huo ili kuzoeza wengine. (Mhu. 3:1) Kufanya hivyo ni kutumia wakati kwa hekima.
UTAYARISHE MOYO WA MWANAFUNZI
11. (a) Ni jambo gani lenye kupendeza kuhusu mapendekezo yenye wazee wa inchi mbalimbali walitoa? (b) Kulingana na Methali 15:22, sababu gani itakuwa jambo la lazima kuchunguza mapendekezo ya wazee wengine?
11 Hivi karibuni, wazee fulani wenye wamepata matokeo mazuri kwa kusaidia ndugu wakomae kiroho waliulizwa ni njia gani wanatumia ili kuzoeza wengine.b Hata kama hali zao zinaachana sana, walitoa mapendekezo yenye kufanana sana. Hilo linaonyesha nini? Linaonyesha kwamba mazoezi yenye kutegemea Biblia inahusu wanafunzi wa “kila mahali katika kila kutaniko,” kama vile ilikuwa katika siku za mutume Paulo. (1 Kor. 4:17) Katika habari hii na ile yenye kufuata, tutachunguza mapendekezo fulani ya wazee hao. (Met. 15:22) Pia, tutatumia neno “walimu” ili kuzungumuzia wale wenye kutoa mazoezi, na neno “wanafunzi” ili kuzungumuzia wale wenye kupokea mazoezi.
12. Mwalimu anapaswa kutayarisha nini, na sababu gani?
12 Mwalimu anapaswa kutayarisha moyo wa mwanafunzi mbele ya kumuzoeza. Mulimaji anapaswa kulima, ao kuregeza udongo mbele apande mbegu; vilevile, mwalimu anapaswa kutayarisha moyo wa mwanafunzi mbele ya kumufundisha ufundi mupya. Kwa hiyo, namna gani mwalimu anaweza kutayarisha moyo wa mwanafunzi? Kwa kufuata njia yenye nabii fulani wa zamani alitumia. Nabii huyo alitumia njia gani?
13-15. (a) Nabii Samweli alipewa mugawo gani? (b) Namna gani nabii Samweli alitimiza mugawo wake? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.) (c) Sababu gani leo wazee wanaweza kufaidika sana na habari ya Biblia kuhusu nabii Samweli?
13 Kumepita zaidi ya miaka 3000, tangu Yehova alizungumuza na Samweli, nabii mwenye kuzeeka na kumuambia hivi: ‘Karibu wakati kama huu kesho nitatuma mutu kwako kutoka katika inchi ya Benyamini. Nawe umutie mafuta akuwe kiongozi juu ya watu wangu Israeli.’ (1 Sam. 9:15, 16) Nabii Samweli alielewa kwamba daraka lake la kuongoza Waisraeli lilikuwa limefikia mwisho na kwamba Yehova amemupatia kazi ya kumutia mafuta mutu mwenye atachukua nafasi yake. Pengine nabii Samweli alijiuliza hivi: ‘Namna gani ninaweza kutayarisha mutu huyo kwa ajili ya daraka hilo?’ Alipata wazo fulani na kisha alipanga namna ya kulitimiza.
14 Siku yenye ilifuata, wakati nabii Samweli alimuona Sauli, Yehova alimuambia hivi: ‘Huyu ndiye mutu.’ Kisha, nabii Samweli alifanya kulingana na namna alikuwa amepanga. Alimualika Sauli ili wakule chakula pamoja katika chumba cha kukulia. Kisha akamupatia Sauli na mutumishi wake viti vizuri vya kuikalia na sehemu nzuri sana ya nyama na kumuambia hivi: ‘Ukule, kwa maana wamekuwekea hicho akiba mupaka wakati uliowekwa.’ Kisha, Sauli na nabii Samweli wakatembea pamoja na kuzungumuza mupaka walifika katika nyumba ya nabii Samweli. Nabii Samweli alipenda kutumia vizuri hali hiyo yenye kufaa kabisa ambayo ilitokezwa wakati wa chakula na wakati wa matembezi yenye kufurahisha. Kwa hiyo, akamuomba Sauli wapande kwenye sehemu ya juu ya nyumba yake. Katika hewa yenye baridi ya mangaribi, Samweli “akaendelea kusema na Sauli darini [sehemu ya juu ya nyumba]” mupaka wakati walienda kulala. Siku yenye ilifuata, Samweli akamutia Sauli mafuta, akamukumbatia, na kumupatia maagizo mengi zaidi. Kisha, akamuacha Sauli aende. Wakati huo, Sauli alikuwa ametayarishwa kwa ajili ya mambo yenye ilikuwa mbele yake.—1 Sam. 9:17-27; 10:1.
15 Bila shaka, kumutia mafuta mutu ili akuwe kiongozi wa taifa ni tofauti kabisa na kuzoeza ndugu ili akuwe muzee ao mutumishi wa huduma katika kutaniko. Hata hivyo, mufano wa nabii Samweli unaweza kufundisha wazee wa leo mambo mengi sana ya lazima. Tuchunguze sasa mambo mawili tu kati ya mambo hayo.
WALIMU WENYE KUWA TAYARI NA MARAFIKI WA KWELI
16. (a) Samweli alijisikia namna gani wakati Waisraeli waliomba mufalme? (b) Samweli alijisikia namna gani wakati Yehova alimuambia amutie Sauli mafuta?
16 Ukuwe tayari, lakini usisite kuzoeza wengine. Wakati nabii Samweli alisikia kwa mara ya kwanza kwamba Waisraeli walipenda wakuwe na mufalme mwanadamu, alivunjika moyo na alijisikia kuwa wamemukataa. (1 Sam. 8:4-8) Kwa hiyo, alisita kufanya jambo lenye watu walikuwa wamemuomba mupaka Yehova aliona kuwa ni lazima amuambie mara tatu kwamba asikilize sauti yao. (1 Sam. 8:7, 9, 22) Hata hivyo, Samweli hakusikia uchungu ao kumuwekea kinyongo mutu mwenye angechukua nafasi yake. Wakati Yehova alimuambia nabii Samweli amutie Sauli mafuta, nabii Samweli hakutii kwa sababu tu alipaswa kutii, lakini kwa sababu alimupenda Yehova.
17. Namna gani leo wazee wanafuata mufano wa nabii Samweli, na hilo linawaletea faida gani?
17 Leo, wazee wenye uzoefu wanafuata mufano wa nabii Samweli kwa kuzoeza wengine kwa upendo. (1 Pet. 5:2) Wazee kama hao hawakatae kuzoeza wengine kwa kuogopa kwamba wanafunzi hao watachukua mapendeleo yao fulani katika kutaniko. Walimu wazuri hawaone wanafunzi wenye kufanya maendeleo kuwa ndugu wenye kufanya mashindano pamoja nao, lakini wanawaona kama ‘wafanyakazi wenzao,’ ni kusema, zawadi ya bei sana kwa ajili ya kutaniko. (2 Kor. 1:24; Ebr. 13:16) Walimu hao wenye upendo wanafurahi sana wakati wanaona namna wanafunzi hao wanatumia uwezo wao kwa faida ya ndugu na dada katika kutaniko.—Mdo. 20:35.
18, 19. Namna gani muzee anaweza kutayarisha moyo wa mwanafunzi, na sababu gani ni jambo la lazima kutumia njia hiyo?
18 Ukuwe rafiki, lakini usikuwe mwalimu tu. Wakati nabii Samweli alikutana na Sauli, angechukua chupa ya mafuta, na kumumwangia mbio-mbio kwenye kichwa. Sauli angeenda kuwa mufalme mwenye mamlaka bila kupewa mazoezi fulani. Lakini, kwa upendo nabii Samweli alichukua wakati ili kutayarisha pole-pole moyo wa Sauli. Kisha kula pamoja chakula kitamu, kufanya matembezi yenye kufurahisha, kuongea kwa muda murefu pamoja naye, na kupumuzika vizuri, nabii Samweli aliona kwamba wakati ulikuwa umefika ili kumutia Sauli mafuta.
Ni lazima kufanya urafiki na mwanafunzi mbele ya kuanza kumuzoeza(Ona fungu la 18, 19)
19 Vilevile, leo walimu wanapaswa kuanza mazoezi kwa kuchukua wakati wa kutafuta nafasi yenye kufaa ili kufanya urafiki pamoja na mwanafunzi. Mambo mbalimbali yenye muzee anaweza kufanya ili kuwa na urafiki pamoja na mwanafunzi, inategemea hali za inchi, eneo, na tabia za watu. Lakini, iwe unaishi wapi, na hata kama uko na kazi nyingi za kufanya katika kutaniko, ikiwa unapitisha wakati pamoja na mwanafunzi, ni kama vile unamuambia hivi: “Ninakuona kuwa wa lazima.” (Soma Waroma 12:10.) Bila shaka, wanafunzi wa kila mahali watakuwa wenye shukrani sana kwa sababu munawahangaikia kwa upendo.
20, 21. (a) Mwalimu mwenye kupata matokeo mazuri anafanya nini? (b) Tutachunguza nini katika habari yenye kufuata?
20 Wazee, mukumbuke kwamba, mwalimu mwenye kupata matokeo mazuri haonyeshe tu kwamba anapenda kuzoeza mwanafunzi, lakini anaonyesha pia kwamba anamupenda mwanafunzi. (Linganisha na Yohana 5:20.) Mwanafunzi anatambua haraka sifa hiyo ya lazima ya mwalimu, na hilo linamufanya afurahie sana mazoezi yenye anapewa. Kwa hiyo, wazee wapendwa, wakati munazoeza wengine, mukuwe marafiki, lakini musikuwe walimu tu.—Met. 17:17; Yoh. 15:15.
21 Kisha kutayarisha moyo wa mwanafunzi, muzee anapaswa sasa kumufundisha ufundi mbalimbali wenye anahitaji. Muzee anapaswa kutumia njia gani? Tutachunguza njia hizo katika habari yenye kufuata.
a Habari hii na ile yenye kufuata zimetayarishwa zaidi sana kwa ajili ya wazee. Hata hivyo, zinahusu wote katika kutaniko. Sababu gani? Kwa sababu zitasaidia wanaume wote wenye kubatizwa waelewe kwamba wanapaswa kuzoezwa ili wafanye mengi zaidi katika kutaniko. Ikiwa wanapata mazoezi, kila mutu katika kutaniko atafaidika.
b Wazee hao wanaishi katika inchi ya Afrika ya Kusini, Australia, Bangladesh, Belgique, Brazili, États-Unis, Guiana ya Ufaransa, Japani, Korea, Meksiko, Namibia, Nigeria, Réunion, Ufaransa, na Urusi.
-
-
Namna Wazee Wanazoeza Wengine ili Wafikie MadarakaMunara wa Mulinzi—2015 | Mwezi wa 4 15
-
-
Namna Wazee Wanazoeza Wengine ili Wafikie Madaraka
‘Mambo uliyoyasikia kutoka kwangu . . . , uwakabizi [uwatolee] watu waaminifu.’—2 TIM. 2:2.
1. (a) Tangu zamani, watumishi wa Yehova wameelewa nini kuhusu kuzoeza wengine, na sababu gani jambo hilo ni lenye kufaa leo? (b) Tutachunguza nini katika habari hii?
TANGU zamani, watumishi wa Yehova wameelewa kwamba kuzoeza wengine kunaleta matokeo mazuri. Muzee wa ukoo Abramu ‘alikusanya watu wake waliozoezwa’ ili kumukomboa Loti, na watu hao walipata matokeo mazuri. (Mwa. 14:14-16) Katika siku za Mufalme Daudi, waimbaji wa nyumba ya Mungu ‘walizoezwa nyimbo kwa Yehova’ ili kumuletea Mungu sifa. (1 Nya. 25:7) Leo, tunapigana vita ya kiroho na Shetani pamoja na wafuasi wake. (Efe. 6:11-13) Pia, tunajikaza ili kumuletea Yehova sifa. (Ebr. 13:15, 16) Kwa hiyo, kama watumishi wa Mungu wa zamani, tunapaswa kuzoezwa ili tupate matokeo mazuri. Yehova amewapatia wazee daraka la kuzoeza wengine. (2 Tim. 2:2) Wazee wenye uzoefu wanatumia njia gani ili kuzoeza ndugu wastahili kushugulikia kundi?
UMUSAIDIE MWANAFUNZI AMUPENDE YEHOVA SANA
2. Mbele ya kufundisha mwanafunzi ufundi fulani, muzee anaweza kufanya nini, na sababu gani?
2 Muzee anaweza kufananishwa na mulimaji. Mbele ya kupanda mbegu, mulimaji anaweza kuona kwamba ni lazima aongeze mbolea katika udongo ili kuufanya utoe mavuno mengi. Vilevile, mbele ya kufundisha mwanafunzi ufundi fulani, unaweza kutambua kwamba ni lazima kuzungumuzia maandiko fulani pamoja naye ili kuchochea moyo wake na kuufanya ukuwe tayari kupokea mazoezi.—1 Tim. 4:6.
3. (a) Namna gani muzee anaweza kutumia maneno ya Yesu katika Marko 12:29, 30 wakati anazungumuza na mwanafunzi? (b) Sala yenye muzee anatoa inaweza kuwa na matokeo gani juu ya mwanafunzi?
3 Ili kujua ni kwa kadiri gani kweli ya Ufalme imechochea mawazo na matendo ya mwanafunzi, unaweza kumuuliza hivi: ‘Namna gani kujitoa kwa Yehova kumebadilisha namna unatumia maisha yako?’ Ulizo hilo linaweza kusaidia kuanzisha mazungumuzo mazuri kuhusu namna tunaweza kumutumikia Yehova kwa moyo wetu wote. (Soma Marko 12:29, 30.) Pengine, kisha mazungumuzo, unaweza kusali pamoja na mwanafunzi ili kumuomba Yehova amupatie roho takatifu ili imusaidie kufaidika kabisa na mazoezi yenye anapata. Ndugu huyo atatiwa moyo sana kwa kusikia unasali kwa moyo wote kwa ajili yake!
4. (a) Ni habari gani za Biblia zinaweza kumuchochea mwanafunzi afanye maendeleo ya kiroho. (b) Wazee wana kusudi gani kubwa wakati wanazoeza wengine?
4 Wakati unaanza kuzoeza mwanafunzi, muzungumuzie habari fulani za Biblia zenye zinaweza kumusaidia aone kwamba ni lazima akuwe tayari kusaidia, mwenye kutegemeka, na munyenyekevu. (1 Fal. 19:19-21; Neh. 7:2; 13:13; Mdo. 18:24-26) Sifa hizo ni za lazima sana kwa mwanafunzi kama vile mbolea ni ya maana sana kwa udongo. Sifa hizo zitamusaidia afanye maendeleo ya kiroho mbio-mbio. Jean-Claude, muzee katika kutaniko moja la Ufaransa, anasema hivi: “Wakati ninazoeza mwanafunzi, kusudi langu kubwa ni kumusaidia akomae kiroho. Ninatafuta nafasi ya kusoma andiko fulani pamoja naye ili ‘kufungua macho’ yake na kumusaidia aone ‘mambo ya ajabu’ yenye kupatikana katika Neno la Mungu.” (Zab. 119:18) Muzee anaweza kutumia njia gani zingine ili kumusaidia mwanafunzi afanye maendeleo ya kiroho?
UTOE MAPENDEKEZO NA UONYESHE SABABU
5. (a) Sababu gani ni jambo la lazima kuzungumuza na mwanafunzi kuhusu miradi yake ya kiroho? (b) Sababu gani wazee wanapaswa kuzoeza ndugu wenye wangali vijana? (Ona maelezo ya chini.)
5 Umuulize mwanafunzi hivi: ‘Uko na miradi gani ya kiroho?’ Ikiwa hana muradi fulani wa kiroho, umusaidie ajiwekee muradi wenye kupatana na uwezo wake na wenye anaweza kufikia. Umuambie muradi fulani wa kiroho wenye ulijiwekea hapo zamani, na umuelezee kwa kuchangamuka furaha kubwa yenye ulipata wakati ulifikia muradi huo. Njia hiyo yenye kuonekana kuwa mwepesi inaleta matokeo mazuri. Victor, muzee na painia huko Afrika, anakumbuka: “Wakati nilikuwa kijana, muzee mumoja aliniuliza maulizo fulani yenye kuchaguliwa vizuri juu ya miradi yangu ya kiroho. Maulizo hayo ilinisaidia nianze kufikiri sana juu ya hali ya utumishi wangu kwa Mungu.” Wazee wenye uzoefu wanaonyesha kwamba ni lazima sana kuanza kuzoeza ndugu wakati wangali vijana, kwa kuwapatia kazi mbalimbali katika kutaniko zenye kulingana na miaka yao. Kuwazoeza wakati wangali vijana kutawasaidia wakazie akili yao juu ya miradi ya kiroho kwa sababu wakati wanaendelea kukomaa, wanakuwa na mambo mengi yenye inaweza kuwakengeusha wasifuatilie miradi yao ya kiroho.—Soma Zaburi 71:5, 17.a
Umufasirie mwanafunzi sababu gani kazi fulani inapaswa kufanywa, na umupongeze kwa bidii yenye anafanya ili kutimiza kazi hiyo (Ona fungu la 5-8)
6. Yesu alitumia njia gani nzuri ili kuwazoeza mitume wake?
6 Unaweza pia kumuchochea mwanafunzi akuwe na hamu ya kutumikia kutaniko wakati unamufasiria mambo yenye anapaswa kufanya, na sababu gani. Unamuiga Yesu, Mwalimu Mukubwa, wakati unamufasiria mwanafunzi sababu gani anapaswa kufanya kazi fulani. Kwa mufano, mbele Yesu awapatie mitume amri ya kufanya wanafunzi, alionyesha sababu gani walipaswa kutii. Aliwaambia hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Kisha aliongeza hivi: ‘Kwa hiyo muende mukafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mt. 28:18, 19) Namna gani muzee anaweza kuiga njia yenye Yesu alitumia ili kuzoeza mitume wake?
7, 8. (a) Namna gani leo wazee wanaweza kuiga njia yenye Yesu alitumia ili kuzoeza mitume wake? (b) Sababu gani ni jambo la lazima kumupongeza mwanafunzi? (c) Ni mapendekezo gani inaweza kusaidia wazee wakati wanazoeza wengine? (Ona kisanduku “Namna ya Kuzoeza wengine,” kwenye ukurasa wa 8.)
7 Umufasirie mwanafunzi sababu gani Maandiko inaomba kufanya kazi fulani. Kwa kufanya hivyo, unamufundisha kufikiri kulingana na kanuni za Biblia. Kwa mufano, unaomba ndugu fulani afanye kazi fulani kwenye Jumba la Ufalme; kama vile kusafisha njia yenye kuenda kwenye Jumba la Ufalme. Unaweza kuchunguza pamoja naye andiko la Tito 2:10 na kumufasiria namna mugawo wake unasaidia ‘kulipamba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu.’ Pia, umuombe mwanafunzi afikirie ndugu na dada wenye kuzeeka katika kutaniko na namna gani kutimiza mugawo wake kunaweza kuwaletea faida. Kuzungumuzia mambo hayo na mwanafunzi wakati wa mazoezi kutamusaidia afikirie sana watu kuliko kukazia sheria. Atafurahi sana kuona namna ndugu na dada katika kutaniko wanafaidika na kazi yenye anatimiza.
8 Zaidi ya hilo, ujikaze sana ili kumupongeza mwanafunzi juu ya bidii yenye anafanya ili kutumikisha mapendekezo yenye unamutolea. Sababu gani ni jambo la lazima kumupongeza mwanafunzi? Kumupongeza kwa moyo wote kutamusaidia afanye maendeleo, kama vile kumuangia mumea maji kunasaidia uchipuke.—Linganisha na Mathayo 3:17.
TATIZO LINGINE
9. (a) Katika inchi tajiri, wazee wanapata tatizo gani wakati wanazoeza wengine? (b) Sababu gani vijana fulani hawatie kazi ya Mungu pa nafasi ya kwanza katika maisha yao?
9 Katika inchi tajiri, wazee wanaweza kupambana na tatizo lingine, ni kusema, wanajiuliza namna gani wanaweza kuchochea ndugu wenye kuwa na miaka kati ya 20 na 30 ili wasaidie katika kazi mbalimbali za kutaniko. Tuliuliza wazee wenye uzoefu wa inchi karibu 20 sababu gani wanafikiri kwamba ndugu fulani vijana hawaone kuwa ni lazima wafanye mengi zaidi katika kutaniko. Muzee mumoja alijibu hivi: Wakati walikuwa wangali wanakomaa, vijana fulani hawakutiwa moyo kujiwekea miradi ya kiroho. Na vijana wengine wenye walijiwekea miradi ya kiroho, wazazi wao waliwatia moyo wafuatilie miradi ya kimwili. Kwa hiyo, hawakutia kazi ya Mungu pa nafasi ya kwanza katika maisha yao.—Mt. 10:24.
10, 11. (a) Namna gani muzee anaweza kumusaidia polepole ndugu mwenye haone kuwa ni lazima kufikia madaraka abadilishe mawazo yake? (b) Muzee anaweza kuzungumuzia Maandiko gani pamoja na ndugu huyo, na sababu gani? (Ona maelezo ya chini.)
10 Ikiwa ndugu fulani haone kuwa ni lazima kufikia madaraka katika kutaniko, itaomba muzee mwenye kumuzoeza atumike sana, na kuonyesha uvumilivu. Na mwishowe mwanafunzi huyo anaweza kufikia kubadilisha mawazo yake. Kama vile mulimaji anaweza kunyorosha polepole mimea yake kwa kutumia miti ili kuitegemeza, wazee pia wanaweza hatua kwa hatua kusaidia ndugu fulani watambue kwamba ni lazima wabadilishe mawazo yao na wafikie kukubali mapendeleo katika kutaniko. Lakini, namna gani wazee wanaweza kufanya hivyo?
11 Muzee anaweza kujiwekea wakati wa kufanya urafiki pamoja na mwanafunzi. Umusaidie atambue kwamba kutaniko linahitaji musaada wake. Kisha muda fulani, muzungumuzie pamoja na mwanafunzi maandiko fulani yenye itamusaidia afikiri juu ya kujitoa kwake kwa Yehova. (Mhu. 5:4; Isa. 6:8; Mt. 6:24, 33; Lu. 9:57-62; 1 Kor. 15:58; 2 Kor. 5:15; 13:5) Unaweza kumuuliza hivi: ‘Wakati ulijitoa kwa Yehova katika sala, ulimuahidi nini?’ Ujikaze kugusa moyo wake kwa kumuuliza hivi: ‘Unawaza Yehova alijisikia namna gani wakati ulibatizwa?’ (Met. 27:11) ‘Na Shetani alijisikia namna gani?’ (1 Pet. 5:8) Usisahau hata kidogo kwamba, Maandiko yenye kuchaguliwa vizuri inaweza kugusa sana moyo wake.—Soma Waebrania 4:12.b
WANAFUNZI, MUONYESHE KWAMBA MUKO WAAMINIFU
12, 13. (a) Elisha alitenda namna gani wakati nabii Eliya alikuwa anamuzoeza? (b) Namna gani Yehova alimubariki Elisha kwa sababu ya uaminifu wake?
12 Vijana, kutaniko liko na lazima ya musaada wenu! Lakini, ni jambo gani litawasaidia mupate matokeo mazuri? Ili kupata jibu, tuchunguze mambo fulani katika maisha ya mwanafunzi mumoja wa zamani.
13 Kumepita miaka karibu 3000, tangu nabii Eliya alimuomba kijana Elisha akuwe mutumishi wake. Elisha alikubali bila kukawia na akaanza kumutumikia kwa uaminifu nabii huyo mwenye kuzeeka, kwa kufanya kazi za hali ya chini. (2 Fal. 3:11) Kisha miaka sita hivi ya mazoezi, Elisha alitambua kwamba kazi ya Eliya ya kutoa unabii katika Israeli ilikuwa karibu kumalizika. Kwa hiyo, nabii Eliya akamuomba mwanafunzi wake mwenye alikuwa amezoezwa vizuri aache kumufuata. Lakini Elisha alimuambia hivi nabii Eliya mara tatu: “Mimi sitakuacha.” Elisha alipenda aendelee kuwa pamoja na mwalimu wake. Kwa hiyo, Yehova alimubariki Elisha kwa sababu ya uaminifu na ushikamanifu wake. Alimuwezesha aone namna nabii Eliya anachukuliwa katika zoruba kwa njia yenye kushangaza.—2 Fal. 2:1-12.
14. (a) Namna gani leo wanafunzi wanaweza kuiga mufano wa Elisha? (b) Sababu gani ni jambo la lazima sana mwanafunzi akuwe mwaminifu?
14 Namna gani leo mwanafunzi anaweza kuiga mufano wa Elisha? Kwa kukubali bila kukawia kufanya kazi, hata zile za hali ya chini. Umuone mwalimu wako kuwa rafiki yako, na umuambie kwamba unafurahia sana bidii yenye anafanya kwa ajili yako. Namna unatenda wakati anakuzoeza ni kama vile unamuambia hivi: “Mimi sitakuacha.” Zaidi ya yote, ufanye kwa uaminifu kazi yoyote yenye unapewa. Sababu gani ni jambo la lazima kufanya hivyo? Kwa sababu wazee watakuwa hakika kwamba Yehova anapenda upewe madaraka mengi zaidi katika kutaniko, wakati tu unaonyesha kwamba uko mwaminifu na mwenye kutegemeka.—Zab. 101:6; soma 2 Timotheo 2:2.
UWAHESHIMU WAZEE WENYE KUKUZOEZA
15, 16. (a) Ni katika njia gani Elisha alionyesha kwamba alimuheshimu mwalimu wake? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.) (b) Namna gani Elisha alifanya manabii wenzake wamutumainie?
15 Habari ya Elisha, mwenye alichukua nafasi ya nabii Eliya, inaonyesha pia namna leo ndugu wanaweza kuonyesha kwamba wanawaheshimu wazee wenye uzoefu. Kisha nabii Eliya na Elisha kutembelea kikundi fulani cha manabii katika muji wa Yeriko, wanaume hao wawili walienda pamoja kuelekea Muto Yordani. Kwenye muto huo, ‘Eliya alichukua vazi lake rasmi, akalifunga, akapiga maji, nayo mwishowe yakagawanyika huku na huku.’ Kisha kuvuka muto kupitia udongo wenye kukauka, wanaume hao wakaendelea ‘kuzungumuza huku wakitembea.’ Ni wazi kwamba, Elisha hakufikiri hata kidogo kwamba wakati huo alikuwa amejua mambo yote. Elisha aliweka katika moyo wake kila neno mwalimu wake alimuambia mupaka wakati waliachana na nabii Eliya. Kisha Eliya akapanda katika zoruba ya upepo. Baadaye, wakati Elisha alifika kwenye Muto Yordani, akapiga maji kwa kutumia vazi la nabii Eliya, na kuita: ‘Iko wapi Yehova Mungu wa Eliya?’ Mara ingine tena, maji ikagawanyika.—2 Fal. 2:8-14.
16 Je, umetambua kwamba muujiza wa kwanza wa Elisha ulifanana kabisa na ule wa nabii Eliya? Sababu gani jambo hilo ni lenye kupendeza? Inaonekana kwamba, Elisha hakufikiri kama kwa sababu alikuwa amepewa mamlaka, alipaswa kufanya mambo vile anapenda. Kwa kufuata mufano wa nabii Eliya, Elisha alionyesha kwamba alimuheshimu mwalimu wake, na jambo hilo lilifanya manabii wenzake wamutumainie. (2 Fal. 2:15) Hata hivyo, katika miaka 60 yenye Elisha alifanya katika kazi ya kutoa unabii, Yehova alimupatia uwezo wa kufanya miujiza mingi zaidi kuliko nabii Eliya. Jambo hilo linaweza kufundisha mwanafunzi nini leo?
17. (a) Namna gani wanafunzi leo wanaweza kuiga mufano wa Elisha? (b) Kisha muda fulani, namna gani Yehova anaweza kutumia wanafunzi waaminifu?
17 Usiwaze kwamba kisha tu kupewa madaraka katika kutaniko, unapaswa kutumia madaraka hayo ili kubadilisha mambo, ni kusema, kufanya mambo kwa njia tofauti kabisa na namna ilikuwa inafanywa mbele. Ikiwa kuna lazima ya kubadilisha mambo fulani, yatabadilishwa si kwa sababu wewe unapenda, lakini kulingana na mahitaji ya kutaniko na muongozo wenye kutolewa na tengenezo la Yehova. Kupitia matendo yake, Elisha alifanya manabii wenzake wamutumainie na alionyesha kwamba alimuheshimu mwalimu wake kwa kutumia njia zenye alitumia. Wewe pia unaweza kufanya waamini wenzako wakutumainie na kuonyesha kwamba unaheshimu wazee wenye uzoefu kwa kuendelea kutumia njia zao zenye kutegemea Maandiko zenye wanatumia. (Soma 1 Wakorintho 4:17.) Hata hivyo, kadiri utaendelea kuwa na uzoefu, bila shaka utaweza kuchangia kufanya mabadiliko yenye itasaidia kutaniko liendelee kutembea pamoja na tengenezo la Yehova. Kwa hiyo, kama vile alimutendea Elisha, Yehova anaweza pia kuwasaidia ninyi wanafunzi waaminifu mufanye mambo makubwa zaidi kuliko walimu wenu.—Yoh. 14:12.
18. Sababu gani leo ni jambo la lazima sana kuzoeza ndugu katika makutaniko?
18 Tunatumaini kwamba mapendekezo yenye kupatikana katika habari hii na katika ile yenye ilitangulia ichochee zaidi wazee wajiwekee wakati wa kuzoeza wengine. Tunatumaini pia kwamba ndugu wenye kustahili watakubali kwa moyo wote mazoezi yenye wanapokea na kuitumikisha kwa hekima wakati wanashugulikia kondoo za Yehova. Kufanya hivyo, kutasaidia makutaniko katika dunia yote na kutasaidia kila mumoja wetu abaki mwaminifu katika nyakati ngumu zenye zinakuja.
a Ikiwa kijana anaonyesha kwamba amekomaa kiroho, ni munyenyekevu, na anatimiza mambo mengine yenye kuombwa katika Maandiko, wazee wanaweza kumupendekeza ili akuwe mutumishi wa huduma, hata kama hajaeneza miaka 20.—1 Tim. 3:8-10, 12; ona Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 7, 1989, ukurasa wa 29, katika Kifaransa.
b Wakati muzee anazungumuza pamoja na mwanafunzi, anaweza kutumia mapendekezo yenye kupatikana katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 4, 2012, ukurasa wa 14-16, fungu la 8-13; na kitabu Mubaki “Katika Upendo wa Mungu,” sura ya 16, fungu la 1-3.
-