MAKALA YA 44
WIMBO 138 Kichwa Chenye Mvi—Taji la Uzuri
Dumisha Shangwe Yako Unapozeeka
“ Wakati wa uzeeni wataendelea kunawiri.”—ZAB. 92:14.
JAMBO KUU
Kwa nini ni muhimu kwa wale wenye umri mkubwa kudumisha shangwe yao, na jinsi wanavyoweza kufanya hivyo.
1-2. Yehova ana maoni gani kuhusu waaminifu wenye umri mkubwa? (Zaburi 92:12-14; tazama pia picha.)
WATU ulimwenguni pote wana mitazamo mbalimbali kuhusu kuzeeka. Wengine wanaona kuwa ni jambo la heshima, lakini wengine hufanya yote wawezayo ili wasionekane wamezeeka. Kwa mfano, fikiria hali hii: Je, unakumbuka mara ya kwanza ulipoona nywele yenye mvi kichwani mwako? Huenda ulitaka kuing’oa nywele hiyo kabla ya wengine kuiona. Lakini ulitambua kwamba kung’oa nywele hiyo hakungezuia nyingine kuota. Mfano huo unaonyesha kwamba hatuwezi kuzuia hali ya kuzeeka.
2 Hata hivyo, Baba yetu wa mbinguni ana maoni gani kuhusu watumishi wake wanaozeeka? (Met. 16:31) Anawafananisha na miti iliyonawiri. (Soma Zaburi 92:12-14.) Kwa nini ulinganisho huo unafaa? Miti ambayo imejaa majani na maua yenye kunukia, mara nyingi huwa na miaka mingi. Mojawapo ya miti maridadi zaidi ni mcheri unaopatikana nchini Japani. Baadhi ya micheri maridadi sana ina umri wa zaidi ya miaka elfu moja. Kama miti hiyo yenye miaka mingi, waaminifu wenye umri mkubwa ni maridadi, hasa machoni pa Mungu. Yehova anaona mengi zaidi ya nywele zenye mvi. Anathamini sifa nzuri za wenye umri mkubwa—kama vile uvumilivu na ushikamanifu wao—pamoja na miaka yao mingi waliyomtumikia kwa uaminifu.
Kama miti yenye miaka mingi iliyo maridadi na inayoendelea kunawiri, ndivyo ambavyo waaminifu wenye umri mkubwa walivyo maridadi na wanaendelea kunawiri (Tazama fungu la 2)
3. Taja mifano ya jinsi ambavyo Yehova aliwatumia wale wenye umri mkubwa kutimiza kusudi lake.
3 Umri wa mtu unaposonga haupunguzi thamani yake mbele za Yehova.a Isitoshe, mara nyingi Yehova huwatumia wale wenye umri mkubwa kutimiza kusudi lake. Kwa mfano, Sara alikuwa na umri mkubwa sana wakati Yehova alipotangaza kwamba angekuwa mama wa taifa lenye nguvu na nyanya (bibi) ya Masihi. (Mwa. 17:15-19) Musa alikuwa na umri mkubwa Yehova alipomwagiza awaongoze Waisraeli kutoka Misri. (Kut. 7:6, 7) Na mtume Yohana alikuwa amezeeka Yehova alipomwongoza kwa roho kuandika vitabu vitano vya Biblia.
4. Kulingana na Methali 15:15, ni nini kinachoweza kuwasaidia wenye umri mkubwa kuvumilia changamoto wanazokabili? (Tazama pia picha.)
4 Wale wenye umri mkubwa wanakabili changamoto nyingi zinazotokana na kusonga kwa umri. Dada mmoja alisema hivi kwa utani, “Kuzeeka si jambo rahisi, ujasiri unahitajika.” Lakini kuwa na shangweb kunaweza kuwasaidia wenye umri mkubwa kuvumilia majaribu yanayotokana na kusonga kwa umri. (Soma Methali 15:15.) Katika makala hii, tutachunguza mambo ambayo watu wenye umri mkubwa wanaweza kufanya ili kudumisha shangwe yao. Tutachunguza pia jinsi wengine wanavyoweza kuwasaidia ndugu na dada wenye umri mkubwa kutanikoni. Kwanza, acheni tuchunguze kwa nini inaweza kuwa changamoto kudumisha shangwe yetu umri unaposonga.
Mtazamo wenye shangwe unaweza kuwasaidia wenye umri mkubwa wavumilie majaribu yanayotokana na kusonga kwa umri (Tazama fungu la 4)
JINSI KUZEEKA KUNAVYOWEZA KUATHIRI SHANGWE YAKO
5. Ni nini kinachoweza kuwavunja moyo wale walio na umri mkubwa?
5 Ni jambo gani ambalo linaweza kukuvunja moyo? Labda umevunjika moyo kwa sababu huwezi kufanya mambo ambayo zamani uliweza kufanya. Huenda ukautamani wakati ulipokuwa kijana na mwenye afya nzuri. (Mhu. 7:10) Kwa mfano, dada anayeitwa Ruby anasema hivi: “Ni vigumu kwangu kuvaa nguo kwa sababu ya maumivu na siwezi kuinua mikono na miguu yangu kama zamani. Jambo rahisi kama vile kunyanyua mguu wangu ili kuvaa soksi ni changamoto. Mikono yangu ina ganzi na ugonjwa wa yabisi-kavu, jambo linalofanya iwe vigumu kwangu kutimiza hata mambo madogo-madogo.” Na Harold, anayetumikia Betheli, anasema hivi: “Simtambui mwanamume ambaye sasa nimekuwa, na pindi fulani hilo hufanya nikasirike. Zamani nilikuwa mwenye nguvu. Nilipenda sana kucheza besiboli. Watu wangesema, ‘Mpe mpira Harold ili tushinde.’ Lakini sasa sidhani kama ninaweza hata kurusha mpira.”
6. (a) Ni mambo gani mengine yanayoweza kusababisha baadhi ya watu wenye umri mkubwa wavunjike moyo? (b) Ni nini kinachoweza kuwasaidia wenye umri mkubwa kuamua ikiwa wanaweza kuendesha gari au la? (Tazama katika toleo hili makala yenye kichwa “Je, Niache Kuendesha Gari?”)
6 Huenda ukavunjika moyo kwa sababu umepoteza uhuru wako kwa kadiri fulani. Hilo ni kweli hasa ikiwa unahitaji msaada wa kutunzwa au ikiwa unahitaji kuishi pamoja na mojawapo ya watoto wako. Au huenda umevunjika moyo sana kwa sababu afya yako si nzuri, au uwezo wako wa kuona umefifia kiasi cha kwamba huwezi kwenda popote peke yako au kuendesha gari. Hali hiyo inavunja moyo sana! Lakini jambo linaloweza kukusaidia ni kukumbuka kwamba thamani yako kwa Yehova na kwa watu wengine haitegemei ikiwa unaweza kujitunza mwenyewe, kuishi peke yako, au kuendesha gari. Na tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaelewa hisia zetu. Jambo muhimu kwake ni jinsi tulivyo moyoni, yaani, moyo unaompenda na kumthamini sana Yehova na waabudu wenzetu.—1 Sam. 16:7.
7. Ni jambo gani linaloweza kuwasaidia wale ambao wanasikitika kwa sababu wanafikiri kwamba hawataona mfumo huu wa mambo ukifikia mwisho wake?
7 Huenda unasikitika kwa sababu unahisi kwamba hutaona mfumo huu wa mambo ukifikia mwisho wake. Ni jambo gani linaloweza kukusaidia ikiwa unahisi hivyo? Jitahidi kukumbuka kwamba Yehova anangojea kwa subira ili kuuharibu ulimwengu huu mwovu. (Isa. 30:18) Lakini Yehova ana sababu nzuri ya kuonyesha subira. Subira yake inawapatia mamilioni ya watu fursa na wakati ili wamjue na kumtumikia. (2 Pet. 3:9) Hivyo, unapovunjika moyo, jitahidi kufikiria ni watu wangapi watakaonufaika kutokana na subira ya Yehova kabla ya mwisho kufika. Huenda baadhi yao watatia ndani watu wa familia yako mwenyewe.
8. Changamoto zinazosababishwa na kusonga kwa umri zinawezaje kuwaathiri wale wenye umri mkubwa?
8 Hata tuwe na umri gani, tunapokuwa wagonjwa ni rahisi zaidi kusema au kufanya mambo ambayo tutajutia. (Mhu. 7:7; Yak. 3:2) Kwa mfano, mwanamume mwaminifu Ayubu alipokuwa akiteseka, maneno yake yalikuwa “mazungumzo ya ovyoovyo.” (Ayu. 6:1-3) Kwa kuongezea, tatizo la afya linaweza kusababisha watu wenye umri mkubwa waseme au kutenda mambo ambayo kwa kawaida wasingefanya. Bila shaka, hakuna hata mmoja wetu ambaye angependa kutumia umri au hali yetu ya afya kama kisingizio cha kutoonyesha fadhili au kudai mengi. Na ikiwa tutagundua kwamba tumesema jambo lisilo na upendo, hatupaswi kusita kuomba msamaha.—Mt. 5:23, 24.
JINSI YA KUDUMISHA SHANGWE
Unawezaje kudumisha shangwe yako licha ya chagamoto zinazotokana na kusonga kwa umri? (Tazama fungu la 9-13)
9. Kwa nini ukubali msaada kutoka kwa wengine? (Tazama pia picha.)
9 Kubali msaada kutoka kwa wengine. (Gal. 6:2) Huenda mwanzoni ukaona jambo hilo kuwa gumu. Dada anayeitwa Gretl anasema hivi: “Nyakati nyingine mimi huona kuwa vigumu kukubali msaada wa wengine kwa sababu ninahisi nitakuwa mzigo kwa wengine. Imechukua muda mrefu kubadili mtazamo wangu na kukubali kwa unyenyekevu kwamba ninahitaji msaada.” Unapokubali msaada kutoka kwa wengine, unawaruhusu wapate shangwe inayotokana na kutoa. (Mdo. 20:35) Na bila shaka utafurahi kuona jinsi wengine wanavyokupenda na kukujali sana.
(Tazama fungu la 9)
10. Kwa nini unapaswa kukumbuka kuonyesha shukrani? (Tazama pia picha.)
10 Onyesha shukrani. (Kol. 3:15; 1 The. 5:18) Watu wengine wanapotutendea mambo mazuri, huenda moyoni tukashukuru lakini tukasahau kuwaambia. Hata hivyo, tukitabasamu na kusema asante, tutafanya rafiki zetu wahisi kwamba tunawathamini. Leah, anayewatunza watu wenye umri mkubwa Betheli, anasema hivi: “Dada mmoja ninayemtunza huniandikia kadi ndogo zenye maneno ya shukrani. Ujumbe huwa mfupi, lakini una maneno mazuri. Ninapenda sana kupokea kadi hizo, na ninafurahi kujua kwamba anathamini msaada wangu.”
(Tazama fungu la 10)
11. Unawezaje kuwasaidia wengine? (Tazama pia picha.)
11 Jitahidi kuwasaidia wengine. Unapotumia wakati na nguvu zako kuwasaidia wengine, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba hutakazia fikira matatizo yako mwenyewe. Methali moja ya barani Afrika inawafananisha wenye umri mkubwa na maktaba iliyojaa vitabu vyenye hekima nyingi. Lakini vitabu vilivyoachwa kwenye rafu havifundishi au kutoa masimulizi. Hivyo, ukiwa “maktaba iliyo hai,” chukua hatua ya kwanza kuwapatia vijana ujuzi na uzoefu wako. Waulize maswali, na uwasikilize. Wafundishe kwa nini kuishi kulingana na viwango vya Yehova sikuzote ndilo jambo bora na litakalowapatia furaha. Bila shaka, utapata shangwe unapowafariji na kuwaimarisha rafiki zako vijana.—Zab. 71:18.
(Tazama fungu la 11)
12. Kulingana na Isaya 46:4, Yehova anaahidi kuwafanyia nini wenye umri mkubwa? (Tazama pia picha.)
12 Sali kwa Yehova ili upate nguvu. Ingawa huenda ukahisi umechoka kimwili au kihisia, Yehova “hachoki kamwe wala haishiwi na nguvu.” (Isa. 40:28) Yehova anatumiaje nguvu zake zisizo na mipaka? Njia moja ni kwa kuwaimarisha ndugu na dada waaminifu wenye umri mkubwa. (Isa. 40:29-31) Kwa kweli, anaahidi kuwasaidia. (Soma Isaya 46:4.) Na sikuzote Yehova hutimiza ahadi zake. (Yos. 23:14; Isa. 55:10, 11) Unaposali na kuhisi upendo na utegemezo wa Yehova kibinafsi, utahisi shangwe.
(Tazama fungu la 12)
13. Kulingana na 2 Wakorintho 4:16-18, tunapaswa kukumbuka nini? (Tazama pia picha.)
13 Kumbuka kwamba hali unazokabili ni za muda mfupi. Tunapokumbuka kwamba hali fulani ngumu tunayokabili ni ya muda mfupi, tunaweza kuivumilia kwa urahisi zaidi. Na Biblia inatuhakikishia kwamba uzee na afya mbaya ni mambo ya muda mfupi. (Ayu. 33:25; Isa. 33:24) Hivyo, unaweza kupata shangwe kwa kujua kwamba wakati ujao utakuwa na maisha bora kabisa. (Soma 2 Wakorintho 4:16-18.) Hata hivyo, watu wengine wanawezaje kutoa msaada?
(Tazama fungu la 13)
JINSI WENGINE WANAVYOWEZA KUTOA MSAADA
14. Kwa nini ni muhimu kuwatembelea au kuwapigia simu wale wenye umri mkubwa?
14 Watembelee au wapigie simu kwa ukawaida ndugu na dada wenye umri mkubwa. (Ebr. 13:16) Wale wenye umri mkubwa wanaweza kuhisi upweke. Ndugu anayeitwa Camille ambaye hawezi kutoka nje, anasema hivi: “Ninalazimika kubaki ndani ya nyumba kuanzia asubuhi hadi jioni. Hivyo, ninachoka sana. Nyakati nyingine, ninahisi kama simba aliyezeeka ambaye amefungwa kwenye banda. Ninakuwa na wasiwasi na kukasirika.” Tunapowatembelea wale wenye umri mkubwa, tunawahakikishia kwamba wao ni wenye thamani kwetu na tunawapenda. Huenda tunakumbuka wakati ambapo tulipanga kumpigia simu au kumtembelea ndugu au dada mwenye umri mkubwa katika kutaniko letu lakini hatukufanya hivyo. Maisha yetu ni yenye shughuli nyingi. Hivyo, ni jambo gani litakalotusaidia ‘kuhakikisha mambo muhimu zaidi,’ kutia ndani kuwatembelea walio na umri mkubwa? (Flp. 1:10) Huenda ikafaa ikiwa utaandika katika kalenda yako kikumbusho cha kuwatumia ujumbe watu wenye umri mkubwa katika kutaniko lenu au kuwapigia simu. Unaweza pia kupanga wakati hususa wa kuwatembelea; badala ya kusubiri nafasi ijitokeze.
15. Vijana na wale wenye umri mkubwa wanaweza kufanya nini pamoja?
15 Ikiwa wewe ni kijana, huenda unafikiria ni mambo gani utakayozungumzia au kufanya pamoja na wale wenye umri mkubwa. Lakini usiwe na wasiwasi. Uwe tu rafiki nzuri. (Met. 17:17) Zungumza na wenye umri mkubwa kabla au baada ya mikutano ya kutaniko. Labda unaweza kuwaomba wakueleze andiko wanalopenda zaidi au kumbukumbu zenye kufurahisha za mambo waliyotenda walipokuwa watoto. Unaweza pia kuwaalika watazame pamoja nawe programu ya JW Broadcasting®. Pia, unaweza kuwasaidia wenye umri mkubwa kwa njia hususa. Kwa mfano, unaweza kuwasaidia kusasisha vifaa vyao vya kielektroni au kupakua machapisho ya kujifunzia ya karibuni zaidi. Dada anayeitwa Carol, anasema hivi: “Jitolee kufanya pamoja na wenye umri mkubwa mambo ambayo wewe unafurahia. Ingawa nina umri mkubwa, bado ninataka kufurahia maisha. Ninapenda kufanya ununuzi, kula kwenye mikahawa, na kufurahia uumbaji.” Na dada anayeitwa Maira, anasema hivi: “Rafiki yangu mmoja ana umri wa miaka 90. Tuna tofauti ya umri wa miaka 57. Lakini mara nyingi mimi husahau tofauti hiyo kwa sababu sisi hucheka pamoja na kutazama sinema pamoja. Na tunapokabili matatizo, sisi hushauriana.”
16. Kwa nini ni jambo linalofaa kuandamana pamoja na wenye umri mkubwa wanapoenda kumwona daktari?
16 Andamana nao wanapoenda kumwona daktari. Zaidi ya kuwapatia usafiri wale wenye umri mkubwa, huenda unaweza kuhakikisha kwamba wahudumu wa afya wanawatendea kwa njia nzuri na kuwapatia msaada wanaohitaji. (Isa. 1:17) Unaweza kumsaidia ndugu au dada mwenye umri mkubwa kwa kuandika mambo ambayo daktari anasema. Dada mwenye umri mkubwa anayeitwa Ruth, anasema hivi: “Mara nyingi ninapoenda hospitali peke yangu, daktari hachukui kwa uzito mambo ninayomwambia. Huenda madaktari wakasema mambo kama vile, ‘Tatizo lako ni la kisaikolojia; unaliwazia tu kichwani.’ Lakini ninapoandamana na mtu mwingine, daktari hunitendea vizuri zaidi. Ninawashukuru sana ndugu na dada wanaotenga wakati ili kuandamana nami.”
17. Ni aina gani za huduma unazoweza kufurahia pamoja na wenye umri mkubwa?
17 Hubiri pamoja nao. Baadhi ya wale wenye umri mkubwa hawana nguvu za kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa mfano, je, unaweza kumwalika dada mwenye umri mkubwa afanye pamoja nawe mahubiri ya kigari? Unaweza hata kumpatia kiti ili aketi karibu na kigari cha machapisho. Au je, unaweza kumpeleka ndugu mwenye umri mkubwa kwenye funzo la Biblia, au hata kuongoza funzo hilo nyumbani kwa ndugu huyo? Wazee wanaweza kufikiria kupanga mikutano ya utumishi katika nyumba za wenye umri mkubwa ili waweze kushiriki katika huduma kwa urahisi zaidi. Jambo lolote tunalofanya ili kuwaheshimu wenye umri mkubwa humfurahisha Yehova.—Met. 3:27; Rom. 12:10.
18. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?
18 Tumekumbushwa kwamba Yehova anawapenda na kuwathamini wenye umri mkubwa. Na sisi sote kutanikoni tunawathamini pia! Kuzeeka si jambo rahisi, lakini kwa msaada wa Yehova unaweza kudumisha shangwe yako. (Zab. 37:25) Inatia moyo sana kujua kwamba wakati ujao utakuwa na maisha bora kabisa! Namna gani ikiwa unamtunza mtu mwenye umri mkubwa, mtoto, au rafiki ambaye ni mgonjwa? Unawezaje kudumisha shangwe yako? Tutazungumzia jibu la swali hilo katika makala inayofuata.
WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu
a Tazama kwenye jw.org na programu ya JW Library® video yenye kichwa Wenye Umri Mkubwa—Mna Daraka Muhimu.