Jumatatu, Julai 28
Yule aliye katika muungano na ninyi ni mkuu kuliko yule aliye katika muungano na ulimwengu.—1 Yoh. 4:4.
Unapoogopa, tafakari mambo ambayo Yehova atafanya wakati ujao Shetani atakapoondolewa. Onyesho lililotolewa kwenye programu ya kusanyiko la eneo la mwaka wa 2014 lilionyesha baba akizungumza na familia yake kuhusu jinsi ambavyo maneno ya 2 Timotheo 3:1-5 yangesomwa ikiwa mistari hiyo iliyotabiriwa ingezungumzia hali zitakavyokuwa katika Paradiso. Alisema hivi: “Katika ulimwengu mpya, kutakuwa na nyakati zenye furaha sana. Maana watu watakuwa wenye kupendana, wenye kupenda mambo ya kiroho, wenye kiasi, wanyenyekevu, wenye kumsifu Mungu, wanaotii wazazi, wenye shukrani, washikamanifu, walio na upendo wa asili, wanaotaka makubaliano, wanaosema mema kuhusu wengine sikuzote, wanaojizuia, wapole, wanaopenda wema, wanaotumainika, wenye kutii, wanyenyekevu katika akili, wanaompenda Mungu badala ya kupenda raha, wakichochewa na upendo wa kweli kwa Mungu; nawe shikamana na watu hao.” Je, wewe huzungumza na watu wa familia yako au waabudu wenzako kuhusu jinsi maisha yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya? w24.01 1:13-14
Jumanne, Julai 29
Nimekukubali.—Luka 3:22.
Tunafurahi sana kujua kwamba Yehova anawakubali watu wake wakiwa kikundi! Biblia inasema hivi: “Yehova anawafurahia watu wake.” (Zab. 149:4) Hata hivyo, wakati mwingine baadhi ya watu wanavunjika moyo na kujiuliza, ‘Je, Mungu ananikubali mimi binafsi?’ Watumishi wengi waaminifu wa Yehova walioishi nyakati za Biblia, pindi fulani walihangaishwa na mawazo kama hayo. (1 Sam. 1:6-10; Ayu. 29:2, 4; Zab. 51:11) Biblia inaonyesha wazi kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kupata kibali cha Yehova. Jinsi gani? Ni lazima tuonyeshe kwamba tunamwamini Yesu Kristo na kubatizwa. (Yoh. 3:16) Hivyo, tunaonyesha hadharani kwamba tumetubu dhambi zetu na tumemwahidi Mungu kuwa tutafanya mapenzi yake. (Mdo. 2:38; 3:19) Yehova anafurahi tunapochukua hatua hizo ili kusitawisha uhusiano mzuri pamoja naye. Maadamu tunaendelea kufanya yote tuwezayo ili kuishi kulingana na ahadi tuliyotoa tulipojiweka wakfu, Yehova anatukubali na kutuona kuwa rafiki zake wa karibu.—Zab. 25:14. w24.03 13:1-2
Jumatano, Julai 30
Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.—Mdo. 4:20.
Tunaweza kuwaiga wanafunzi hao kwa kuendelea kuhubiri hata ikiwa wenye mamlaka watatuamuru tuache kuhubiri. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia kutimiza huduma yetu. Hivyo, sali ili upate ujasiri na hekima na umwombe Yehova akusaidie uvumilie licha ya matatizo. Wengi wetu tunakabiliana na changamoto za magonjwa au za kihisia, kufiwa na mpendwa wetu, hali fulani ngumu katika familia, mateso, au matatizo mengine. Na mambo kama vile mlipuko wa magonjwa na vita yamefanya iwe vigumu hata zaidi kushughulika na changamoto hizo. Mmiminie Yehova moyo wako. Mwambie kuhusu hali yako kama ambavyo ungemwambia rafiki wa karibu. Uwe na uhakika kwamba Yehova “atatenda kwa niaba yako.” (Zab. 37:3, 5) Kudumu katika sala kutatusaidia ‘kuvumilia chini ya dhiki.’ (Rom. 12:12) Yehova anajua mambo ambayo waabudu wake wanavumilia—yeye “husikia kilio chao cha kuomba msaada.”—Zab. 145:18, 19. w23.05 20:12-15