Jumanne, Septemba 16
Tumeamini na tumejua kwamba wewe ndiye Mtakatifu wa Mungu.—Yoh. 6:69.
Mtume Petro alikuwa mshikamanifu; hakuruhusu jambo lolote limzuie kuendelea kumfuata Yesu. Kwa mfano, pindi fulani alionyesha ushikamanifu wake Yesu aliposema jambo ambalo wanafunzi wake hawakuelewa. (Yoh. 6:68) Bila kusubiri ufafanuzi, wengi waliacha kumfuata Yesu. Lakini Petro hakuacha. Alitambua kwamba Yesu tu ndiye aliyekuwa na “maneno ya uzima wa milele.” Yesu alijua kwamba Petro na wale mitume wengine wangemwacha. Ingawa hivyo, Yesu alikuwa na uhakika kwamba Petro angerudi na kuendelea kuwa mwaminifu. (Luka 22:31, 32) Yesu alielewa kwamba “roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” (Marko 14:38) Hivyo, hata baada ya Petro kukana kwamba hamjui Yesu, Yesu hakumwacha mtume huyo. Baada ya kufufuliwa Yesu alimtokea Petro—inaonekana Petro alikuwa peke yake. (Marko 16:7; Luka 24:34; 1 Kor. 15:5) Hilo lilimwimarisha mtume huyo ambaye alikuwa amehuzunika sana! w23.09 40:9-10
Jumatano, Septemba 17
Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa na ambao dhambi zao zimefunikwa.—Rom. 4:7.
Mungu anasamehe au kufunika dhambi za wale wanaoweka imani kwake. Anawasamehe kabisa na hatahesabu dhambi zao kamwe. (Zab. 32:1, 2) Yehova anawaona watu hao kuwa hawana hatia na waadilifu kwa msingi wa imani yao. Ingawa Abrahamu, Daudi, na waabudu wengine waaminifu wa Mungu walitangazwa kuwa waadilifu, bado walikuwa watenda dhambi wasio wakamilifu. Lakini kwa sababu ya imani yao, Mungu aliwaona kuwa wasio na hatia hasa alipowalinganisha na wale ambao hawakuwa na imani kwake. (Efe. 2:12) Kama mtume Paulo anavyoeleza waziwazi kwenye barua yake, ni lazima mtu awe na imani ili kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Abrahamu na Daudi, na ni hivyo kwetu pia. w23.12 50:6-7
Alhamisi, Septemba 18
Sikuzote na tumtolee Mungu dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo yetu ambalo hulitangaza jina lake hadharani.—Ebr. 13:15.
Leo, Wakristo wote wana pendeleo la kumtolea Yehova dhabihu kwa kutumia wakati, nguvu, na mali zao, ili kuendeleza kazi ya Ufalme wa Mungu. Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini pendeleo letu la kumwabudu Yehova kwa kumtolea dhabihu zetu zilizo bora kabisa. Mtume Paulo anataja mambo mbalimbali kuhusu ibada yetu ambayo hatupaswi kamwe kuyapuuza. (Ebr. 10:22-25) Mambo hayo yanatia ndani kumkaribia Yehova katika sala, kutoa tangazo la hadharani la tumaini letu, kukutana pamoja tukiwa kutaniko, na kutiana moyo “zaidi kwa kadiri [tunavyoona] siku ile [ya Yehova] ikikaribia.” Karibu na mwisho wa simulizi la Ufunuo, malaika wa Yehova anasema maneno yafuatayo mara mbili ili kusisitiza: “Mwabudu Mungu!” (Ufu. 19:10; 22:9) Acheni tuendelee kukumbuka kweli hizi zenye kina za kiroho kuhusu hekalu kubwa la kiroho la Yehova na pendeleo letu lenye thamani la kumwabudu Mungu wetu Mkuu! w23.10 45:17-18