BARUA YA PILI KWA TIMOTHEO
1 Paulo, mtume wa Kristo Yesu kwa mapenzi ya Mungu kulingana na ahadi ya uzima ambao ni kupitia Kristo Yesu,+ 2 kwa Timotheo, mtoto mpendwa:+
Na uwe na fadhili zisizostahiliwa, rehema, na amani kutoka kwa Mungu Baba na Kristo Yesu Bwana wetu.
3 Ninamshukuru Mungu, ninayemtolea utumishi mtakatifu kama mababu zangu walivyofanya, na nikiwa na dhamiri safi, siachi kamwe kukukumbuka katika dua zangu usiku na mchana. 4 Ninapokumbuka machozi yako, ninatamani kukuona ili nijawe na shangwe. 5 Kwa maana ninaikumbuka imani yako isiyo na unafiki,+ ambayo kwanza ilikuwa ndani ya nyanya yako Loisi na mama yako Eunike, lakini ambayo nina hakika imo ndani yako pia.
6 Kwa sababu hii ninakukumbusha uichochee kama moto zawadi ya Mungu iliyo ndani yako uliyopokea nilipoweka mikono yangu juu yako.+ 7 Kwa maana Mungu hakutupatia roho ya woga,+ bali roho ya nguvu+ na ya upendo na ya utimamu wa akili. 8 Basi usione aibu kuhusu ushahidi juu ya Bwana wetu,+ au kunihusu mimi, mfungwa kwa ajili yake, bali shiriki katika kuvumilia dhiki+ kwa ajili ya habari njema kwa kutegemea nguvu za Mungu.+ 9 Yeye alituokoa na kutuita kwa mwito mtakatifu,+ si kwa sababu ya matendo yetu, bali kwa sababu ya kusudi lake mwenyewe na fadhili zisizostahiliwa.+ Tulipewa fadhili hizo kuhusiana na Kristo Yesu kabla ya nyakati za kale, 10 lakini sasa zimefanywa kuwa wazi kabisa kupitia ufunuo wa Mwokozi wetu, Kristo Yesu,+ ambaye amefuta kifo+ na kuangaza nuru juu ya uzima+ na kutoweza kuharibika+ kupitia habari njema,+ 11 ambayo kwa ajili yake mimi niliwekwa rasmi kuwa mhubiri na mtume na mwalimu.+
12 Ndiyo sababu ninavumilia pia mambo haya,+ lakini sioni aibu.+ Kwa maana ninamjua Yule ambaye nimemwamini, nami nina uhakika kwamba anaweza kulinda kile nilichoweka amana kwake mpaka siku hiyo.+ 13 Endelea kushika kigezo cha* maneno yenye manufaa*+ uliyosikia kutoka kwangu kwa imani na upendo unaotokana na muungano pamoja na Kristo Yesu. 14 Linda amana hii nzuri kupitia roho takatifu, inayokaa ndani yetu.+
15 Unajua jambo hili, kwamba watu wote katika mkoa wa Asia+ wameniacha, Figelo na Hermogene ni kati yao. 16 Bwana na aionyeshe rehema nyumba ya Onesiforo,+ kwa maana aliniburudisha mara nyingi, naye hakuaibika kwa sababu ya minyororo yangu ya gereza. 17 Kinyume chake, alipokuwa Roma, alinitafuta kwa bidii mpaka akanipata. 18 Bwana na amruhusu apate rehema kutoka kwa Yehova* katika siku ile. Nawe unajua vema utumishi wote aliofanya huko Efeso.
2 Kwa hiyo, wewe mwanangu,+ endelea kujipatia nguvu katika fadhili zisizostahiliwa zilizo katika Kristo Yesu; 2 na mambo uliyoyasikia kutoka kwangu yaliyothibitishwa na mashahidi wengi,+ mambo hayo uwakabidhi wanaume waaminifu, ambao watastahili vya kutosha kuwafundisha wengine. 3 Ukiwa mwanajeshi mwema+ wa Kristo Yesu, shiriki katika kuvumilia dhiki.+ 4 Mtu anayetumikia akiwa mwanajeshi hajihusishi* katika shughuli za kibiashara* za maisha, ili apate kibali cha yule aliyemwandikisha kuwa mwanajeshi. 5 Hata katika michezo, yeyote anayeshindana havikwi taji asiposhindana kulingana na sheria.+ 6 Mkulima anayefanya kazi kwa bidii lazima awe wa kwanza kula matunda. 7 Fikiria daima mambo ninayosema; Bwana atakupatia uelewaji* katika mambo yote.
8 Kumbuka kwamba Yesu Kristo alifufuliwa kutoka kwa wafu+ na alikuwa uzao wa Daudi,*+ kulingana na habari njema ninayohubiri,+ 9 ambayo kwa ajili yake ninavumilia na kufungwa gerezani kama mhalifu.+ Hata hivyo, neno la Mungu halifungwi.+ 10 Kwa sababu hiyo ninaendelea kuvumilia mambo yote kwa ajili ya wale waliochaguliwa,+ ili wao pia wapate wokovu ambao ni kupitia Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele. 11 Maneno haya yanategemeka: Hakika ikiwa tulikufa pamoja, tutaishi pamoja pia;+ 12 tukiendelea kuvumilia, tutatawala pamoja pia tukiwa wafalme;+ tukimkana, naye pia atatukana sisi;+ 13 tukikosa kuwa waaminifu, yeye anabaki kuwa mwaminifu, kwa maana hawezi kujikana mwenyewe.
14 Endelea kuwakumbusha mambo haya, ukiwaagiza* mbele za Mungu wasipigane kuhusu maneno, jambo hilo halina faida kabisa kwa sababu linawadhuru* wale wanaosikiliza. 15 Fanya yote unayoweza ili ujitoe kwa Mungu ukiwa mtu aliyekubaliwa, mfanyakazi asiye na lolote la kuonea aibu, ukilitumia sawasawa neno la kweli.+ 16 Lakini kataa maneno matupu ambayo huchafua mambo matakatifu,+ kwa maana yataongoza kwenye kutomwogopa Mungu zaidi na zaidi, 17 na neno lao litaenea kama kidonda kinachooza. Himenayo na Fileto ni kati yao.+ 18 Watu hao wamegeuka kutoka kwenye kweli, wakisema kwamba tayari ufufuo umetukia,+ nao wanapindua imani ya wengine. 19 Ingawa hivyo, msingi imara wa Mungu unakaa ukiwa umesimama, ukiwa na muhuri huu: “Yehova* anawajua walio wake,”+ na “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova*+ na aukatae ukosefu wa uadilifu.”
20 Basi ndani ya nyumba kubwa kuna vyombo vya dhahabu na fedha, na pia kuna vyombo vya miti na vya udongo, na vingine ni vya matumizi yanayoheshimika lakini vingine ni vya matumizi yasiyoheshimika. 21 Kwa hiyo, yeyote akijiepusha na hivyo vya mwisho, atakuwa kifaa* cha matumizi yanayoheshimika, kilichotakaswa, chenye faida kwa bwana wake, kilichotayarishwa kwa ajili ya kila kazi njema. 22 Basi zikimbie tamaa za ujana, lakini fuatilia uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na wale wanaomwitia Bwana kwa moyo safi.
23 Isitoshe, kataa mabishano ya kipumbavu na ya kijinga,+ ukijua kwamba hayo hutokeza mapigano. 24 Kwa maana mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole* kwa wote,+ mwenye uwezo wa kufundisha, anayejizuia anapokosewa,+ 25 akiwafundisha kwa upole wale wasio na mwelekeo unaofaa.+ Huenda Mungu akawasaidia kutubu* na kupata ujuzi sahihi wa kweli,+ 26 nao warudiwe na fahamu na kutoka kwenye mtego wa Ibilisi, kwa kuwa amewanasa wakiwa hai ili wafanye mapenzi yake.+
3 Lakini ujue jambo hili, kwamba katika siku za mwisho+ kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. 2 Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, 3 wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia,* wakali, wasiopenda wema, 4 wasaliti, wenye vichwa vigumu, waliojaa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu, 5 wakionekana kama watu wanaomwogopa Mungu lakini wakizikana nguvu zake;+ nawe jiepushe nao. 6 Kutoka miongoni mwao huinuka watu wanaoingia kwa ujanja katika nyumba na kuwachukua mateka wanawake walio dhaifu ambao wamelemewa na mizigo ya dhambi, wakiongozwa na tamaa mbalimbali, 7 wakijifunza sikuzote lakini hawawezi kamwe kupata ujuzi sahihi wa kweli.
8 Basi kama vile Yane na Yambre walivyompinga Musa, vivyo hivyo hawa pia wanaendelea kuipinga kweli. Watu hao wamepotoshwa akili kabisa, wakiwa wamekataliwa kuhusiana na imani. 9 Hata hivyo, hawatafanya maendeleo zaidi, kwa maana upumbavu* wao utakuwa wazi kwa watu wote, kama ilivyokuwa kwa watu hao wawili.+ 10 Lakini wewe umefuata kwa ukaribu fundisho langu, mwendo wangu wa maisha,+ kusudi langu, imani yangu, subira yangu, upendo wangu, uvumilivu wangu, 11 mateso na shida kama zile nilizopata huko Antiokia,+ Ikoniamu,+ na Listra.+ Nilivumilia mateso hayo, naye Bwana aliniokoa kutoka katika hayo yote.+ 12 Kwa kweli, wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu* katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.+ 13 Lakini watu waovu na wajanja wataendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi, wakipotosha na kupotoshwa.+
14 Hata hivyo, endelea kufuata mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini,+ ukijua ulijifunza mambo hayo kutoka kwa nani, 15 na kwamba tangu utoto mchanga+ umeyajua maandishi matakatifu,+ ambayo yanaweza kukufanya uwe mwenye hekima ili upate wokovu kupitia imani katika Kristo Yesu.+ 16 Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu+ nalo ni lenye faida kwa kufundisha,+ kwa kukaripia, kwa kunyoosha* mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu,+ 17 ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.
4 Ninakuagiza kwa uzito mbele za Mungu na Kristo Yesu, ambaye atawahukumu+ walio hai na wafu,+ na kwa ufunuo+ wake na Ufalme wake:+ 2 Lihubiri neno;+ fanya hivyo kwa uharaka katika nyakati zinazofaa na nyakati ngumu; karipia,+ kemea, himiza, kwa subira yote na ustadi wa kufundisha.+ 3 Kwa maana kutakuwa na wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye manufaa,*+ bali, kulingana na tamaa zao, watajikusanyia walimu ili masikio yao yafurahishwe.*+ 4 Wataacha kuisikiliza ile kweli, nao watageukia hadithi za uwongo. 5 Ingawa hivyo, wewe tunza akili zako katika mambo yote, vumilia hali ngumu,+ fanya kazi ya mweneza-injili,* timiza kikamili huduma yako.+
6 Kwa maana mimi tayari ninamiminwa kama toleo la kinywaji,+ na wakati wangu wa kufunguliwa+ umekaribia sana. 7 Nimepigana pigano zuri,+ nimekimbia mbio mpaka mwisho,+ nimeishika imani. 8 Tangu sasa na kuendelea nimewekewa akiba ya taji la uadilifu,+ ambalo Bwana, aliye mwamuzi mwadilifu,+ atanipa kuwa thawabu katika siku ile,+ lakini si mimi tu, bali pia wote ambao wamependa kufunuliwa kwake.
9 Jitahidi kabisa ili uje kwangu upesi. 10 Kwa maana Dema+ ameniacha kwa sababu aliupenda mfumo wa mambo* wa sasa, naye ameenda Thesalonike, Kresensi ameenda Galatia, Tito ameenda Dalmatia. 11 Luka tu ndiye aliye pamoja nami. Mchukue Marko uje pamoja naye, kwa maana ni mwenye faida kwangu katika huduma. 12 Lakini nimemtuma Tikiko+ aende Efeso. 13 Utakapokuja, ilete ile kanzu niliyomwachia Karpo kule Troa, na vile vitabu vya kukunjwa, hasa vile vya ngozi.
14 Aleksanda yule fundi wa shaba alinisababishia madhara mengi. Yehova* atamlipa kulingana na matendo yake.+ 15 Nawe pia jihadhari naye, kwa maana aliupinga ujumbe wetu kwa kadiri kubwa sana.
16 Katika kujitetea kwangu mara ya kwanza hakuna yeyote aliyekuja upande wangu, bali wote waliniacha—wasihukumiwe kwa jambo hilo. 17 Lakini Bwana alisimama karibu nami na kunitia nguvu, ili kupitia kwangu kazi ya kuhubiri itimizwe kikamili na mataifa yote yaisikie;+ nami niliokolewa kutoka katika kinywa cha simba.+ 18 Bwana atanikomboa kutoka katika kila tendo la uovu naye ataniokoa kwa ajili ya Ufalme wake wa mbinguni.+ Utukufu na uwe kwake milele na milele. Amina.
19 Uwape salamu zangu Priska na Akila+ na nyumba ya Onesiforo.+
20 Erasto+ alibaki Korintho, lakini nilimwacha Trofimo+ akiwa mgonjwa huko Mileto. 21 Jitahidi kabisa ili ufike kabla ya majira ya baridi kali.
Eubulo anakutumia salamu zake, na pia Pudensi na Lino na Klaudia na ndugu wote.
22 Bwana na awe pamoja na roho unayoonyesha. Fadhili zake zisizostahiliwa na ziwe pamoja nawe.
Au “kielelezo cha.”
Au “yenye afya; yenye faida.”
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “hajifungi.”
Au labda, “shughuli za kila siku.”
Au “utambuzi.”
Tnn., “wa mbegu ya Daudi.”
Tnn., “ukiwatolea ushahidi kamili.”
Au “linawaharibu; linawavuruga.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “chombo.”
Au “mwenye busara.”
Au “kubadili mawazo.”
Au “wasiojidhibiti.”
Au “ujinga.”
Angalia Kamusi.
Au “kurekebisha.”
Au “lenye afya; lenye faida.”
Au “waambiwe mambo wanayotaka kusikia.”
Au “endelea kuhubiri habari njema.”
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A5.