‘Kuvua Watu katika Aktiki’
Kila wakati wa kiangazi wengi wa mashahidi wa Yehova wanahubiri katika kaeneo “yasiyogawiwa mtu”—maeneo yaliyo mbali yasiyo na makundi yaliyoanzishwa huko. Wengi wao ni watu wanaofanya kazi ya kuajiriwa na wanafunzi wanaotumia likizo yao kufanya hivyo. Wengine ni mapainia wa wakati wote wanaopanua huduma yao. Wanapata furaha ya kuleta habari njema kwa watu walio peke yao na ya kuletwa karibu zaidi na jamaa na ndugu zao wa kiroho. Hili ni simulio la safari kama hiyo katika kaskazini ya mbali.
POLEPOLE mashua ya kuvua samaki iitwayo Skagstein iliteremka kutoka kwa gati. Ilikuwa jioni mapema mwa kiangazi. Upepo mwanana wa mashariki ulitokeza viwimbi kwenye bahari na kuleta burudiko lenye kutuliza kutokana na munuko wa samaki na mafuta ya samaki. Tukiwa tumesimama kwenye staha, tulipunga mikono na kusema kwaheri kwa Batsfjord, kijiji kilicho kikubwa zaidi cha kuvulia samaki katika Finnmark Mashariki, Norwei.
Ndani ya mashua lilikuwamo kundi la watu wanane. Øivind na Åshild walikuwa wamekuja Batsfjord miaka 11 mapema iii kusaidia katika kazi ya kuhubiri katika eneo hilo lisilogawiwa mtu. Sasa, walipokuwa wakihamia eneo jingine, kundi la wahubiri wa Ufalme karibu 40 lilikuwa linasitawi hapa. Wale wengine katika kundi hilo la mabahari walikuwa ni nahodha, Janie (ambaye alijipatia riziki kwa kuvua samaki na alikuwa painia “wa wakati kwa wakati“), dada wawili mapainia, mwendeshaji mmoja wa mashine ya kuchimbulia, mfanya kazi mmoja wa viwandani, na karani mmoja wa afisi kutoka Makao ya Betheli ya Norwei. Ni kitu gani kilichokuwa kimeleta kikundi hiki pamoja? Na ni safari ya baharini ya namna gani waliyokuwa wanaanza?
Kwenda Kisiwa kwa Kisiwa
Wakati huu Janie hakuwa anatafuta samaki-kodi. Mpango ulikuwa kwamba sisi tutembelee kisiwa kwa kisiwa na mtaa wa pwani kwa mtaa mtaa wa pwani tukiwa ndani ya mashua Skagstein kutoka Batsfjord katika kaskazini ya mbali kufika neysund katika jimbo la Nordland. Tungekuwa tukieneza zaidi ya nusu ya pwani ya Norwei. Kwa sababu gani? Basi, nyingi za sehemu hizi zingeweza kufikiwa tu kwa mashua ya mtu binafsi, na ni mara moja tu kwa kila miaka kadha kwamba Mashahidi wa Yehova hutembelea sehemu hizi wakiwa na ujumbe wa Ufalme. Tulikuwa tumeamua twende ‵kuvua watuʼ katika hii mitaa iliyo pwani.—Mathayo 4:18, 19.
Mashua ikaondoka kwenye ghuba ya Båtsfjorden ikaelekea magharibi kufuata pwani usiku wote. Ilikuwa tarehe moja Julai. Jua la usiku wa manane, likifichwa na mawingu laini mfano wa blanketi, liliangaza kwa mwangaza mwanana, wa rangi ya kijivu. Maelfu ya ndege wa baharini shakwe na kitiwake walikuwa wakionekana wakiwa juu ya majabali. Hali ya mawimbi ya bahari kuu ilikuwa nzuri, kulingana na nahodha. Lakini kwa baadhi yetu sisi watu wa mashambani tusiojua lo lote juu ya bahari na vyombo baharini, ilikuwa yenye mchafuko kidogo.
Kesho yake asubuhi tuliingia kwenye gati katika Honningsvag. Hapa ndipo kazi yetu ya kuhubiri—“kuvua“—ingeanza. Watu wa kaskazini mwa Norwei wana sifa ya kuwa wakaribishaji wageni. Tulipokwisha kutoa habari fupi ya tume yetu, kwa kawaida tulikuwa tunapewa kiti cha kukalia jikoni na kupewa kahawa. Kisha ilikuwa lazima tueleze kikamili sisi ni nani, ni wapi tulikotoka, kazi yetu, jina na ukubwa wa mashua yetu, kama tulikuwa tumevua samaki wo wote kufikia sasa, na sehemu iliyobaki ya safari yetu. Ni baada tu ya hayo kuwa yamekwisha kuelezwa ndipo tungeweza kuingia kwenye sababu hasa ya ziara yetu—habari njema za Ufalme wa Mungu.
Itikio Changamfu Katika Aktik Iliyogandamana kwa Baridi
Je! ujumbe huo ungevutia watu hawa walio kwenye kisiwa kilicho kilometa 480 kaskazini mwa Duara ya Aktiki? Ni nini yaliyokuwa mahangaikio yao hasa? Ni yale yale yanayohangaikiwa na watu kila mahali penginepo: ukosefu wa haki za kijamii, ukosefu wa kazi za kuajiriwa, pesa, jamaa na matatizo ya kibinafsi. Pia walikuwa na wasiwasi juu ya hali yenye wasiwasi ya ulimwengu—mahusiano ya kaskazini na kusini na pambano kati ya mashariki na magharibi.
Ilikuwa rahisi kwetu kuelekeza kwenye suluhisho la Biblia—Ufalme wa Mungu. Na ilithawabisha kama nini kuona hali ya kutazamia mabaya tu na mashaka ikitoweka na mahali payo pakichukuliwa na furaha na tumaini! Watu wengi katika sehemu hizi zilizo mbali wameomba Ufalme tangu utotoni, lakini hawajapata kamwe kufahamu kweli kweli maana ya sala hiyo. (Mathayo 6:9-13) Tuliachia wengi wa wakaaji hao wa kisiwa vichapo vya Biblia na tukapanga kuandikiana nao iii kuendeleza kupendezwa kwao.
Ingawa ulikuwa wakati wa kiangazi, hali ya joto ilikuwa digrii 2 sentigredi katika Rolvsøy, na upepo wenye nguvu ulikuwa ukivuma. Akitetemeka na akiwa amevalia koti lake na kulifunga kabisa, mmoja wa akina ndugu alimwendea mwanamume aliyekuwa anasimama ukingoni mwa bahari.
“Unahisi baridi?“ akauliza yule mwanamume. “Eh . . . “ yule ndugu akasitasita. “Njoo upate kitu chenye moto cha kula na kunywa!“ Ndani ya nyumba, yule ndugu akaongozwa jikoni, ambamo mke wa yule mwanamume alikuwa na shughuli nyingi. “Je! una kahawa kwa kijana huyu?“ akauliza yule mwanamume
Akapewa kahawa yenye moto na vipande vya mkate, jam iliyotengenezewa nyumbani inayoitwa cloudberry, na samaki-salmoni. Baada ya mazungumzo yenye kupendeza, yule ndugu akaacha vichapo vya Biblia na akaendelea na mahubiri yake, akiwa amepashwa joto na kutiwa moyo. Hayo ndiyo yaliyokuwa mambo yaliyoonwa katika kutoa ushuhuda kwa watu wenye urafiki na ukaribishaji wageni katika sehemu hizi za mbali, zilizo peke yazo
Ono Lenye Kutajirisha
Mashua Skagstein ilipokuwa ikikata njia yayo kupitia mawimbi ya bahari kutoka kisiwa kimoja kwenda kingine, kikundi cha mabaharia kilichokuwamo kililetwa pamoja katika njia zaidi ya moja. Watu wanane wakiishi pamoja karibukaribu kwa siku na majuma katika mashua ya urefu wa meta 12 wanapata kujua upesi tabia za pekee za kila mmoja zilizowatofautisha. Tulijifunza kuishi pamoja na kuwa wenye kufikiriana. Zile tabia zisizopendeza zililainishwa, nao utu wetu wa Kikristo ukafanyiwa maendeleo. (Wakolosai 3:9, 10) Kwa hiyo yale mambo tuliyoyaona yalithibitika kuwa yenye kuthawabisha zaidi.
Tukiwa pamoja, tulizungumza andiko la Biblia la kila siku na tukazungumza juu ya mambo tuliyoyaona siku hiyo. Tungerudia yale yaliyokuwa yamesemwa na kufanywa na yale yangaliweza kuwa yamesemwa na kufanywa. Hilo lilitusukuma sisi tufanye jitihada zaidi tuwe na matokeo zaidi katika kuzungumza na watu. Wale waliokuwa wachanga na wapya zaidi walipokea shauri thabiti na kitia-moyo wapanue zaidi huduma yao
“Mimi nimekuwa nikifikiria huduma ya wakati wote tangu nilipobatizwa,“ akasema Bjorn mwenye miaka 27. “Wakati wa safari yetu, ile tamaa na ushujaa wa ‵kumjaribu Yehovaʼ ilikua ndani yangu kidogo kidogo. Nilipata kuona jinsi tunavyoweza kuwa na uhakika mkubwa katika Yehova. Safari hiyo ilifanya iwe rahisi kwangu kuingia katika kazi ya painia.“—Malaki 3:10
Safari hiyo ilisaidia sisi pia tuone kwa njia iliyo wazi zaidi uharaka wa nyakati. Mingi ya mitaa tuliyotembelea ilikuwa inatoweka polepole. Viwanda vya kutengeneza samaki vilikuwa vinafunga kazi. Afisi za posta na maduka yalikuwa yanafunga kazi. Watu walikuwa na wasiwasi wakiona vijana wakiondoka na kwenda kutafuta nafasi za kazi katika na miji iliyo mbali, wakiacha nyuma yao nyumba nzuri mpya-mpya na ile njia ya maisha ya kikawaida. Kuzunguka ulimwengu, mamilioni ya watu hawana makao nao wanakufa njaa. Hapa unapata kuona nyumba zisizo na watu na chakula tele kutoka baharini. Hata hivyo, ni wachache kwa kulinganisha wanaotaka hayo. Yote haya ni ushuhuda usio na maneno wa ulimwengu usio na usawaziko.
Kuendelea na Safari
Safari ikaelekea upande wa kaskazini mwa Soroya kwenda Kvnangen. Kwenye vituo fulani, tulilazimika kufika ukingoni mwa bahari kwa mtumbui wenye kuvutwa kwa makasia. Lakini kwenye sehemu nyingine Skagstein ingeweza kwenda mpaka kwenye gati. Wengi wa watu wa mahali hapo walisongamana kutuzunguka iii waone wageni hao walikuwa akina nani kwa sababu kwa hakika hatukuonekana kama wavuvi wa samaki kwao. Walipopata kujua kwamba sisi tulikuwa Mashahidi wa Yehova tukija na habari njema kutoka Biblia, kwa kawaida mazungumzo yenye shauku yalifuata.
Baada ya kueneza eneo hili, tulisafiri kuelekea Tromsø, ambapo baadhi yetu tungehudhuria “Amani ya Kimungu“ Mkusanyiko wa Wilaya. Sehemu hii ya safari yetu ilikuwa ono lenye kutokeza kweli kweli. Ulikuwa wakati wa usiku, lakini jua la usiku wa manane liliangaza kwa mwangaza wenye kungʼaa kwenye upeo wa macho. Upande wa kulia, visiwa vikubwa na vidogo vilivyotiwa giza vilisimama vikionekana kama vivuli. Kwa upande wa kushoto, milima iliyofunikwa na theluji ilimetameta katika mwangaza wa jua. Bali ya hewa ilikuwa tulivu, nayo bahari iliyo shwari ilisukwa-sukwa tu na wimbi dogo. Kila kitu kilikuwa kitulivu na kimya, isipokuwa sauti yenye mwendo wa utaratibu ya injini na muziki kidogo wenye kutuliza kutoka kwenye redio yetu. Ilikuwa hali yenye kupendeza kama nini!
Baada ya ule mkusanyiko katika Tromso, kulikuwako badiliko dogo katika kikundi chetu cha mabaharia. Kisha safari ikaendelea, ikipitia karibu na Senja na kupitia kikundi cha visiwa Vesteralen ikafika Bodo na kisha ikafika noysund, kituo chetu cha mwisho. Katika sehemu nyingi tulipokuwa njiani, kama vile Rodoy, tulikuta watu ambao walikuwa hawajapata kamwe kusema na Mashahidi wa Yehova. Miaka mingi ilikuwa imepita tangu ziara za kuhubiri zifanywe, na sasa kizazi kipya kilikuwa kimekwisha kukua na kuwa watu wazima.
Safari ya Baharini Isiyosahaulika
Kufikia wakati tulipofika Bronnoysund, ilikuwa mwisho wa Agosti. Tulipotazama nyuma kwenye majuma yaliyotumiwa tukiwa ndani ya Skagstein, tulihisi kwamba kweli kweli ilikuwa safari ya baharini isiyosahaulika. Katika safari hii tulikuwa tumetumia saa 880 kuhubiri habari njema na tukaangusha vitabu 126 na magazeti 1,026, pia tukapata maandikisho 12 ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Mbegu nyingi sana za Ufalme zilikuwa zimepandwa katika maeneo haya yanayokaliwa na watu wachache.
“Ilikuwa ndiyo likizo nzuri sana niliyopata kuwa nayo!“ akapaaza sauti mmoja wa wahubiri vijana aliyekuwa katika safari hiyo. Wale miongoni mwetu tuliopendelewa kushiriki katika safari hii tukakubali kwa moyo. Tulihisi kwamba haikuwa tu likizo nzuri bali pia mojapo mambo yenye kunufaisha na kuthawabisha zaidi kiroho tuliyokuwa tumepata kufanya.
[Ramani katika ukurasa wa 25]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
SWEDEN
FINLAND
U.S.S.R.
Brønnøysund
Rødøy
Bodø
NORWAY
Senja
Tromsø
Kvænangen
Sørøya
Rolvsøy
Honningsvåg
Båtsfjord