Alhamisi, Oktoba 23
Iweni na mizizi na kuimarishwa juu ya ule msingi.—Efe. 3:17.
Tukiwa Wakristo, haturidhiki kujua mambo ya msingi tu kuhusu Biblia. Kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu, tunatamani kujifunza “hata mambo mazito ya Mungu.” (1 Kor. 2:9, 10) Kwa nini usianze mradi wa kujifunza kibinafsi ambao utakusaidia kumkaribia Yehova hata zaidi? Kwa mfano, unaweza kuchunguza jinsi alivyowaonyesha upendo watumishi wake wa zamani na jinsi hilo linavyothibitisha kwamba anakupenda wewe pia. Unaweza kuchunguza mpango wa ibada ambao Yehova aliweka katika Israeli la kale na jinsi tunavyomwabudu leo tukiwa Wakristo. Au labda unaweza kujifunza kwa undani unabii mbalimbali ambao Yesu alitimiza wakati wa maisha na huduma yake hapa duniani. Unaweza kupata shangwe nyingi kwa kujifunza habari hizo kwa msaada wa Fahirisi au Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Kujifunza Biblia kwa kina kunaweza kuimarisha imani yako na kukusaidia upate “ujuzi kumhusu Mungu.”—Met. 2:4, 5. w23.10 18-19 ¶3-5
Ijumaa, Oktoba 24
Zaidi ya mambo yote, pendaneni sana, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.—1 Pet. 4:8.
Neno linalotafsiriwa kuwa “sana” ambalo mtume Petro ametumia, kihalisi linamaanisha “kujinyoosha” au “kuvutika.” Sehemu ya pili ya mstari huo inafafanua matokeo ya kupendana sana. Tukiwapenda sana ndugu zetu tutafunika dhambi zao. Tunaweza kuwazia hali hiyo kwa njia hii: Tunaushika upendo wetu kwa mikono miwili, kana kwamba tumeshika kitambaa kinachovutika, na tunakivuta zaidi na zaidi hadi kinafunika, si dhambi moja au mbili, bali “dhambi nyingi.” Kufunika kunamaanisha kusamehe. Kama kitambaa kinavyoweza kufunika doa, upendo unaweza kufunika udhaifu na kutokamilika kwa wengine. Upendo wetu kwa wengine unapaswa kuwa na nguvu sana hivi kwamba tunaweza kusamehe kutokamilika kwa waabudu wenzetu—hata ikiwa ni vigumu kufanya hivyo. (Kol. 3:13) Tunapowasamehe wengine, tunaonyesha kwamba upendo wetu ni wenye nguvu na tunataka kumfurahisha Yehova. w23.11 11-12 ¶13-15
Jumamosi, Oktoba 25
Shafani akaanza kukisoma mbele ya mfalme.—2 Nya. 34:18.
Alipokuwa na umri wa miaka 26, Mfalme Yosia alianza kazi ya kurekebisha hekalu. Kazi hiyo ilipokuwa ikiendelea, “kitabu cha Sheria ya Yehova kilichotolewa kupitia Musa” kilipatikana. Mfalme aliposikia kikisomwa, alichochewa kuchukua hatua na kutenda kulingana na mambo yaliyoandikwa humo. (2 Nya. 34:14, 19-21) Je, ungependa kusoma Biblia kwa ukawaida? Ikiwa tayari unafanya hivyo je, unafurahia? Je, unaweka kumbukumbu ya mistari ambayo inaweza kukusaidia kibinafsi? Yosia alipokuwa na umri wa miaka 39, alifanya uamuzi mbaya uliomsababishia kifo. Alijitegemea mwenyewe badala ya kumwomba Yehova mwongozo. (2 Nya. 35:20-25) Tunapata somo fulani hapa. Hata iwe tuna umri gani au tumekuwa tukijifunza Biblia kwa muda mrefu kadiri gani, tunapaswa kuendelea kumtafuta Yehova. Hilo linatia ndani kusali kwake kwa ukawaida ili kupata mwongozo, kujifunza Neno lake, na kusikiliza ushauri wa Wakristo wakomavu. Tukifanya hivyo, tutapunguza uwezekano wa kufanya makosa mazito na tutakuwa wenye furaha zaidi.—Yak. 1:25. w23.09 12 ¶15-16