Jumanne, Oktoba 7
Mtembee kwa kumstahili Yehova.—Kol. 1:10.
Mwaka wa 1919, watu wa Mungu waliwekwa huru kutoka katika Babiloni Mkubwa. Mwaka huo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alianza kufanya kazi ili watu wenye mioyo minyoofu waanze kutembea katika ‘Njia hiyo mpya ya Utakatifu’ iliyofunguliwa. (Mt. 24:45-47; Isa. 35:8) Kazi iliyofanywa na “watengeneza-barabara” waliotangulia, iliwasaidia wale walioanza kutembea katika barabara hiyo kuu wajifunze mengi zaidi kumhusu Yehova na makusudi yake. (Met. 4:18) Pia, wangeweza kupatanisha maisha yao na viwango vya Yehova. Yehova hakutarajia watu wake wafanye marekebisho yote yaliyohitajika kwa wakati mmoja. Badala yake, amekuwa akiwasafisha watu wake hatua kwa hatua. Tutafurahi sana wakati ambapo tutaweza kumfurahisha Mungu wetu katika kila jambo tunalofanya! Kila barabara inahitaji kudumishwa kwa ukawaida. Tangu mwaka wa 1919, kazi ya kutengeneza “Njia ya Utakatifu” imekuwa ikiendelea, ili kufanya iwezekane kwa watu wengi zaidi kuondoka katika Babiloni Mkubwa. w23.05 17 ¶15; 19 ¶16
Jumatano, Oktoba 8
Sitakuacha kamwe.—Ebr. 13:5.
Washiriki wa Baraza Linaloongoza wamekuwa wakiwazoeza kibinafsi wasaidizi katika halmashauri mbalimbali za Baraza Linaloongoza. Kwa sasa wasaidizi hao wanashughulikia majukumu mazito kwa uaminifu. Wako tayari kabisa kuendeleza kazi ya kuwatunza kondoo wa Kristo. Watiwa-mafuta wa mwisho watakapochukuliwa na kwenda mbinguni mwishoni mwa ile dhiki kuu, ibada safi itaendelea hapa duniani. Kwa sababu ya uongozi mzuri wa Yesu Kristo, waabudu wa Mungu hawatakosa chochote. Ni kweli kwamba wakati huo tutakuwa tukishambuliwa na Gogu wa Magogu, muungano wa mataifa yenye chuki. (Eze. 38:18-20) Lakini shambulizi hilo fupi halitafaulu; halitawafanya watu wa Mungu waache kumwabudu Yehova. Bila shaka atawaokoa! Katika maono, mtume Yohana aliona “umati mkubwa” wa kondoo wengine wa Kristo. Yohana aliambiwa kwamba ‘umati huo mkubwa’ unatoka “katika ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:9, 14) Naam, tuna uhakika kwamba watakuwa salama! w24.02 5-6 ¶13-14
Alhamisi, Oktoba 9
Msiuzime moto wa roho.—1 The. 5:19.
Tunaweza kufanya nini ili tupokee roho takatifu? Tunaweza kusali ili tupate roho takatifu, kujifunza Neno la Mungu lililoongozwa na roho, na kushirikiana na tengenezo lake linaloongozwa na roho. Kufanya hivyo, kutatusaidia kusitawisha sifa za “tunda la roho.” (Gal. 5:22, 23) Mungu huwapa roho yake wale tu ambao wanadumisha mawazo safi na mwenendo safi. Hataendelea kutupatia roho yake ikiwa tutaendelea kuwa na mawazo yasiyo safi na kutenda kulingana na mawazo hayo. (1 The. 4:7, 8) Ili tuendelee kupokea roho takatifu, pia hatupaswi ‘kuutendea unabii kwa dharau.’ (1 The. 5:20) Hapa “unabii” unamaanisha ujumbe uliotokezwa na roho ya Mungu, kutia ndani ujumbe kuhusu siku ya Yehova na uhitaji wa kutenda haraka katika nyakati zetu. Hatuahirishi siku hiyo katika akili zetu na kufikiri kwamba Har–Magedoni haitakuja tukiwa hai. Badala yake, tunaiweka karibu akilini kwa kudumisha mwenendo unaofaa na kuendelea kuwa na bidii katika “vitendo vya ujitoaji-kimungu.”—2 Pet. 3:11, 12. w23.06 12 ¶13-14