Jumatano, Agosti 13
Nitakufanya kuwa taifa kubwa.—Mwa. 12:2.
Yehova alitoa ahadi hiyo kwa Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 75 na bila mtoto. Je, Abrahamu aliona ahadi hiyo ikitimizwa? Hakuona ikitimizwa kikamili. Baada ya kuvuka Mto Efrati na kusubiri kwa miaka 25, Abrahamu aliona mwana wake, Isaka, akizaliwa kimuujiza, na baada ya miaka mingine 60, wajukuu wake, Esau na Yakobo walizaliwa. (Ebr. 6:15) Lakini Abrahamu hakuona kamwe wazao wake wakiwa taifa kubwa na kurithi Nchi ya Ahadi. Hata hivyo, mwanamume huyo mwaminifu alifurahia urafiki wa karibu pamoja na Muumba wake. (Yak. 2:23) Na Abrahamu atakapofufuliwa, atasisimka sana kujua kwamba imani na subira yake ilitokeza baraka kwa mataifa yote! (Mwa. 22:18) Somo ni nini? Huenda sisi binafsi hatutaona ahadi zote za Yehova zikitimizwa moja kwa moja. Hata hivyo, ikiwa tutakuwa wenye subira kama Abrahamu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatuthawabisha sasa na kwa njia kubwa hata zaidi katika ulimwengu mpya alioahidi.—Marko 10:29, 30. w23.08 24 ¶14
Alhamisi, Agosti 14
Wakati alipokuwa akimtafuta Yehova, Mungu wa kweli alimfanikisha.—2 Nya. 26:5.
Alipokuwa kijana Mfalme Uzia alikuwa mnyenyekevu. Alijifunza “kumwogopa Mungu wa kweli.” Aliishi kwa miaka 68, na kwa sehemu kubwa ya maisha yake Yehova alimbariki. (2 Nya. 26:1-4) Uzia aliwashinda maadui wengi na aliimarisha ulinzi wa jiji la Yerusalemu. (2 Nya. 26:6-15) Bila shaka, Uzia alifurahia mambo yote ambayo Mungu alimsaidia kufanya. (Mhu. 3:12, 13) Mfalme Uzia alizoea kuwapa watu maagizo. Je, hilo lilimfanya afikiri kwamba angeweza kufanya chochote alichotaka? Siku moja, Uzia aliingia katika hekalu la Yehova na kwa kimbelembele alijaribu kufukiza uvumba kwenye madhabahu, jambo ambalo wafalme hawakuruhusiwa kufanya. (2 Nya. 26:16-18) Kuhani Mkuu Azaria alijaribu kumrekebisha, lakini Uzia alikasirika sana. Kwa kusikitisha, Uzia aliharibu rekodi yake ya kutumikia kwa uaminifu na Yehova akampiga kwa ukoma. (2 Nya. 26:19-21) Maisha yake yangekuwa tofauti sana ikiwa angeendelea kuwa mnyenyekevu! w23.09 10 ¶9-10
Ijumaa, Agosti 15
Akajitenga kwa kuwaogopa wale waliotahiriwa.—Gal. 2:12.
Hata baada ya kuwa Mkristo aliyetiwa mafuta, bado mtume Petro alipambana na udhaifu wake mbalimbali. Mwaka wa 36 W.K., Petro alikuwepo wakati Kornelio, Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa, alipotiwa mafuta kwa roho takatifu, jambo lililothibitisha wazi kwamba “Mungu hana ubaguzi” na kwamba watu wa mataifa wangekuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo. (Mdo. 10:34, 44, 45) Baada ya hapo, Petro alijihisi huru kula chakula pamoja na Watu wa Mataifa, jambo ambalo hangeweza kufanya kamwe hapo awali. Hata hivyo, baadhi ya Wakristo Wayahudi walihisi kwamba Wayahudi na Watu wa Mataifa hawapaswi kula pamoja. Baadhi ya watu waliokuwa na maoni hayo walipokuja huko Antiokia, Petro aliacha kula pamoja na ndugu zake waliokuwa Watu wa Mataifa, inawezekana ni kwa sababu aliogopa kuwakasirisha Wakristo Wayahudi. Mtume Paulo alipoona unafiki huo alimkemea Petro hadharani. (Gal. 2:13, 14) Licha ya kufanya kosa hilo, Petro aliendelea kuwa mwaminifu. w23.09 22 ¶8