Alhamisi, Agosti 14
Wakati alipokuwa akimtafuta Yehova, Mungu wa kweli alimfanikisha.—2 Nya. 26:5.
Alipokuwa kijana Mfalme Uzia alikuwa mnyenyekevu. Alijifunza “kumwogopa Mungu wa kweli.” Aliishi kwa miaka 68, na kwa sehemu kubwa ya maisha yake Yehova alimbariki. (2 Nya. 26:1-4) Uzia aliwashinda maadui wengi na aliimarisha ulinzi wa jiji la Yerusalemu. (2 Nya. 26:6-15) Bila shaka, Uzia alifurahia mambo yote ambayo Mungu alimsaidia kufanya. (Mhu. 3:12, 13) Mfalme Uzia alizoea kuwapa watu maagizo. Je, hilo lilimfanya afikiri kwamba angeweza kufanya chochote alichotaka? Siku moja, Uzia aliingia katika hekalu la Yehova na kwa kimbelembele alijaribu kufukiza uvumba kwenye madhabahu, jambo ambalo wafalme hawakuruhusiwa kufanya. (2 Nya. 26:16-18) Kuhani Mkuu Azaria alijaribu kumrekebisha, lakini Uzia alikasirika sana. Kwa kusikitisha, Uzia aliharibu rekodi yake ya kutumikia kwa uaminifu na Yehova akampiga kwa ukoma. (2 Nya. 26:19-21) Maisha yake yangekuwa tofauti sana ikiwa angeendelea kuwa mnyenyekevu! w23.09 10 ¶9-10
Ijumaa, Agosti 15
Akajitenga kwa kuwaogopa wale waliotahiriwa.—Gal. 2:12.
Hata baada ya kuwa Mkristo aliyetiwa mafuta, bado mtume Petro alipambana na udhaifu wake mbalimbali. Mwaka wa 36 W.K., Petro alikuwepo wakati Kornelio, Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa, alipotiwa mafuta kwa roho takatifu, jambo lililothibitisha wazi kwamba “Mungu hana ubaguzi” na kwamba watu wa mataifa wangekuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo. (Mdo. 10:34, 44, 45) Baada ya hapo, Petro alijihisi huru kula chakula pamoja na Watu wa Mataifa, jambo ambalo hangeweza kufanya kamwe hapo awali. Hata hivyo, baadhi ya Wakristo Wayahudi walihisi kwamba Wayahudi na Watu wa Mataifa hawapaswi kula pamoja. Baadhi ya watu waliokuwa na maoni hayo walipokuja huko Antiokia, Petro aliacha kula pamoja na ndugu zake waliokuwa Watu wa Mataifa, inawezekana ni kwa sababu aliogopa kuwakasirisha Wakristo Wayahudi. Mtume Paulo alipoona unafiki huo alimkemea Petro hadharani. (Gal. 2:13, 14) Licha ya kufanya kosa hilo, Petro aliendelea kuwa mwaminifu. w23.09 22 ¶8
Jumamosi, Agosti 16
Atawapa msingi imara.—1 Pet. 5:10.
Jichunguze kwa unyoofu ili kutambua udhaifu wowote ulio nao, lakini usivunjike moyo. “Bwana ni mwenye fadhili,” na atakusaidia kufanya maendeleo. (1 Pet. 2:3) Mtume Petro anatuhakikishia hivi: “Mungu . . . mwenyewe atamaliza mazoezi yenu. Atafanya muwe imara.” Pindi moja, Petro alihisi kwamba hastahili kuwa pamoja na Mwana wa Mungu. (Luka 5:8) Lakini kwa msaada wa upendo kutoka kwa Yehova na Yesu, Petro aliendelea kuwa mwaminifu akiwa mfuasi wa Kristo. Hivyo, Petro alipata kibali cha “kuingia katika Ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:11) Hiyo ilikuwa baraka iliyoje! Ikiwa utaendelea kuwa mwaminifu kama Petro alivyofanya na kukubali kuzoezwa na Yehova, wewe pia utapata thawabu ya uzima wa milele. ‘Utafikia lengo la imani yako, wokovu wako.’—1 Pet. 1:9. w23.09 31 ¶16-17