Ijumaa, Agosti 15
Akajitenga kwa kuwaogopa wale waliotahiriwa.—Gal. 2:12.
Hata baada ya kuwa Mkristo aliyetiwa mafuta, bado mtume Petro alipambana na udhaifu wake mbalimbali. Mwaka wa 36 W.K., Petro alikuwepo wakati Kornelio, Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa, alipotiwa mafuta kwa roho takatifu, jambo lililothibitisha wazi kwamba “Mungu hana ubaguzi” na kwamba watu wa mataifa wangekuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo. (Mdo. 10:34, 44, 45) Baada ya hapo, Petro alijihisi huru kula chakula pamoja na Watu wa Mataifa, jambo ambalo hangeweza kufanya kamwe hapo awali. Hata hivyo, baadhi ya Wakristo Wayahudi walihisi kwamba Wayahudi na Watu wa Mataifa hawapaswi kula pamoja. Baadhi ya watu waliokuwa na maoni hayo walipokuja huko Antiokia, Petro aliacha kula pamoja na ndugu zake waliokuwa Watu wa Mataifa, inawezekana ni kwa sababu aliogopa kuwakasirisha Wakristo Wayahudi. Mtume Paulo alipoona unafiki huo alimkemea Petro hadharani. (Gal. 2:13, 14) Licha ya kufanya kosa hilo, Petro aliendelea kuwa mwaminifu. w23.09 22 ¶8
Jumamosi, Agosti 16
Atawapa msingi imara.—1 Pet. 5:10.
Jichunguze kwa unyoofu ili kutambua udhaifu wowote ulio nao, lakini usivunjike moyo. “Bwana ni mwenye fadhili,” na atakusaidia kufanya maendeleo. (1 Pet. 2:3) Mtume Petro anatuhakikishia hivi: “Mungu . . . mwenyewe atamaliza mazoezi yenu. Atafanya muwe imara.” Pindi moja, Petro alihisi kwamba hastahili kuwa pamoja na Mwana wa Mungu. (Luka 5:8) Lakini kwa msaada wa upendo kutoka kwa Yehova na Yesu, Petro aliendelea kuwa mwaminifu akiwa mfuasi wa Kristo. Hivyo, Petro alipata kibali cha “kuingia katika Ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:11) Hiyo ilikuwa baraka iliyoje! Ikiwa utaendelea kuwa mwaminifu kama Petro alivyofanya na kukubali kuzoezwa na Yehova, wewe pia utapata thawabu ya uzima wa milele. ‘Utafikia lengo la imani yako, wokovu wako.’—1 Pet. 1:9. w23.09 31 ¶16-17
Jumapili, Agosti 17
Mwabuduni Yule aliyeziumba mbingu na dunia.—Ufu. 14:7.
Hema la ibada la kale lilikuwa na ua mmoja—eneo lililo wazi ambalo lilikuwa limezungushiwa wigo au ukingo, mahali ambapo makuhani walitimiza majukumu yao. Madhabahu kubwa ya shaba ya dhabihu za kuteketezwa ilikuwa katika ua pamoja na beseni kubwa la maji la shaba ambalo makuhani walitumia kujitakasa kabla ya kutimiza utumishi wao mtakatifu. (Kut. 30:17-20; 40:6-8) Leo, watiwa-mafuta waliobaki duniani ambao ni ndugu za Kristo wanatumikia kwa uaminifu katika ua wa ndani wa hekalu la kiroho duniani. Kuwepo kwa beseni kubwa la maji ni kikumbusho muhimu kwao, na kwa Wakristo wote cha kuendelea kuwa safi kiadili na kiroho. Basi, wale wanaofanyiza “umati mkubwa,” wanamwabudu Yehova wakiwa wapi? Mtume Yohana aliwaona wakiwa “wamesimama mbele ya kiti cha ufalme,” sehemu ambayo inalingana na ua wa nje duniani, ambapo “wanamtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufu. 7:9, 13-15) Tunathamini sana pendeleo la kushiriki katika mpango wa ibada safi ya Yehova! w23.10 28 ¶15-16