Ijumaa, Agosti 29
Nimewajulisha jina lako.—Yoh. 17:26.
Yesu alifanya mengi zaidi ya kuwaambia tu watu kwamba jina la Mungu ni Yehova. Wayahudi ambao Yesu aliwafundisha tayari walilijua jina la Mungu. Lakini Yesu ndiye aliyekuwa mstari wa mbele akiwa yule ‘aliyeeleza kumhusu.’ (Yoh. 1:17, 18) Kwa mfano, Maandiko ya Kiebrania yanafunua kwamba Yehova ni mwenye rehema na huruma. (Kut. 34:5-7) Yesu alifafanua kweli hiyo hata zaidi aliposimulia kuhusu mfano wa mwana mpotevu na baba yake. Tunaposoma kuhusu jinsi baba huyo anavyomwona mwana wake aliyetubu “akiwa mbali,” anavyokimbia ili kukutana naye, anavyomkumbatia, na kumsamehe kutoka moyoni, tunapata picha kamili zaidi ya rehema na huruma ya Yehova. (Luka 15:11-32) Yesu aliwasaidia wengine waelewe vizuri kabisa utu wa Baba yake. w24.02 10 ¶8-9
Jumamosi, Agosti 30
[Tuwafariji] wengine . . . kwa faraja ambayo tunapokea kutoka kwa Mungu.—2 Kor. 1:4.
Yehova anawaburudisha na kuwafariji wale wanaokabili hali ngumu. Tunawezaje kumwiga Yehova kwa kuwaonyesha wengine huruma na kuwafariji? Njia moja tunayoweza kufanya hivyo ni kwa kusitawisha sifa zitakazotusaidia kuonyesha huruma na kuwafariji wengine. Baadhi ya sifa hizo ni zipi? Ni nini kitakachotusaidia tudumishe upendo wetu na ‘kuendelea kufarijiana’ kila siku? (1 The. 4:18) Tunahitaji kusitawisha sifa nyororo kama vile hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, na fadhili. (Kol. 3:12; 1 Pet. 3:8) Sifa hizo zitatusaidiaje? Tunapowahurumia ndugu zetu na kuwajali kikweli, tutakuwa na tamaa yenye nguvu ya kuwafariji wanapoteseka. Kama Yesu alivyosema, “kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni. Mtu mwema hutoa mambo mema katika hazina yake njema.” (Mt. 12:34, 35) Kuwafariji ndugu na dada zetu wenye uhitaji ni njia muhimu sana ya kuwaonyesha kwamba tunawapenda. w23.11 10 ¶10-11
Jumapili, Agosti 31
Wale walio na ufahamu wataelewa.—Dan. 12:10.
Tunahitaji kuomba msaada ili tuelewe unabii wa Biblia. Fikiria mfano ufuatao. Wazia kwamba unatembelea eneo fulani ambalo hulifahamu, lakini rafiki yako ambaye mnasafiri pamoja analielewa vizuri eneo hilo. Anajua kabisa mahali mlipo na anajua kila barabara katika eneo hilo. Bila shaka, utafurahi kwamba rafiki yako alikubali kusafiri pamoja nawe! Vivyo hivyo, Yehova anajua mahali tulipo katika mkondo wa wakati na mambo yatakayotokea wakati ujao. Basi, ili kuelewa unabii wa Biblia, tunapaswa kumwomba Yehova msaada kwa unyenyekevu. (Dan. 2:28; 2 Pet. 1:19, 20) Kama mzazi mwenye upendo, Yehova anataka watoto wake wawe na wakati ujao wenye furaha. (Yer. 29:11) Lakini tofauti na wazazi wa kibinadamu, Yehova anaweza kutabiri kuhusu wakati ujao kwa usahihi kabisa. Aliagiza unabii uandikwe katika Neno lake ili tujue matukio muhimu kabla hayajatokea.—Isa. 46:10. w23.08 8 ¶3-4