Jumapili, Agosti 31
Wale walio na ufahamu wataelewa.—Dan. 12:10.
Tunahitaji kuomba msaada ili tuelewe unabii wa Biblia. Fikiria mfano ufuatao. Wazia kwamba unatembelea eneo fulani ambalo hulifahamu, lakini rafiki yako ambaye mnasafiri pamoja analielewa vizuri eneo hilo. Anajua kabisa mahali mlipo na anajua kila barabara katika eneo hilo. Bila shaka, utafurahi kwamba rafiki yako alikubali kusafiri pamoja nawe! Vivyo hivyo, Yehova anajua mahali tulipo katika mkondo wa wakati na mambo yatakayotokea wakati ujao. Basi, ili kuelewa unabii wa Biblia, tunapaswa kumwomba Yehova msaada kwa unyenyekevu. (Dan. 2:28; 2 Pet. 1:19, 20) Kama mzazi mwenye upendo, Yehova anataka watoto wake wawe na wakati ujao wenye furaha. (Yer. 29:11) Lakini tofauti na wazazi wa kibinadamu, Yehova anaweza kutabiri kuhusu wakati ujao kwa usahihi kabisa. Aliagiza unabii uandikwe katika Neno lake ili tujue matukio muhimu kabla hayajatokea.—Isa. 46:10. w23.08 8 ¶3-4
Jumatatu, Septemba 1
Tutapata mapambazuko kutoka juu.—Luka 1:78.
Mungu amempa Yesu nguvu za kutatua matatizo yote ya wanadamu. Kupitia miujiza yake, Yesu alionyesha kwamba ana nguvu za kutatua matatizo yote ambayo hatuwezi kusuluhisha. Kwa mfano, ana uwezo wa kutuweka huru kutoka kwa chanzo cha matatizo ya wanadamu, yaani, dhambi tuliyorithi na matokeo yake, ugonjwa na kifo. (Mt. 9:1-6; Rom. 5:12, 18, 19) Miujiza aliyofanya inathibitisha kwamba anaweza kuponya “kila aina ya ugonjwa” na hata kuwafufua wafu. (Mt. 4:23; Yoh. 11:43, 44) Pia, ana nguvu za kudhibiti dhoruba kali ya upepo na kuwashinda roho waovu. (Marko 4:37-39; Luka 8:2) Tunafarijika kujua kwamba Yehova amempa Mwana wake nguvu hizo! Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba baraka za wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu zitatimia. Miujiza ambayo Yesu alifanya alipokuwa mwanadamu duniani, inatufundisha mambo atakayofanya kwa kiwango kikubwa zaidi akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu ulio mbinguni. w23.04 3 ¶5-7
Jumanne, Septemba 2
Roho huchunguza ndani ya mambo yote, hata mambo mazito ya Mungu.—1 Kor. 2:10.
Ikiwa upo kwenye kutaniko kubwa na unahisi kwamba mara nyingi hupati nafasi ya kutoa maelezo, huenda ukashawishiwa kutoinua mkono tena. Lakini usiache kujitahidi kutoa maelezo. Tayarisha maelezo kadhaa kwa ajili ya kila mkutano. Kisha ikiwa hutachaguliwa kutoa maelezo mwanzoni mwa funzo, bado utakuwa na nafasi nyingine ya kutoa maelezo mkutano unapoendelea. Unapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi, fikiria jinsi kila fungu linavyohusiana na kichwa kikuu cha makala. Ukifanya hivyo, inaelekea kwamba utakuwa tayari kutoa maelezo wakati wowote wa funzo. Isitoshe, unaweza kujitayarisha kutoa maelezo katika mafungu ambayo yanazungumzia mafundisho mazito ya Biblia ambayo ni vigumu zaidi kuyaelezea. Kwa nini? Kwa sababu huenda si watu wengi watainua mkono katika sehemu hiyo. Namna gani ikiwa unatambua kwamba baada ya mikutano kadhaa bado hujapata nafasi ya kutoa maelezo? Kabla ya mkutano, mweleze yule anayeongoza swali ambalo ungependa kujibu. w23.04 21-22 ¶9-10