Jumatatu, Septemba 1
Tutapata mapambazuko kutoka juu.—Luka 1:78.
Mungu amempa Yesu nguvu za kutatua matatizo yote ya wanadamu. Kupitia miujiza yake, Yesu alionyesha kwamba ana nguvu za kutatua matatizo yote ambayo hatuwezi kusuluhisha. Kwa mfano, ana uwezo wa kutuweka huru kutoka kwa chanzo cha matatizo ya wanadamu, yaani, dhambi tuliyorithi na matokeo yake, ugonjwa na kifo. (Mt. 9:1-6; Rom. 5:12, 18, 19) Miujiza aliyofanya inathibitisha kwamba anaweza kuponya “kila aina ya ugonjwa” na hata kuwafufua wafu. (Mt. 4:23; Yoh. 11:43, 44) Pia, ana nguvu za kudhibiti dhoruba kali ya upepo na kuwashinda roho waovu. (Marko 4:37-39; Luka 8:2) Tunafarijika kujua kwamba Yehova amempa Mwana wake nguvu hizo! Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba baraka za wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu zitatimia. Miujiza ambayo Yesu alifanya alipokuwa mwanadamu duniani, inatufundisha mambo atakayofanya kwa kiwango kikubwa zaidi akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu ulio mbinguni. w23.04 3 ¶5-7
Jumanne, Septemba 2
Roho huchunguza ndani ya mambo yote, hata mambo mazito ya Mungu.—1 Kor. 2:10.
Ikiwa upo kwenye kutaniko kubwa na unahisi kwamba mara nyingi hupati nafasi ya kutoa maelezo, huenda ukashawishiwa kutoinua mkono tena. Lakini usiache kujitahidi kutoa maelezo. Tayarisha maelezo kadhaa kwa ajili ya kila mkutano. Kisha ikiwa hutachaguliwa kutoa maelezo mwanzoni mwa funzo, bado utakuwa na nafasi nyingine ya kutoa maelezo mkutano unapoendelea. Unapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi, fikiria jinsi kila fungu linavyohusiana na kichwa kikuu cha makala. Ukifanya hivyo, inaelekea kwamba utakuwa tayari kutoa maelezo wakati wowote wa funzo. Isitoshe, unaweza kujitayarisha kutoa maelezo katika mafungu ambayo yanazungumzia mafundisho mazito ya Biblia ambayo ni vigumu zaidi kuyaelezea. Kwa nini? Kwa sababu huenda si watu wengi watainua mkono katika sehemu hiyo. Namna gani ikiwa unatambua kwamba baada ya mikutano kadhaa bado hujapata nafasi ya kutoa maelezo? Kabla ya mkutano, mweleze yule anayeongoza swali ambalo ungependa kujibu. w23.04 21-22 ¶9-10
Jumatano, Septemba 3
Yosefu akaamka . . . na kufanya kama alivyoambiwa na malaika wa Yehova, akampeleka mke wake nyumbani.—Mt. 1:24.
Yosefu alikuwa tayari kufuata mwongozo wa Yehova, na hilo lilimfanya awe mume mzuri. Katika pindi tatu tofauti, alipata mwongozo kutoka kwa Yehova kuhusu familia yake. Kila mara, alitii bila kusita, hata ilipomaanisha kufanya mabadiliko makubwa. (Mt. 1:20; 2:13-15, 19-21) Kwa kufuata mwongozo wa Yehova, Yosefu alimlinda Maria, akamtegemeza, na kumwandalia mahitaji yake. Wazia jinsi matendo ya Yosefu yalivyomfanya Maria ampende na kumheshimu hata zaidi! Waume, mnaweza kumwiga Yosefu kwa kutafuta ushauri katika Biblia kuhusu jinsi ya kutunza familia zenu. Unapofuata ushauri huo, hata ikimaanisha kufanya mabadiliko fulani, unaonyesha kwamba unampenda mke wako na unaimarisha ndoa yenu. Dada mmoja nchini Vanuatu ambaye amefunga ndoa kwa zaidi ya miaka 20 anasema hivi: “Mume wangu anapotafuta na kufuata mwongozo wa Yehova, ninamheshimu hata zaidi. Ninajihisi salama, na nina uhakika katika maamuzi anayofanya.” w23.05 21 ¶5